Analogia Malenga
JF-Expert Member
- Feb 24, 2012
- 5,001
- 9,866
- Hadi kufikia robo ya pili ya mwaka 2020, watumiaji wa intaneti walikuwa milioni 27.1 kutoka milioni 26.8 robo ya kwanza mwaka huu.
- Intaneti hiyo hutumiwa zaidi na simu za janja.
- Hiyo inaongeza idadi ya Watanzania wanaonufaika na fursa za mtandaoni.
Dar es Salaam. Huenda idadi ya Watanzania wanaonufaika na fursa za mtandaoni imeongezeka, baada ya takwimu mpya za mawasiliano kuonyesha kuwa idadi ya Watanzania wanaotumia intaneti imeongezeka hadi milioni 27.1 mwezi Juni mwaka huu.
Fursa zinazopatikana mtandaoni ni pamoja na biashara, ujuzi na maarifa yanayohitajika kuboresha maisha.
Ripoti ya takwimu mpya za robo ya pili ya mwaka 2020 za Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) zilizotolewa hivi karibuni, zinaonyesha watumiaji wa intaneti wameongezeka hadi kufikia milioni 27.1 mwezi Juni kutoka milioni 26.8 Machi mwaka huu.
Hilo ni sawa na ongezeko la watumiaji 268,057 katika kipindi cha miezi mitatu au sawa na asilimia 56.3 ya watumiaji wa simu za mkononi Tanzania ambao katika robo ya pili ya mwaka 2020 wamefikia milioni 48.2.
Hata hivyo, ripoti hiyo haijaweka wazi ni aina gani ya intaneti inayotumiwa zaidi na Watanzania kama ambavyo imekuwa ikifanyika miaka iliyopita, ambapo intaneti inayohamishika (mobile wireless) ambayo hutumika zaidi na simu za mkononi, tableti na kompyuta mpakato ndiyo imekuwa ikitumiwa zaidi na Watanzania.
Kwa takwimu za mwaka 2019, watumiaji wa intaneti inayohamishika ambayo hutumiwa zaidi na simu janja walikuwa asilimia 99.8 ya intaneti yote inayotumika nchini ambayo hujumuisha intaneti inayohamishika na isiyohamishika (wired internet).
Wakati ukiendelea kufurahia intaneti, kuna njia mbalimbali ambazo zinaweza kupunguza kiwango cha matumizi yasiyo ya lazima ya intaneti na kuokoa kiwango cha fedha. Yafuatayo yanaweza kusaidia jambo hilo hasa kipindi ambacho vyuma vimekaza.