jamadari
JF-Expert Member
- Feb 13, 2010
- 295
- 92
Muasisi wa Muungano Hayati Baba wa Taifa, Julius Kambarage Nyerere
Muasisi wa Muungano Hayati Abeid Amani Karume.
Watanzania wametakiwa kuheshimu maamuzi magumu ya waasisi wa Muungano, Julius Kambarage Nyerere na Abeid Amani Karume ambayo yalilenga kuhakikisha wananchi wanakuza uchumi na kulinda amani.
Pia wameshauriwa kuwa na utamaduni wa kuzungumzia namna ya kutatua matatizo ya Muungano ambao umekuza kwa kiasi kikubwa amani na utulivu miongoni mwa jamii badala ya kujenga hoja ya kuuvunja.
Kauli hiyo ilitolewa na Mkuu wa Wilaya ya Mkuranga, Henry Clemens wakati akizungumza katika sherehe za miaka 46 ya Muungano katika viwanja vya shule ya msingi Mbezi Msufini wilayani humu.
Clemens alishangazwa na baadhi ya watu wanaohoji uhalali wa Muungano.
"Maadui hawakuondoka kwa hiyari waliondoka kwa nguvu za bunduki na mapanga, Karume aliongoza waasi hakufanya makosa leo hii wasiopigana vita ya ukoloni ndio wanaotaka kuua udhaifu wa Muungano kwa kutaka kujua uhalali wake mbona hawaulizi mambo mengine," alisema.
Clemens alisema Muungano umechangia kuwepo kwa lugha moja ambayo imefuta tofauti kwa kuwaunganisha wa Bara na Visiwani.
"Mkuranga tuendelee kuboresha maisha ya vizazi vijavyo tudumishe Muungano wetu hilo ndilo lengo la uhuru na Muungano damu ilimwagika kwasababu hiyo," alisema.
Aidha, alisema kuwa wakoloni walichukua raslimali hivyo dawa pekee iliyobaki ni kujikita zaidi katika kuboresha uchumi wa nchi kwa kufanya kazi kwa bidii na kujenga ushirikiano ili watu wote waondokane na umaskini.
"Bidii, ushirikiano na dhamira ya dhati katika kuutokomeza umaskini kwa kufanya kazi tuwe na msimamo huo huku tukiendelea kuudumisha Muungano wetu," alisema.
CHANZO: NIPASHE