YALIYOSEMWA NA MSEMAJI WA SERIKALI, DKT. HASSAN ABBAS LEO JUMATANO JULAI 25, 2018
Mkutano huu ni mwendelezo wa mikutano ya kila mwezi kati ya Msemaji Mkuu wa Serikali na wanahabari kwa lengo la kutoa mrejesho kwa umma kuhusu utekelezaji wa ahadi za Serikali.
Nawapongeza na kuwashukuru wanahabari kwa ushirikiano mkubwa waliutoa kwa Serikali katika mwaka wa fedha 2017/2018 katika kusaidia kuhabarisha umma masuala mbalimbali ya utekelezaji wa shughuli za Serikali.
Kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari na. 12, 2016 vyombo vya habari vinapaswa, kutekeleza kazi zao kwa mujibu wa maadili ya kiwango cha juu.
Niwakumbushe wamiliki wa magazeti kuhuisha leseni zao mwaka huu kuanzia mwezi agosti.
Tunashuhudia kuwepo kwa vitendo vya ukiukwaji wa maadili ya taaluma kwani pale Serikali itakapochukua hatua tusilaumiane.
Hali ya Uchumi wa Taifa
Hadi kufika Machi 2017, Pato la Taifa lilikua kwa wastani wa asilimia 7.1 ikilinganishwa na ukuaji wa asilimia 7.0 kwa mwaka 2016.
Ukuaji huu ulitokana na utekelezaji wa miradi mikubwa ya maendeleo na kuimarika kwa shughuli mbalimbali za kiuchumi.
Makusanyo ya Kodi Yaongezeka
Katika Mwaka wa Fedha 2017/2018 Serikali kupitia TRA ilifanikisha kukusanya jumla ya Shilingi Trilioni 15.5 kuanzia Julai 2017 hadi Juni 2018 ikilinganishwa na Shilingi Trilioni 14.4 ambazo zilikusanywa katika kipindi kama hicho kwa mwaka wa Fedha 2016/2017, kiasi hiki ni sawa na ukuaji wa asilimia 7.5.
Kwa niaba ya Serikali niwapongeze watendaji wote waliosimamia hili na wananchi waliolipa kodi na tuendelee na mshikamano huu huu.
Ninyi kama Wanahabari, tunaomba mtumie kalamu zenu na kamera zenu kufichua wale wote wanaokwepa kodi na pia kutangaza mashujaa wa kulipa kodi nchini.
Makampuni Yaanza Kulipa Gawio na Mapato kwa Serikali
Kutokana na utendaji makini wa Rais Magufuli na Serikali ya Awamu ya Tano kwa ujumla hata mashirika ambayo yalikuwa hayatoi gawio kwa Serikali sasa yanatoa.
Zaidi ya TZS Bilioni 700 zimekusanywa kama gawio na mgawo wa asilimia 15 kutoka taasisi na mashirika ya umma na binafsi 43 na taarifa za sasa ni kuwa fedha hizo zitaongezeka hadi zaidi ya bilioni 800 ikiwa ni baada ya taasisi nyingine kuhamasika na hii ni ongezeko la asilimia zaidi ya 500.
Utekelezaji Katika Sekta Muhimu kwa Wananchi
Serikali imetimiza ndoto ya kuendelea kulifufua Shirika la Ndege kwa kuleta Boeing 787 Dreamliner, Ndege nyingine 2 za C Series zinakuja Novemba na Boeing nyingine 1 itawasili Januari 2020.
Tangu ujio wa ndege hizi abiria wa ATCL wameongezeka hadi kufikia 107,207 katika mwaka 2016/2017 kutoka 49,174 mwaka 2015/2016 hii ni sawa na ongezeko la asilimia 118.
Mwaka 2017, Serikali iliendelea kutekeleza miradi ya maji vijijini kupitia programu ya kuendeleza sekta ya maji kwa lengo la kuongeza kiwango cha upatikanaji wa maji vijijini.
Katika mwaka 2017 barabara kuu, barabara za mikoa na barabara za wilaya kwa kiwango za lami na changarawe zilikuwa na urefu wa kilometa 32,170 ikilinganishwa na kilometa 30,265 kwa mwaka 2016 sawa na ogezeko la asilimia 6.3.
Serikali pia iliunda wakala maalumu wa kusimamia barabara za vijijini na miji midogo TARURA ambapo wameshaanza kazi na inasogeza zaidi huduma vijijini.
Serikali inaendelea kukamilisha miradi mbalimbali ya umeme nchini, ambapo Kinyerezi 1- extension tayari mitambo imeanza kufungwa na kuzalisha megawati 185.
Mradi ujao ni mradi mkubwa wa kihistoria, Mradi wa Stiglers wa megawati 2,100 na utekelezaji wake utaanza mwaka huu wa fedha.
Serikali imeendelea kutekeleza agizo la kuhamia Dodoma ambapo takribani watumishi 6,400 wameshahamia.
Imeandaliwa na Idara ya Habari- MAELEZO