TANZIA Waziri wa Baraza la kwanza la Mawaziri, Balozi Job Lusinde afariki dunia

Rufiji dam

JF-Expert Member
Feb 20, 2020
3,803
8,794
Mzee muungwana na mwenye hekima amefariki katika hospital ya Muhimbili.

========

Lusinde.jpeg

1. Usuli:
Mh. JOB MALECELA LUSINDE, ambaye ni ndugu wa Mh. JOHN SAMWEL CIGWEYIMISI MALECELA, alizaliwa huko Kikuyu, Idodomia tarehe 10.9.1930, siku ya Ijumaa.

2. Masomo:
Mh. JOB alisoma shule ya msingi ya misheni hukohuko Idodomia. Baada ya kufaulu vizuri, alichaguliwa kujinga na shule ya sekondari ya "Alliance Sec. School". Shule hii ilikuja kubadilishwa jina na kuitwa "Mazengo Sec. School"(jina la Chifu maarufu wa Kigogo).

Mh. JOB baadae miaka ya mwisho ya 1940s, alifaulu mtihani wake na hivyo akaendelea na masomo "Tabora Boys Sec. School", shule iliyopika viongozi karibu wote wa mwanzo wa taifa hili. Shuleni hapo alisoma na watu maarufu mf. Mh. Sir G. KAHAMA na Mh. O. KAMBONA. Wakati huo, Mwalimu JK NYERERE alikuwa mwalimu wa "St. Marys Sec School" (Milambo Sec. School).

Mh. JOB, baada ya kumaliza "Boys school", alikwenda "Makerere university" alikosomea Ualimu toka mwaka 1950 hadi 1953, kisha akaanza kufundisha chuoni hapo.




3. Kujiunga na TANU:
Ingawa Mh. JOB alianza kupenda siasa tangu akiwa kijana wa miaka 15, lakini alijiunga rasmi na TANU mwezi Machi 1955 baada ya kurejea toka Makerere. Mwalimu NYERERE mwezi Machi 1955 ndipo pia alifanya uamuzi wa busara kuacha ualimu na kubakia kwenye siasa.

Mh. JOB pia akawa anafundisha na Mh. O. KAMBONA shule ya "Alliance" huku pia wakijikita na vuguvugu la uhuru. Mwaka 1960, baada ya uchaguzi mkuu, Mh. JOB alichaguliwa kuwemo kwenye "Legislative Council".

4. Uhuru wa Tanganyika:
Tarehe 9.12.1961, Tanganyika ilipata uhuru. Mh. JOB alikuwa mmoja wa mawaziri 11 wa kwanza wa Tanganyika. Mwalimu hakuwa mbaguzi wa rangi ndio maana Baraza hilo lilikuwa na Waafrika 8, Wazungu 2 na Mhindi 1.


Lusinde 2.jpeg

Siku hiyo ya uhuru ilipigwa picha ya Baraza hilo la Mawaziri. Katika picha hiyo, anakosekana Sir GEORGE KAHAMA aliyekuwa ametumwa kikazi "Zaire" na Mwalimu. Aliporejea nchini ikapigwa picha nyingine ya pili iliyomjumuisha lakini cha ajabu picha ile ya kwanza ndio imetamalaki nchini hadi leo huku ikielezwa ndio Baraza la Kwanza la Mawaziri!.

Katika Baraza hilo la Kwanza, Mh. JOB aliteuliwa kuwa Waziri wa kwanza wa Tawala za Mikoa na Serikali za mitaa.

5. Waziri Wizara Mbalimbali:
Mh. JOB amehudumu wizara tofauti: 1961-63(Local govt), 1963-65 (Home Affairs), 1965-67 (Communications, Labour & Works), 1967-70, (Communications, Transport and Labour, 1970-74(Communications &Works), 1974-75 (Works).


Lusinde 3.jpeg

6. Maasi ya 1964:
Usiku wa MANANI, tarehe 19.1.1964, wanajeshi wa 'Colito baracks'(ambayo baadaye ilibadilishwa na kuitwa Lugalo kuheshimu eneo ambalo "Mnyalukolo wa Ukweli" Chifu MKWAWA alilopigana na Wajerumani, waliasi na kuzua songombingo ya aina yake! Mh. JOB alikuwa Waziri wa Mambo ya Ndani wakati huo.

Usiku huo wa MANANI (manane sio Kiswahili sanifu), Mh. JOB aliamshwa na askari waliotumwa na aliyekuwa IGP, ELANGWA SHAIDI, na kuelezwa kuhusu maasi hayo. Wakitumia gari la askari hao, walielekea Ikulu lakini wakakuta wanajeshi wameishateka na wakamkataza kuingia. Akawasiliana na aliyekuwa DG-TISS, EMILIO CHARLES MZENA, ambaye alimueleza wamemficha Mwalimu JK NYERERE na KAWAWA, sehemu maalum bila kuitaja.

Mh. JOB akaenda wizarani kwake na akapanda ghorofani. Wakati wa kushuka akakutana na wanajeshi waliomwambia anyooshe mikono na wakaondoka nae akapelekwa karibu na Twiga hotel, Samora. Akawakuta mwanahabari wa Ikulu na watu wengine. Yeye na wenzake wakawa wamechuchumalishwa. Askari mmoja akamuuliza Mwalimu yuko wapi? Mh. JOB akajibu kuwa hajui kwani yeye alipotaka kuingia Ikulu alizuiliwa na wanajeshi. Askari huyo akasema kuwa wao hawataki kumuua Mwalimu kwani wanampenda bali wanataka 'Africanization" (Vyeo vya wazungu wapewe Waafrika).

Walikalishwa hapo hadi saa 12 asubuhi ambapo askari wa hapo walitaarifiwa na wenzao kuwa wameishamalizana hivyo warudi Colito ndipo wakaachiwa na Mh. JOB akaenda Ikulu. Huko, alimkuta Mama MARIA NYERERE na kisha akaenda kwa mama SOPHIA KAWAWA na kuwakuta ni wazima. Kisha akawapigia simu mawaziri wote kuwataarifu wasitoke majumbani ili kuokoa maisha yao.

Wanajeshi walikuwa wamemchukua Mh O. KAMBONA na kwenda nae huko Colito kumweleza madai yao. Pia walimweleza Mh. JOB kuwa wanamtaka Luteni ELINA KAVANA apandishwe cheo awe Brigedia. Luteni KAVANA alipotafutwa akakataa hicho cheo na walipotakakumfyatulia risasi akakubali. Askari waliingia mjini wakaanza kuleta fujo na kunywa bia za bure! Magomeni waliliteketeza duka la mwarabu na kuwaua wote waliokuwepo kasoro mtoto wa miaka 6 aliyenusurika!.

Ilipofika saa 12, KAVANA akatoa amri askari wote warudi kambini. Mh. JOB, Mh. KAMBONA na Mh. BHOKE MUNANKA walijitahidi sana kutuliza hali kwani hakukuwa na viongozi wengine wa serikali zaidi yao waliokuwa wakitoa maamuzi. Kisha wao na waasi wakaenda TBC na kisha airport kuweka mambo sawa ambapo waasi walielezea ni kwanini waliasi.

Mwalimu na KAWAWA walikuwa wametoroshwa usiku na mlinzi wa Mwalimu (PETRO BWIMBO) na kupelekwa Kigamboni. Mh. JOB, Mh. MUNANKA na Mh. KAMBONA mwanzoni hawakujua walipo viongozi hawa.

Baada ya hali kutulia, Mh. JOB na Mh. KAMBONA, wakiongozwa na MZENA waliwafuata viongozi hao Kigamboni saa 8 mchana kwenye nyumba walimojificha ya Bw. SULTAN KIZWEZWE (Huyu alikuja baadae kupewa baiskeli na serikali baada ya kukataa kujengewa nyumba kwakuwa alifanya hivyo kwa uzalendo tu). BWIMBO aliposkia wanagonga hodi akawaamuru wanyooshe mikono juu na wajitambulishe wao ni kina nani. Alipowatambua na kujiridhisha, ndipo alipowakaribisha. Walipoingia ndani waliwakuta viongozi hao wamechokekelea mbali! Wakawachukua viongozi hao na kuwasimulia kilichojiri jijini Dar es salaam na wakawarudisha Ikulu na Mwalimu akalihutubia taifa.

Mwalimu, baada ya hapo, akaitisha kikao cha Baraza la Mawaziri na kueleza kuwa "Hii ni siku ya aibu sana kwa taifa letu kwani askari wetu wametuvua nguo, wanajijia tu mjini wanaleta vurugu wanakuwa kama walevi tu, sasa tufanyeje?" Ikakubalika kuwaomba Waingereza ili kuzima maasi hayo. Waingereza walikubali na "usiku wa shughuli" ilibidi kumwondoa Mwalimu Ikulu na kumweka mahali salama Ikulu. Waingereza walipokuja walizima maasi hayo kwa urahisi"kama wanamsukuma mlevi"!.


Lusinde 1964.jpeg

7. Muungano wa 1964:
Mh. JOB alikuwa ni mmoja wa Mawaziri walioshiriki kikamilifu matayarisho ya Muungano na pia alishuhudia utiaji saini wa Hati za muungano, tarehe 22.4.1964 pamoja na wengine kama Mh. O. KAMBONA na Mh. KASSIM HANGA.

Mh. JOB akawa Waziri wa Kwanza wa Mambo ya Ndani wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

8. Kuteuliwa Balozi:
Tarehe 6.10.1975, Mh. JOB aliteuliwa na Rais JK NYERERE kuwa Balozi wa Tanzania nchini China.

Alihudumu huko hadi Septemba 1984 alipoteuliwa kuwa Balozi wa Tanzania nchini Kenya.

9. Uzalendo, Uadilifu na Uchapakazi Uliotukuka:
Mh. JOB, wakati wa utumishi wake, alikuwa ni mzalendo mkubwa kwa nchi yake, mchapakazi hodari na mwadilifu wa hali ya juu kama viongozi wengi wa wakati huo kwani Mwalimu hakuwa na mchezo na viongozi wasio waadilifu!.

Kuna mwaka kulikuwa na RC mmoja alikuwa amekengeuka maadili na kutumia madaraka yake vibaya. RC huyo alikuwa ametelekeza mke wake wa ndoa na kupora mke wa mtu na akawa akiiishi nae kama kimada kisha akamuoa kabisa!. Mwalimu alipotembelea mkoa huo akamuuliza RC huyo: "Mkeo hajambo?" RC akajibu kwa bashasha-"Wife hajambo kabisa Mwalimu, yu buheri wa afya, namshukuru Mungu".

Mwalimu aliporejea Dar es salaam "akamfyekelea mbali" RC huyo na kumwambia "Kiongozi gani wewe unapora wake za watu?". Mwalimu hakuwa na simile na Viongozi wenye kulewa madaraka. Mh. Rais JPM anapowatumbua viongozi mara moja "wanapochemsha" mjue anafuata nyayo za Baba wa Taifa!.

Mh. JOB aliwahi kufanya tukio kubwa la uadilifu na kupelekea kupongezwa sana na Mwalimu.

Kuna mwaka zabuni ilitangazwa na kisha Baraza la Mawaziri likawalimempatia Mfanyabiashara mmoja maarufu sana nchini zabuni hiyo baada ya kuwa na vigezo kuwashinda wenzake na kisha kumuagiza Mh. JOB amwandikie barua rasmi Mfanyabiashara huyo kibopa .

Kesho yake asubuhi, bila kujua kuwa yeye ndiye mshindi wa zabuni hiyo, Mfanyabiashara huyo alienda ofisini kwa Mh. JOB akiwa na "briefcase" iliyojaa mamilioni na akataka kumhonga huku akimwaga mbwembwe kuwa hizo ni _"kishika uchumba tu"_Mh. JOB aseme tu zingine awakewe wapi!!!.

Mh. JOB alimtimulia mbali na mara moja akamtaarifu Mwalimu kuhusu kitendo hicho cha kibaradhuri. Mwalimu alimpongeza sana Mh. JOB na kisha zabuni akapewa mtu mwingine. Mfanyabiashara huyo akawa na msongo mkubwa wa mawazo na akajifia miaka 3 baadae!.

10. Misala 2 Mikubwa iliyompata Mh. JOB Kipindi cha Mwalimu:

10.1 Msala wa 1:

Mh. JOB alipokuwa Waziri wa Ujenzi alibaini barabara iendayo Msasani, nyumbani kwa Mwalimu, haina lami. Kwa kutambua kuwa wageni wengi wa kimataifa walikuwa wakienda Msasani, akamwendea Mwalimu na kumuelezea kuwa watajenga lami na fedha zimeishatengwa. Mwalimu alitaharuki na kuwa mbogo na akasema 'Nonsense. Fedha hizo ni kodi ya wananchi hivyo zipelekwe kujenga mahospitali na mashule. Hiyo kodi si kwaajili ya kujenga lami nyumbani kwa Rais".

Mh. JOB, na wenzake, wakategea Mwalimu kaenda nje ya nchi kwa mwezi mmoja wakajenga lami 'fastafasta' kwa wiki mbili.

Siku Mwalimu aliporejea wakaenda kumpokea 'airport'. Walipokata kona ya kuingia Msasani na alipoiona lami, ghafla Mwalimu akauliza- "Nimepotea?. Hii lazma itakuwa ni kazi ya JOB tu".

Walipofika Msasani na kushuka tu, Mwalimu akamwita Mh. JOB huku akiwa "amechafuka" vibaya sana na kuhamaki kwelikweli. Akamuuliza ni kwanini amekiuka maagizo yake. Mh. JOB, huku akitweta balaa, alijitahidi kadri ya uwezo wake kumweleza Mwalimu nia njema ya kujenga lami hiyo. Mwalimu hakutaka kabisa kuskia hizo Hekaya za Abunuwasi na Hadithi za Esopo". Kwa hakika, 'hakuna rangi Mh. JOB aliacha kuiona" siku hiyo!. Mwalimu alikuwa amefura kwelikweli na mwishowe akasema "Siitaki tena hii nyumba". Na kweli, serikali ikabidi kuichukua ingawa baadae ikarudishwa kwa Mwalimu. Mwalimu hakuwa mtu wa Spoti-Spoti!!!.

10.2 Msala wa 2:
Mwalimu hakupenda kabisa mbwembwe na mikogo. Siku moja, Mh. JOB akiwa Waziri wa Mambo ya Ndani, kulikuwa na Kikao cha NEC, Ofisi ndogo ya Bunge, Karimjee Hall, Dar es salaam. Wakapanga "lunch" iwe sehemu ingine. Mwalimu akamwambia Mh. JOB kuwa hataki msururu wa magari bali anataka pikipiki moja, gari lake na la nyuma tu.

Msafara wake huo mfupi ulipotoka hapo ulipata dhoruba kali njiani. Wajumbe wa NEC waliporejea kutoka 'lunch', "walimgombania Mh. JOB kama mpira wa kona" wakimtaka ajiuzulu kwa kuhatarisha usalama wa Rais! Ilikuwa ni songombingo ya "kufa mtu"!.

Mh. JOB akafanikiwa kuwaelewesha wajumbe hao kuwa hayo yalikuwa ni maelekezo mahsusi ya Mwalimu mwenyewe. Wajumbe, walipomuelewa Mh. JOB, wakamgeukia Mwalimu na kumwambia ni lazma atenganishe kofia ya NYERERE na ya RAIS. Mwalimu alielewa na akakubaliana nao ingawa alisisitiza magari yasiwe mengi sana na kuwa kero kwa wananchi!.

11. Mh. JOB Kutunukiwa Tuzo:
Katika maadhimisho ya miaka 47 ya Muungano tarehe 26.4.2011, Mh. JOB alitunukiwa na Rais wa awamu ya 4, Mh. JM KIKWETE tuzo maalum- "The Order of Union First Class" kwa uzalendo na utumishi wake uliotukuka kwa Taifa lake.

11. Maisha yake:

Mh. JOB, ambaye alimuoa Bi. Sarah na kubarikiwa kupata watoto 5, aliishi Idodomia akiwa ni Waziri pekee wa Baraza la Kwanza la Mawaziri aliye hai mpaka anafariki dunia.


Lusinde.jpg

Kassim Majaliwa, akimjulia hali Mwenyekiti Mstaafu wa Baraza la Wazee Dodoma, Marehemu Balozi, Job Lusinde, nyumbani kwake, Uzunguni jijini Dodoma, May 19, 2020, ( Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
 
TANZIA

Aliyewahi kuwa Balozi na Waziri katika Serikali ya awamu ya kwanza Mzee Job Lusinde amefariki dunia jijini DSM alikokuwa amelazwa.

Mzee Job Lusinde aliwahi kushika nyadhifa mbalimbali zikiwemo Mkuu wa Mkoa , Mkuu wa Wilaya , na pia amewahi kuwa Mwenyekiti Mstaafu wa Wazee Mkoani Dodoma.

1.jpeg
 
Pole kwa wote walioguswa na msiba huo. Hivi ndiye baba wa Kibajaji au?
 
Pole kwa familia yake, lakini unfortunately hajaaacha mtoto, yaani lusinde huyu wa sasa ni hovyo kuliko Mlinga na msukuma.

Lakini pia mbali na mazuri yake atalaumiwa kwa kutoshauri serikali iliyopo madarakani namna ya kuongoza.
 
TANZIA

Aliyewahi kuwa Balozi na Waziri katika Serikali ya awamu ya kwanza Mzee Job Lusinde amefariki dunia jijini DSM alikokuwa amelazwa.

Mzee Job Lusinde aliwahi kushika nyadhifa mbalimbali zikiwemo Mkuu wa Mkoa , Mkuu wa Wilaya , na pia amewahi kuwa Mwenyekiti Mstaafu wa Wazee Mkoani Dodoma.

View attachment 1499779
Sawa. Ila kuna ukakasi hapo kwenye ukuu wa Mkoa na Wilaya.
 
Mwenzetu akipatwa na umauti huwa ni mazingatio kwa sisi ambao bado tupo hai.
R.I.P Mzee wetu mpendwa.
 
pole kwa familia yake, lakini unfortunately hajaaacha mtoto, yaani lusinde huyu wa sasa ni hovyo kuliko Mlinga na msukuma.

Lakini pia mbali na mazuri yake atalaumiwa kwa kutoshauri serikali iliyopo madarakani namna ya kuongoza.
Kibajaji si mtoto wa Job Lusinde. Not to my knowledge.

R.I.P Amb. Lusinde.

The Last of The Mohicans.
 
Back
Top Bottom