Zaidi ya 90,200 kutinga kidato cha 5, vyuo

kalulukalunde

JF-Expert Member
May 27, 2016
1,056
1,083
JUMLA ya wanafunzi 90,248 wamechaguliwa kujiunga na kidato cha tano na vyuo vya ufundi mwaka 2016 ambapo kati yao wasichana ni 28,911 na wavulana 36,050. Hata hivyo, jumla ya wanafunzi 24,258 sawa na asilimia 27.2 wenye sifa wamekosa nafasi za kujiunga na kidato cha tano kutokana na ufinyu wa nafasi za shule hizo.

Matokeo ya uchaguzi wa wanafunzi hao yalitangazwa jana na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), George Simbachawene (pichani) na kubainisha kuwa jumla ya shule 326 zikiwemo mpya 47 zimepangiwa wanafunzi wa kidato cha tano.

Aliagiza wanafunzi wote kuripoti katika shule walizopangiwa kabla ya Julai 25, mwaka huu na kwamba mwanafunzi atakayechelewa kuripoti nafasi yake itachukuliwa na aliyekosa nafasi. Alisema idadi hiyo imeongezeka kwa wanafunzi 9,958 sawa na asilimia 18.1 ikilinganishwa na wanafunzi 55,003 waliochaguliwa mwaka 2015.

Kati ya wanafunzi waliochaguliwa 34,064 wakiwemo wasichana 13,466 na wavulana 20,598 sawa na asilimia 52.4 watajiunga na masomo ya sayansi na hisabati, wanafunzi 30,897 wakiwemo wasichana 15,445 na wavulana 15,542 sawa na asilimia 47.56 wamechaguliwa kusoma masomo ya sanaa na biashara.

Jumla ya wanafunzi 393,734 wakiwemo wasichana 200,919 na wavulana 192,815 walihitimu kidato cha nne mwaka 2015. Kati yao, wanafunzi 90,380 wakiwemo wasichana 36,005 na wavulana 54,375 walifaulu daraja la kwanza hadi la tatu sawa na asilimia 22.95 ya wanafunzi wote.

Akizungumzia wanafunzi waliochaguliwa kujiunga na vyuo vya ufundi alisema jumla ya wanafunzi 759 wakiwemo wasichana 220 na wavulana 539 wamechaguliwa kujiunga na vyuo vya ufundi, idadi ya wanafunzi hao imeongezeka kwa wanafunzi 280 sawa na asilimia 58.46 ikilinganishwa na wanafunzi 479 waliochaguliwa mwaka 2015.

Aidha kutokana na ufaulu kuongezeka, idadi ya wanafunzi wa kike waliochaguliwa kujiunga na vyuo hivyo imeongezeka kutoka wanafunzi 147 mwaka 2015 hadi wanafunzi 220 mwaka 2016 sawa na ongezeko la wanafunzi 73 ambao ni sawa na asilimia 49.66 Alisema wanafunzi hao ndio walishindanishwa kwenye uchaguzi wa kujiunga na kidato cha tano na vyuo vya ufundi kwa mwaka 2016 na walionekana kuwa na sifa za kuchaguliwa kujiunga na kidato cha tano na vyuo vya ufundi kwa mwaka 2016, sifa hizo ni pamoja na kuwa na ufaulu wa krediti tatu na usiopungua daraja la tatu pointi 25.

Akizungumzia taratibu za uchaguzi wa wanafunzi hao alisema kulingana na utaratibu uliowekwa na serikali, mwanafunzi mwenye sifa za kuchaguliwa kuendelea na kidato cha tano na vyuo vya ufundi ni yule aliyejaza fomu ya uchaguzi.

Alisema kwa kutumia fomu hiyo mwanafunzi hujaza machaguo matano ya tahasusi (combinations) kwa masomo anayotaka kusoma na shule anayotarajia kujiunga nayo kwa kila chaguo.

Kuhusu wanafunzi waliokosa nafasi, Waziri Simbachawene alisema jumla ya wanafunzi 24,528 sawa na asilimia 27.2 ya wenye sifa wakiwemo wasichana 6,789 na wavulana 17,739 wamekosa nafasi ya kujiunga na kidato cha tano na vyuo vya ufundi kutokana na ufinyu wa nafasi za shule za kidato cha tano.

Alisema katika idadi hiyo kuna wanafunzi 348, wasichana 120 na wavulana 228 wana umri zaidi ya miaka 25 ambao wanakosa sifa za kuchaguliwa na wanafunzi 625, wasichana 323 na wavulana 302 wamekosa tahasusi. “Wanafunzi hawa watadahiliwa na Baraza la Taifa la Ufundi (NACTE) kwenye fani mbalimbali ambazo ni ualimu.

Afya, maendeleo ya jamii, kilimo, Aidha Tamisemi itafanya uchaguzi wa pili (second selection) mara tu baada ya muda waliopewa wanafunzi kuripoti shuleni kupita,” alisema.

Kuhusu wanafunzi kuripoti shuleni Waziri huyo alisema muhula wa kwanza kwa wanafunzi wa kidato cha tano mwaka 2016, utaanza Julai 11, mwaka huu kwa kuwa uchaguzi wa wanafunzi wa kujiunga na kidato cha tano umefanyika kwa kutumia mfumo wa kompyuta kwa kuzingatia machaguo ya wanafunzi ya tahasusi, ufaulu na nafasi zilizopo katika shule husika.

“Naagiza wanafunzi wote kuripoti kwa muda uliopangwa la sivyo nafasi zao zitachukuliwa na walikosa nafasi hizo,” alisema na kuongeza kuwa si kila anayepangiwa shule za serikali huripoti na ifikapo Julai 27, mwaka huu watapitia na kuangalia nafasi ngapi zimeachwa wazi ili wale walioachwa wapate nafasi.

Alitoa mwito kwa Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya, Wakurugenzi wa Halmashauri, Miji, Manispaa na Majiji kuhakikisha kwamba azma ya serikali ya kila tarafa kuwa na shule ya kidato cha tano inatekelezeka ili kuwawezesha wanafunzi wote waliofaulu kupata nafasi ya kuendelea na masomo ya kidato cha tano na sita.

“Kutokana na ongezeko la ufaulu wa masomo ya sayansi, ninahimiza shule zitakazoanzishwa za kidato cha tano ziwe na vyumba vitatu vya maabara za masomo ya sayansi ili kuongeza idadi ya wanafunzi wa tahasusi za sayansi ambao ufaulu wao unakuwa bora zaidi kila mwaka,” alisema na kuwahimiza pia wadau wa elimu kuhakikisha shule zote zinazoanzishwa kwa ajili ya kidato cha tano zinakuwa za bweni kwa kuwa shule hizo ni za kitaifa na zinatakiwa kupokea wanafunzi kutoka maeneo mbalimbali nchini.

Awali Simbachawene alisema Tamisemi ina jukumu la kusimamia, kuratibu na kufuatilia shughuli za elimu kwenye mamlaka za serikali za Mitaa kuanzia ngazi ya elimu ya awali, msingi na sekondari.

Alisema kuanzia mwaka 2014 uchaguzi wa wanafunzi wa kujiunga na kidato cha tano na vyuo vya ufundi ni moja ya majukumu yanayosimamiwa na Tamisemi baada ya kugatuliwa kutoka Wizara ya elimu sayansi na teknolojia. Simbachawene alisema kazi za Wizara ya Elimu ni kutunga sera ya elimu, mitaala, kusimamia ubora wa elimu kwa shule za serikali, mashirika ya dini na watu binafsi.
 
Back
Top Bottom