nngu007
JF-Expert Member
- Aug 2, 2010
- 15,862
- 5,797
Waandishi Wetu - RaiaMwema
Dodoma
Mjumbe wa NEC ya CCM, Edward Lowassa
Lowassa, Chenge utata, Rostam Aziz milango yafunguka
Wabunge wawekewa kikwazo, Wassira, Lukuvi wapinga
MIPANGO ya siri iliyoandaliwa kumng'oa Rais Jakaya Kikwete kwenye uenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) imekwama, huku marekebisho ya Katiba yanayomng'oa Edward Lowassa na baadhi ya mahasimu wake kisiasa, katika Halmashauri Kuu mpya ya chama hicho itakayochuja majina ya wagombea urais katika Uchaguzi Mkuu ujao 2015, yakiridhiwa, imefahamika.
Kwa mujibu wa vyanzo mbalimbali vya habari kutoka ndani ya kikao cha NEC-CCM iliyokutana mwisho ni mwa wiki iliyopita mjini Dodoma, mipango hiyo ya siri mzungumzaji wake mkuu anadaiwa kuwa Kingunge Ngombale-Mwiru, ambaye hata hivyo, katika mazungumzo yake na gazeti hili, hakutaka kuzungumzia masuala hayo.
Mpango wa kwanza wa siri ulikuwa ni kuzuia kupitisha marekebisho ya Katiba ya CCM ambayo sasa inawaengua wabunge kugombea nafasi za ujumbe wa Halmashauri Kuu (NEC) ya chama hicho, kutoka wilayani.
NEC ndicho "chombo" ambacho baada ya uchaguzi wake kukamilika baadaye mwaka huu, kitakuwa na dhima ya kuchuja na kupitisha mgombea urais kwa tiketi ya chama hicho katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015.
Kama mpango huo wa kwanza ungefanikiwa, mtoa habari wetu anaeleza kuwa ungesaidia kurahisisha utekelezaji wa mpango wa pili ambao ulipaswa kuibuliwa katikati ya mjadala wa hali ya kisiasa nchini, kwenye kikao hicho cha NEC.
Mipango hiyo ilitarajiwa kufanyika katika wakati ambao, Rais Kikwete analaumiwa na baadhi ya wana-CCM kwa kujadiliana na vyama vya upinzani na hasa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kuhusu marekebisho ya sheria ya mabadiliko ya Katiba, yaliyopitishwa na Bunge wiki iliyopita.
Mpango wa kwanza
Katika mpango wa kwanza, ilikuwa ni kufanikisha kuzuia mabadiliko ya Katiba ya CCM ambayo yangekuwa na athari kubwa zaidi kwa mitandao ndani ya chama hicho iliyojipanga kwa ajili ya mchakato wa kumpata mgombea urais akayepeperusha bendera katika Uchaguzi Mkuu wa 2015.
Kikubwa ambacho kinavuruga mipango ya mitandao mingi ya urais kwenye CCM ni kubadili nafasi za wajumbe wa NEC kutoka ngazi ya mikoa hadi wilaya. Kwa sasa, baada ya mabadiliko hayo, nafasi ya NEC itagombewa ngazi ya wilaya.
Lakini kubwa zaidi hapo ni masharti mapya ya kazi yaliyowekwa kwa mtu anayepaswa kugombea na hata kuchaguliwa kuwa m-NEC kutoka wilayani.
Masharti hayo ni kugeuza kazi ya mjumbe wa NEC wilaya kuwa ni kazi ya kudumu na anayegombea hatapaswa kuwa na kazi nyingine ya kudumu ambayo chimbuko lake ni CCM.
Kazi hizo ambazo ni za kudumu ambazo sasa zinamfunga mhusika kugombea u-NEC ni pamoja na ubunge kama inavyoelezwa katika kitabu cha kanuni za uchaguzi wa CCM.
Katika kitabu hicho cha kanuni za uchaguzi ndani ya CCM, toleo la Februari, 2010 ambalo hata hivyo litafanyiwa mabadiliko ili kukidhi marekebisho ya sasa, kanuni katika kipengele cha 22 inaeleza; "mwanachama ambaye anaomba nafasi ya uongozi ambayo ni kazi ya muda wote, hataruhusiwa kushika nafasi ya aina hiyo zaidi ya moja katika chama isipokuwa kama Kamati Kuu imeamua vinginevyo."
Lakini kanuni ya 23 inafafanua kuhusu kazi za kudumu; "Nafasi za uongozi zenye kazi ya muda wote ni kama vile mwenyekiti wa tawi la kijiji au la mitaa, mwenyekiti wa kata/wadi, mwenyekiti wa jimbo, mwenyekiti wa wilaya, mwenyekiti wa mkoa, makatibu wa halmashauri kuu wa ngazi zinazohusika, diwani, mwakilishi na mbunge. Nafasi nyingine za uongozi ni za uwakilishi tu, hivyo wahusika wataendelea na kazi zao za kawaida isipokuwa wakati wa vikao."
Kutokana na kanuni hizo za 22 na 23 kutoka kitabu cha kanuni za uchaguzi wa CCM, ni dhahiri sasa kuwa wabunge wanazuiwa na mabadiliko mapya ambayo yatalazimu kufanya mabadiliko ya kanuni ya 23 ili kazi ya mjumbe wa NEC wilaya iongezwe kuwa ni kazi ya kudumu.
Wabunge wanajikuta wakizuiwa kutokana na tayari kuwa na nafasi moja ya kazi za muda wote ambayo ni ubunge na hivyo watashindwa kuwa na kazi ya pili ya muda wote, ambayo sasa ni u-NEC.
Kwa maana hiyo, wajumbe wa sasa wa NEC ambao ni wabunge watatupwa nje ya NEC ijayo isipokuwa wale waliogombea nafasi hizo kupitia kundi maalumu la taasisi. Kwa mujibu wa taratibu za CCM, Bunge huchagua miongoni mwao kwa idadi maalumu, wajumbe wa NEC-CCM-Taifa.
Kwa hiyo, wakati sasa akina Edward Lowassa, Andrew Chenge na wengine wakitolewa nje ya ulingo wa NEC mpya, akina Samuel Sitta, Christopher ole Sendeka na wengine, wataingia NEC mpya kwa sababu waligombea kupitia kundi la wabunge.
Pengine kwa kujua madhara haya, mpango wa kwanza ulihakikisha mabadiliko haya ya Katiba yanazimwa. Ni Kingunge Ngombale-Mwiru, ambaye anadaiwa kuwa kinara wa kupinga kuridhia mabadiliko hayo, kiasi cha kukataa kuunga mkono wakati wa kupiga kura, huku wenzake wakipima upepo na hatimaye kuamua kuunga mkono.
Mpango wa pili
Katika mpango wa pili, ambao hata hivyo, utekelezaji wake ulikuwa mgumu kutokana na mpango wa kwanza kufeli, kuliibuliwa shinikizo la kutaka mjadala wa hali ya kisiasa nchini upewe nafasi katika kikao hicho cha NEC.
Kama ilivyokuwa katika mpango wa kwanza, Kingunge tena aliendelea, akinukuliwa kueleza kuwa hali ya kisiasa nchini ni mbaya na kwamba, nchi inayumba na kwa hiyo, hali hiyo ni lazima ijadiliwe na hata kuazimiwa.
Ni katika mjadala huo, inadaiwa kuwapo kwa wajumbe kadhaa ambao kwa kadiri ya mwenendo wa mjadala, walipanga kuibua hoja ya kumtaka Mwenyekiti, Rais Kikwete kujiuzulu ili kuwekeza muda wake zaidi katika shughuli za Serikali na kukiacha chama mikononi mwa mtu mwingine.
"Kingunge alieleza kwa nguvu zake zote ni kama vile kulikuwa na malengo ya ziada yaliyojificha. Mwenyekiti aliona ni busara kutoacha kutolewa kwa taarifa za Serikali kuhusu masuala ambayo yametumiwa na Kingunge kufanikisha hoja yake. Kwa hiyo, alichofanya Mwenyekiti ni kuahirisha kikao ili wajumbe wakale chakula na baadaye kurejea kikaoni.
"Tuliporejea kwenye kikao, Serikali iliwasilisha taarifa kupitia kwa Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, kuhusu masuala aliyotumia Kingunge kujenga hoja zake, kwa mfano, suala la madaktari na hili la mchakato wa Katiba mpya," anaeleza mtoa habari wetu.
Kwa mujibu wa mtoa habari mwingine, mpango huo nao ulikufa kwa sababu ulitolewa taarifa tu na haukuletwa kama ajenda na kwamba, kikao hicho cha NEC kilikuwa cha dharura tu chenye ajenda maalumu.
Maelezo ya Kingunge
Mwandishi wetu aliwasiliana na Mzee Kingunge ili pamoja na kueleza baadhi ya yaliyojiri NEC lakini kuizungumzia hali halisi ya kisiasa nchini kwa kuzingatia mtazamo wake.
"Siwezi kuzungumzia masuala hayo kwa sasa. Sipo Dar es Salaam. Hayo si masuala ya kuzungumzia kijuu juu tu," alisema Kingunge ambaye, hata hivyo, hakuwa tayari kuahidi moja kwa moja kukutana na mwandishi wetu kwa ajili ya kuzungumzia kwa kina masuala hayo.
Wassira, Lukuvi "wafeli"
Katika kile kinachoweza kuelezwa kuwa, baadhi ya wabunge bado kuendelea kutamani kushiriki mipango ya juu ya CCM, licha ya wao tayari kuwa na madaraka mengine, wabunge walijipanga kuhakikisha wanaendelea kuwa na fursa ya kugombea ujumbe wa NEC ambao sasa ni ngazi ya wilaya na si mkoa.
Wabunge hao wa CCM baada ya kubaini wamejengewa mazingira ya ‘kuchomolewa' kuwania NEC walijipanga kupinga suala hilo ikiwa ni pamoja na kulijadili na kupitisha azimio ambalo liliwasilishwa kwenye uongozi wa CCM na Katibu wao, Mbunge wa Peramiho, Jenista Muhagama.
Hata hivyo, vyanzo vyetu vya habari vinaeleza kuwa sababu zilizoainishwa na wabunge hao kujinusuru hazikuwa na nguvu ya hoja, zikielemea kukifanya chama chao kuendelea kuwa tegemezi.
"Eti wabunge wanajenga hoja wanasema ni muhimu waendelee kuweza kugombea u-NEC wilayani kwa sababu wao ndiyo wafadhili wa shughuli za chama karibu kila wakati, wao ndiyo wanafadhili mikutano na hata kusafirisha wabunge. Yaani ni mawazo ya kuzidi kukifanya chama tegemezi, kitegemee mifuko yao...na inawezekana ndiyo maana wanang'ang'ania posho nyingi," alieleza mtoa habari wetu ambaye ni kiongozi wa CCM mkoani Dodoma.
Ili kuhakikisha malengo hayo ya wabunge yanasimamiwa, inaelezwa kuwa Jenista Muhagama, alikuwa akisaidiana na mawaziri, Steven Wassira na William Lukuvi, kupinga wabunge kuenguliwa.
Hata hivyo, kwa kujua au kutokujua, vinara hao walijikuta wakiunga mkono yale waliyokuwa wakiyapinga.
"Hoja ilitolewa kwamba wajumbe wa NEC ijayo wilayani wanahitaji kufanya kazi ya chama kwa karibu na wananchi, watembelee matawi na shughuli nyingine ikiwamo kusimamia moja kwa moja maazimio ya vikao vya NEC na ikapendekezwa kazi yao iwe ya muda wote. Inawezekana walisahau kanuni za uchaguzi zinasemaje na hasa kipengele kwamba mwanachama hawezi kuwa na kazi mbili za muda wote na nadhani pia walisahau kama ubunge ni kazi ya muda wote, wakaridhia hili tena Jenista alizungumza vizuri akiunga mkono kwenye Kamati Kuu.
"Baada ya Kamati Kuu kumaliza kikao, hawakugundua na walijipanga upya kulikabili suala lao ndani ya NEC kama lingejitokeza. Nako kwenye NEC hawakuliona, walitaraji lingeandikwa wazi wazi. Kule ilikuja tu hoja ya wajumbe wapya wa NEC wafanye kazi zao kama shughuli za muda wote, wakaunga mkono.
Wassira anadaiwa kumuuliza mjumbe mwenzake wa Kamati Kuu na NEC, Abdulrahman Kinana; "Hivi hili suala la wabunge kutogombea u-NEC limefia wapi? Naye Kinana baada ya kucheka akamjibu; "aaah, mbona limeshapitishwa muda mrefu!"
Wanaoguswa na mabadiliko
Mabadiliko hayo sasa si tu yanawagusa Lowassa na Chenge, bali yatawagusa wabunge wengine ambao bado ni wajumbe wa NEC ya sasa, ambao ni pamoja na Profesa Mark Mwandosya na Dk. Harrison Mwakyembe.
Wengine ni Profesa Peter Msolla, Bernard Membe na mfanyabiashara maarufu, Mohamed Dewji. Kwa upande mwingine, mabadiliko haya pia yanawazuia wafanyabiashara wakubwa ambao ni wabunge kupenya kirahisi NEC kama wana nia hiyo, ambao ni pamoja Aboud Aziz na Ahmed Shabib, lakini Rostam Aziz, anaweza kurudi kuwania u-NEC kwa sababu alijiuzulu ubunge ambao ni kikwazo kwa mujibu wa mabadiliko ya sasa.