Wizara ya mambo ya ndani kuna cancer

Msharika

JF-Expert Member
May 15, 2009
947
69
Trafiki Dar wachangiana sh 10,000,000 kwa siku
• Ni matokeo ya 'mabao' ya sh 3000 wanayopiga daladala, teksi

na Kulwa Karedia na Martin Malera


amka2.gif
RUSHWA ndogondogo za barabarani zimewanufaisha baadhi ya askari wa Usalama Barabarani, jijini Dar es Salaam (trafiki) ambao wanakusanya zaidi ya sh 10,000,000 kila siku kila mmoja, kutokana na mchezo wa kupokezana fedha (upatu) waliouanzisha hivi karibuni.
Askari zaidi ya 100 huchangishana Sh 100,000 za upatu huo kila siku, kila mmoja, Tanzania Daima limebaini.
Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili kwa zaidi ya mwezi mmoja, umeonyesha kuwa idadi ya wanaoshiriki upatu ni kati ya 150 na 180, na kwamba makusanyo hayo hutokana na “mabao” wanayopiga madereva wa magari ya daladala katika vituo vya barabara mbalimbali za jijini Dar es Salaam.
Baada ya kukusanya fedha hizo, kila askari huziwasilisha kwa trafiki mwenzao wa kike anayeishi Buguruni, ambaye jina lake limehifadhiwa kwa sasa, ambaye ndiye humkabidhi askari mwenye zamu ya kupokea fedha zake siku hiyo.
Vyanzo vikubwa vya mapato vya askari hao wa barabarani ni rushwa ndogo ndogo wanayokusanya kutoka kwa madereva na makondakta wa daladala, magari ya mizigo, teksi na magari binafsi yanayofanya makosa ya usalama barabarani.
Jiji la Dar es Salaam na vitongoji vyake lina zaidi ya daladala 6,000 zinazofanya kazi kila siku. Nusu ya magari hayo hulipishwa faini kinyemela kila siku kutoka kwa askari hao kwa kisingizio cha makosa mbalimbali.
Idadi hiyo haijumuishi teksi, ambazo idadi yake inakadiriwa kuwa nusu ya idadi ya daladala, huku magari ya mizigo na binafsi yakiwa hayana idadi kamili inayojulikana.
Makosa yanafanywa na madereva wa magari hayo na kusababisha yatoe ‘kitu kidogo’ kwa upande wa daladala ni pamoja na kukatisha njia, ubovu wa gari, kuendesha bila kuzingatia sheria za usalama, kutokuwa na leseni, lugha chafu kwa abiria na makosa mengine ya sheria za usalama barabarani.
Makosa hayo kama yangelipwa kwa faini iliyowekwa kwa mujibu wa sheria, yanapaswa kulipiwa kati ya sh 40,000 na 50,000; lakini askari hao hupokea wastani wa sh 3,000 kwa kila gari kila siku. Kwa sababu hiyo, kila askari anaweza kukusanya zaidi ya sh 200,000 kwa siku.
Kwa mujibu wa uchunguzi huo, uwezo huo wa kifedha, ndio unaofanya trafiki kuwa na ukwasi wa kupindukia.
Baadhi ya askari walioanza kazi hivi karibuni, huku wakilipwa mshahara kidogo sana, tayari wanamiliki magari, hasa daladala na teksi na wengine wana majumba ya kifahari ambayo hayaendani kabisa na malipo yao halali.
“Mi’ sioni kama hili ni jambo la ajabu maana kila ofisi, hata kina mama ntilie, nao wanacheza michezo ya kupokezana pesa, na kila kundi lina kiwango chake, sasa hapo kosa liko wapi? Au kwa sababu ni trafiki….?” aliuliza mmoja wa askari hao ambaye aliomba jina lake lihifadhiwe.
Askari huyo ambaye alikuwa mkali kuzungumzia suala hilo huku akimtahadharisha mwandishi wa habari hizi kwamba yasije yakamfika yaliyompata Mwandishi wa Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC 1), Jerry Murro, aliyeibua habari za rushwa ya trafiki na baadaye kunaswa na tuhuma za rushwa, alisema waandishi wa habari wamekuwa wakifuatilia mambo ya trafiki na kuacha sekta nyingine zilizokithiri kwa rushwa.
Mmoja madereva wa daladala aliliambia gazeti hili: “Gari ninaloendesha mimi, bosi wangu ni dada mmoja trafiki na ana muda mfupi tangu ahamie jijini Dar es Salaam, lakini hadi sasa anamiliki daladala mbili na teksi mbili, mambo yake supa.”
Akizungumzia suala hilo, Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani nchini, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP), Mohamed Mpinga, alisema ameshtushwa na taarifa hiyo na kuwa ofisi yake inaanza mara moja kufanya uchunguzi ili kubaini wahusika.
“Nimeshtushwa na taarifa hii, ninachoweza kukwambia ni kwamba nitaanza kushughulikia suala hili mapema tu, tumekuwa na matatizo makubwa ambayo tumedhamiria kupambana nayo ili siku ya siku jeshi letu liwe safi mbele ya jamii.
Nimepata kusikia taarifa kama hizi, hivi sasa nina wiki moja tu hapa ofisini tangu niteuliwe... lakini naomba kukuhakikishia kuwa baada ya mkutano wetu wa Dodoma, moja ya azimio kubwa tulilokubaliana ni kuhakikishia tunapambana na rushwa kwani hii ni aibu kubwa kwa jeshi letu,” alisema Kamanda Mpinga.
Alisema ili kuhakikisha vita hiyo inafanikiwa, jeshi hilo limeanza mkakati wa kufanya semina kwa kushirikiana na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) ili kutoa elimu kwa kila askari.
Alisema moja ya sababu ya kuwepo tatizo hilo, inawezekana ni kutokana na mfumo wa utendaji uliopo unaochangia kwa kiasi kikubwa mianya ya rushwa.
“Katika hili naweza kukubaliana nalo kabisa kwamba mfumo wa utendaji unaweza kuwa unachangia.... tunaona namna ya kufanya mabadiliko ndani ya jeshi. Lakini pia nawaomba wananchi watusaidia kutoa taarifa zaidi,” alisema Kamanda Mpinga. Hata hivyo, baadhi ya wadau wa usalama barabarani wanadai kwamba rushwa ya trafiki na polisi kwa ujumla inasababishwa na serikali ambayo haifanyi lolote kuwainua kutoka hali duni za maisha. Badala yake inawalipa mishahara isiyotosheleza mahitaji yao, huku ikiwapa majukumu ya kusimamia vyanzo vikubwa vya pesa.
 
Back
Top Bottom