Watanzania tumejifunza nini kutoka kwa Obama?

Jasusi

JF-Expert Member
May 5, 2006
11,551
5,434
Watawala mmemsikia Obama?
ban.maswali.jpg


Ansbert Ngurumo​

amka2.gif

KASI ya wananchi kuishutumu na kuituhumu Serikali ya Awamu ya Tatu iliyoongozwa na Rais Benjamin Mkapa, hasa mashambulizi yanayomlenga yeye moja kwa moja, imewapa fursa watawala wa sasa kupumua.
Walau wanajua kuwa sasa tumerudi kule walikoanzia, kule walikotaka tuelekeze nguvu zetu tangu mwaka 2006, kule tulikokataa kujielekeza kwa makusudi, maana naamini kuwa, kama tungemwandama Rais Mkapa vilivyo kuanzia mwaka 2006, yangeibuka mengi makubwa ya awamu ya tatu, ambayo yangeficha makubwa ya awamu ya nne.
Hii ingewasaidia wenzetu kupeta kwa muda na ingewafanya wananchi waone kwamba Rais Mkapa alivurunda na Rais Jakaya Kikwete anasawazisha.
Kisiasa udhaifu wa serikali ya Mkapa ulikuwa mtaji tosha kwa serikali ya Kikwete kama angekuwa makini na jasiri wa vitendo. Lakini hawakuwa na bahati hiyo.
Miaka mitatu ya kuichokonoa serikali ya Kikwete imewafanya baadhi ya wananchi sasa waanze kusema kuwa licha ya makosa ya Mkapa na mawaziri wake, licha ya ubabe na hata matumizi mabaya ya madaraka anayotuhumiwa kufanya, serikali yake ilikuwa makini, ilichapa kazi na ilikuwa na nidhamu.
Tutatofautiana katika kujadili umakini, uchapa kazi na nidhamu hiyo, lakini ulinganifu unaofanywa unatokana na udhaifu mkubwa wa kimaamuzi na kiutendaji ulioonekana katika miaka mitatu ya awamu ya nne na unaonyesha tofauti ya wazi ya uwezo wa kiuongozi katika awamu mbili hizi.
Ndiyo maana wapo watu wanaojitokeza kumtetea Rais Mkapa sasa, si kwa kukubali makosa yake, bali kwa hoja (ambazo mimi nimeziita dhaifu) kuwa serikali yake ilifanya makubwa na mazuri mengi (ingawa wanajua kuwa haikuwa hisani bali wajibu).
Wengine wanamtetea wakidhani kwamba haya yanayotokea sasa dhidi ya Rais Mkapa ni mkakati wa makusudi wa watawala wa sasa ili wapate upenyo lakini wao si wema wala waadilifu zaidi.
Miaka mitatu tu imeonyesha kasi mpya waliyokuwa nayo katika kujisimika kwenye ulaji na kulinda masilahi yao na wapambe wao. Bahati mbaya upepo umewageuka.
Kama si Watanzania kushtuka na kuanza kuwarushia mawe mapema, hawa wangekuwa hawasemeki wala hawashikiki.
Kwa kujua mbinu ya awali ya watawala wa sasa, watetezi wa Rais Mkapa wanadhani kwamba mtu wao anaandamwa na watetezi wa serikali hii.
Kuna ukweli kidogo katika hoja hii, lakini msukumo wa sasa wa tuhuma dhidi ya Rais Mkapa umeshavuka mbinu za watawala wa sasa, ni jitihada za wananchi kuirejesha serikali katika misingi tuliyopewa na waasisi wa taifa hili kuhusu dhamana ya uongozi na utumishi wa umma, na kwa baadhi yetu, kauli zetu na maandishi yetu ni msaada na ushauri tunaompatia Rais Jakaya Kikwete ili asijitumbukize katika ulevi wa madaraka, na ulinzi wa masilahi binafsi na ya wapambe wake.
Ni onyo kwake kwamba miaka mitano au 10 ikulu si mingi sana. Aongoze au atawale nchi akijua kuwa muda wake unakaribia kwisha na akiutumia vibaya, historia ya utumishi wake itamwandama hadi popote atakapokuwa kama mstaafu.
Naamini hadi sasa amegundua kuwa Watanzania wamebadilika, na mtu pekee wa kuwarudisha nyuma ni yule atakayerudi kwenye misingi.
Jambo moja lisilomfurahisha ni kwamba wananchi wametambua hulka yake ya kweli, uwezo na udhaifu wake mapema kuliko alivyotarajia katika miaka mitatu iliyopita, wananchi wamepata fursa ya kutafsiri kwa vitendo maana halisi ya kauli mbiu ya ari mpya, nguvu mpya na kasi mpya ambayo siku hizi imefichwa kabatini.
Wameunganisha unasaba wa kimasilahi na kimadaraka kati ya vigogo wa sasa na wa awamu zilizopita. Wamebaki watu wachache ambao bado wanaamini kwamba Serikali ya Awamu ya Nne ina tofauti yoyote ya kimsingi na iliyopita.
Labda wanatazama sura, majina na vyeo vya watu. Lakini sisi tunaotazama katiba, sera na sheria tunaona kwamba awamu ya nne ni kizazi kile kile cha nyoka yule yule aliyetung’ata miaka kadhaa iliyopita, tofauti ni kwamba huyu kajivua ngozi, imeota nyingine.
Na nilipokuwa natafakari tukio kubwa la kisiasa wiki hii nilijikuta natazama mafunzo kadhaa yaliyotolewa na Rais Barack Obama wa Marekani kwa dunia nzima, hasa kwa wanasiasa wenzake katika siku chache zilizopita. Nitajadili machache yenye uhusiano na maisha yetu ya kisiasa.
Hata Wamarekani wenyewe wanakiri kwamba miaka miwili iliyopita, haikufikiriwa kwamba umefika wakati wa taifa hilo kumchagua rais mweusi.
Dhana hii ya kipuuzi iliendelea hata wakati wa kampeni lakini uwezo binafsi wa Obama na mikakati makini ya timu yake ya kampeni, viliweza kushinda ugonjwa huu wa ubaguzi.
Leo hii, ingawa ubaguzi haujaisha, Wamarekani wamebadilika kiasi na dunia imepata fundisho.
Watawala wetu bado wanatulazimisha kuendeleza kasumba ya ‘wakati haujafika’ kuwa na rais mwanamke; ‘wakati haujafika’ kuwa na mgombe binafsi; ‘wakati haujafika’ CCM kuondolewa madarakani, eti kwa sababu wengine hawana uzoefu huku wengine wanaleta hoja za kikabila na kidini.
Obama ametufundisha kwamba tulilofikiria haliwezekani jana, linawezekana leo iwapo wananchi watalitaka.
Kikwazo cha Obama hakikuwa rangi tu, bali hata umri na uzoefu wake katika masuala ya uongozi kitaifa. Anapolinganishwa na wagombea wote waliokuwa wanawania urais kutoka vyama vyote, Obama ndiye alikuwa kijana zaidi na mwenye uzoefu mdogo zaidi wa siasa za wakubwa serikalini.
Hoja hizi zilirudiwarudiwa sana wakati wa kampeni, lakini alizishinda kwa hoja. Wamarekani hawakusikiliza hoja za kipropaganda za wapinzani wa Obama.
Na kwa kuwa yeye hakuogopa midahalo na alikuwa tayari kujadili lolote hata pale alipodhihakiwa, wananchi walichunguza mantiki ya hoja zake, wakapima dhamira yake, wakagundua uwezo wake, na wakatazama mahitaji mapya ya wakati huu wakaamini kwamba anafaa.
Funzo la tatu ni jinsi alivyoingia ofisini na kuanza kutekeleza ahadi zake siku ya kwanza. Na ameanza na baadhi ya masuala magumu ya kisera, ambayo wapinzani wake waliwahi kusema kwamba hayawezekani, bali ni kauli za kutafutia kura.
Kabla hajakaa ofisini na kulewa madaraka, ameamua kuchukua hatua kurekebisha mambo kadhaa ya kisera ndani na nje.
Tutampima baadaye kama ameweza au ameshindwa, lakini ameonyesha kwamba heshima ya mwanasiasa itatokana zaidi na ujasiri wa vitendo kuliko kauli na ahadi tupu na kwamba baadhi ya hatua inabidi zichukuliwe mapema.
Obama haombi Wamarekani ‘wampe muda.’ Ameshapewa muda na ameanza kazi. Anafanya kile anachokiamini, alichowaambia wananchi wakati anaomba kura.
Hatuhitaji kuwasimanga viongozi wetu kwa kumtumia kiongozi wa taifa jingine. Lakini tunaamini nao wameona na wamejifunza, hata kama wamechelewa. Kiongozi anapoomba ridhaa ya watu, akawaahidi kutekeleza jambo fulani, wanapomuamini na kumchagua halafu akashindwa kulitekeleza, au akaliahirisha bila maelezo ya kina, anakuwa amewasaliti.
Sote tunajua kinachowatafuna watawala wetu sasa. Walituahidi kutekeleza mambo mengi kwa kasi ambayo hawakuwa nayo. Tazama masuala yanayowasumbua leo. Ni ya kisera. Wameendelea kusimamia sera za zamani, wameshindwa kuandaa misingi mipya ya kutatua matatizo yanayotusumbua katika mfumo wa elimu, afya, muungano, masuala ya uongozi na utumishi, mawasiliano na mengine.
Wamebaki kujivunia utekelezaji wa ‘miradi’ya serikali kama ujenzi wa barabara, uchimbaji wa visima na ujenzi wa madarasa kwenye sekondari za kata.
Kwa mtazamo wangu, mabadiliko makubwa katika nchi hayawezi kutokea bila mabadiliko ya kisera na kikatiba. Hapa ndipo watawala walipaswa kujikita tangu siku ya kwanza.
Najua wapo wanaodhani kwamba miaka hii mitano itatumika kujifunza, na kwamba kama watapata tena miaka mitano ijayo ndiyo miaka ya kazi.
Hii ni kejeli kwa watawala waliojinadi kwa uzoefu (wana zaidi ya miaka 30 serikalini) na waliojiandaa kwa zaidi ya miaka 10. Ndiyo maana nasema kwamba Rais Obama ametoa funzo, kwamba wakati mwingine uzoefu tunaozungumzia si wa manufaa, bali ni uzoefu wa kukaa na kuongoza katika mifumo ya kifisadi. Haupaswi kupewa nafasi.
Lakini Rais Obama ametukumbusha jambo la ziada katika siku yake ya kwanza ofisini kwa kauli na vitendo. Amesisitiza kurejea katika misingi ya uwazi, ukweli na uwajibikaji katika utumishi wa umma ili wananchi waweze kuiamini tena serikali. Siku ya kwanza kabisa, aliwaambia watumishi wa umma wanaofanya kazi ikulu kwamba utumishi wa umma si fursa ya kujinufaisha binafsi au kuwanufaisha rafiki zetu na wapambe wetu na wala si fursa ya kutukuza itikadi za kisiasa.
Amewakumbusha kwamba utumishi wa umma ni dhamana na fursa adhimu kwa ajili ya kulinda na kutetea masilahi ya wananchi wote.
Hakuhitaji siku mbili au nne za kuwapeleka kwenye hoteli za kifahari kuwafunda katika suala wanalolijua vema, bali aliweka wazi msimamo na mwelekeo wa utawala wake, na kwamba ni jukumu lao wote kuifanya serikali iaminike mbele ya macho ya umma kwa kuondoa usiri usio wa lazima.
Watanzania si wageni wa kauli za namna hii. Ndivyo tulivyolelewa wakati wa kujenga misingi ya taifa, lakini ufisadi umetafuna tunu hizi taratibu hadi zimetoweka kadiri miaka illivyopita na viongozi kubadilika badilika.
Kama watawala wetu wangeendelea kusimamia misingi hii, sina shaka baadhi ya tuhuma zinazowakumba vigogo leo zisingekuwapo na kama zingekuwapo zisingekuwa nyingi hivi na zisingekuwa za viwango vikubwa kiasi hiki.
Wala tusingekuwa na jamii ya watu wachache ambao wanaona fahari katika kutetea ufisadi wa watawala, kwa kigezo kuwa yapo mazuri machache waliyotenda. Lakini tumefika hapa tulipo kwa sababu, kama nilivyowahi kusema kuwa tumekosa uongozi makini.
Najua kauli hii haiwapendezi walio madarakani kwa sababu wao wanajiona makini, kwa sababu wanasahau au hawajui kwamba viwango vya utambuzi na uelewa wa Watanzania vimepanda na vimekuzwa na udhaifu wa watawala ambao wana akili kama ya Rais mstaafu wa Marekani George W. Bush.
Mnamo Mei mwaka jana, rais huyo mstaafu aliwaambia waandishi wa Kiisraeli, jijini Washington, kwamba: “Nitakuwa nimeshasahaulika kabisa kabla mtu yeyote makini hajagundua kilichotokea katika ikulu hii.’’
Anajua alichokuwa anamaanisha. Ndivyo watawala wetu wanavyoendesha nchi zetu; ndivyo wanavyotufikiria. Ndivyo wanavyochukulia nafasi walizonazo. Na ndiyo maana wanaendekeza ulaji na kulindana.
Wanaamini kwamba kwa muda mrefu ujao, ni wao tu na watoto wao watakaokuwa wanashikilia nafasi za juu za uongozi wa nchi na kwamba kwa yoyote yatakayoharibika sasa, watalindana hadi hapo atakapotokea kiongozi makini wa kugundua uchafu uliotendeka ikulu, wakati huo wao walishatoweka kabisa.
Bahati mbaya kwao, tumeanza kugundua uchafu huo hata kabla hawajatoka ikulu, na wengine kabla hawajatoweka kabisa. Ndiyo maana tunapiga kelele. Tunataka kurudi kwenye misingi.
 
Tumejifunza kuwa

Rais aliyeko madarakani ni mmoja tu, anapaswa kupewa ushirikiano ili atimize kazi zake.

Serikali iliyoko madarakani ni moja tu, kwahiyo inabidi ipewe ushirikiano wa kuweza kutimiza kazi zake.

Somo kubwa sana!
 
Jasusi,

....I wish tungejifunza..............hii mibichwa yetu sijui imejaa nini wallah
 
Kwa maoni yangu, pamoja na tathmini nzuri iliyotolewa na Jasusi hapo juu, nadhani ushindi wa Obama umetufanya tuelewe zaidi wapi ambapo tunakosea na kuendelea kuwa nyuma katika kila nyanja. Ukiacha uwezo/umahiri wa Obama, inaelekea taratibu zetu na hasa Katiba yetu haiwezi kutusaidia kufikia malengo yoyote ya maana.

Ukweli ni kwamba, Katiba yetu imeundwa na wachache (Bungeni) kwa kisingizio cha kutuwakilisha tulio wengi. Ila pia, Katiba hiyo hiyo inaacha mianya mingi kwa Serikali kuamua kufanya mambo inavyotaka. Katiba inatoa nguvu nyingi sana kwa Rais, Bunge na Tume ya Uchaguzi tu. Sina nia ya kusema sana kuhusu hili, kwa kuwa sio kusudio la thread hii.

Mafunzo tunayopata kutoka kwa Obama na hasa ushindi wake ni kuwa;
1. Kila kitu kinawezekana, endapo itakuwepo nia thabiti ya kukifanikisha
2. Nchi ili iendelee, ni lazima kila mwananchi ashirikishwe kuijenga na kuithamini nchi yake kwa vitendo na ustadi mkubwa
3. Taifa huru na lenye ufanisi litatokana na juhudi ya kazi, elimu nzuri, afya bora na mafunzo yatokanayo na historia ya nchi hiyo (na hasa marekebisho ya makosa yaliyotendeka)
4. Maslahi ya Taifa ndio sababu ya kuwa na serikali. Serikali inatakiwa kujali na kuthamini maisha ya binadamu kuyatunza na kuyalinda kwa nguvu zake zote
5. Kila serikali/kiongozi ana mwisho wake, na mwisho wake ndio nafasi muhimu ya mwanzo mpya
6. Linalowezekana leo, lisingoje kesho. Unachofanya leo ndio mafanikio yako ya kesho. Nafasi yoyote ya kiongozi au mtumishi wa umma kurekebisha au kusababisha maisha bora kwa wananchi wake ndio nafasi ya pekee aliyonayo. Nafasi hiyo ikipotea, ni wazi kuwa nafasi nyingine yoyote itakayokuwepo/tokea ni ya marekebisho mapya tu na itakuwa imechelewa.
7. Ustawi wa nchi yoyote utatokana na jitihada za wananchi wake tu, wengine wote wanaweza kuchangia kwa kiasi fulani.
 
Kwa maoni yangu, pamoja na tathmini nzuri iliyotolewa na Jasusi hapo juu, nadhani ushindi wa Obama umetufanya tuelewe zaidi wapi ambapo tunakosea na kuendelea kuwa nyuma katika kila nyanja. Ukiacha uwezo/umahiri wa Obama, inaelekea taratibu zetu na hasa Katiba yetu haiwezi kutusaidia kufikia malengo yoyote ya maana.

Ukweli ni kwamba, Katiba yetu imeundwa na wachache (Bungeni) kwa kisingizio cha kutuwakilisha tulio wengi. Ila pia, Katiba hiyo hiyo inaacha mianya mingi kwa Serikali kuamua kufanya mambo inavyotaka. Katiba inatoa nguvu nyingi sana kwa Rais, Bunge na Tume ya Uchaguzi tu. Sina nia ya kusema sana kuhusu hili, kwa kuwa sio kusudio la thread hii.

Mafunzo tunayopata kutoka kwa Obama na hasa ushindi wake ni kuwa;
1. Kila kitu kinawezekana, endapo itakuwepo nia thabiti ya kukifanikisha
2. Nchi ili iendelee, ni lazima kila mwananchi ashirikishwe kuijenga na kuithamini nchi yake kwa vitendo na ustadi mkubwa
3. Taifa huru na lenye ufanisi litatokana na juhudi ya kazi, elimu nzuri, afya bora na mafunzo yatokanayo na historia ya nchi hiyo (na hasa marekebisho ya makosa yaliyotendeka)
4. Maslahi ya Taifa ndio sababu ya kuwa na serikali. Serikali inatakiwa kujali na kuthamini maisha ya binadamu kuyatunza na kuyalinda kwa nguvu zake zote
5. Kila serikali/kiongozi ana mwisho wake, na mwisho wake ndio nafasi muhimu ya mwanzo mpya
6. Linalowezekana leo, lisingoje kesho. Unachofanya leo ndio mafanikio yako ya kesho. Nafasi yoyote ya kiongozi au mtumishi wa umma kurekebisha au kusababisha maisha bora kwa wananchi wake ndio nafasi ya pekee aliyonayo. Nafasi hiyo ikipotea, ni wazi kuwa nafasi nyingine yoyote itakayokuwepo/tokea ni ya marekebisho mapya tu na itakuwa imechelewa.
7. Ustawi wa nchi yoyote utatokana na jitihada za wananchi wake tu, wengine wote wanaweza kuchangia kwa kiasi fulani.




Naunga mkono maoni yako asilimia kubwa,ila mimi kwa kuongeza tu kuhusu suala la umoja,wenzetu Marekani rais akichaguliwa anakuwa rais wa wamarekani wote,hakuna tena harufu ya kusema wapinzani kwenye hotuba za rais wao zaidi ya kuwapongeza. Kwetu sisi rais awe kwenye ziara ya kiserikali hasiwe yeye kazi kuwasema wapinzani "ooh wanabeza maendeleo" ndio lugha za marais wetu. Jambo lingine ni suala la ushabiki wa chama kwenye mambo ya kitaifa wenzetu hayo mambo hayapo ndio maana tuliona bendera nyingi za taifa la marekani siku ya kuapishwa rais wao,kwetu sisi zingezagaa bendera za CCM na Mashati ya kijani kofia,T shirt za Njano,kijani NK. wakati mwingine rais au Waziri mkuu anapokuwa ziarani mikutano yao inapambwa na rangi za kijani,Njano( Nembo za chama)huu ni ushaidi kuwa bado hatujajenga umoja thabiti kwenye masuala la kitaifa,bado tuna weka mbele ushabiki wa vyama hata kama ushindani haupo (kampeni za uchaguzi),nimechangia eneo hili ambalo linaweza kuonekana dogo lakini linamchango mkubwa sana katik maendeleo ya nchi,ndio maana tumekuwa tukisikia kauli za viongozi za kuwalaani wapinzania wanaodaiwa kuchochea wananchi wasishiriki shughuli za maendeleo,sababu ni hizo hizo ambazo nimezitaja hapo juu, huwezi kuwahamasisha watu wafanye shughuli za maendeleo huku unashabikia chama kwenye mambo ya kitaifa ni upumbavu,kwani wewe ni kiongozi wa wote unapokuwa kwenye shughuli za chama fanya za chama unapokuwa katika shughuli za kitaifa unapaswa kutofautisha ingawa unaweza kuelezea mafaniko ya sera za chama katika nanma ya kuhamasisha maendeleo na si kwa lengo la kukejeri wapinzani kama ambavyo tumekuwa tukishuhudia kwetu.Kwa hiyo mimi nasifu umoja wa wamerekani kwani ni changamoto kubwa kwa mataifa yetu haya ya kiafrika,kwao upinzani unakwisha mara anapochaguliwa rais mpya na wanabaki wamoja,kwetu sisi upinzani,CCM uendendelea na kampeni miaka yote mitano mpaka uchaguzi mwingine unapowaidia,je unatarajia maendeleo kweili?
 
Somo jingine muhimu tunalopaswa kuzingatia kutokana na ushindi wa Obama ni kwamba experience isitumiwe kama kigezo cha kuwanyima wapinzani nafasi ya kuongoza. CCM imekuwa inatumia kigezo hicho na kuwafanya wapinzani kama watu watakaoleta mtafaruku ili kuendelea kutawala ilhali walishapoteza dira siku nyingi. Obama ametuonyesha kuwa inawezekana, kama alivyosema Mwalimu enzi zile, it can be done.
 
Naunga mkono maoni yako asilimia kubwa,ila mimi kwa kuongeza tu kuhusu suala la umoja,wenzetu Marekani rais akichaguliwa anakuwa rais wa wamarekani wote,hakuna tena harufu ya kusema wapinzani kwenye hotuba za rais wao zaidi ya kuwapongeza. Kwetu sisi rais awe kwenye ziara ya kiserikali hasiwe yeye kazi kuwasema wapinzani "ooh wanabeza maendeleo" ndio lugha za marais wetu. Jambo lingine ni suala la ushabiki wa chama kwenye mambo ya kitaifa wenzetu hayo mambo hayapo ndio maana tuliona bendera nyingi za taifa la marekani siku ya kuapishwa rais wao,kwetu sisi zingezagaa bendera za CCM na Mashati ya kijani kofia,T shirt za Njano,kijani NK. wakati mwingine rais au Waziri mkuu anapokuwa ziarani mikutano yao inapambwa na rangi za kijani,Njano( Nembo za chama)huu ni ushaidi kuwa bado hatujajenga umoja thabiti kwenye masuala la kitaifa,bado tuna weka mbele ushabiki wa vyama hata kama ushindani haupo (kampeni za uchaguzi),nimechangia eneo hili ambalo linaweza kuonekana dogo lakini linamchango mkubwa sana katik maendeleo ya nchi,ndio maana tumekuwa tukisikia kauli za viongozi za kuwalaani wapinzania wanaodaiwa kuchochea wananchi wasishiriki shughuli za maendeleo,sababu ni hizo hizo ambazo nimezitaja hapo juu, huwezi kuwahamasisha watu wafanye shughuli za maendeleo huku unashabikia chama kwenye mambo ya kitaifa ni upumbavu,kwani wewe ni kiongozi wa wote unapokuwa kwenye shughuli za chama fanya za chama unapokuwa katika shughuli za kitaifa unapaswa kutofautisha ingawa unaweza kuelezea mafaniko ya sera za chama katika nanma ya kuhamasisha maendeleo na si kwa lengo la kukejeri wapinzani kama ambavyo tumekuwa tukishuhudia kwetu.Kwa hiyo mimi nasifu umoja wa wamerekani kwani ni changamoto kubwa kwa mataifa yetu haya ya kiafrika,kwao upinzani unakwisha mara anapochaguliwa rais mpya na wanabaki wamoja,kwetu sisi upinzani,CCM uendendelea na kampeni miaka yote mitano mpaka uchaguzi mwingine unapowaidia,je unatarajia maendeleo kweili?

Mwanaluguma, Point yako ni muhimmu sana. Katika ustaarabu wowote, ni lazima kukubali kuwa Taifa linatakiwa kuwekwa mbele hasa baada ya kumalizika kwa ushindani wowote. Mapungufu yetu mengi yanatokana na kukosekana kwa kuvumiliana kama ulivyoweka bayana hapo juu.

Ubarikiwe sana Mwanaluguma
 
Somo kubwa sana kutoka kwa Obama ni transparency, sincerity na people mindedness.

Tukiweza kupata serikali ambyo ina sifa kama hizo alizonazo obama tutapiga hatua sana.
 
Nilichojifunza ni kuwa mfumo wa demokrasia unaweza kukupa BUSH na pia ukakupa OBAMA....

Inatisha...

Tanzanianjema
 
Back
Top Bottom