Watanzania tunakatishana tamaa

Sumaku

Member
Feb 17, 2009
53
1
( Kutoka kwanzajamii.com)

Andrew Mushi
NITAMZUNGUMZIA Michael Jackson aliyefariki wiki jana ili kuweza kuona tunachoweza kujifunza kwake na kukitumia katika maisha yetu. Michael Jackson ni taasisi, tena taasisi ya Kimataifa, ndio maana ya kumjadili.
Tunamjadili ili kuweza kujifunza mbinu na mikakati aliyoitumia na kuweza kufikia kiwango cha juu na kuwa maarufu kupitiliza. Niweke wazi hapa kuwa sina nia ya kuangalia madhaifu yake. Mtu yeyote mwenye busara akiona kitu kizuri kwa mtu anakibeba na yale mabaya anamwachia. Ila wasio na busara hukimbilia kuzoa ‘uchafu’ na mazuri huishia kuwatia kinyaa.
Rafiki yangu na mwandishi wa kitabu cha ‘Seasons of Life’ , Timothy Kyara, anasema Michael Jackson hakufukia kipaji na vipawa vyake. Kitendo cha Michael Jackson kutambua kipaji chake cha uimbaji tangu akiwa mdogo na kuanza kukitumia ipasavyo, ndio kinaifanya dunia mzima leo hii itikisike kwa kifo chake.
Katika jamii yetu, na wewe unayesoma hii makala ukiwa mmoja wao, tuna vipaji vingi sana, ila tumefukia, na labda wewe umekifukia cha kwako, na hata kikiibuka kidogo unajaribu kuweka hata mawe juu yake ili kisifurukute.
Kama una kipaji hata kama umri umesogea jaribu kutafuta mbinu na mikakati ya kukitumia vizuri ili kionekane, kifaidishe wengine na kikutajirishe. Ninaposema kipaji au kipawa ninamaanisha chochote katika maisha na si mambo ya burudani na michezo tu. Yaweza ikawa masomo, kazi yako, biashara, uongozi, siasa, familia, urafiki, ujuzi fulani, na wewe ongezea ya kwako.
Kwa mazingira ya Tanzania, kukatishana tamaa ndio kwingi kuliko kutiana moyo. Mtu akifanya kitu kidogo tu tofauti na wenzake utasikia, ‘huyo anajishaua nini’ . Kama una tabia ya kukatisha watu tamaa acha. Ninakumbuka mwaka 2003 baba yangu alifariki dunia. Nikajisemea moyoni, watu wanahangaika kuwaenzi wanasiasa na watu wenye majina makubwa. Mie nitajitahidi kumuezi baba yangu kwa kujenga tabia ya kuwatia watu moyo. Na tangu hapo, nimejikuta muda mwingi sana natumia kuwatia watu moyo kuliko kuwakatisha tamaa.
Michael Jackson hakupoteza muda kusikiliza wanaompiga vita na kumkatisha tamaa. Mambo mabaya aliyojikuta anashughulika nayo ni pale alipopelekwa mahakamani. Akiwa huko mitaani au kwenye muziki hata siku moja hakupoteza muda kuwajibu maadui zake au hata vyombo vya habari.
Hii tabia hapo juu inanikumbusha kuwa Michael Jackson alikuwa siku zote aliangalia namna ya kutimiza lengo lake la kuimba , kupiga, na kucheza musiki kwa kiwango cha juu. Alikuwa ‘focused’ kama wasemavyo kwa Kiingereza.
Kupoteza muda kuwasikiliza na kujibizana na wanaotukatisha tamaa ndio dhambi kubwa tunafanya. Najua sio rahisi kuacha mara moja kusikiliza sauti za kukatisha tamaa, lakini ukidhamiria taratibu utajikuta unazoe kuziipuza. Na uzuri usipozisikiliza wanaokuambia huwezi au hutafanikiwa, ukiwapuuzia, baada ya muda wanapunguza makali na hata kupotea moja kwa moja.
Dr. Muidimi Ndosi anasema kikubwa kilichomsaidia Michael Jackson ni kuwa karibu na watu waliomsaidia akaweza kutumia kipaji chake kung;aa. Watu kama Cordy wakati akiwa mdogo na kundi la ndugu zake la Jackson 5, na baadaye kina Quincy Jones na Andrae Crouch aliyemsaidia kutoa album ya ‘man in the mirror” walimsaidia sana kulea kipaji chake.
Hilo la kujiweka karibu na watu watakaokusaidia na kukubeba ili ufikie ndoto na maono yako ndio kosa wengi tunafanya. Kuna watu wanaona sifa kufanya kila kitu wenyewe. Wanapenda sifa kama ‘yule bwana ni hatari kafanikiwa bila msaada wa mtu yeyote’, matokeo yake hawaendi popote.
Kwa mtu yeyote unayependa kufanikiwa jaribu kuainisha kwa umakini kabisa watu ambao ukiwa nano karibu utafaikiwa. Kuna rafiki yangu mmoja amefanya kitu kizuri labda na sie tunaweza kuiga. Yeye amechaguwa watu kama watatu wa kumlea ili akuwe katika biashara, wengine watatu wa kuwa nao karibu katika mambo ya imani/ibada. Halafu wengine watatu wa kumpika kisiasa maana anataka kuwa mwanasiasa safi. Na pia alipokuwa anasoma, maana ana shahada ya udakitari wa falsafa alijiweka karibu na watu wa kumjenga kielimu.
Kingine ambacho bado kwa Watanzania ni utata na tunatakiwa kukifanyia kazi ni hii ya kutumia kipawa na kipaji kutengeneza pesa. Michael Jackson aliamua kutumia kipaji chake kutengeneza pesa.
Sie tunaridhika kutumia vipaji vyetu kuburudisha tu. Na hapa najaribu kukumbuka baadhi ya waumini wa kikriso wanapowalaumu wanamuziki wakiristo kutumia muziki wa injili kujipatia kipato. Wengi wamewalaumu watu kama Rose Mhando. Ila wakati hajaanza kuvuma na kulea watoto wake watatu ilikuwa ni mgogoro, hakuna aliyesema kitu. Kila dakika tuangalie ni kwa namna gani tunaweza kugeuza kipaji, kipawa, utaalamu, na ujuzi wetu ukawa pesa.
Pia Michael Jackson alijishughulisha na kuondoa umasikni duniani. Unakumbuka ule wimbo wa ‘We Are The World’ alikusanya wanamuziki wenzake wakatengeneza mamilioni ya dola za kusaidia wenye njaa huko Ethiopia miaka ya 1980.
Sisi kinachotukera mara nyingi ni matatizo yetu. Umasikini unaotuzunguka ulioko katka jamii yetu. Hatuweki mkakati wowote wa kupambana nao. Tunatumia muda mwingi kuwalaumu wanasiasa kuwa ufisadi wao unoaleta umasikini. Ili ni kweli, ila baada ya hapo hatupigi hata hatua moja ya kuweka mikakati ya kuwadhibiti wasipate nafasi ya kukwapua pesa kama ya EPA ambayo inatosha kujenga hospital kila wilaya hapa nchini.
Tuuchukie umasikini , Micahel Jackson aliuchukia umasikini katika ngazi binafsi na ya jamii, tupambane nao mchana na usiku.Tututumie vipaji vyetu. Na tukiona mwenye kipaji, kama hajashtuka anacho tumshtue, anaweza akawa yeye ndio Michael Jackson wa Tanzania. Au si ajabu mtoto, binamu, au mjukuu wako au wewe ndio Michael Jackson wetu!
amushi1@yahoo.com
CHANZO: http://www.kwanzajamii.com
 
thread ni nzuri lakini kwa nini hukuweka aya, ikawa na mtiririko mzuri?
 
Inatia moyo kama tukiwa na mawazo positive hivi, kinachohitajika ni kuyaweka kwenye utekelezaji.
 
Jambo moja naamini Baadhi ya watu au familia itakuwa wamesoma katika mazishi ya jackson kama alivyotowa maoni mwanachama mmoja wa Jf ya kuwa sio muda mrefu tutashuhudia watu wakiwa mazikoni na suti nyeusi huku wakiwa na miwani nyeusi na clove nyeupe hilo lipo na kama halipo lipo njiani
 
Back
Top Bottom