Watanzania kuleni nyama ya panya ina vitamini adimu mwilini

Amavubi

JF-Expert Member
Dec 9, 2010
30,141
13,215
panya+clip.jpg

Mwananchi Jumapili Mei 25 Ndio Chanzo
 
Watanzania wameshauriwa kufuga na kula panya aina ya ndezi wakieleza kuwa nyama hiyo haina mafuta mengi, ikiwa pia na virutubisho muhimu na vilivyo adimu.

Rai hiyo imetolewa na wataalamu kutoka Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine (SUA) katika Maonyesho ya Vyuo Vikuu nchini yaliyofanyika jijini Dar es Salaam hivi karibuni. Wataalamu hao walisema kuwa ili kukabiliana na uharibifu wa kuchoma moto misitu kwa ajili ya kuwatafuta wanyama hao, ni vyema wananchi wakaanza kuwafuga kwa kuwa nyama yao ina ladha nzuri na ni laini.

Mhadhiri Mwandamizi wa SUA, Idara ya Uzalishaji, Mirende Matiko alisema kuwa ingawa wanyama hao wanafugwa kwa wingi katika nchi za Afrika Magharibi, hapa nchini ufugaji wake unakabiliwa na changamoto nyingi.

"Wakulima wetu hapa tunawapa wafuge, siku chache baadaye ukienda utaambiwa walikufa, lakini ukiwauliza majirani wanakuwambia ‘jamaa aliwachinja', ni sawa na kumpa mkulima mbegu halafu anakula," alisema Matiko.

Akizungumzia namna nyama hiyo inavyoliwa, Matiko alisema: " Nyama yake ina viinilishe vingi, yanatupwa manyoya na miguu yake tu, vitu vingine vyote vinaliwa. Tena utumbo ndiyo mtamu sana, si unajua wanakula nyasi tu."

Alisema wanyama hao wana faida nyingi kiuchumi ikiwamo kuongeza pato la kaya, kuchangia uwindaji endelevu, kutunza bioanuwai pia nyama yao ni gharama nafuu, ikilinganishwa na nyingine.

"Mtu akitaka kufuga wanyama hao anatakiwa kuwa na banda madhubuti lenye ubora, chakula na maji safi yawepo bandani muda wote na upandishaji ufanyike katika muda mwafaka," alisema.

Mhadhiri huyo alitoa hadhari kwa wafugaji akiwataka kuwakamata wanyama hao kwa umakini kutumia chandarua, kuepuka kusababisha majeraha.

Ndezi ni jamii ya nungunungu na pimbi, wakiwa wa aina mbili, ambapo wadogo huwa na uzito wa kati ya kilo nne hadi sita na wakubwa hufikia hadi kilo tisa. Wanyama hao hupendelea kuishi kwenye maeneo yanayolimwa mashamba ya miwa, ulezi na mpunga.

Hata hivyo, Dk Loth Mulungu alisema kuwa wawindaji wa ndezi porini husababisha madhara makubwa ikiwamo uchomaji wa misitu, uharibifu wa bioanuwai, kukanyaga mazao mashambani na upotevu wa muda.

Mmoja wa watazamaji waliotembelea Banda la SUA, Elizabeth Maro alisema kuwa ingawa kwa muda mrefu amesikia watu wakila mnyama huyo. Binafsi hawezi kula nyama yake kwa kuwa anaamini hana tofauti na panya wengine.

"Siwezi kumla kwa namna yoyote, huyu ni panya tu ndiyo maana hata jina lake kwa Kiingereza anaitwa ‘canerat', maana yake panya mla miwa," alisema.
 

Similar Discussions

0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom