Watanzania kuweni makini na wanasiasa

jamadari

JF-Expert Member
Feb 13, 2010
295
92



TUMEMALIZA uchaguzi lakini ni vizuri Watanzania tukawa makini sana na wanasiasa, kwani wengi hawa ni waongo.Wanatoa ahadi nzuri, vitendo vyao kwa walio wengi si vya kuridhisha.

Nafikiri tutakubaliana kuwa kuna baadhi ya wanasiasa hata kurudi kwenye majimbo na kuwashukuru wananchi wao ni suala gumu.
Ni lazima sasa tuwe makini nao kwa kila wanachokifanya. Hatuna sababu za kuwapenda kama wanaonekana kutotujali.

Ni kwamba hatupaswi kuwa na rafiki wa kudumu wala uadui wa kudumu na wanasiasa; kama leo wanashindwa kutusaidia tuwe na maisha bora, kuturekebishia miundo mbinu nk, ni lazima katika uchaguzi ujao tuachane nao.

Ingawa uchaguzi mwingine bado sana, ninachotaka tuelewe hapa ni kuliweka hili kichwani kwamba kama wanashindwa kutuletea maendeleo, hakuna sababu ya kuendelea kuwa nao karibu kwa sababu zozote zile.
Hakuna sababu za kuwa na mwanasiasa ambaye hana maana katika maisha yetu. Ni lazima Watanzania tubadilike sana katika hili.

Najua baadhi yetu tuna kadi za vyama mbalimbali, ambavyo kwa hakika havina maana, hasa kama chama chako hakionyeshi msaada katika kuhakikisha unakuwa na maisha bora.

Tanzania ni nchi maskini ni lazima tuwe na viongozi ambao kweli wanasaidia wananchi. Muda wa kukubali kuendelea kudanganywa umekwisha, ni lazima sasa tuwahukumu wanasiasa kutokana na namna wanavyotufanyia mambo, ndio kusema kama wanashindwa kutuletea maendeleo, tunapaswa kuachana nao.

Kwani kuna maana gani kuwa na kadi ya chama fulani, ikiwa chama hicho kinashindwa kukuletea maendeleo? Ni swali ambalo kila Mtanzania anapaswa kulipatia jibu. Kama kweli Watanzania tunataka maendeleo ya haraka, ni lazima tuwe na mwelekeo tofauti wa namna tunavyowachukulia wanasiasa na tunavyoendesha mambo yetu.

Ni aibu kwa mfano jana mwanasiasa amekuahidi kitu fulani, hajafanya, leo anakuahidi kitu kingine, na unampenda. Iko wapi akili katika hali kama hii?

Amkeni ndugu zangu Watanzania ni wakati wa kutupa mashuka na kuanza kusaka haki bila woga…amkeni ndugu zangu.

Amri Bawaziri Kingoda
Tanga
 
Back
Top Bottom