Influenza
JF-Expert Member
- Jul 1, 2018
- 1,445
- 3,403
MIRADI mikubwa mitatu ya kimkakati inayotekelezwa na Serikali ya Awamu ya Tano imewezesha kutoa ajira kwa Watanzania 15,009 hadi kufikia Oktoba mwaka huu.
Miradi hiyo ni ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR) kutoka Dar es Salaam hadi Mwanza unaotekelezwa kwa awamu, Mradi wa Kufua Umeme wa Maji katika Maporomoko ya Mto Rufiji wa Julius Nyerere (JNHPP) na ununuzi wa ndege kwa ajili ya Kampuni ya Ndege Tanzania (ATCL).
Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Ashatu Kijaji ametoa takwimu hizo bungeni jijini Dodoma wakati akifafanua hoja za wabunge waliochangia Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa na Mwongozo wa Bajeti ya Mwaka 2020/2021.
Akitoa ufafanuzi huo juzi bungeni, Dk Kijaji alisema miradi hiyo mikubwa ya kimkakati imekuwa na faida ya moja kwa moja katika maendeleo ya kiuchumi nchini.
Akitoa mifano na takwimu, alisema kwa upande wa SGR, hadi kufikia Septemba mwaka huu, mradi umetoa ajira 13,117 kwa Watanzania katika awamu ya kwanza.
Pia umetoa fursa kwa makandarasi 640 wa nchini ambao wamefaidika na jumla ya Sh bilioni 664.7, huku bidhaa kama saruji, nondo na malighafi nyingine zikinunuliwa kutoka ndani ya nchi. “Asilimia 30 ya gharama za mradi huu zimetumika kununua bidhaa kutoka ndani ya nchi,” alisema.
Aliongeza kuwa kukamilika kwa mradi huo kutaokoa Sh bilioni 6.7 ambazo zinatumika kwa matengenezo ya barabara kila mwaka nchini.
Kuhusu Mradi wa Umeme wa Rufiji wa Julius Nyerere, alisema hadi kufikia Oktoba mwaka huu, mradi umetoa ajira 1,456 na wakandarasi wa ndani 10 wamenufaika kwa kupata kazi katika mradi huo utakaofua megawati 2,115 za umeme ndani ya miaka mitatu ijayo.
Aidha, alisema mradi huo una ongezeko la matumizi ya bidhaa za ndani kama saruji, nondo, kokoto na vyakula, na mradi huo ni muhimu kwani bila umeme wa uhakika na bei nafuu, hakuna viwanda.
Akizungumzia ununuzi wa ndege, alisema ndege ambazo zimeshaletwa nchini, zimewezesha kupatikana kwa ajira 436 kwa Watanzania hadi kufikia Septemba mwaka huu.
Naibu Waziri aliongeza kuwa ndege hizo zimerahisisha huduma na kufikia vituo 11 nchini na sita nje ya nchi, huku zikiongeza mapato pamoja na idadi ya watalii wanaotembelea nchi.
Akizungumzia kilimo, alisema serikali inafahamu umuhimu wake na itaendelea kutenga fedha zaidi kwa sekta hiyo ili kufikia Azimio la Maputo linalotaka nchi za Afrika kutenga asilimia 10 ya bajeti kwa kilimo.
Kuhusu maji, alisema upatikanaji wake umezidi kuongezeka kwani kwa sasa kwa Jiji la Dar es Salaam upatikanaji ni asilimia 85, miji mingine asilimia 80, miji midogo ni asilimia 64 na vijijini ni asilimia 64.8.
Alisema serikali imejipanga kusimamia kikamilifu Mamlaka ya Maji Vijijini (RUWASA) na Mfuko wa Maji ili kuhakikisha upatikanaji wa maji unaboreka.
Akizungumzia maboma yaliyojengwa na wananchi katika sekta za afya na elimu ambayo hajakamilishwa, alisema serikali imekuwa ikitoa fedha kukamilisha maboma hayo.
Alibainisha kuanzia Julai 2018 hadi Oktoba mwaka huu, serikali imetoa Sh bilioni 104 katika ujenzi huo sekta ya elimu na Sh bilioni 38.9 katika sekta ya afya kwa ajili ya kukamilisha maboma ya vituo vya afya.
Pia imetoa Sh bilioni 29.9 kukamilisha madarasa 2,392 ya sekondari na Mpango wa Lipa Kutokana na Matokeo Makubwa (EP4R), Sh bilioni 32.2 zimejenga vyumba 2,760 na matundu ya vyoo 670 shule za msingi nchini.
Amesema serikali imekuwa ikitekeleza mpango huo wa maendeleo kwa mujibu wa sheria na matokeo makubwa yanaonekana katika miaka hii minne.
Amesema ni kwa msingi huo, Juni mwaka huu, Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) iliitaja Tanzania kuwa miongoni mwa nchi zenye uchumi unaokua kwa kasi ikitanguliwa na Djibouti, Ethiopia na Rwanda.
Akihitimisha mjadala huo, Spika wa Bunge, Job Ndugai alimsifu Rais John Magufuli,Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa na mawaziri kwa jinsi wanavyochapa kazi.
Chanzo: Habari Leo