Waziri wa Mkapa amshukia Kikwete ataka CCM imtose 2010

Kubwajinga

JF-Expert Member
Jan 23, 2008
2,194
297
Waziri wa Mkapa amshukia Kikwete ataka CCM imtose 2010

ATAKA CCM IMTOSE 2010 KAMA HAWEZI KUFANYA MAAMUZI MAZITO

Ramadhan Semtawa

WAZIRI wa zamani katika serikali ya awamu ya tatu, Matheo Qares ameshauri kuwa CCM isimsimamishe tena Rais Jakaya Kikwete kutetea wadhifa huo iwapo atashindwa kufanya maamuzi magumu ya kusafisha watu wachafu ndani ya chama hicho.

Wakati Qares akisema hayo, waziri mwingine katika serikali ya awamu ya pili, Mussa Nkangaa amesema CCM imepoteza hadhi yake ya kuwa chama cha wafanyakazi na wakulima na ndio maana inashindwa kuwashughulikia watuhumiwa katika kashfa za Richmond na Kagoda.

Wawili hao walikuwa wakichangia mada katika siku ya mwishoni ya kongamano la siku tatu la kumuenzi muasisi wa taifa la Tanzania, Mwalimu Julius Nyerere lililoandaliwa na Taasisi ya Mwalimu Nyerere na kufanyika jijini Dar es salaam.

"Ninayemzungumzia sasa kwamba achukue maamuzi magumu si mwingine, ni Rais wa Jamhuri ya Muungano," alisema Qares ambaye aliwahi kuwa mkuu wa mkoa wa Mbeya wakati akizungumzia kushuka kwa maadili ya uongozi nchini katika miaka ya kifo cha Nyerere.

"Anaweza kuchukua maamuzi magumu kwa kufumba macho na kuwashughulikia hao wanaosema hakujuana nao barabarani, kwa kupitisha wino mwekundu akawa rais mzuri tu. Lakini kama atashindwa, basi ashauriwe miaka yake mitano inamtosha.

"Chama kitafute mwanachama mwingine atakayekuwa na uwezo wa kufanya maamuzi magumu; kwanza huu utaratibu wa miaka kumi ni hisani yetu tu ndani ya CCM, naomba hili lizingatiwe."

Makombora hayo mazito ya Qares yalimfanya mwenyekiti wa kongamano hilo, Dk Salim Ahemd Salim kulazimika kutoa ufafanuzi mwishoni kuwa kazi ya kongamano hilo ni kukusanya maoni na kwamba mtu yeyote anaweza kutoa mawazo mbadala.

Qares, ambaye alionekana kujiandaa vema kurusha makombora hayo, alisema CCM sasa imechafuka kutokana na kushikwa na matajiri wachache wakubwa ambao ni wachafu na ambao hawajui historia ya chama hicho.

Kwa mujibu wa Qares, ambaye aliwahi kushika wizara nyeti ya Menejimenti na Utumishi wa Umma iliyokuwa chini ya Ofisi ya Rais, chama hicho kinavurugwa na watu hao ambao pia alisema wanavuruga nchi.

Alisema hoja ya msingi ni mwenyekiti wa CCM ambaye pia ni rais kujiandaa kufanya maamuzi magumu kwani hiyo itamuweka katika nafasi nzuri, lakini vinginevyo ashauriwe mwakani apumzike kwa kuwa miaka mitano aliyoongoza inamtosha.

"Siku moja niliwahi kumuuliza (katibu mkuu wa CCM, Yusuf) Makamba kwanini matajiri wachafu ndani ya chama wasing'oke, akanijibu sasa wewe unataka matajiri waende chama gani?" alimnukuu Makamba.

"Nilikaa kimya, baadaye nikafikiri sana, lakini sasa ni wakati wa maamuzi magumu."

Qares alisema kibaya zaidi ni kwamba baadhi ya matajiri hao waliovamia CCM ni wageni.

"Matajiri hao hawana wala hawajui hata historia ya CCM, wengine kwanza uraia wao una utata ni wageni."

Baada ya kumaliza kutoa mchango wake ulioufanya ukumbi kuzizima, Dk Salim, ambaye alionekana kumudu vema mkutano huo, alisema: "Ndiyo maana ya mkutano huu. Hapa tunapokea maoni ya watu mbalimbali, lakini si lazima yakubalike na wote, wengine wanaweza kupinga au kukubali."

Dk Salim alisema kongamano hilo lilikuwa la maana kwa ajili ya kujaribu kuzuia mianya ya kuivuruga nchi na kusisitiza umuhimu wa maadili ya uongozi.

Awali, waziri mwingine wa awamu ya pili, Musa Nkangaa aliituhumu CCM kuwa imepoteza hadhi yake na kujikuta ikikumbatia matajiri wachafu.

Kwa mujibu wa Nkangaa, CCM imekuwa si chama cha wakulima na wafanyakazi tena, bali kimebaki kuwa chama cha matajiri.

"Ndiyo maana imekuwa ikiweweseka kuwashughulikia watuhumiwa wa Richmond na Kagoda," alisema akimaanisha kashfa ya utoaji zabuni ya ufuaji umeme wa dharura kwa Richmond Development Company LLC na tuhuma za wizi wa mabilioni ya fedha kutoka BoT.

Nkangaa, ambaye aliwahi kuwa Waziri wa Maji na pia Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), alisema ni lazima wananchi watambue nafasi yao katika kufanya maamuzi katika nchi.

Kwa mujibu wa Nkangaa, Watanzania wanapaswa kujitambua kwa kuwa bila ya kufanya hivyo mambo yatazidi kuwa ya ovyo na kujikuta wakiendelea kuwa maskini katika nchi yao yenye utajiri.

Aliitaka Taasisi ya Mwalimu Nyerere, ambayo iliandaa kongamano hilo la siku tatu, iandae sifa za mtu kuwa kiongozi na kuweka bayana kwamba wala rushwa hawafai kuongoza nchi.

Katibu mkuu wa Jumuiya ya Kikristo (CCT), Peter Kikula alitoa tahadhari kwa vyama vya siasa kuacha kuingiza mambo ya Mahakama ya Kadhi na mpango wa Tanzania kujiunga katika Jumuiya ya Nchi za Kiislam (OIC), kwa kuwa masuala hayo yatavunja katiba ya nchi.

Kiongozi huyo alisema tayari halmashauri kuu ya jumuiya hiyo ilitoa mapendekezo yake na kuyawasilisha serikalini ili kuepusha vyama kutumia dini kujipatia kura hapo mwakani.

Naye Nape Nnauye alieleza wasiwasi wake kama mfumo uliopo wa mamlaka za uwajibishaji unaweza kutoa ufumbuzi wa kudumu wa matatizo ya msingi ya kimaadili katika uongozi, hasa wa umma.

Nape alihoji kuwa kama mkurugenzi mkuu wa Takukuru, Dk Edward Hoseah alipaswa kuwajibishwa na mamlaka ya juu, lakini hakuwajibishwa, nini kitafuata baada ya mamlaka hiyo kushindwa kumwajibisha.

"Ninachosisitiza ni kujaribu kuangalia mfumo wetu ukoje, kwa mfano mkurugenzi wa Takukuru alipaswa kuwajibishwa, lakini anapita mitaani na kutamba hajiuzulu... lakini anayepaswa kumwajibisha naye hamwajibishi, sasa hapo tunafanye?"

Naye Profesa Issa Shivji alionya kwamba maadili ya uongozi ni kitu muhimu ambacho kinapaswa kupewa kipaumbele na kusimamiwa vema.
 
Wamtose ASAP;

Sio tu kwa kushindwa kufanya maamuzi mazito, bali pia kwa kukosa mwelekeo na kutokujua majukumu yake.
 
Qares, ambaye alionekana kujiandaa vema kurusha makombora hayo, alisema CCM sasa imechafuka kutokana na kushikwa na matajiri wachache wakubwa ambao ni wachafu na ambao hawajui historia ya chama hicho.


Kwa mujibu wa Nkangaa, CCM imekuwa si chama cha wakulima na wafanyakazi tena, bali kimebaki kuwa chama cha matajiri.
Kazi kweli kweli
 
qaes kajitahidi,

wangapi wanweza kutamka hayo nani ya ccm. japo alifulia siku nyingi lakini angalau anaonyesha anaweza kubweka akiamua. nimemsoma na nkhangaa yule aliyepata kuwa waziri wa kwanza wa mkapa wa tamisemi.

lakini tujiulize. wote hawa wanajua bahati haiji mara mbili, walipopata madaraka hatukuona wakifanya hayo wanayoita maamuzi magumu (wasitake kutuaminisha kuwa maamuzi magumu hufanywa na rais tu), leo hawana madarak ndio wanaona haja ya hayo maamuzi magumu. tupokee mawazo na changamoto zao, tusikatae kwa kuwa wametoa wao lakini kwa wale walio madarakaniau watakaopatta madaraka, kumbukeni mtatutendea wannchi haki zaidi "mkikumbuka shuka kabla usiku haujaisha"

nawasilisha
 
Wamtose ASAP;

Sio tu kwa kushindwa kufanya maamuzi mazito, bali pia kwa kukosa mwelekeo na kutokujua majukumu yake.


Naona hao wote walipata nafasi ya kupunguza pressure zao. Kwani kitu gani kipya ambacho walikisema hapo? Kinachoniudhi ni hii tabia ya watu kukumbatia upuuzi eti kwa sababu wanataka kubaki ndani ya chama. Kama matajiri, wageni na watu wasio na maadili wamekiteka chama kwa nini waendelee kuking'ang'ania? Mbona Mwalimu mwenyewe alishasema kuwa CCM siyo mama wala baba yake? Hawa naona wanajitafutia maadui pasipo sababu. Kama hawana ubavu wa kuwashawishi wengine ndani ya chama kufanya maamuzi mazito ya kumtosha Rais asiye na dira basi wajiengue wenyewe! Nao wanaonekana wasanii kuendelea kulia lia tu bila kuchukua hatua.
 
Waziri wa Mkapa amshukia Kikwete ataka CCM imtose 2010


"Chama kitafute mwanachama mwingine atakayekuwa na uwezo wa kufanya maamuzi magumu; kwanza huu utaratibu wa miaka kumi ni hisani yetu tu ndani ya CCM, naomba hili lizingatiwe."

Alisema hoja ya msingi ni mwenyekiti wa CCM ambaye pia ni rais kujiandaa kufanya maamuzi magumu kwani hiyo itamuweka katika nafasi nzuri, lakini vinginevyo ashauriwe mwakani apumzike kwa kuwa miaka mitano aliyoongoza inamtosha.

"Nkangaa, ambaye aliwahi kuwa Waziri wa Maji na pia Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), alisema ni lazima wananchi watambue nafasi yao katika kufanya maamuzi katika nchi. "

"Kwa mujibu wa Nkangaa, Watanzania wanapaswa kujitambua kwa kuwa bila ya kufanya hivyo mambo yatazidi kuwa ya ovyo na kujikuta wakiendelea kuwa maskini katika nchi yao yenye utajiri. "

.

Huu ni wito wa mabadiliko, mabadiliko ndani ya chama na mabadiliko kwa watanzania wote mana sisi ndio wapiga kura.

Kelele, Kengele na baragumu zinapigwa kila kona lakini tutashangaa 2010 hiyooo.... yule yule ataukwaa.

Jamani nani ametuloga watanzania?

Yetu Macho
 
Hawa nao ni sehemu ya uchafu wanaouzungumziaaa...tena huenda ni WACHAFU zaidi ya hao matajiri, na wale wanaowahisi kutokuwa na uraia..

Hata Taasisi ya Mwalimu haina hadhi ya sifa za mwalimuuu...inawewesekaaaaa...
 
Safi sana tunahitaji whistleblowers kama hawa nchi iende mbele hakuna kumuonea haya mtu hapa Tanzania sisi ni vijana wa karne ya 21 tuna uchu wa maendeleo sio kila siku ukitoka nje ofisini unakutana na mtu anakuomba sh 200 aibu aisee!!!
 
Mzee wetu Kikwete nadhani he has to realise he is the boss and any action or decision kuna watu watafurahia wengine watalia so it is time maamuzi kama hayo yafanyike kwa faida ya taifa
 
Hawa nao ni sehemu ya uchafu wanaouzungumziaaa...tena huenda ni WACHAFU zaidi ya hao matajiri, na wale wanaowahisi kutokuwa na uraia..

Hata Taasisi ya Mwalimu haina hadhi ya sifa za mwalimuuu...inawewesekaaaaa...

Inawezekana

Ila hii haiwaondolei haki ya kukemea maovu yanayoendelea ktk utawala huu wa kidhalimu wa JK ambao hata kipofu anauna na hata Kiziwi anausikia.

Imetosha
 
"Chama kitafute mwanachama mwingine atakayekuwa na uwezo wa kufanya maamuzi magumu; kwanza huu utaratibu wa miaka kumi ni hisani yetu tu ndani ya CCM, naomba hili lizingatiwe."
Huu ni wito wa mabadiliko, mabadiliko ndani ya chama na mabadiliko kwa watanzania wote mana sisi ndio wapiga kura.

Nakubaliana na wewe kabisa, huu ni wito kwa CCM ku-revolt dhidi ya kilaza JK.
 
Qares leo anazunzumzia umuhimu wa kutoa maamuzi magumu, what a joke! Qares huyu huyu alikuwa anavunja press conference kwa sababu kamera za ITV hazipo!
 
Siku moja niliwahi kumuuliza (katibu mkuu wa CCM, Yusuf) Makamba kwanini matajiri wachafu ndani ya chama wasing'oke, akanijibu sasa wewe unataka matajiri waende chama gani?" alimnukuu Makamba.

"Nilikaa kimya, baadaye nikafikiri sana, lakini sasa ni wakati wa maamuzi magumu

Hii kali kabisa!
 
waliofulia nao bana...mhhh...haya mbona hawakutuambia nani anyechukua nafasi ya kikwete?

Mimi sadhani hapo kama kuna hoja ya wamefulia au anaesema hiyo kauli ni nani, cha muhimu ni kupima uzito wa hiyo kauli,

kama angeisema Zitto nadhani ndio ungejua kuwa ni kauli kuntu
 
Subirini hotuba ya Rais siku ya kusheherekea Uhuru wa TANGANYIKA ,mtayashuhudia mamuzi yake.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom