Yahusu umuhimu wa nidhamu kwa taifa.

Shayu

Platinum Member
May 24, 2011
608
1,653
Tabia za watu zina mchango mkubwa katika maendeleo ya taifa lolote lile. Ili tuendelee lazima tujenge nidhamu na tabia za watu wetu. Taifa lenye watu wasiokuwa na nidhamu haliwezi kuendelea. Huu ni ukweli ambao tunapaswa kufahamu. Ili tuendelee lazima tujenge tabia za watu wetu kwenye mkondo fulani wa mawazo na matendo na jambo hili linahitaji nidhamu.

Kitu cha kwanza kama tunataka kuendelea lazima tujenge nidhamu na raia na viongozi wanaotii sheria. Na Taifa kutunga sheria nzuri zitakazo tu guide vyema.

Kwanini taifa letu linashindwa katika mambo mengi ni kwasababu hatujawajenga watu wetu kuwa na nidhamu. Nidhamu huleta dira. Hakuna malengo yeyote ambayo tutajipangia kama taifa tukafanikiwa, kama taifa hili watu wake hawana nidhamu na kama hawatokuwa na malengo ya pamoja .

Hizi nguvu za kiakili na kimaadili ndizo zilizofanya mataifa yakue na kuendelea. Tunaangalia kuendelea kwa jamii yeyote ile kwa vitu wanavyotengeneza, na vitu hivi ndivyo vilivyowafanya wao wapige hatua na kufanya mapinduzi kutawala mataifa mengine.

Bila uwezo wa kugundua ambao uko ndani ya uwezo wa kila binadamu hakuna taifa ambalo litaweza kuendelea na pengine kutawala mataifa mengine.

Maendeleo ya kiakili ya watu hupimwa na vitu walivyogundua na uduni wa jamii nyingine hupimwa pia na maendeleo ya kiakili ya jamii husika kwa kuangalia nyenzo zao wanazozitumia katika maisha yao ya kila siku. Gunduzi hizi ndizo zinazopima maendeleo ya kiakili ya jamii husika.

Kwetu sisi bado tunatumia vitu vingi ambavyo chimbuko lake sio kwetu bali kutokana na maendeleo ya jamii nyingine za ulaya. Wao waliendelea wakagundua mambo mengi ambayo faida zake na sisi tunazipata kama magari, ndege, simu na mambo mengine mengi yanayofanya maisha haya ya kisasa na kurahisisha maisha yetu. Kwa gunduzi zao ni dhahiri waliendelea kiakili mapema zaidi yetu. Kitu kinachotofautisha jamii zilizoendelea na ambazo hazijaendelea ni gunduzi walizofanya na maarifa ambayo wanayo.

Maendeleo yote ya binadamu yametokana na gunduzi alizofanya kwahiyo tunapozungumzia maendeleo ya binadamu hatuwezi kuepuka kuongelea gunduzi alizofanya na ukuaji wa kiakili wa jamii husika.

Huu ugunduzi na uzalishaji mali ndio ulikuwa chimbuko la maendeleo na biashara katika jamii nyingi.

Jamii zilizozalisha zaidi zilifanya biashara na kupata faida. Waliuza bidhaa walizogundua na kujiongezea mitaji na mahitaji pia ya malighafi yaliongezeka, yaliyowafanya watoke kutoka katika nchi zao kwenda nchi nyingine kuyatafuta, pamoja pia na kutafuta masoko ya bidhaa zao. Kwahiyo pasipo gunduzi maendeleo ya binadamu yangeendelea kuwa duni.

Harakati za binadamu kutaka kutawala mazingira yake ndizo zilizomnyanyua na kumfanya kutoka katika hali ile ambayo yenye kufanana na wanyama na kumfanya kuwa kiumbe bora na aliyejuu ya viumbe wengine.

Mihangaiko hii ya kutaka kumnyanyua binadamu kuwa zaidi ya binadamu, kuwa na nguvu na mamlaka inayotaka kufanana na Muumba, ndio iliyowafanya watu wa magharibi wanyanyuke na kutawala mazingira yao. Binadamu hawezi kuwa na nguvu ile ile kama ya muumba wake, lakini anaweza kunyanyua nguvu zake za kiakili na kiroho na kutawala mazingira yake.

Nidhamu ndio inayofanya kujulikana nani kiongozi nani mfuasi. Bila nidhamu huwezi kuweka kundi pamoja na uongozi unakuwa mgumu. Ili dira iwepo kunahitajika utii. Na taifa haliwezi kuendelea pasipo utii. Kwanza viongozi lazima wawe na maono na nidhamu na raia kuwa na utii bila hivyo hatuwezi kuendelea..
 
5 Reactions
Reply
Back
Top Bottom