Yahusu makuzi ya watoto wetu na utaifa

Shayu

Platinum Member
May 24, 2011
608
1,653
Taifa linalofanya mzaha kwenye maisha ya kifamilia haliwezi kuendelea, kwakuwa huko ndipo watoto hukuzwa na mazao yake kuonekana baadae katika ngazi ya Taifa. Na hao huingia katika taasisi zetu, na katika uongozi wa taifa. Wengine huingia jeshini, polisi, ualimu na wengine madaktari na wengine kwenye vyama vyetu vya siasa hawa wote hutegemea makuzi yao.

Kwahiyo tusipoangalia kwa umakini malezi ya watoto wetu na kujenga maisha yetu ya kifamilia na kijamii kuwa bora tusahau kujenga taifa imara na bora. Kwasababu taifa huanza huko chini kwenye ngazi ya familia na mahusiano yao na jamii eg familia na familia kisha jamii.

Sio lengo langu kutaja tabia mbaya ambazo zina hatarisha taasisi ya familia na kuidhoofisha, nafikiri mnajua, kwasababu wengi wetu tunaishi katika familia. Na ningependa mnaonisoma mzitaje. Kuna uhusiano mkubwa sana kati ya amani ya nchi na order katika familia. Sehemu ya chini kabisa ya utawala katika nchi ni ngazi ya familia kama huko chini hakuko vizuri juu pia hakutokuwa vizuri.

Nataka kuonyesha umuhimu wa familia katika taifa, ili tuweke mkazo katika kujenga familia zetu, na katika malezi ya watoto wetu. Watoto wetu wakiwa na tabia mbaya baadae ya taifa hili itakuwa hatarini. Kwasababu hao ndio watakaoingia kwenye taasisi za nchi yetu, na kwenye uongozi wa taifa letu, na kulifanya taifa letu kama shamba linalokuza mimea bila kupaliliwa, ambalo magugu yameota humo kwa hakika hakuna tutakachovuna. Mavuno yetu hayatokuwa mengi.

Lakini hao pia ndio watakaokuwa wazazi wa baadae, watakaolea watoto wao bila misingi na maadili, kwakuwa na wao hawakujengwa katika misingi iliyobora na imara, matokeo yake pia watoto wao watakua sio bora pia.

Maadili ya nchi yatayumba na nchi itakosa dira. Lakini ukiangalia kwa ukaribu haya yote hutokana na malezi na makuzi duni katika ngazi ya familia. Mavuno yake huonekana katika jamii, na katika ngazi ya taifa.

Kwahiyo kama jamii tunapaswa kuwajibika kwa pamoja kama tunataka kujenga nchi iliyo bora na imara. Ujenzi wa taifa sio nguvu ya mtu mmoja bali ni uwajibikaji wa pamoja wa kila raia kutaka kuona nchi yake ikiendelea.

Ni dhahiri kwamba tumeyatupa maisha ya kijamii na kitaifa, ndio maana Taifa letu lina mvurugano. Tunafikiria zaidi kuhusu ubinafsi wetu kuliko ujenzi wa taifa letu pamoja na ushirikiano wetu. Tusipoelewana hatutaweza kujenga taifa hili. Tunapaswa kujenga umoja wetu. Our division will not help us to go forward.

Ni lazima tulinde maadili yetu ili taifa letu liendelee na watu wetu wawe na furaha.

Taifa huanza kujengwa katika familia, jamii, shuleni na katika taasisi za dini, kama tutashindwa kujenga tabia za watu wetu huko, kuwa bora na zenye manufaa kwa taifa, tusahau kuhusu amani na maendeleo ya taifa hili, na wala utii wa raia kwa sheria na kwa serikali. Kama wazazi wameshindwa kuwatala watoto wao kuwa watii na wenye nidhamu, serikali haiwezi kufanya kikubwa kwa kutumia nguvu ya jeshi.

Kazi ya kujenga taifa sio ya mtu mmoja inahitaji uwajibikaji wa pamoja katika familia na ndani ya jamii. Kwasababu utii unaanzia huko. Taifa huwa bora ikiwa watu wote ambao wameunda taifa, wakitimiza wajibu wao.

Kuna vitu ambavyo tunaviona ambavyo havitupi dira nzuri kwa mweleko wa taifa letu. Ni jambo la kimsingi sana kuvizungumzia. Kama tunataka kuliokoa taifa hili. Sio tu jinsi gani tunavyo watayarisha watu wetu kuingia kwenye uongozi wa nchi yetu, bali pia tunavyowajenga watu wetu kuwa raia bora, na kuwa walezi bora na wasimamizi wa familia zao.

Kizazi chetu kijacho kitategemea sana malezi tunayowapa vijana sasa. Majaliwa yetu yanategemea jinsi gani tunawalea vijana wetu sasa hivi. Ubora wa kizazi kijacho unategemea sana malezi yetu ya sasa. Kama tunataka taifa letu kuwa bora ni muhimu na ni lazima tuanze sasa kujenga kizazi chetu na kuangalia tabia za vijana wetu na malezi ya watoto wetu.

Kama sisi sio bora tusitegemee vizazi vyetu kuwa bora, kwasababu sisi ndio tunaowalea wao, watarithi tabia zetu na wao watakuwa kama sisi, kama hatutafanya mabadiliko sasa ya kitabia, mpaka hapo tutakapofanya mabadiliko ya kina kwenye mioyo yetu na fikra zetu, ndipo nuru kwa kizazi chetu kijacho itakapokuwepo.



Sent using Jamii Forums mobile app
 
Back
Top Bottom