Ghazwat
JF-Expert Member
- Oct 4, 2015
- 23,718
- 66,261
Dk. Shein aliyasema hayo Ikulu mjini Zanzibar, wakati alipofanya mazungumzo na Mabalozi wanaokwenda kuiwakilisha Tanzania katika nchi hizo, waliofika Ikulu kumuaga Rais pamoja kujitambulisha na hatimaye kufanya mazungumzo.
Mabalozi hao ni balozi Wilbroad Peter Slaa, balozi wa Tanzania nchini Sweden na balozi Muhidin Ally Mboweto, balozi wa Tanzania nchini Nigeria.
Katika maelezo yake Dk. Shein alisema kuwa shabaha kuu ya serikali zote mbili, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ni kuimarisha sekta za kiuchumi na huduma za jamii ikiwemo sekta ya viwanda, utalii, uvuvi pamoja na elimu na utamaduni.
Dk. Shein alieleza kuwa Serikali zote mbili zimedhamiria kutekeleza Diplomasia ya uchumi katika kuhamasisha uwekezaji hasa katika sekta ya viwanda kwani ndio kiu ya uchumi wa Tanzania hivi sasa.
Akizungumza kwa upande wa Zanzibar, Dk Shein alisema kuwa licha ya Zanzibar kuwa ni visiwa ambavyo vimezungukwa na bahari sambamba na kuwa na azma ya kutekeleza uchumi wa bahari lakini bado hakuna viwanda vya samaki au viwanda vyenye kutumia rasilimali za bahari.
Hivyo, Dk Shein alitumia fursa hiyo kuwaeleza mabalozi hao kuwa Zanzibar inawakaribisha wawakezaji kutoka Sweden na Nigeria kuja kuwekeza katika viwanda vya samaki.
Sambamba na hayo Dk Shein aliwatakia heri na fanaka mabalozi hao katika utendaji wao wa kazi kwenye balozi hizo na kuwaahidi kuwa ataendelea kutoa ushirikano wake kwa mabalozi hao kwa lengo kutekeleza dhamira zao hizo.
Na Mabalozi hao walimthibitishia Dk Shein kuwa wamepokea maelekezo na miongozo yote aliyowapa na kumuahidi kuyafanyia kazi hasa kwa maeneo maalum ya Zanzibar na yale ya Tanzania Bara sambamba na kuimarisha uhusiano na ushirikano kati ya Tanzania na nchi hizo wanazoenda kufanya kazi.