Yanga noma; Ambani aondoka na mpira wake

Pdidy

JF-Expert Member
Nov 22, 2007
50,956
22,148
Yanga yaifyeka Majimaji 3-0
• Ambani aondoka na mpira wake

na Makuburi Ally


amka2.gif
MABINGWA watetezi wa Ligi Kuu Tanzania Bara, Yanga, jana, ililipa kisasi kwa Majimaji ya Ruvuma baada ya kuifunga mabao 3-0 kwenye Uwanja wa Uhuru, jijini Dar es Salaam, hivyo kufikisha pointi 30.
Ni kisasi kwani katika mechi ya raundi ya kwanza ya ligi hiyo iliyoanza Agosti 23, zikicheza kwenye Uwanja wa Majimaji Songea Septemba 5, Yanga ilifunga bao 1-0.
Shujaa wa mechi ya jana ni mshambuliaji wa kimataifa wa Kenya, Boniface Ambani, aliyeifungia Yanga mabao yote matatu, hivyo kuondoka na mpira.
Ambani mfungaji bora wa msimu uliopita, alianza kuzifumania nyavu katika dakika ya 19 akipokea pasi safi kutoka kwa Jerry Tegete na kuukwamisha mpira wavuni. Dakika ya 35, Ambani tena nusura aifungie timu yake bao baada ya mabeki wa Majimaji kudhani alikuwa ameotea, lakini mpira ukatoka nje.
Dakika ya 42, kiungo Juma Mpola wa Majimaji ya Songea, alishindwa kufunga kwani licha ya kupata pasi nzuri kutoka kwa Ally Jazza, shuti lake lilikwenda nje ya lango la Yanga, hivyo hadi mapumziko, Yanga ilikuwa mbele kwa bao 1-0.
Kipindi cha pili, Yanga walirejea uwanjani kwa nguvu na dakika 46, Jerry Tegete alipata nafasi nzuri, lakini shuti lake likapaa juu ya lango la Majimaji baada ya kupokea pasi safi ya Ambani.
Dakika ya 64, Ambani alifunga bao la pili akiunganisha krosi safi ya kiungo Shamte Ally na kuukwamisha mpira wavuni.
Akionyesha kurejea katika kiwango chake cha upachikaji mabao, dakika ya 70, Ambani alifunga bao la tatu baada ya kupokea pasi ya Steven Bengo.
Baada ya kufunga bao hilo, Ambani alikwenda kwenye kibendera cha upande wa Kusini mwa uwanja na kuking’oa, hivyo kulimwa kadi ya njano na mwamuzi Martin Saanya.
Dakika ya 80, Wisdom Ndlovu alitolewa nje baada ya kulimwa kadi ya pili ya njano kwa kosa la kuunawa mpira kwa makusudi.
Baada ya mechi hiyo, Kocha wa Majimaji, David Mwamwaja, alikiri timu yake kufungwa kihalali na kulaumu viungo na washambuliaji wake.
Naye kocha wa Yanga, Kostadin Papic, alisema timu yake ilistahili kushinda kwa sababu ya maandalizi bora wanayoyafanya.
Yanga iliwakilishwa na Obren Curcovic, Shadrack Nsajigwa, Amir Maftah, Nadir Haroub Cannavaro, Wisdom Ndlovu, Athumani Idd, Shamte Ally/George Owino, Godfrey Bonny, Jerry Tegete/Idd Mbaga, Boniface Ambani na Kiggi Makasi/Steven Bengo.
Majimaji iliwakilishwa na Said Mohamed, Abdallah Ausi, James Mwakababu, Gerald Lukindo, Evarist Maganga, Lusio Almas, Kulwa Mobby/Omar Mnubi, Juma Mpola, Sixmund Mwakasege, Iddy Ajiro/Selemani Kibuta, Ally Jazza/Henry Morris.
Ligi hiyo itaendelea tena leo kwa vinara Simba kucheza na Toto Africa katika Uwanja wa CCM Kirumba, jijini Mwanza.
Simba inashuka dimbani ikiwa na rekodi ya kutofungwa katika mechi 13 zilizopita, hivyo kuongoza ligi ikiwa na pointi 39.
Kama Simba itashinda, itazidi kuboresha rekodi yake na kuzidi kuukaribia ubingwa kwani kabla ya mechi ya leo, imebakisha mechi tano tu kati ya tisa zilizosalia. Ligi hiyo itaendelea kwenye Uwanja wa Manungu, Morogoro, kwa Mtibwa Sugar kuikaribisha JKT Ruvu; African Lyon kukwaana na Prisons katika Uwanja wa Uhuru, jijini Dar es Salaam na Manyema Rangers kuifuata Kagera Sugar kwenye Uwanja wa Kaitaba, Bukoba.
 
Cha kushangaza siku ile hawakumpa mpira, refa aliondoka nao yeye, nikabatika kuongea na Mrisho Ngasa ambaye na yeye mechi zid ya Manyema alifunga goli tatu akasema hakupewa mpira sababu TFF wanasema hawana mipira ya kutoa
 
Back
Top Bottom