Kikwete azusha gumzo
IDDI SIMBA AONGEZWA KATIKA KAMATI
na Waandishi Wetu
Tanzania Daima
UAMUZI wa Rais Jakaya Kikwete kuitangaza Kamati ya Kuangalia Mikataba ya Uchimbaji wa Madini nchini, akimjumuisha Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe, umeibua maswali mengi na kugubika mazungumzo na mijadala ya kisiasa nchini.
Watu wa kada mbalimbali kwa siku nzima jana walikuwa wakijadili kuhusu uamuzi huo wa aina yake, ukimjumuisha mwanasiasa wa upinzani ambaye hivi sasa angali akitumikia adhabu ya kusimamishwa kuhudhuria vikao vya Bunge, kwa sababu ya kutoa hoja ya kuhoji kuhusu mikataba ya madini na hususan uamuzi wa Waziri wa Madini na Nishati, Nazir Karamagi, kusaini mkataba mpya wa uchimbaji wa dhahabu wa Buzwagi.
Miongoni mwa watu walioguswa na uamuzi huo wa Rais ni Zitto mwenyewe, ambaye jana katika mahojiano ya ana kwa ana na gazeti hili aliuelezea uamuzi huo wa Kikwete kuwa ni changamoto muhimu kwa wabunge 272 wa Chama Cha Mapinduzi, ambao Agosti 14, mwaka huu waliungana kuhakikisha akisimamishwa ubunge.
Zitto ambaye alikuwa akizungumza na gazeti hili muda mfupi kabla hajapanda ndege kwenda Kigoma kutembelea jimbo lake, alisema anavyoona yeye ni kwamba, uamuzi huo wa Rais Kikwete unakinzana kimantiki na ule wa wabunge wa chama ambacho yeye (Kikwete) ni mwenyekiti wake wa taifa.
Mbali ya hilo, mbunge huyo mdogo kuliko wote kiumri kwa wabunge wa kuchaguliwa, akiwa na miaka 31 sasa, alisema Kikwete amefanya hivyo akiitikia kilio cha wananchi ambao siku zote wamekuwa wakitaka kuona mikataba ya madini ikipitiwa upya.
"Ninachokiona mimi ni kwamba rais amewasikia wananchi. Kwa kuniteua kuwa mjumbe wa kamati hiyo ya kuchunguza mikataba ya madini, wakati nikiendelea kutumikia adhabu, amefanya kitu ambacho ni tofauti kabisa na kile kilichofanywa na wabunge 272 wa chama chake, Agosti mwaka huu, walioungana kunisimamisha," alisema Zitto.
Alipoulizwa iwapo uamuzi huo wa Rais Kikwete hauwezi kuwa mbinu ya kusambaratisha upinzani au kumnyamazisha yeye binafsi, Zitto pasipo kutaka kuingia kwa undani, alikiri kufahamu kuwapo kwa wasiwasi wa namna hiyo miongoni mwa watu mbalimbali.
"Wako watu ambao wameonyesha wasiwasi huo. Kazi ya upinzani ni kupigania maendeleo. Upinzani maana yake ni kujenga nchi, kwa watu wanaoangalia masilahi yao, uteuzi kama huu unaweza ukaonekana kuwa ni mtego, wakati kwangu si hivyo.
"Sikubaliani hata kidogo na mawazo kwamba rais eti ameniteua katika kamati hiyo ili kunifunga mdogo au kudhoofisha upinzani. Angekuwa na mawazo kama hayo asingeniteua," alisema Zitto kwa kujiamini.
Kuhusu msimamo wa chama chake kuhusu uteuzi wake huo, Zitto ambaye ni Naibu Katibu Mkuu wa Chadema, alisema katiba ya chama hicho inaeleza bayana kwamba, katika masuala yenye masilahi kitaifa chama hicho kinayaangalia kwa upeo wa juu nje ya matakwa ya kichama.
Wakati Zitto akitoa kauli hizo, uchunguzi uliofanywa na Tanzania Daima unaonyesha kuwa, makada kadhaa ndani ya Chadema, wanauchukulia uteuzi huo kwa tahadhari kubwa, huku baadhi yao wakikiona kitendo hicho kuwa kinacholenga kukihujumu.
Kutokana na hali hiyo, tangu uteuzi huo utangazwe juzi jioni na hadi kufikia jana, viongozi wa chama hicho walio katika maeneo mbalimbali nchini, walikuwa wakibadilishana maoni kwa njia ya simu na ujumbe wa maandishi katika simu zao za viganjani kuhusu uteuzi huo huku kila mmoja akiwa na maoni yake.
Jitihada za mwandishi wa habari wa gazeti hili aliye Dodoma kuzungumza na Waziri Karamagi aliye katikati ya sakata la mgodi wa Buzwagi, kuhusu uamuzi huo wa Rais Kikwete, uligonga mwamba kwani alipofuatwa wakati Bunge lilipoahirishwa jana mchana, hakuwa tayari kufungua mdomo wake, zaidi tu ya kunyosha mkono akitoa ishara ya kutokuwa tayari kusema lolote.
Akizungumzia uteuzi huo, mmoja wa viongozi wa Chama cha Wananchi (CUF), Ismael Jussa, aliuelezea uteuzi huo kuwa ni moja ya matukio yanayoweza yakathibitisha kuwa, ‘Rais Kikwete akiamua anaweza.'
Jussa, mmoja wa vijana wenye ushawishi mkubwa ndani ya CUF na mtu aliyepata kuwa msaidizi wa karibu wa Katibu Mkuu wa chama hicho, Maalim Seif Sharif Hamad, aliieleza Tanzania Daima kwamba, hata yeye mwenyewe hakuna na uhakika iwapo Kikwete angeweza kuchukua hatua inayokinzana na kile kilichodanywa na wabunge wa chama chake miezi mitatu tu iliyopita.
"Rais amechukua maamuzi ambayo ni kinyume cha maamuzi ya Bunge. Ameonyesha kwa vitendo kuwa akitaka anaweza. Ameunda kamati nzuri yenye watu wenye uwezo, Jaji Mark Bomani anafahamika, Harisson Mwakyembe ni mtu makini, nimepata kuwa naye ndani ya Tume ya Muafaka. Hii ni kamati nzito na isiyo ya kibabaishaji," alisema Jussa.
Mwananchi mmoja wa Dar es Salaam, Charles Mbowe, yeye alisema Kikwete amechukua hatua hiyo lengo likiwa ni kurudisha imani ambayo wananchi walianza kuipoteza kwa serikali yake.
Waziri Kivuli wa Nishati na Madini, ambaye pia ni mjumbe wa Kamati ya Bunge ya Uwekezaji na Biashara, Mohammed Mnyaa (CUF), yeye alieleza kutokubaliana na kamati hiyo ya Kikwete, na kushauri kuwa kusingekuwepo na wabunge, kwa sababu ikifanya makosa wabunge wataadhibiwa.
Kwa maoni ya Mnyaa, Rais Kikwete alipaswa kutafuta wanasheria kutoka vyama vinne vya siasa na wataalamu wa madini, ili kuweka usawa na kusema wabunge walitakiwa kupewa matokeo ya kamati tu.
"Wasiwasi wangu ni pale wabunge watakapobebeshwa lawama," alisema Mnyaa huku akimsifu Rais Kikwete kwa kutimiza ahadi yake kwa wakati katika kipindi kisichozidi siku 10 tangu aitoe kwa mara ya kwanza.
Mwenyekiti wa Chama cha Tanzania Labour (TLP), Augustine Mrema, alisema hatua ya Kikwete kuunda kamati hiyo, kumedhihirisha kwamba amezinduka kutoka usingizini, kwa sababu tangu mwaka 2005 alikuwa akielezwa kwamba rasilimali za nchi zimekuwa zikiporwa, lakini alipuuza suala hilo.
"Tunampongeza kwa kuunda hiyo kamati ila sasa ajue Tanzania ina wenyewe na wenyewe ni Watanzania wote, siyo ‘wanamtandao' au wabunge wa CCM peke yao, na kuanzia sasa atambue hao wabunge wake ni wanafiki, wazandiki na hawamsaidii chochote.
"Uamuzi wa kuunda hiyo kamati aliyoitangaza, angeufanya tangu alivyoingia madarakani, heshima yake isingeporomoka kama ilivyoshuka hivi sasa…isije akawa ameunda kamati ya kiini macho, kwa kuwa kuunda kamati ni kitu kingine na kutumia mapendekezo ya kamati ni jambo jingine, hivyo wananchi wasifurahie sana hadi Rais atakapotekeleza kwa vitendo mapendekezo ya kamati hiyo," alisema Mrema.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama cha Democratic (DP), Mchungaji Christopher Mtikila, alisema amefurahishwa na uundwaji wa kamati hiyo, ila ametaka watu watakaobainika kuhusika wachukuliwe hatua mara moja.
Aidha, alisema uteuzi wa Zitto kuwa mmoja wa wajumbe katika kamati hiyo umedhihirisha kwamba uamuzi uliotolewa na Bunge kumsimamisha kuhudhuria vikao haukuwa sahihi na pia umemshushia heshima Spika, Samuel Sitta na wabunge wa CCM.
"Wabunge wa CCM na Spika, wote kwa pamoja walikubali kumfukuza Zitto bungeni, sasa Mwenyekiti wa chama chao na Rais wa nchi, ameona mbunge huyo ni bora zaidi ya wao na ni mbunge anayetanguliza masilahi ya taifa mbele na ndiyo maana amemteua kuwa mjumbe wa kamati hiyo," alisema Mtikila.
Naye Profesa Mwesiga Baregu, alisema: "Kikao cha Bunge kilichopita, Waziri wa Nishati na Madini, Nazir Karamagi, alisema kazi ya kupitia mikataba ya madini ilishakamilika ….juzi Kikwete kaunda kamati ya kupitia upya mikataba hiyo ya madini, sasa hatuoni kwamba Karamagi alilidanganya Bunge?" alihoji.
Naye, Katibu Mkuu wa Chama cha Wafanyakazi wa Shughuli za Meli na Bandari (DOWUTA), Abdallah Kibunda, alisema kutokuwepo kwa mmoja wa viongozi wa masuala ya migodi kutakosesha kupatikana kwa mambo nyeti.
"Rais amechelewesha, sisi kama chama cha wafanyakazi tulitarajia katika kamati hiyo kungekuwepo na mwakilishi kutoka Chama cha Wafanyakazi wa Migodi, Nishati, Ujenzi na Kazi Nyingine (TAMICO).
"Hawa watu wana wafanyakazi wao kule ndani ya migodi, hivyo wanafahamu mambo mengi kuhusiana na masuala ya madini, kuwepo kwao kungeweza kusaidia vitu vingi nyeti kupatikana," alisema Kibunda.
Naye mchimba madini ambaye pia ni Mwenyekiti wa taasisi ya wachimba madini wanawake nchini, Matha Bitwale, alipongeza hatua iliyochukuliwa na Rais Kikwete ya kumweka Zitto katika kamati hiyo, kwani inaonyesha kutaka kuweka wazi, ukweli wa mambo ulivyo katika mkataba huo.
"Ni uamuzi mzuri ambao utasaidia hata wananchi kujua ukweli wa kila kitu kwa sababu Zitto ndiye aliyeibua hoja hiyo, hivyo kamati itafanya kazi kwa uangalifu, hata majbu yatakayotoka hapo wananchi wanaweza kuwa na imani nayo, kuliko ingekuwa na wanachama wa chama kimoja," alisema.
Juzi Rais Kikwete aliunda kamati ya kuangalia upya mikataba ya uchimbaji wa madini nchini, yenye wajumbe kutoka vyama mbalimbali vya siasa, taasisi za serikali na zisizo za kiserikali.
Kamati hiyo itakayofanya kazi kwa miezi mitatu, itaongozwa na Mwanasheria Mkuu wa kwanza mzalendo nchini, Jaji Mark Bomani.
Mbali ya Bomani na Zitto, wajumbe wengine wanaounda kamati hiyo ni Mbunge wa Bariadi Mashariki, John Cheyo (UDP) na Mbunge wa Kyela, Dk. Harrison Mwakyembe (CCM).
Wengine ni Mbunge wa Msalala, Ezekiel Maige (CCM), Peter Machunde anayetoka Soko la Hisa, Dar es Salaam na David Tarimo, kutoka Kampuni ya Price Water Coopers.
Pia wamo Maria Kejo, ambaye ni Mkurugenzi wa Madai na Sheria za Kimataifa kutoka Wizara ya Katiba na Sheria, Mwanasheria wa Wizara ya Nishati na Madini, Salome Makange, Kamishna wa Sera Wizara ya Fedha, Mugisha Kamugisha, na Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Makazi, Wizara ya Ardhi, Edward Kihundwa.
Jana, Ikulu ilitangaza kumwongeza mbunge wa zamani wa Ilala, aliyepata kuwa Waziri wa Viwanda na Biashara, Iddi Simba, kuwa mmoja wa wajumbe wanaounda kamati hiyo.
Hadidu za rejea za kamati hiyo ni kupitia mikataba ya madini na nyaraka nyingine zinazohusu migodi mikubwa na kuchambua mfumo wa kodi unaotumika katika sekta ya madini.
Aidha, itapitia mfumo wa usimamizi wa shughuli za uchimbaji mkubwa unaofanywa na serikali, itachambua na kuainisha haki na wajibu wa mwekezaji na mwenye rasilimali (serikali), na pia itakutana na ‘Chamber of Minerals' na wadau wengine.
Taarifa hii imeandaliwa na Happiness Katabazi, Irene Mark, Hellen Ngoromera na Mkolo Kimenya.