Wasomi wa Tanzania wametoa mchango gani kwenye Taifa letu mpaka sasa?

Ritz

JF-Expert Member
Jan 1, 2011
46,877
32,270
Wanabodi.

Kila siku najiuliza sipati jibu sahihi kuhusu wasomi wetu wa Tanzania..

Kwa mujibu wa data za World Bank na IMF Tanzania ipo kwenye kundi la nchi 20 maskini wa kutupwa duniani.

Baadhi ya nchi zimekuwa masikini kutokana kuwa na vita vya muda mrefu vya wenyewe kwa wenyewe kama vile Rwanda, DRC, Burundi, Somalia..

Hawa wasomi wetu kila kukicha wanajitapa na kijisifia na wengine wapo humu JF kuwa ni wasomi..

Ni kipi cha maana hawa wasomi wetu wa Tanzania wamelisadia taifa letu kutoka kwenye dimbwi la umasikini?

Kama kuna wasomi tunaomba mnijibu ni kipi mlichoifanyia taifa letu la Tanzania..

Nawakilisha..


Swali
Ritz, heshima mkuu..

Ningependa kuchangia thread yako NZURI, lakini kabla ya kufanya hivyo, ningependa kujua definition yako ya msomi/wasomi? Na je, wewe ni miongoni mwao(wasomi)?

Jibu
Mkuu hippocratessocrates,

Tunapoengelea "usomi" wa utawala unaitaji elimu ya chuo kikuu ili kuweza kufahamu sheria za mikataba na mambo ya utawala, Mkuu wewe ni msomi kwenye fani yako ya udaktari huwezi kuwa mtaalamu wa tiba bila kuwa msomi wa fani hiyo.

Kuna usomi wa mazingira ni mtu yeyote mwenye uwezo wa kuyamiliki mazingira yanayomzunguka kwa ajili ya maendeleo yake na jamii yake kwa ujumla.

Mkuu ukiangalia mikataba inayoingiwa na wanasheria wetu ambayo ni wasomi inasikitisha sana mfano Chenge alivyokuwa mwanasheria wa serikali kapewa hiyo nafasi kutokana na usomi wake.

Nyongeza
Okay, kumbe linaloongelewa hapa ni usomi wa utawala
"administration"!!

Nadhani mkuu, katika hili tungeweza kuangalia UWEZO wa Taifa, MAHITAJI ya Taifa na VIPAUMBELE vya Taifa.

1. UWEZO:
Sidhani kuna haja ya kuongelea katika hili, kwamba tuna uwezo mkubwa hasa kwa maana ya vyanzo asilia(Natural Resources) vilivyopo nchini kwetu, na kuna hili la wataalamu "wasomi" wa fani/kada husika ambao nao pia si haba.

2. MAHITAJI:
Kama Taifa tuna mahitaji mengi (kila sekta/wizara/n.k), haya yote ni muhimu kufanyika, kwamba yatekelezwe kulingana na hoja namba moja hapo juu(UWEZO).


3.VIPAUMBELE:
Nionavyo mimi, hapa ndiyo kwenye shida...mfano tinaweza kuwa na vitu D, E, F na G. Lakini kwa kuangalia uwezo ulionao/tulionao na kuona huwezi kufanya yote..Ndipo pale unaweza kuchagua kufanya jambo E, ili kwamba kwa lenyewe lifanikishe jambo F na G. ..yaani;

Badala ya kuepuka KUTIBU magonjwa(yanayotomana na kujikinga), kuepusha watu kuwa wategemezi na KUTOA MISAADA kila siku nk...unaamua kuwekeza katika ELIMU, ukitegemea wanafunzi wanapohitimu(na kukiwa na channel za ajira, au ukimwezesha kwa kiasi kidogo sana) ataweza ku-excel kwa kutumia elimu aliyopata kujikinga na magonjwa, kujiajiri.n.k

Sasa nadhani hata kama TAIFA ZIMA tukiwa ni "WASOMI" lakini hakuna kuweka vipaumbele vya msingi hatutafika popote..we seriously need to priotize our priorities.

Michango kutoka kwa Wadau

Mkuu @Ritz umeleta mada nzuri ambayo haina hata mjadala mrefu kwani jibu lake liko wazi.
Tatizo hapa ni serikali ambayo haithamini wataalamu wake na hivyo kutokuwa na mikakati ya kuwatumia kwa ajili ya Maendeleo ya nchi.

Hapa Tanzania wanasiasa wamegeuka ndio wataalamu. Wataalamu hawapewi kazi zao za kitaalamu.

Nchi yoyote ile ili wasomi wake wawe na mchango unaoonekana na jamii ni lazima serikali iliyopo madarakani iwe na sera za wazi zinazoshirikisha wasomi na wataalamu wake kwenye kutekeleza mipango mikubwa ya Maendeleo ya nchi.

Ni lazima serikali iwe na mikakati ya kuandaa na kutumia wasomi na wataalamu wake kwenye miradi mikubwa ya nchi badala ya kutegemea wataalamu kutoka nje.

Tuchukue tu mfano mdogo na wa wazi. serikali tangu uhuru inajua nchi hii tuna dhahabu na madini mengine lukuki. lakini serikali haiandai wananchi wake wawe na uwezo wa kutafiti, kuchinba na ku-process hayo madini.

Matokeo yake wanaleta watu kutoka nje kana kwamba kilikuwa ni kitu cha dharura. Badala ya nchi na wananchi wake kufaidika, nchi inafaidiwa na washenzi. Nchi yetu na sisi wananchi wenyewe tunaendelea kuwa masikini. Halafu hawa washenzi wanatudharau na kutuona watanzania wote ni wajinga!

Kutothaminiwa na kudharauliwa kwa wasomi wa nchi hii kunajionyesha dhahiri. Wewe mwenyewe angalia hata mishahara wanayopata wataalamu wetu, utasikitika. Angalia madaktari wanavyonyanyaswa, angalia ma-injinia, angalia watumishi wengine wa serikali-pasipo na malalamiko ni pale ambapo watumishi wanashirikisna na wanasiasa kutuibia.

On the contrary, nenda TRA, Benki kuu nk; mshahara anaopata hata mtu anaepanga mafaili utadhani wao hawako Tanzania.

Wasomi hawathaminiwi wao na kazi zao, mfano pia angalia ukienda library, utakuta tafiti nyingi sana za hawa wasomi zimezikwa huko na Hakuna mpango wa kuzitumia kwa manufaa ya nchi.

Wataalamu na wasomi katika nchi hii Wamekata tamaa. Baadhi yao ndio unawashuhudia wameamua kutokomea nje ya nchi, wengine kuacha taaluma zao na kujiingiza kwenye biashara, na wengine ndio Kama hao maprofesa na madaktari walioamua kuacha taaluma zao na kujiunga na chama chako cha CCM ili wapate ulaji! Hata wewe Nadhani uko huko kwa sababu umehakikishiwa ulaji.

Halafu nikuambie Mkuu Ritz, hawa wataalamu si kwamba hawana uwezo, ni wataalamu wazuri na nchi wanazolowea wanakuwa asset kubwa sana. Mfano kwa mtu aliyewahi kufika Malaysia zile Barabara unaziziona pale miongoni mwa Architect wakuu wa nchi ile ni watanzania. Nenda kama Botswana utawakuta ma-injinia na madaktari wanafanya kazi ambazo hapa mnawapa wazungu.

Nenda na baadhi ya nchi zingine za ulaya na marekani, utakuta wataalamu wa kitanzania wanaoaminika na kutegemewa. Huko wanasiasa wanathamini wataalamu.

Ndugu yangu Ritz, mchango wa wasomi na wataalam wetu utaonekana pale tu nchi hii itakapopata serikali inayosimamia maslahi ya wananchi.

Mimi ni mmoja wao. Yes, nina masters (MSCIS) in Information Technology. Niliporudi Tanzania miaka kama 10 iliyopita nilijaribu kuomba kazi wizara ya mawasiliano na nikapata ila bahati nzuri nilipata offer nyingine ya NGO ambayo inalipia almost two times and half kwa hiyo nikaenda kwa NGO. Nilihamua hivyo kwa sababu serikali yetu hii is a joke haizingatii usomi wa mtu.

Utakuta wewe umesoma shinda bosi wako lakini yeye ndo ana mamlaka zaidi shinda wewe uliyesoma na kujua zaidi yake. Mfano ulio hai; si unaona wewe Ridhiwani Kikwete, huna chochote cha maana kwani hata waliosoma nawe wanakucheka, ila Sitashangaa kama wewe una mamlaka zaidi ya wakili mkuu wa serikali.

Kwa hiyo inakuwa vigumu kwa wasomi kuja nchini kuchangia maendeleo kutokana na ujinga kama huu. Hakuna nchi inayoendeshwa kihuni kimakusudi ikawa na maendeleo, uongo?

Zifuatazo ni baadhi ya sababu:

-Hakuna utashi wa kisiasa kuruhusu wasomi kuwa washauri wa namna ya kuendesha nchi. Wanasiasa wamekuwa waamuzi wa kila kitu hata kama hawana utaalamu.

-Elimu ya Tanzania imepotoshwa; kwa wengi elimu inamaanisha mshahara na hili ndilo limekuwa lengo kuu la watu kusoma. Kwa maana nyingine, mtu anasoma kwa ajili yake si kwa ajili ya Taifa, akishapata kazi hafikirii chochote kuhusu Taifa.

-Nafasi za kitaalamu hupewa watu wasio na utaalamu, kigezo ni kufahamiana na 'wakubwa'!!

SERIKALI KUBEZA MCHANGO WA WASOMI, ISHARA YA KIFO

Kama ambavyo sasa imezoeleka, kwa mara nyingine mwaka huu, Kumbukizi ya miaka kumi na moja ya kifo cha Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Oktoba 11, imepita kimya kimya bila Serikali kuinua macho wala kuipa uzito unaostahili.

Si Kiongozi wa Serikali wala wa Chama tawala kitaifa, aliyetoa hotuba kuwakumbusha Watanzania nafasi ya Mwalimu katika kuleta uhuru wa nchi hii, mshikamano wa kitaifa na huduma za kijamii kwa usawa wa watu wote, ambayo ni misingi mikuu aliyotuachia, lakini imeachwa kwa uzembe na kutojali kuanza kubomoka.

Hilo ni jambo lililo dhahiri, kwa sababu, kwa nchi iliyokosa maadili ya kitaifa, sera na dira ya uchumi, mshikamano na umoja wa kitaifa; kwa wadhalimu, kupigia debe fikra za Mwalimu ni kaa la moto lenye kuunguza. Kwa baadhi ya Viongozi wa leo, wanafiki, wenye kuhubiri wasichokiamini na kuamini wasichokihubiri, hawawezi kuuhadaa umma kwa kuzungumzia kwa maneno pekee, neema ya fikra za Mwalimu bila umma kuwatemea mate usoni.

Na katika kuuhadaa umma kwamba Mwalimu anakumbukwa; na ili kuficha lengo na kusudio lao la kufifisha fikra hizo, Kumbukizi la kifo cha Baba wa Taifa limeunganishwa na Sherehe ya kuzima mwenge, ambazo zinapewa umaarufu zaidi badala ya Kumbukizi hilo.

Ni kwa sababu hii kwamba, mwaka huu ni Wanataaluma wa Chuo Kikuu cha Dar Es Salaam [UDASA] pekee ndio waliojitosa kuitisha na kushiriki kwenye mhadhara/mdahalo wa kujadili fikra za Mwalimu katika mazingira magumu, ikiwa ni pamoja na wanachuo vijana kuongezewa siku za likizo wasiweze kushiriki mdahalo huo na uchaguzi mkuu wa mwaka huu.

Yaliyosemwa na Wasomi hao ndiyo lile kaa la moto ninalosema, ambalo wanasiasa wanafiki hawawezi kuuambia umma kiasi kwamba wangependa hiki kinachoitwa Nyerere Day ifutiliwe mbali.

Ukweli uliotawala mdahalo ni ule kwamba, Serikali ya sasa madarakani [na hata zilizotangulia] si sikivu, Chama na Viongozi wamekiuka misingi iliyowekwa na mwasisi huyo, kama vile utaifa, uzalendo na miiko ya uongozi.

Mmoja wa Washiriki, Dakta Azaveli Lwaitama alisema, ni vigumu kuwa na taifa lenye uzalendo mahali ambapo kuna tofauti kubwa ya kipato miongoni mwa wanajamii kama inavyotokea sasa nchini. Na katika hali iliyoonyesha kupandwa jazba, msomi huyo alisema: Naomba kukipa pumziko la milele Chama hiki [CCM] ingawa mimi mwenyewe ni mwanachama wa chama hiki.

Dakta Lwaitama aliweza kubaini kero inayokera wanachama wengi [wa CCM] sasa na kuahidi alisema: Matajiri waliopata fedha kwa rushwa wakihama, ndiyo [nami] naweza kurudi CCM.

Ni kiapo cha usomi kwamba: Nitafuatilia ukweli popote utakaponipeleka; na ndivyo Wasomi hao walivyothibitisha kwenye mawasilisho yao kwenye Kumbukizi hiyo.

Lakini Profesa Mathew Luhanga [aliyewahi kuwa Makamu wa Mkuu wa Chuo hicho kwa miaka 16] alikuwa mwepesi kubaini kuwa, Wasomi wengi sasa wamekuwa waoga kukemea Viongozi wanapokosa, wameshindwa kuwajibika kwa jamii kama vile kutetea haki na maslahi ya wengi nchini; wamekuwa watu wa kujikomba kwa wanasiasa.

KunaHiyo ni tuhuma nzito lakini iliyosheheni ukweli. Isingekuwa hivyo, Bunge lisingepitisha Muswada wa Sheria kupiga marufuku siasa za wanafunzi Vyuo Vikuu mwaka 2005 na hali ikakalika, eti kwa sababu tu Wanafunzi walijitambua na vyama vya siasa wakati wa Uchaguzi Mkuu wa 2005.

Isingekuwa hivyo, Wanafunzi wasingenyimwa haki yao ya Kikatiba ya kushiriki katika Uchaguzi Mkuu mwaka huu, kwa tarehe ya kufungua Vyuo kusogezwa mbele kwa siku nne zaidi kwa mbinu. Kinacholengwa wanakijua wanafunzi hao, lakini wanaogopa kusema ukweli [wasije kunyimwa mikopo?]; kwa hofu hiyo wameasi viapo vya usomi.

Kitendo cha Bunge kupitisha Muswada kuzuia harakati za kimapinduzi Vyuoni, kinatukumbusha enzi za ukoloni ambapo Serikali na mfumo wa elimu haukuruhusu siasa za Wanafunzi [Student Politics] vyuoni, kama tu ambavyo Serikali haikuruhusu demokrasia kufanya kazi kwa watawaliwa.

Elimu ilitolewa katika mfumo na mazingira ya kudumaza akili na fikra za Mwafrika ili aendelee kubakia kikaragosi tegemezi katika gurudumu la unyonyaji, akitenda na kutekeleza maagizo ya wenye mfumo kama roboti.

Serikali tafsiri yake ni taasisi ya kijamii inayotokana na migongano ya matabaka yasiyoshabihiana ambapo tabaka lenye nguvu [watawala] ndilo lenye maamuzi kwa kutumia nguvu kulitawala tabaka nyonge, na kulinyonya kwa kutumia Sheria linazotunga.

Madhumuni yote haya ni kuliwezesha tabaka hilo lenye nguvu kujijengea, kulinda na kuimarisha matakwa na nguvu zake za kiuchumi kisiasa na kiutamaduni, dhidi ya na kwa hasara ya watawaliwa [Frederick Engels: Origin of Family, Private Property and the State].

Kwa Serikali kupiga marufuku siasa katika Vyuo Vikuu, maana yake ni kuinyima jamii ya kisomi haki ya kushiriki katika kuhoji au kutoa mwelekeo kwa jamii ilimo na kufanya mgongano ndani yake isipate ufumbuzi kwa manufaa ya kitabaka.

Jumuiya ya Wanafunzi wa Vyuo Vikuu na Wasomi ni sehemu ya jamii ya Kitanzania inayoguswa na yale yanayotendwa na Serikali. Isitoshe, jumuiya ya Wasomi ni sehemu ya jamii yenye upeo wa kuona mbali kwa nyenzo ya elimu, na hivyo ina wajibu kuimulikia njia jamii na kuielekeza njia sahihi ili iweze kufikia malengo na matarajio yake. Unapowazuia wasomi kuhoji kwa uhuru mwelekeo wa jamii yao unaua jamii.

Vijana wasomi sio watu wanaoishi katika ulimwengu wa kufikirika; wala hawatawaliwi, kutekwa au kufungwa na minyororo ya kibiashara, ubeberu, ubaguzi wa kiuchumi na kijamii, kama walivyo baadhi ya baba au babu zao.

Hawatawaliwi na mawazo ya Ubwana na Utwana; au majivuno kwamba baba yangu alikuwa Mfalme, Waziri au Mtemi, kwa hiyo na mimi lazima niwe. Hawatawaliwi na fikra za uhuru wa bendera, njozi za ukuu wa kufikirika, wala dhana ya kuwagandamiza na kuwanyanyasa wengine chini ya uficho wa demokrasia batili au sera huria za bandia na utandawazi, unaopewa jina la Ushirikiano [mwema] wa dunia badala ya jina halisi la ukoloni mamboleo na utandawizi.

Wajibu wa vijana Wasomi ni kuchambua na kuhoji mhimili wa kilimwengu na sera ambazo zimeshikilia hatima ya maisha ya wengi. Wanahoji pia kama kweli mhimili huo na sera za uchumi za wakati wao ni sahihi kuweza kutumika katika ulimwengu wa leo na kesho kwa manufaa ya walio wengi, wakiwamo wao wenyewe.

Ule ukweli kwamba wao hawana vyeo kuweza kufungwa nira na mfumo wa sasa, ni nguvu tosha kwao kuweza kuitazama jamii na kutenda kwa mawazo na akili iliyo wazi zaidi, ikizingatiwa pia kwamba wengi wao wanatoka katika familia na jamii masikini. Kwa hiyo hawana cha salia Mtume kwa anayechezea haki ya jamii.

Ni kwa sababu hii kwamba, kwa miaka mingi Wanafunzi wa Vyuo Vikuu wameshikilia nafasi ya kuwa upande wa Wakulima na Wafanyakazi katika harakati za kuikomboa jamii ya Kitanzania kisiasa, kiuchumi na kijamii.

Kwa mfano, ni makosa kudhani kwamba maandamano ya Wanafunzi wa Vyuo vya elimu ya juu kupinga kujiunga na Jeshi la Kujenga taifa, Oktoba, 22, 1966, yalikuwa potofu au jeuri ya kisomi. Ukweli ni kwamba Wanavyuo hao hawakuwa wakipinga JKT; walichokuwa wakilalamikia ni wao kukatwa mishahara [baada ya masomo] kwa njia ya kujifunga mkanda kwa jina la Ujenzi wa taifa, wakati watawala waliendelea kujiongezea mishahara na marupurupu katikati ya jamii masikini. Na pale Mwalimu alipoyaelewa madai yao, kwa kubaini kwamba alikuwa amepotoshwa na vyombo vyake, alipunguza sawia mishahara ya watawala, akianzia na wake mwenyewe; na wengine wakalazimika kuonyesha mfano kwa kujiunga na Jeshi hilo angalau kwa muda mfupi. Katika sakata hilo, wanavyuo walishinda. Na ili kuutafsiri ushindi huo kwa usahihi, Mwalimu aliandika na kutangaza Azimio la Arusha.

Miparanganyiko ya kiutawala na ambayo Wasomi wameikabili kiume ni mingi, inaanzia enzi za Chama kushika hatamu [1965], Ubepari wa Serikali kwa mfumo wa Azimio la Arusha [1967], Mgogoro wa Kikatiba [1977] na ulegezaji Masharti ya Siasa na Biashara ulioashiria kifo cha suluhisho la miparanganyiko iliyotangulia [1992].

Umakini wa Wanavyuo Vijana katika kuainisha matatizo ya jamii na huruma yao kwa wanyonge unajionyesha dhahiri katika kazi za wasomi hao enzi za nyuma, vikiwamo vitabu viwili vya Mwanafunzi wa mwaka wa pili, Issa Shivji: The Silent Class Struggle in Tanzania, na Class Struggle Continues, vinavyoweka wazi migongano ya kitabaka inayoikabili jamii yetu.

Si hivyo tu, baadhi ya wanafunzi walitumia muda wao wa likizo kwenda kushiriki katika harakati za ukombozi wa nchi za Kusini mwa Afrika, kuonyesha uanamapinduzi wao kwa bara letu. Kwa nini Serikali inaua uanaharakati huo?.

Nchi yetu inakabiliwa na mtihani mgumu, kati ya kubakia kama taifa huru au kugeuka taifa lililofungwa minyororo chini ya Ufalme wa demokrasia ya Ki-Magharibi na sera za utandawazi. Uchumi wetu unaendelea kuwa tegemezi kila kukicha, huku taifa likipoteza kwa kasi ya kutisha, utamaduni na maadili ya kitaifa yaliyotuunganisha kuwa jamii moja.

Demokrasia inazidi kusinyaa na kuwa mikononi mwa walio nacho pekee; huku ufa kati ya matajiri na masikini ukipanuka haraka. Tunazidi kubiasharisha kila kitu, toka ubinadamu, utu na hata imani za dini, chini ya altare ya sera huria.

Kwa walio nacho, wanajifanya kutoona hatari iliyo mbele yetu, kana kwamba wanajiandaa kustaafu na kukimbilia kuishi nchi za nje. Pengine hii ndiyo sababu ya kusudio la kuunda Muswada juu ya Uraia wa Nchi mbili.

Tumetekwa na vinono vya Wawekezaji katikati ya umma masikini na kushindwa kuhoji aina ya jamii tunayojenga kwa manufaa ya wengi; na ili kujihakikishia utafunaji mwanana wa kile tunachopora tunawatungia Sheria Wasomi vijana kuwafunga midomo, na hata kuwanyima haki yao ya kupiga kura!.

Vyama vyetu vya Wafanyakazi tumevigawa katika makundi dhaifu TUGHE, TPAWU, TUICO n.k., ili kuvipunguza nguvu kwa sera za akina Frederick Lugard za wagawe uwatawale tawala [devide and Rule].

Tumerekebisha Sheria za Kazi kuwapa nguvu nyingi Waajiri badala ya kuwalinda Wafanyakazi kwa wimbo ule ule wa Kujenga mazingira safi kwa Wawekezaji, wasibughudhiwe na siasa za Wafanyakazi, kama tulivyopiga marufuku siasa Vyuoni.

Wakati huo huo, tumejionea jinsi demokrasia ya uwakilishi [Bungeni] ilivyogeuka mradi wa kitabaka ambapo Wabunge wanatetea vyama vyao badala ya wananchi waliowapa kura. Na ni Wabunge hao hao wanaowatungia Sheria wasomi wa nchi hii, kuwanyima uhuru wa kuhoji. Kama huu si usaliti kwa umma, ni nini?.

Sheria hii ya kuziba midomo wasomi si ya wananchi, bali ni ya Wawekezaji na mawakala wao nchini, ambao wamegeuka wala nyama ya wasomi [intellectual cannibals]. Hii haiashirii uhai kwa Taifa, bali ni harufu ya kifo kwa Taifa ambalo hatima yake sasa imo mikononi mwa wapiga ramli kama kina Sheikh Yahya Hussein!

Kuna sababu nyingi zinazofanya watawala wapate hofu na kugeuka nyamaume intellectual cannibals. Kwanza, ni kule Serikali kuendelea kujiweka mbali na wananchi kwa njia ya rushwa iliyokithiri, ulaji wa makeke [Conspicuous consumption] na mfumo wa maisha ya mbwembwe kutosha umma kufungua masikio.

Wameiga maisha ya raha na starehe mithili yale ya Wabenzi wa enzi za ukoloni, wakishindana kuoa na kutaliki mabibi na aina ya magari ya sifa, lakini yasiyofaa kwa kazi za vijijini waliko watu wanaodai kuwatumikia.

Tumepoteza dira na kuendesha nchi na Serikali bila itikadi madhubuti. Tunaimba Ujamaa huku tukicheza ngoma ya kibepari.

Hali hii haiishii hapo pekee; hata mfumo wa elimu na mitaala tumebadili ili kutoa wasomi hohe hahe wasioweza kuisemea na kuitumikia vyema jamii yao; lengo ni kupata wasomi dhaifu, wabeba vipeperushi wakati wa Kampeni za uchaguzi.

Inapokuwa hivyo, kama anavyotabiri Professa Alvin Toffler, katika kitabu chake The Third Wave: The Revolution That Will Change Our Lives, tusitegemee kwamba Viongozi wetu wa leo Marais na Wanasiasa, Wabunge na Wajumbe wa Kamati Kuu, wataichukia mifumo hii [na kutaka iondoke] hata kama inawaumiza wanyonge, ilimradi inawapa shibe yao, madaraka na nguvu ya kutawala.

Tujifunze kutoka kwa Serikali ya Ufaransa baada ya Mapinduzi maarufu ya 1789, ambayo ilishindwa kujifunza kutokana na makosa ya Serikali ya awali [The ancien regime] na kujutia kurudia makosa hayo kwa gharama kubwa.

Wadau salamu zenu!

Kama mjuavyo elimu ina mchango mkubwa sana katika maendeleo ya taifa lolote lile duniani, hasa elimu bora. Kwa hapa Tanzania kuna baadhi ya wasomi wa ngazi za juu ambao kwa namna moja ama nyingine wamekuwa wakitoa michango yao ya kifikra bila woga kwa nia njema ya kujenga taifa lao. Wapo wachache walio maarufu na wapo wengi wasio maarufu.

Kuna wasomi wengi sana hapa Tanzania ambao hawawezi kuthubutu kukemea jambo lolote lile kwa utashi wa elimu yao. Wengi wao aidha wanaamua kukaa kimya ama wanaongea chini chini. Kwa kifupi hawana ujasiri bali wamemezwa na uwoga na kutawaliwa na ubinafsi. Kwa mfano wanaotaka kuleta mfumo wa Div 5 ni wasomi wetu. Walioingia mkataba kati ya tanesco na makampuni ya nje ni wasomi wetu. Yapo mambo mengi ambayo kwa kiasi kikubwa yanasababishwa na uwoga wa wasomi wetu.

Naombeni tutumie jukwaa hili kuwatia nguvu wale wachache ambao wameonyesha dhahiri pasipo shaka kuwa elimu yao si kwa ajili ya manufaa yao peke yao bali ni kwa ajili ya taifa zima la Tanzania.

Kwa kuanza, naomba niwataje hawa wachache:

1. Prof Issa Shivji.
Mchango wa prof issa shivji hasa katika kuwafumbua macho watanzania kuhusu katiba ni mkubwa sana. Historia ya taifa hili itaikumba siku zote.

2.Dr Azaveli Lwaitama(maarufu kama mwanachama mfu wa ccm)
Uchambuzi wa masuala mbalimbali ya kisiasa humu nchini unaofanywa na Dr Azaveli Lwaitama ni mkubwa sana. Binafsi nimekuwa nikimwona kama mmoja wa watanzania walio na nia njeama ya kuijenga kizazi cha leo na kizazi kijacho cha watanzania.

3.Dr Wilbroad Peter Slaa.
Kupitia hoja za Dr Slaa ndani ya bunge na kupitia chama chake cha CHADEMA ni kama taifa zima liliamshwa kutoka uzingizini. Sasa kila mtanzania anahoji kuhusu elimu, afya, miundombinu, nk. Dr Slaa wengi wanamwona kama kiongozi jasiri kuwahi kutokea katika ardhi ya Tanzania.

4.Mh Tundu Antipas Lissu
Wengi wamemfahamu lissu baada ya kuwa mbunge lakini historia ya lissu ni ndefu sana katika kulilitetea taifa lake, hasa katika masuala ya migodini, na huko ndiko lissu alikoanza kupata umaarufu kabla ya kupata umaarufu wa bungeni

5.Mh Deo Filikunjombe(Sina uhakika na elimu yake)
Huyu amekuwa kiongozi jasiri sana kutetea kila anachokiamini. Ni kama yupo tayari kwa lolote ndani ya chama chake. Amekuwa akiungana na wapinzani pale bungeni pindi anapoona kuna hoja nzuri walionayo wapinzani. Hufanya hivi kwa ajili ya taifa lake, si kwa ajili ya chama chake ama kwa ajili ya upinzani bali kwa ajili ya taifa lake.

6.Dr Harrison Mwakyembe
Huyu anajitahidi sana kuonyesha kuwa ana nia njema na taifa lake, ila amezungukwa na mfumo mgumu wa utawala. Mfumo huo unamnyima uwezo wa kufanya kazi kama anavyotaka lakini anaonekana akipata nafasi nzuri na sahihi ana kiu ya kuwatumikia watanzania wenzake

7.Dr John Pombe Magufuli
Kiongozi huyu ana namna yake ya utendaji kazi. Hawana tofauti sana na Dr Mwakyembe. Tatizo linalomkabili ndio hilohilo linalomkabili Dr Mwakyembe. Mfumo wa utawala.

8.Nehemia Mchechu(Sina uhakika na elimu yake)
Huyu ni mkurugenzi mkuu wa NHC kwa wale wasiomfahamu. Ni kati ya watanzania wenye utashi mkubwa wa kuwatumikia watanzania wenzake lakini tatizo linalomkumba Dr Magufuli na Mwakyembe ndilo hilo hilo linalomkumba na yeye. Mtakumbuka alivyoingia NHC kwa mara ya kwanza alionyesha kweli ana kiu ya kufanya vizuri katika nafasi yake lakini mfumo ulimpiga stop

9.Mwl Christopher Mwakasege
Huyu ni msomi wa uchumi ambae mara nyingi amekuwa akitoa elimu ya kiroho sambamba na elimu ya dunia. Kiukweli mara nyingi mwalimu huyu hujaribu kuwafungua watanania macho na fikra zao kuhusu elimu ya kiroho na elimu ya dunia. Tofauti na wengine wengi wanaofundisha elimu ya kiroho yeye sijawahi kusikia akikemea wala kuonyesha mrengo wowote wa kisiasa katika mafundisho yake. Kiukweli amejikita zaidi katika kuhusisha elimu ya kiroho na elimu ya dunia.

10.Edward Ngoyai Lowassa
Huyu mtanzania aliangushwa na mfumo wa utawala, lakini kwa kipindi chote cha kuwa waziri na hatimae kuwa waziri mkuu kwa kipindi kifupi sana, alidhihirisha kuwa ana uwezo na utashi mkubwa wa kuwatoa watanzania toka point A kwenda point B lakini mfumo ulimlang'ai na akalang'aika na hatimae akaingia mtegoni. Ila pamoja na yote bado ameonekana kama kiongoi, msomi alietayari kuwatumikia watanzania wenzake.

Wadau mtiririko uliotumika kuwataja haina maana kuwa wa kwanza kutajwa basi ndio bora zaidi ya wengine, bali nimetaja tu kwa kadri jina linavyowahi akilini. Sasa naombeni tuendelea kuwaorodhesha taratibu kama ishara ya kuthamini michango yao na pia kuwaamsha na wengine ambao wametawaliwa na uwoga pamoja na ubinafsi.

Naomba kuwasilisha!

WASOMI WA TANZANIA WAMEKUWA WASALITI?

Nchi zote zilizoendelea na zinazozidi kuinuka kiuchumi duniani zimepata maendeleo makubwa kwa kuwasomesha watu wake. Napenda niwagawe wasomi wote katika makundi mawili makubwa kama ifuatavyo:

Kundi la kwanza ni la wasomi ambao ni wanasiasa kama Rais, Mawaziri, Wabunge, Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya, nk. Kundi la pili ni la wasomi waajiriwa ambao sio wanasiasa. Kila kundi linategemewa kwa namna yake kuleta maendeleo nchini. Nchi yenye wasomi wengi wa makundi yote mawili inatarajiwa kuwa na maendeleo zaidi kuliko nchi ambayo ina wasomi wachache. Jambo hili kwa Tanzania ni tofauti kabisa. Kwa Tanzania kuwa na wasomi wengi kumekuwa ni chanzo cha kupiga hatua kubwa nyuma maana kila msomi wa Tanzania anafikiria ni jinsi gani ya kupata maendeleo binafsi ya haraka kwa njia zisizo halali. Kwa kudanganya, kuiba, kula rushwa, nk. Msomi wa Tanzania akipata kazi anafikiria jinsi ya kutoka haraka haraka ili marafiki zake waone kuwa ni mjanja kweli.

Kutoka kwenyewe ni kwa wizi. Ni wachache sana wanaofikiria kupata kazi na kuitumikia nchi kwa uaminifu. Msomi wa Tanzania akipata kazi anafikiria kununua gari na kununua kiwanja kama sio kuanza kujenga ndani ya mwaka mmoja. Hata akifanikiwa kutimiza hayo ya msingi katika muda mfupi bado haridhiki. Starehe kwa mbele na kwa kina. Hulka hii ni kubwa sana kwa wasomi waliopata fursa ya kuwa viongozi wa kisiasa. Viongozi wa kisiasa ni viongozi wa umma. Vitu alivyoibiwa Naibu Waziri wa Wizara ya Nishati na Madini Adamu Kighoma Malima akiwa hotelini huko Morogoro ni ushuhuda mzuri wa starehe zilizokithiri za wasomi. Wasomi kama hawa ndo wamechangia sana kuwaharibu wasomi waajiriwa wasiokuwa wanasiasa. Kuwa msomi wa kuheshimika Tanzania siku hizi maana yake ni kuwa mtu wa dili.

Dili ni mipango ya wizi tu wala hakuna kitu kingine. Kama hujaiba au kufisadi unakofanyakazi unaonekana huna maana, unaonekana umezubaa, unaonekana mpumbavu, unaonekana usomi wako ni wa kutiliwa mashaka. Ukiwa mtu wa kufuata maadili ya kazi unaonekana una matatizo katika kichwa chako. Siku hizi kumpata msomi asiyefikiria kuiba ni kazi kubwa kweli. Naye akipatikana usalama wa kazi yake unakuwa hatarini. Hakubaliki kwenye jamii kubwa ya wasomi. Kuanzia kwa Rais mwenyewe hakuna aliye na moyo wa kuiletea maendeleo nchi yake. Kitendo cha Rais kunyamazia vitendo vya ufisadi vya akina Andrew Chenge na wenzake kinaonesha wazi kuwa Rais naye anahusika katika ufisadi. Tena yeye ndiye fisadi mkuu.

Lakini wasomi hawa wanapotembelea nchi zilizoendelea ndo wa kwanza kuanza kusifia hatua ya maendeleo iliyofikiwa katika nchi hizo. Utafikiri maendeleo hayo yalikuja yenyewe. Wakirudi wanaishia kutoa takwimu tu kutoka katika nchi hizo ili waonekane mbele ya jamii kuwa wamefika huko. Usomi wao unadhihirishwa kwa kutoa takwimu tu. Hawajifunzi na kufanya chochote cha kubadilisha maisha hapa nchini. Kazi yetu ni kwenda kuomba misaada kwa nchi hizo bila aibu hata kama nchi zenyewe zina raslimimali chache kuliko zetu.

Wasomi wetu hawa ndo wa kwanza kuingiza nchi katika mikataba ya kinyonyaji isiyo na masilahi kwa nchi. Wanafanya hayo wakijua wala sio kwa bahati mbaya. Hawa hawana njaa ya fedha wala nini, ni uchu wa utajiri uliopitiliza mipaka. Kama watu hawa wanaosaini mikataba hiyo wangekuwa hawana ujuzi wa kutosha tungeona tunanyonywa kutokana na ukosefu wa wasomi. Tungejihurumia sana kwa kukosa wasomi.

Wasomi wetu hawa ndo wa kwanza kula njama na makampuni ya kigeni kuleta vitu feki nchini. Hata kama vitu hivyo vina athari za kiafya. Wako tayari watanzania na ndugu zao wafe lakini wamesaidia wageni kutajirika.

Wasomi hawa ndo wa kwanza kula njama za kuwasaidia wafanya biashara kukwepa kodi mbalimbali wakati wanajua maendeleo ya nchi yanategemea kodi. Maendeleo ya nchi yetu kwao sio muhimu. Muhimu ni maendeleo ya nchi nyinginezo. Ndo wasomi wetu tuliowalilia kuwapata tangu enzi za ukoloni.

Wasomi wetu hawa ndo wa kwanza kwenda mahakamani kutetea mikataba ya kifisadi nchini. Hivi kuwa mwanasheria mahiri ni kutetea hata kitu ambacho hakina uhalali? Mimi nafikiri mwanasheria mzuri ni yule anayehakikisha haki inapatikana. Kama mtu kaiba kweli na kama haki yake ni kwenda jela, basi mwanasheria ahakikishe mtu huyo anaenda jela na sio kumsaidia asiende jela kwa kupindisha ukweli. Wakili wa mtu sio kumwepusha mtu adhabu kwa kuficha au kupindisha ukweli bali ni kumtetea mteja asikandamizwe na vifungu vya sheria ambavyo sio halali na kumsaidia apate adhabu sahihi. Na mahakimu wanatoa hukumu zisizo za haki wakijua kabisa wanaumiza nchi. Ndo wasomi wetu tunaowategemea kuleta maendeleo.

Wasomi wetu hawa ndo wanaotunga, kupitisha na kusaini sheria za kuifilisi nchi. Mfano sheria ya manunuzi. Sheria ya manunuzi inahitaji wazabuni ndo wanunue bidhaa kwa ajili ya serikali. Wazabuni hawa wanauzia bidhaa serikali kwa bei mara tatu zaidi ya bei iliyoko sokoni. Serikali yetu inalipa tu licha ya kujua ukweli kuwa bei iliyotolewa ni ya kugushi. Wanapitisha malipo kwa kuwa tayari wameishapewa kitu. Hata kama makampuni ya uzabuni ni ya viongozi WETU kuna shida gani kutoa bei ya kweli? Tatizo kubwa la wafanya biashara ni kupata soko. Sasa umeishapata soko, kwa nini usiuze kwa bei ya haki?

Wasomi wetu hao ndo wa kwanza kulilia maendeleo duni kwa nchi yetu wakati wao wakipata nafasi ndo wanachangia uduni huo. Hawafanyi kazi kwa uaminifu. Wasomi hawa wanakuwa kazini kwa ajili ya kupata utajiri usio wa haki. Hawaoni kwamba kuwa tajiri katika kundi la masikini ni hatari. Unakuwa tajiri katika kundi la watu walio na njaa. Utaendeleza utajiri wako kwa amani? Unakuwa na gari lako la kifahari lakini hakuna barabara nzuri ya kupita kutokana na ufisadi wako. Utajiri wako unaufurahiaje?

Wasomi hawa ndo wa kwanza kutoa kauli kuwa nchi bila wasomi haiwezi kuendelea na wakati huo wao ndo wanahujumu elimu nchini kwa kutotatua matatizo ya elimu yanayoikumba nchi yetu. Elimu ya Tanzania inazidi kushuka kila kukicha. Wasomi waliosomeshwa kwa pesa ya watanzania wote hawataki tena kujishughulisha na matatizo ya elimu nchini. Kutatua matatizo kwao ni kukaa vikao lukuki na kulipana posho kibao. Mwisho wa yote hakuna kinachofanyika. Hawa ndo wasomi tunaowategemea watuletee maendeleo.

Wasomi hawa ndo wa kwanza kukimbilia nje kwa matatibabu wanapougua. Sijui wanadhani hao wataalamu wa afya walioko nje wameshuka kutoka mbinguni! Hao wataalamu wamesomeshwa vizuri na serikali zao. Hospitali nzuri wanazoenda zimejengwa na wananchi wao kupitia kodi zao. Serikali zao zimewekeza vya kutosha kwenye elimu ambayo wasomi wetu wanaikandamiza.

Wasomi hawa ndo wanatoa lawama kali kwa wakoloni waliotutawala kwamba walikuja kutunyonya. Wakoloni waliotutawala ndo wanaotuonea huruma na kurudisha fedha zilizoibiwa nchini na wenzetu kutokana na mikataba ya kifisadi ya rada. Ni nani mkoloni mzuri basi? Anayekuambi kuwa umeibiwa na kukurudishia ulichoibiwa au anayejifanya mzalendo na kukuibia hicho kidogo ulicho nacho na kwenda kukificha ughaibuni? Ebu watanzania tutoe hukumu ya haki kati ya pande hizo mbili. Akili za wasomi hawa zinasikitisha sana.

Wasomi hawa ndo wanaolaumu na kudharau sana mababu zetu walioingia mikataba ya ulaghai na wakoloni akina Karl Peters. Kwamba walidanganywa kwa kuwa hawakuwa na elimu. Sasa leo wao wana elimu lakini wanaingia mikataba bomu kuliko ya enzi hizo. Bora hata wao waliingia mikataba hiyo wakiwa hawajui hata kusoma. Mikataba waliyoingia wao ni bora mara mia kuliko hii inayosainiwa sasa.

Tanzania ni nchi nzuri iliyo na raslimali za kumwaga. Kila mtu sasa hivi anajua ukweli huu. Lakini nchi yetu imebaki katika umaskini wa kutisha. Viongozi wa nchi hii ambao ni wasomi waliopewa madaraka ya kutumikia wananchi wamegeuka wanyonyaji na maharamia wakubwa wa uchumi katika nchi yao. Ni viongozi ambao hawana shida za maisha. Kiu yao kubwa ni utajiri wa kukufuru, tena wa wizi. Hata wasomi wasio kuwa viongozi wamekuwa hali moja. Wanafanya mashindano ya kutafuta utajiri wa haraka.

Kwa ujumla nashindwa kuona faida ya kuwa na wasomi wengi nchini. Enzi za uhuru wakati wasomi walikuwa wachache nchi haikuwa na matatizo ya ukosefu wa maadili ya kazi kama yaliyoko sasa baada ya kuwa na wasomi wa kumwaga. Je wasomi wa sasa hivi wamekuwa ni wasaliti wa nchi yetu? Wasomi wasio wanasiasa ni kawaida kuwashutumu na kuwanyooshea vidole wasomi wenzao ambao ni wanasaidia. Lakini nao kwa nafasi zao wanafanya hayo hayo ya wizi. Kwa nini wameamua kuiga tabia hiyo ovu? Wao watajitenga vipi na uozo huo? Wanachokilalamikia ni nini basi kama hata wao hawawezi kuridhika na vipato vyao halali? Nchi yetu inaenda wapi? Rais wetu ambaye ni kiongozi wa kwanza mwenye dhamana ya kuongoza nchi hii anawaza nini? Anafurahia hali hii? Haoni kuwa yeye ndo anachangaia matatizo haya? Yeye akiwa kwenye mstari bila kuweka upendeleo naamini kila mtu atageuka na kufuata mstari. Lakini kwa kuwa yeye anawachekea wezi basi wizi utaendelea tu. Hao wezi wanamwona hana nguvu za kuwafanya lolote. Ni kama nchi haina rais.

MUNGU ISAIDIE TANZANIA.


Ruberts Witta

mrtrusted@hotmail.com

Wasomi wa Tanzania wamegeuka mafisadi

MLOLONGO wa matukio ya ufisadi na ubadhilifu wa mabilioni pesa za umma, kwa asilimia 99 umefanywa na wasomi. Ripoti ya Richmond imeweka wazi jinsi wasomi walivyopangana kusalitii na kufuja kodi za Watanzania. Mikataba yote mibovu imetungwa na wasomi na kutiwa sahihi na wasomi. Makubaliano yote ya kishetani, hata yaliyofanyika Ulaya na Asia, yaliyofanyika hotelini, bafuni au sokoni yalifanywa na wasomi ili kuwaangamiza Watanzania masikini.

Tena baada ya kuipitia ripoti ya uchunguzi wa Ricmond, nilijaribu kupitia historia za maisha na usomi(CV) za wale wote waliotajwa katika kashifa ya ufisadi wa benki kuu na Zabuni ya Richmond. Kwa kweli nilipata mshangao mkubwa sana! Wengi wana digriii nyingi. Ni wasomi kwelikweli, wana digrii, 2, 3 4, hadi 5. Zimo digrii za uzamivu (PhD) pamoja na wingi wa vyeti vya heshima na uzoefu wa kazi wa kutosha.

Wamesoma sana hadi wakaitwa madokta, si kwa sababu ya kutibu watu, ni kwa sababu ya kubobea katika fani zao hadi wakatunukiwa shahada za uzamivu. Je, ni kweli watu hawa walisomeshawa na serikali kwa kodi za wananchi ili waje kudididmiza maisha ya wananchi?

Itakumbukwa kuwa wengi wa mafisadi hawa ambao ni wasomi sana walisoma enzi za Mwalimu Nyerere kwa kodi za wananchi. Yaani bure! Wamesoma sekondari hadi vyuo vikuu bila wazazi wao kutoa hata shilingi moja. Isitoshe Serikali ikaamua kuwapeleka ng'ambo (Ulaya au Marekani) ili wakapate maarifa waje kuwasaidia wananchi wenzao kubainisha suluhu za matatizo yanayaoikabili jamii.

Mwalimu alikuwa na lengo zuri sana, maana alijua wakisoma hadi ng'ambo watapata maarifa ya hali ya juu na watakuwa mstari wa mbele katika kuwaongoza watanzania wenzao kwenye maendeleo. Na wengi tilitarajia hilo toka kwa wasomi wetu! Serikali chini ya Mwalimu iliwasomesha hadi ngámbo ikijua, wasomi hawa watarudi na maarifa ya kutosha, watakuwa wabunifu, watakuwa na ujuzi na watawaongoza wenzao kwenye neema na sio ufisadi na utapeli mkubwa uliopo sasa.

Lakini wengi wao waliosomeshwa na Serikali kwa pesa za umma, wamegeuka wezi wakubwa wa mali za umma. Mafisadi wakubwa, wavunja sheria na kanuni za serikali wakubwa wanazodai wanazisimamia. Je wasomi hawa walikwenda kusomea digriii za ufisadi na wizi huko ng'ambo?

Inashangaza sana kuona wasomi ambao wangekuwa mstari wa mbele kutafuta na kubuni njia za kutatua matatizo ya wananchi kwa kutumia maarifa waliyopata darasani, wanageuka mzigo mkubwa kwa Taifa na wananchi. Wengine tangu wapate digrii au uprofesa hatujawahi hata kuona kazi zao hata siku moja. Wamebaki kutamani vyeo vikubwa tu, mishahara mikubwa tu, posho kubwa, ofisi kubwa na starehe kubwa. Wao wamegeuka mzigo kwa Taifa na kwa jamii yetu. Maana jamii inajitahidi kulipa kodi ambazo zinakwenda kulisha wasomi hawa waliojipenyeza kwenye taasisi nyeti za Serikali. Wakigawiana posho na marupurupu kwa kukaa tu kwenye viti vya kuzunguka na kwenda Ulaya kutalii, huku kodi za Watanzania zinaangamia kwenye hoteli kubwa Ulaya na Marekani.

Kazi zao ofisini zimebaki zinafanywa na wasaidizi wao wenye elimu duni lakini wachapa kazi. Wakirudi kutoka ziara za Ulaya hakuna walichojifunza huko bali utamaduni wa Kizungu; uchoyo, ubinafsi, utapeli wa kutumia kalamu na kusifia maendeleo ya wenzetu huko Ulaya kwa lugha ya Ulaya ili Watanzania wasielewe na wawaone wa maana sana. Kweli wasomi wa Afrika!

Wapo wasomi wengi wanaoisaliti jamii yao kwa kushindwa hata kuieleza nini cha kufanya. Tena wengine walipopata tu shahada za juu na kurudi kutoka Ulaya hawapendi hata kuwaona wananchi masikini, hawaendi hata kwao. Wanajifugia tu ofisni huku wakicheza michezo ya kwenye kompyuta na kusoma barua pepe. Siku inaisha, mwisho wa mwezi wanahitaji mishahara mikubwa.

Wapo wengine wamejipenyeza kwenye siasa na kuwa mawaziri au wabunge. Lakini wapo huko kwa minajili ya kushibisha matumbo yao tu. Hawazijui hata sera wanazosimamia na kuziimba majukwaani. Siku zote wanapenda kuitwa waheshimiwa, huku uheshimwa wao ukiwa hauonekani, na sijui kama utakuja kuonekana.

Nilishawahi kuandika kuwa wapo maprofesa wetu hapa wamesomea uhandisi wa madaraja, lakini hawawezi hata kujenga daraja la kupita kuku wake nyumbani. Wanaajiri watu wa kuwajengea madaraja ya kupita mifugo yao. Serikali ikitaka kujenga madaraja inaingia gharama tena ya kuagiza Wachina, Wajapani au Wahindi waje kutengeneza miundombinu yetu.

Wachina wanavuna mabilioni ya pesa, wanarudi kwao na utajiri mkubwa. Kweli wajinga ndio waliawo. Je, wasomi wa namna hii kweli wanafaa kuheshimika katika jamii? Inakuwa afadhali kuwaita 'waheshimiwa 'watumishi wao wa ndani wanaoweza hata kufua nguo na kubuni bustani nzuri ya kupendezesha mazingira ya nyumbani.

Pia wapo wasomi wengi ambao wanajiita wataalamu wa tafiti na hata wengine wanaiita wanaharakati wa haki za binadamu. Kweli, wapo wachache makini sana na wachapa kazi sana, nawapongeza kwa kazi zao nzuri. Lakini wengi ni matapeli wakubwa walioanzisha NGO za mifukoni zisizo na kichwa wala miguu.

Wamegeuka vibaraka wa Wazungu wanaowatumia kuharibu mila na desturi za Waafrika kwa kutoa mafundisho potofu yanayaozitukana mila zetu na kuukumbatia Uzungu uliojaa uchoyo na ubinafsi. Na kwa sababu wanapatiwa pesa na Wazungu kampeni zao za kuangamiza watoto wetu zinaonekana kila siku kwenye vyombo vya habari. Eti kulaaani mila na desturi za Kiafrika zilizotukuka. Hawa ni mawakalai wa Wazungu na si wasomi. Tena hawa ni kipingamizi kikubwa cha maendeleo ya Taifa. Maana hakuna taifa lisilo na utamaduni wake. Na siku zote hawataji hata sehemu ndogo ya utamaduni wa Kizungu kuwa ni potofu. Yote ya Wazungu, hata kama ni kinyesi ni mema kwao. Na wanasambaa vijijini kuwapotosha Watanzania ili wadharau Uafrika na mila zao, wakumbatie Uzungu na laana ili ziangamize vizazi vyao na rasilimali zao zije kuuzwa kwa Wazungu wanaoitamani sana Tanzania.

Hawa nao wamesomeshwa kwa kodi zetu. Leo wamegeuka kuisaliti jamii, tena wapo wengi na wanaonekana kila siku. Wanatukana mila za Watanzania huku Watanzania huko vijijini wakiwa na shida za barabara, dawa, shule, walimu, soko, maji, umeme. Matatizo haya wanayaacha kando kwa sababu wao wanaishi Dar es Salaam au Arusha ila wakampeni mila potofu. Huu kama si usaliti mkubwa ni nini? Watu wana shida ya umeme, maji, dawa, wewe unakwenda kuwaambia waache mila zao, kama si ukichaa ni nini?

Kibaya zaidi, unamkuata msomi anakwenda vijijini kufanya utafiti juu ya hali za wananchi. Wananchi kwa ridhaa yao wanajitolea kumpa taarifa muhimu wakidhani atazifanyia kazi. Tena taarifa za shida na mahitaji yao. Wanampa taarifa nyingi kwa lugha yao ya Kiswahili. Lakini yeye kwa sababu ana ajenda yake, anachukua taarifa hizo kwa Kiswahili, anakwenda kuandika ripoti ya utafiti kwa Kiingereza, tena Kiingereza kigumu sana halafu harudishi mrejesho kwa wananchi waliompa taarifa. Hapa anamdanganya nani? Kwa nini uandike ripoti kwa Kiingereza wakati wananchi wamekupa taarifa kwa Kiswahili na lugha ya Taifa ni Kiswahili na wananchi wote wanaongea Kiswahili? Hii si ni kukata mawasiliano ya jamii wanayoimba kuitetea? Huu ni uongo, uzandiki na utapeli kwa Watanzania. Ripoti ya matatizo ya uhaba wa zahanati wa watu wa Kijiji cha Matare, Sikonge Tabora unaiandika kwa Kiingereza ili iweje?

Ni afadhali hata mapendekezo hayo ukayaandika kwa Kinyamwezi na Kiswahili ili wananchi waelewe. Na kwa nini matokeo ya tafiti inakuwa rahisi sana kupelekwa Ulaya kuliko kwa walengwa wenyewe? Huu ni zaidi ya ufisadi. Tena ni laana kwa Taifa. Ndio maana yapo maelfu kwa maelfu ya ripoti za kitafiti, yamekaa tu makabatini hayana msomaji. Tena hata wananchi waliotoa taarifa hawajui kinachoendelea. Huu kama si uzandiki ni nini kwa wasomi hawa?

Matokeo yake ripoti nyingi za kitafiti zimelundikwa kwenye mashelfu tu, hazitumiwi na wananchi wala wasomi hao matapeli. Wanafanya kazi ya kuwafurahisha wafadhili wao tu na si kuwaendeleza Watanzania. Hawa ndio wasomi wetu. Wananchi wanaendelea kuteseka kwa shida zisizoisha ambazo mbinu za utatuzi wake zimeandikwa kwa lugha ya uatapeli (inayojulikana kama lugha ya kitaalamu). Wakati huo huo tuna wingi wa rasilimali na wingi wa rasilimali watu wakiwemo wasomi. Je huu sio usaliti mkubwa?

Nne, unawakuta wasomi wanakwenda kuhutubia wananchi vijijini, wananchi wanajua Kiswahili na lugha za kikabila. Lakini wasomi wetu wanajitahidi kuwavuruga wananchi kwa kuchanganya lugha za kitapeli ambazo wao wanaziita lugha za kitaalamu.

Katika hotuba moja unakuta amechanganya maneno mengi ya Kiingereza au Kifaransa huku akijua asilimia 99 ya wanaoamsikiliza hawataelewa lugha hiyo. Je, hapa wanaficha nini wasomi wetu? Na ni kweli hawajui Kiswahili? Au ndio kasumba ya kukidunisha Kiswahili na kukuza utamaduni wa Wazungu wa Kiingereza? Tena ikiwa kiongozi anahitaji kutoa taarifa za maendeleo ya mradi fulani, hapo ndio Kiingereza kinaibuka maradufu.

Hata Wazungu wenyewe wanashangaa. Maana wengi wazungumza Kiswahili bila hata kuchanganya na Kiingereza, japo si lugha yao. Hata Katiba ya nchi inahimiza watu wote kuheshimu na kulinda utamaduni wetu. Lakini wasomi wetu ndio vinara wa kuvunja utamaduni wetu na kubeza kila cha Mtanzania kwa sababu eti walikuwa Ulaya. Au watapatiwa pesa na Wazungu. Huu kama si uzandiki ni nini? Na jamii iwaweke wapi wasomi wa namna hii?

Wazungu walikuja kwetu, wakatutawala na kuchukua utajiri wetu, mila zetu wakaziacha. Sisi tunakwenda Ulaya badala ya kuchukua utajiri wa maarifa na mali za huko, tunachukua laana na kuileta nchini mwetu. Tunarudi vichwani hatuna kitu mbali na utamaduni wa huko tu. Tutapata maendeleo kweli kwa mwendo huu?

Inashanagza sana, hata wala rushwa na watoa rushwa wakubwa ni wasomi. Tena inawezekana wamejiundia na Taasisi ya Kulinda Kula Rushwa (TAKUKURU) ili iwalinde wasomi na iwaaangamize wananchi masikini. Ndio maana wakati fulani rushwa ya wasomi ikabarikiwa na kupewa jina takrima. Na wasomi wakasambaza rushwa kila mahali, hasa wakati wa uchaguzi. Wakapigiwa kura wakaingia madarakani huku wakiwa wachafu mno. Sasa wanajitahidi kuiba kodi za wananchi ili kufidia mamilioni waliyotapanya kwenye uchaguzi.

Wananchi wanawajua na kuishi nao. Lakini kwa sababu wameshika kwenye mpini na wananchi masikini wameshika kwenye makali, wananchi wakaamua kunyamaza tu na kutukutia moyoni. Nani asiyeona wasomi wanavyotoa rushwa kila leo katika mikataba, uchaguzi, ununuzi na kampuni binafsi za uvunaji misitu? Hao ndio wasomi waliosomeshwa kwa kodi za wananchi masikini sasa wamegeuka mzigo kwa Taifa. Nao ndio wengi, tena wanabebana migongoni wakipata madaraka na kufungana mbeleko ili wazile vizuri kodi za wananchi masikini wasiosoma. Hadi lini Tanzania?

Nimalizie kwa kuwapongeza tena wasomi wachache wanaotumia maarifa, ujuzi na uwezo wao wa kufikri na kutenda kwa manufaa ya jamii nzima. Hawa wapo lakini ni wachache sana. Wananchi wanafaa kutambua umuhimu wa msomi si kwa kuangalia wingi wa vyeti bali kwa kuangalia 'nini anafanya' kuisadia jamii kuleta maendeleo. Wengine, tena wengi sana wana wingi wa vyeti vya ulaghai na ufisadi tu. Hawana maarifa yeyote. Wakiwa kwenye baa utadhani ni wehu. Wanaongea lugha chafu, wanajisaidia hovyo, wanarudi kulala na kusubiri mishahara minono na posho za safari za nje. Wapo wengi mno. Hawa inabidi tuwaogope kama ukoma wanapokuja kuomba kura ili wajipenyeze serikalini. Uprofesa, udokta, uinjinia na hata utabibu haupimwi kwa wingi wa vyeti walivyotoka navyo Ulaya, bali unapimwa kwa matendo yao ya kitaalamu. Wapo maprofesa digrrii zao zinaishi kwenye baa tu. Wanatambulika kwenye baa na gesti tu. Hawajulikani hata kwenye mtaa wao. Ila wahudumu wa baa na gesti ndio wanawajua kuwa ni maprofesa au wabunge. Kwenye baa wanajulikana
kwa sababu ndipo wanapotumia akili zao nyingi, muda wao mwingi, na fedha zao nyingi. Kwenye jamii hawajulikani kwa sababu hakuna wanachokifanya na wala hawana lolote la kufanya, japo wamesomeshwa kwa kodi za jamii zao.

Wapo wasomi wengi wanasikika na kuonekana kwenye misafara ya rais tu, na sahihi zao zinaonekana magazetini lakini ukiuliza kazi zao hazijawahi kuonekana. Tuendeleee kuwakumbatia wasomi hawa wanaoliangamiza Taifa hadi lini? Jamii ya Watanzania iendelee kuwaamini wasomi wa namna hii hadi lini? Watudanganye na kutuhadaa huku wakila kuku kwa mrija kwa kodi zetu hadi lini?

Nchi za wenzetu usomi haupimwi kwa wingi wa digrii ya mtu. Na wala kuwa msomi hakufanyi mtu aheshimike. Wenzetu wanaheshimu juhudi za mtu na mchango wake katika maendeleo ya jamii yake taifa, na majirani. Ndio maana hata mtu mwenye elimu ya msingi akigundua kitu au kuunda kitu kipya na muhimu anapewa hadhi kubwa hadi kufa kwake.

Ndio maana hadi leo tunawasoma akina Newton, James Watt, Galileo, Abbot na wengine wengi wanaoheshimika siku zote kwa sababu ya mchango wao kwa maendeleo ya mataifa yao na dunia nzima. Wengi wa wataalamu walioibadili dunia hawakuwa hata na elimu ya sekondari, lakini kwa mchango wao wamekufa na wingi wa shahada za heshima na kumbukumbu zao hazitafutika katika ulimwengu huu.

Wanatambuliwa kwa kazi zao si kwa wingi wa vyeti vyao na kujivika uheshimiwa feki. Tanzania tunao mfano wa wazi. Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere hakuwa na tamaa ya utajiri wala sifa za ajabu ajabu. Ameitumikia nchi kwa juhudi kubwa tena bila kujali anapata nini. Ndio maana ulimwengu mzima unamkumbuka hadi leo.

Tena karibu vyuo vikuu 10 maarufu duniani vilimzawadia shahada za heshima kwa sababu ya mchango wake mkubwa kwa Taifa na Afrika kwa ujumla. Nani asiyelijua hili? Mwalimu amekufa na wingi wa shahada zisizohesabika, lakini hakutaka hata kuitwa daktari wala mheshimiwa. Hakutaka kuishi kwenye makasri wanayoishi mafisadi wa leo. Amekufa akiwa Butiama analima kwa jembe la mkono, tena si kwa kuweka watumishi, yeye mwenyewe kwa mkono wake!

Nyerere ndiye msomi na mheshimiwa. Tutamheshimu na kumkumbuka hadi mwisho wa dunia. Tuliobaki nao sasa wengi ni wasomi bandia na wasanii tu. Ripoti ya Richmond imedhihirisha ukweli huu unaojaribu kufichwa siku zote. Wasomi hawa hata wakifa, baada ya wiki moja tu majina yao husahaulika kabisa.

Ninukuu kauli ya aliyekuwa Rais wa Marekani, Abraham Lincoln: "Unaweza kuwahadaa baadhi ya watu muda wote, na watu wote muda fulani. Lakini huwezi kuwadanganya watu wote wakati wote." Tumechoka kudanganywa na kuibiwa na hao wanaojiita wasomi. Wananchi tuamke. Tudai haki zetu na hata kupinga mambo yaliyo kinyume cha maendeleo yetu. Tuliadhibu hili tabaka la wasomi uchwara waliojenga tabaka la kifisadi na kukamata taasisi zote nyeti za Serikali. Tuwaunge mkono wasomi wachache wenye nia ya kuendeleza nchi. Tukiamua tunaweza. Na nguvu pekee ya kufanya hivyo ipo katika uchaguzi. Yaani kupiga kura ya 'hapana' na kugomea michango ya ajabu ajabu inayotutaka tuuze kuku, huku mafisadi wakizoa mabilioni ya kodi zetu kushibisha matumbo yao. Mungu ibariki Tanzania.

0773960606

Wasomi wetu hawathaminiwi na wanasiasa

Majira ya saa moja jioni ya leo, nilikuwa na rafiki yangu maeneo ya Mlimani City, Dar er Salaam tukijadili masuala ya kimaisha na kisiasa sawia. Katikati ya mazungumzo yetu, rafiki yangu huyo aliibua hoja ambayo ilituingiza katika tafakuri nzito. Alinieleza kuwa jirani tu na eneo tulilokuwepo kulikuwa na pilika pilika na hamasa zisizo kifani za watu wakijiandaa kuingia Mlimani City Conference Hall kushuhudia utoaji tuzo za Kilimanjaro Music.

Akikubaliana na kauli iliyopata kutolewa na Ernesto Che Guavara, mara baada kutoka kusaidia harakati za ukombozi nchini Congo, kuwa Waafrika kwa hulka zao, wanapenda sana starehe,waoga na wasio tayari kujitoa mhanga kwa ajili ya kujikomboa wao wenyewe, rafiki yangu huyo,alitanabaisha kuwa tabia na matendo ya wanasiasa wetu,kama zao la jamii yetu, yanaweza kuthibitisha dai hili:

Wakati Mhadhiri mwandamizi wa UDSM, Prof. Chachage S. Chachage, anafariki dunia, wakati huo yeye akiwa mwaka wa mwisho Mlimani, hakuona viongozi wa ngazi za juu wa kisiasa na kiserikali wakati wa kuaga mwili wa marehemu Chachage katika ukumbi wa Nkurumah. Aidha, kila mwaka UDSM hufanya kongamano la kumkumbuka Chachage, lakini viongozi wetu wa kisiasa na kiserikali,kama kawaida yao, hawahudhurii kabisa.

Nikakumbuka matukio kadhaa ya miaka ya karibuni:
Prof. Haroub Othumani aliaga dunia, wanasiasa na viongozi wachache wa serikali walihudhuria mazishi. Hali ilikuwa hivyo pia siku chache baada ya kifo chake, Jumuiya ya Wanataaluma wa UDSM, UDASA ilipoandaa mhadhara wa kumbukumbu ya marehemu.

Mwaka mmoja, baada ya kifo chake, UDASA waliandaa tena mhadhara wa wazi kumkumbuka marehemu na kama ilivyo ada yao, wanasisa na viongozi wetu wa serikali hawakujitokeza.

Mwaka 2010, Prof. Jwani Mwakyusa wa UDSM alifariki dunia, na mwili wake uliagwa katika ukumbi wa Nkurumah. Mbali na Dkt. Harison Mwakyembe na Prof. Mark Mwandosya na wanasheria wengine waandamizi, viongozi wetu wengine wa kitaifa, kwa mara nyingine tena, hawakuonekana. Hali ilikuwa hivyo pia katika misiba ya Prof. Christant Kamuzora, Prof. Sam Mushi, Dkt. Ndibalema Alphonce na wengine wengi.

Hivi karibuni, taifa limempoteza ndugu yetu mpendwa, Steven Kanumba ,ambaye kwa kweli ana mchango mkubwa katika kukuza sanaa yetu kimataifa. Sote tumeshuhudia jinsi viongozi wetu wa kisiasa na kiserikali walivyojitokeza kwa wingi kabisa na kikamilifu kabisa nyumbani kwa Marehemu, katika kumuaga na hatimaye katika mazishi yake.Sitaki nieleweke kuwa ninapinga viongozi wetu kuhudhuria mazishi ya wasanii wetu.

Hoja yangu ni kuwa kwanini sasa inaonekana ni kawaida, wanasiasa na viongozi wetu na Watanzania kwa ujumla wetu tunakuwa wazito kuhudhuria katika misiba ya Wanataaluma wetu ambao wamepata kutoa mchango mkubwa katika maeneo yao ya kitaaluma ikiwemo kuandaa wataalamu mbalimbali na michango yao katika kuleta maarifa mapya kupitia tafiti, machapisho na vitabu vyao?
Kwanini tunaenenda hivi? Na kwanini tusibadilike?

Karibu tujadili.


Usitegemee maendeleo kwa Taifa la watu wanaokamata madaraka kwa kuhonga, kupewa vimemo, na kuteuliwa kutokana na kuwa na ushikaji au nasaba na Rais, au mwandamizi mwingine.

Wasomi wapo, hilo halina ubishi, tena ni wengi.

Shida ya kukosekana kwa maendeleo ni kwamba hao viongozi wa hapo juu niliowasema wanakosa guts za kusimamia effectively utendaji ndani ya serikali na mashirika kwa vile wao wenyewe ni toothless, hawapo pale kwa qualities zinazotakiwa.

Pia wataalam siku hizi wanaongozwa na wanasiasa.

Ulishawahi kusikia mwanasiasa anaagiza wataalamu wa kuleta mvua wewe? kama hujasikia hiyo ipo Tanzania.
Katika medium na context kama hiyo unategemea wataalamu na wasomi wana nafasi gani?

Ni mara ngapi umesikia loggerheads kati ya ushauri wa kitaalamu na mapendekezo ya wanasiasa?

Una habari UDOM imejengwa kwa matakwa ya wanasiasa?

Na unajua jinsi sasa wananchi watakavyoanza kulipia gharama za maamuzi hayo ya mwanasiasa? Je wataalamu na wasomi hawakuwepo? na je wangekuwana guts za kumstopisha mwanasiasa huyo asiliingize taifa katika maisha ya mashaka ya kubadilishiwa taratibu za mafao ya akic zao?

Wasomi wetu wamekatwa miguu na mikono short n clear.
 
Poor inference (generalization)UFISADI hauna ELIMU. Unataka kusema nini sasa? Kama tatizo la ufisadi ni elimu basi suluhisho liwe ni wote kuwa wajinga! Think twice, tatizo haliwezi kuwa elimu/usomi.
 
Too general in my view..kuna wengi wamerudi na kutumikia Tanzania mpaka kufa (Ubalozini, UDSM na secta mbalimbali)..na wananchi tukawashukuru kwa kusema "mwone kasoma mpaka phd kafa hana kitu"..

I rest my case....
 
Jamani mwandishi ametoa upande mmoja wa shilingi,upande ambao unaonesha wasomi wa Tanzania wamegeuka mafisadi.Ingilia idara zilizosheheni rushwa mfano polisi,mahakama,TRA NK. Ni wasomi waliobobea ndio wanasababisha hii outrcry.

Mind You, sio wasomi wote wamegeuka mafisadi. Angalia EPA,RICHMOND,Vogue la Mbowe,BUZWAGI,BULYANHULU NK. Ni wasomi 99% ndio waliohusika.

Therefore wasomi wa Tanzania wamegeuka mafisadi.
 
Ni maoni mazuri lakini umejumuisha sana.

Jaribu kuelezea kidogo ukiweka vielelezo va hoja yako.

Ukiambia labda msomi mmoja hivi ananufaika na mfumo mzima wa Virsual Cirle, ambapo ni watu wachache katika nchi ndio wana nafasi ya kufaidika na mfumo wa kuhujumu uchumi wa nchi,mimi ntakuunga mkono.

Lakini unanikumbusha wakati nikiwa shule ya bweni ambapo wakati wa kuchukua barua assembly watu tulikuwa tukitaniana kwamba kijiji kilichokutuma kusoma kinataka maelezo ya maendeleo ya shuleni.

Sasa labda wananchi wanajukumu la kuwahoji wabunge kwamba wamewafanzia nini tangu wawape ridhaa ya kuwawakilisha bungeni.
 
poor inference (generalization)UFISADI hauna ELIMU. Unataka kusema nini sasa? kama tatizo la ufisadi ni elimu basi suluhisho liwe ni wote kuwa wajinga! Think twice, tatizo haliwezi kuwa elimu/usomi.

Kwenye kundi la mafisadi kuna wasomi na wngine ni ngumbaru tu na vyeti vyao vya bandia. Kuwaweka wasomi wote kwenye kundi la mafisadi si sawa.
 
Kwenye kundi la mafisadi kuna wasomi na wngine ni ngumbaru tu na vyeti vyao vya bandia. Kuwaweka wasomi wote kwenye kundi la mafisadi si sawa.

Heshma mbele, nakubaliana na wewe, tatizo siyo elimu. MAFISADI ni watu WABINAFSI wanaopata FURSA ya kufanya uisadi. Hiyo FURSA ndiyo inaweza kuwa ni elimu/nafasi aliyonayo (cheo)/Madaraka, ukaribu na wenye madaraka, nguvu ya pesa nk.
 
Mzindakaya kasoma?

KWANI NAYE YUMO .....! BASI KAMA KAWA TUMUANGUKIE....!
AU TUNAMUOGOPA KWA........ (kaulozi?)NASIKIA NA HUYU NI KATI YA WALE WATU WALIOWAPITISHA WATOTO WAO KWENYE VIJINAFASI....(sijui ubunge,sijui nec?)
HAPA HAPENDWI MTU NI TANZANIA TU.....NA UTAIFA......!
UKILETA UKUWADI WA KUWATETEA MAFISADI UNAANGAMIZA NCHI YAKO ILA UNAJENGA CHAMA CHAKO......! JF BADILIKA....! BE FLEXIBLE....!
 
Bwana Gervas Zombe eeh, labda nikukumbushe tu kuwa Mwalimu Nyerere alikuwa na shahada ya uzamili, hivyo naye alikuwa msomi hata kabla ya kutunukiwa shahada za heshima za udaktari. Huo mfano mmoja tu unaodhihirisha kuwa madai yako kuwa wasomi wetu wote wamegeuka kuwa mafisadi siyo kweli.

Kama walivyotangulia kusema wengine, kusoma au kutokusoma siyo chanzo cha ufisadi. Ufisadi mizizi yake ni kwenye hulka au tabia ya mtu, watu hawasomei ufisadi!
 
Mitomingi

Labda mimi nina makengeza, ila hii kazi nimeipenda.

na ninadhani JF imejaa wasomi na ndio maana tunajaribu kuficha ukweli.

hata mimi ninarudia maneno ya mwandishi anonymous

wasomi waoga wa inchi yangu
siku moja watawekwa kizimbani
tena na wananchi wa kawaida
hawataulizwa kuhusu mavazi yao
hawataulizwa kuhusu fedha zao
hawataulizwa kuhusu falsafa zao za kigiriki
wataulizwa
mlifanya nini wakati maskini wanaumia,
siku ambayo furaha na huruma ya maisha ilikuwa mbali nao.

msomi anategemea kufanya kisomi ndio maana yule M/kiti wa Kenya wa tume ya uchaguzi alitakiwa kunyanganywa shahada ya sheria na UDSM yenyewe wakiongozwa na prof. Othman.

iweje leo tuwaongelee akina Dr. Hosea na Hon. Myika kuwa elimu yao wameihaibisha, watu waanze kupiga miruzi ya kejeli? kwa sababu sio wakenya. uo ninaona ni uzandiki na ulimbukeni.

na hayo ndiyo yanayotuponza hapa Tanzania.

what i know is that Education is to liberate a person and the society. sasa kama hawa watu na elimu yao hawajawa liberated au wameshindwa kuliberate society what next name do they reserve?

au tulisoma hii elementary education tofauti.
 
Last edited by a moderator:
SERIKALI KUBEZA MCHANGO WA WASOMI, ISHARA YA KIFO

Kama ambavyo sasa imezoeleka, kwa mara nyingine mwaka huu, Kumbukizi ya miaka kumi na moja ya kifo cha Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Oktoba 11, imepita kimya kimya bila Serikali kuinua macho wala kuipa uzito unaostahili.

Si Kiongozi wa Serikali wala wa Chama tawala kitaifa, aliyetoa hotuba kuwakumbusha Watanzania nafasi ya Mwalimu katika kuleta uhuru wa nchi hii, mshikamano wa kitaifa na huduma za kijamii kwa usawa wa watu wote, ambayo ni misingi mikuu aliyotuachia, lakini imeachwa kwa uzembe na kutojali kuanza kubomoka.


Hilo ni jambo lililo dhahiri, kwa sababu, kwa nchi iliyokosa maadili ya kitaifa, sera na dira ya uchumi, mshikamano na umoja wa kitaifa; kwa wadhalimu, kupigia debe fikra za Mwalimu ni kaa la moto lenye kuunguza. Kwa baadhi ya Viongozi wa leo, wanafiki, wenye kuhubiri wasichokiamini na kuamini wasichokihubiri, hawawezi kuuhadaa umma kwa kuzungumzia kwa maneno pekee, "neema" ya fikra za Mwalimu bila umma kuwatemea mate usoni.

Na katika kuuhadaa umma kwamba Mwalimu anakumbukwa; na ili kuficha lengo na kusudio lao la kufifisha fikra hizo, Kumbukizi la kifo cha Baba wa Taifa limeunganishwa na Sherehe ya kuzima mwenge, ambazo zinapewa umaarufu zaidi badala ya Kumbukizi hilo.

Ni kwa sababu hii kwamba, mwaka huu ni Wanataaluma wa Chuo Kikuu cha Dar Es Salaam [UDASA] pekee ndio waliojitosa kuitisha na kushiriki kwenye mhadhara/mdahalo wa kujadili fikra za Mwalimu katika mazingira magumu, ikiwa ni pamoja na wanachuo vijana kuongezewa siku za likizo wasiweze kushiriki mdahalo huo na uchaguzi mkuu wa mwaka huu.

Yaliyosemwa na Wasomi hao ndiyo lile kaa la moto ninalosema, ambalo wanasiasa wanafiki hawawezi kuuambia umma kiasi kwamba wangependa hiki kinachoitwa "Nyerere Day" ifutiliwe mbali.

Ukweli uliotawala mdahalo ni ule kwamba, Serikali ya sasa madarakani [na hata zilizotangulia] si sikivu, Chama na Viongozi wamekiuka misingi iliyowekwa na mwasisi huyo, kama vile utaifa, uzalendo na miiko ya uongozi.

Mmoja wa Washiriki, Dakta Azaveli Lwaitama alisema, ni vigumu kuwa na taifa lenye uzalendo mahali ambapo kuna tofauti kubwa ya kipato miongoni mwa wanajamii kama inavyotokea sasa nchini. Na katika hali iliyoonyesha kupandwa jazba, msomi huyo alisema: "Naomba kukipa pumziko la milele Chama hiki [CCM] ingawa mimi mwenyewe ni mwanachama wa chama hiki".

Dakta Lwaitama aliweza kubaini kero inayokera wanachama wengi [wa CCM] sasa na kuahidi alisema: "Matajiri waliopata fedha kwa rushwa wakihama, ndiyo [nami] naweza kurudi CCM".

Ni kiapo cha usomi kwamba: "Nitafuatilia ukweli popote utakaponipeleka"; na ndivyo Wasomi hao walivyothibitisha kwenye mawasilisho yao kwenye Kumbukizi hiyo.

Lakini Profesa Mathew Luhanga [aliyewahi kuwa Makamu wa Mkuu wa Chuo hicho kwa miaka 16] alikuwa mwepesi kubaini kuwa, "Wasomi wengi sasa wamekuwa waoga kukemea Viongozi wanapokosa, wameshindwa kuwajibika kwa jamii kama vile kutetea haki na maslahi ya wengi nchini; wamekuwa watu wa kujikomba kwa wanasiasa".

KunaHiyo ni tuhuma nzito lakini iliyosheheni ukweli. Isingekuwa hivyo, Bunge lisingepitisha Muswada wa Sheria kupiga marufuku siasa za wanafunzi Vyuo Vikuu mwaka 2005 na hali ikakalika, eti kwa sababu tu Wanafunzi walijitambua na vyama vya siasa wakati wa Uchaguzi Mkuu wa 2005.

Isingekuwa hivyo, Wanafunzi wasingenyimwa haki yao ya Kikatiba ya kushiriki katika Uchaguzi Mkuu mwaka huu, kwa tarehe ya kufungua Vyuo kusogezwa mbele kwa siku nne zaidi kwa mbinu. Kinacholengwa wanakijua wanafunzi hao, lakini wanaogopa kusema ukweli [wasije kunyimwa mikopo?]; kwa hofu hiyo wameasi viapo vya usomi.

Kitendo cha Bunge kupitisha Muswada kuzuia harakati za kimapinduzi Vyuoni, kinatukumbusha enzi za ukoloni ambapo Serikali na mfumo wa elimu haukuruhusu siasa za Wanafunzi [Student Politics] vyuoni, kama tu ambavyo Serikali haikuruhusu demokrasia kufanya kazi kwa watawaliwa.

Elimu ilitolewa katika mfumo na mazingira ya kudumaza akili na fikra za Mwafrika ili aendelee kubakia kikaragosi tegemezi katika gurudumu la unyonyaji, akitenda na kutekeleza "maagizo" ya wenye mfumo kama roboti.

Serikali tafsiri yake ni taasisi ya kijamii inayotokana na migongano ya matabaka yasiyoshabihiana ambapo tabaka lenye nguvu [watawala] ndilo lenye maamuzi kwa kutumia nguvu kulitawala tabaka nyonge, na kulinyonya kwa kutumia Sheria linazotunga.

Madhumuni yote haya ni kuliwezesha tabaka hilo lenye nguvu kujijengea, kulinda na kuimarisha matakwa na nguvu zake za kiuchumi kisiasa na kiutamaduni, dhidi ya na kwa hasara ya watawaliwa [Frederick Engels: Origin of Family, Private Property and the State].

Kwa Serikali kupiga marufuku siasa katika Vyuo Vikuu, maana yake ni kuinyima jamii ya kisomi haki ya kushiriki katika kuhoji au kutoa mwelekeo kwa jamii ilimo na kufanya mgongano ndani yake isipate ufumbuzi kwa manufaa ya kitabaka.

Jumuiya ya Wanafunzi wa Vyuo Vikuu na Wasomi ni sehemu ya jamii ya Kitanzania inayoguswa na yale yanayotendwa na Serikali. Isitoshe, jumuiya ya Wasomi ni sehemu ya jamii yenye upeo wa kuona mbali kwa nyenzo ya elimu, na hivyo ina wajibu kuimulikia njia jamii na kuielekeza njia sahihi ili iweze kufikia malengo na matarajio yake. Unapowazuia wasomi kuhoji kwa uhuru mwelekeo wa jamii yao unaua jamii.

Vijana wasomi sio watu wanaoishi katika ulimwengu wa kufikirika; wala hawatawaliwi, kutekwa au kufungwa na minyororo ya kibiashara, ubeberu, ubaguzi wa kiuchumi na kijamii, kama walivyo baadhi ya baba au babu zao.

Hawatawaliwi na mawazo ya Ubwana na Utwana; au majivuno kwamba "baba yangu alikuwa Mfalme, Waziri au Mtemi, kwa hiyo na mimi lazima niwe". Hawatawaliwi na fikra za uhuru wa bendera, njozi za ukuu wa kufikirika, wala dhana ya kuwagandamiza na kuwanyanyasa wengine chini ya uficho wa "demokrasia" batili au sera huria za bandia na utandawazi, unaopewa jina la "Ushirikiano [mwema] wa dunia" badala ya jina halisi la "ukoloni mamboleo" na "utandawizi".

Wajibu wa vijana Wasomi ni kuchambua na kuhoji mhimili wa kilimwengu na sera ambazo zimeshikilia hatima ya maisha ya wengi. Wanahoji pia kama kweli mhimili huo na sera za uchumi za wakati wao ni sahihi kuweza kutumika katika ulimwengu wa leo na kesho kwa manufaa ya walio wengi, wakiwamo wao wenyewe.

Ule ukweli kwamba wao hawana vyeo kuweza kufungwa nira na mfumo wa sasa, ni nguvu tosha kwao kuweza kuitazama jamii na kutenda kwa mawazo na akili iliyo wazi zaidi, ikizingatiwa pia kwamba wengi wao wanatoka katika familia na jamii masikini. Kwa hiyo hawana cha salia Mtume kwa anayechezea haki ya jamii.

Ni kwa sababu hii kwamba, kwa miaka mingi Wanafunzi wa Vyuo Vikuu wameshikilia nafasi ya kuwa upande wa Wakulima na Wafanyakazi katika harakati za kuikomboa jamii ya Kitanzania kisiasa, kiuchumi na kijamii.

Kwa mfano, ni makosa kudhani kwamba maandamano ya Wanafunzi wa Vyuo vya elimu ya juu "kupinga" kujiunga na Jeshi la Kujenga taifa, Oktoba, 22, 1966, yalikuwa potofu au jeuri ya kisomi. Ukweli ni kwamba Wanavyuo hao hawakuwa wakipinga JKT; walichokuwa wakilalamikia ni wao kukatwa mishahara [baada ya masomo] kwa njia ya kujifunga mkanda kwa jina la Ujenzi wa taifa, wakati watawala waliendelea kujiongezea mishahara na marupurupu katikati ya jamii masikini. Na pale Mwalimu alipoyaelewa madai yao, kwa kubaini kwamba alikuwa amepotoshwa na vyombo vyake, alipunguza sawia mishahara ya watawala, akianzia na wake mwenyewe; na wengine wakalazimika kuonyesha mfano kwa kujiunga na Jeshi hilo angalau kwa muda mfupi. Katika sakata hilo, wanavyuo walishinda. Na ili kuutafsiri ushindi huo kwa usahihi, Mwalimu aliandika na kutangaza Azimio la Arusha.

Miparanganyiko ya kiutawala na ambayo Wasomi wameikabili kiume ni mingi, inaanzia enzi za Chama kushika hatamu [1965], Ubepari wa Serikali kwa mfumo wa Azimio la Arusha [1967], Mgogoro wa Kikatiba [1977] na ulegezaji Masharti ya Siasa na Biashara ulioashiria kifo cha suluhisho la miparanganyiko iliyotangulia [1992].

Umakini wa Wanavyuo Vijana katika kuainisha matatizo ya jamii na huruma yao kwa wanyonge unajionyesha dhahiri katika kazi za wasomi hao enzi za nyuma, vikiwamo vitabu viwili vya Mwanafunzi wa mwaka wa pili, Issa Shivji: "The Silent Class Struggle in Tanzania", na "Class Struggle Continues", vinavyoweka wazi migongano ya kitabaka inayoikabili jamii yetu.

Si hivyo tu, baadhi ya wanafunzi walitumia muda wao wa likizo kwenda kushiriki katika harakati za ukombozi wa nchi za Kusini mwa Afrika, kuonyesha uanamapinduzi wao kwa bara letu. Kwa nini Serikali inaua uanaharakati huo?.

Nchi yetu inakabiliwa na mtihani mgumu, kati ya kubakia kama taifa huru au kugeuka taifa lililofungwa minyororo chini ya Ufalme wa demokrasia ya Ki-Magharibi na sera za utandawazi. Uchumi wetu unaendelea kuwa tegemezi kila kukicha, huku taifa likipoteza kwa kasi ya kutisha, utamaduni na maadili ya kitaifa yaliyotuunganisha kuwa jamii moja.

Demokrasia inazidi kusinyaa na kuwa mikononi mwa walio nacho pekee; huku ufa kati ya matajiri na masikini ukipanuka haraka. Tunazidi kubiasharisha kila kitu, toka ubinadamu, utu na hata imani za dini, chini ya altare ya sera huria.

Kwa walio nacho, wanajifanya kutoona hatari iliyo mbele yetu, kana kwamba wanajiandaa kustaafu na kukimbilia kuishi nchi za nje. Pengine hii ndiyo sababu ya kusudio la kuunda Muswada juu ya Uraia wa Nchi mbili.

Tumetekwa na "vinono" vya Wawekezaji katikati ya umma masikini na kushindwa kuhoji aina ya jamii tunayojenga kwa manufaa ya wengi; na ili kujihakikishia utafunaji mwanana wa kile tunachopora tunawatungia Sheria Wasomi vijana kuwafunga midomo, na hata kuwanyima haki yao ya kupiga kura!.

Vyama vyetu vya Wafanyakazi tumevigawa katika makundi dhaifu – TUGHE, TPAWU, TUICO n.k., ili kuvipunguza nguvu kwa sera za akina Frederick Lugard za "wagawe uwatawale" tawala" [devide and Rule].

Tumerekebisha Sheria za Kazi kuwapa nguvu nyingi Waajiri badala ya kuwalinda Wafanyakazi kwa wimbo ule ule wa "Kujenga mazingira safi kwa Wawekezaji", wasibughudhiwe na "siasa" za Wafanyakazi, kama tulivyopiga marufuku "siasa" Vyuoni.

Wakati huo huo, tumejionea jinsi demokrasia ya uwakilishi [Bungeni] ilivyogeuka mradi wa kitabaka ambapo Wabunge wanatetea vyama vyao badala ya wananchi waliowapa kura. Na ni Wabunge hao hao wanaowatungia Sheria wasomi wa nchi hii, kuwanyima uhuru wa kuhoji. Kama huu si usaliti kwa umma, ni nini?.

Sheria hii ya kuziba midomo wasomi si ya wananchi, bali ni ya Wawekezaji na mawakala wao nchini, ambao wamegeuka wala nyama ya wasomi [intellectual cannibals]. Hii haiashirii uhai kwa Taifa, bali ni harufu ya kifo kwa Taifa ambalo hatima yake sasa imo mikononi mwa wapiga ramli kama kina Sheikh Yahya Hussein!

Kuna sababu nyingi zinazofanya watawala wapate hofu na kugeuka nyamaume "intellectual cannibals". Kwanza, ni kule Serikali kuendelea kujiweka mbali na wananchi kwa njia ya rushwa iliyokithiri, ulaji wa makeke [Conspicuous consumption] na mfumo wa maisha ya mbwembwe kutosha umma kufungua masikio.

Wameiga maisha ya raha na starehe mithili yale ya "Wabenzi" wa enzi za ukoloni, wakishindana kuoa na kutaliki mabibi na aina ya magari ya sifa, lakini yasiyofaa kwa kazi za vijijini waliko watu wanaodai kuwatumikia.

Tumepoteza dira na kuendesha nchi na Serikali bila itikadi madhubuti. Tunaimba "Ujamaa" huku tukicheza ngoma ya kibepari.

Hali hii haiishii hapo pekee; hata mfumo wa elimu na mitaala tumebadili ili kutoa wasomi hohe hahe wasioweza kuisemea na kuitumikia vyema jamii yao; lengo ni kupata "wasomi" dhaifu, wabeba vipeperushi wakati wa Kampeni za uchaguzi.

Inapokuwa hivyo, kama anavyotabiri Professa Alvin Toffler, katika kitabu chake "The Third Wave: The Revolution That Will Change Our Lives", "tusitegemee kwamba Viongozi wetu wa leo – Marais na Wanasiasa, Wabunge na Wajumbe wa Kamati Kuu, wataichukia mifumo hii [na kutaka iondoke] hata kama inawaumiza wanyonge, ilimradi inawapa shibe yao, madaraka na nguvu ya kutawala".

Tujifunze kutoka kwa Serikali ya Ufaransa baada ya Mapinduzi maarufu ya 1789, ambayo ilishindwa kujifunza kutokana na makosa ya Serikali ya awali [The ancien regime] na kujutia kurudia makosa hayo kwa gharama kubwa.
 
Mmh,hii story ni ndefu ila nimeipenda unapomalizia kwa kututaka tujifunze kutopuuza wasomi ila kwa serikali iliyopo hilo hawalioni.Tubadilike
 
Umeshawahi kujiuliza "Ulipata faida gani kwa kuikariri ramani za nchi mbalimbali kama ujerumani wakati unasoma masomo mbalimbali?" Kama unafaham faida yoyote ya kukariri ramani hizo au hata kujua nchi hizo zinalima mazao gani na viongozi wao ni kina nani naomba mnijuze.

Nachotaka kusema hapa ni jinsi syllabus yetu inavyong'ang'ana na mambo yasiyo na msingi kwa kumjenga mtoto wa kitanzania anayemaliza elimu hiyo kwa kufaulu "ETI VIZURI SANA" huku akienda mtaani kuhangaika asijue ashike wapi kwa kukosa maarifa ya msingi kabisa kupambana na mandhali ya ukosefu wa ajira.

Kwanini tusibadili mtaala wetu ili umuandae mtu kupambana na ukweli mtaani (ukosefu wa ajira) ili akitoka shule (hapa namaanisha darasa la saba na kidato cha nne) ajue ataendesha vipi maishayake? Kama hata hao wazungu hawajui kuchora hata ramani za nchi zao, kwanini sisi tuzijue? (au tunawaandaa vijanawetu waje kuwa-"koloni" wazungu kama wao walivyotufanya sisi hapo kitambo)

Mtaala ukibadilika ukamfundisha mtu stadi mbalimbali za maisha akiwa shuleni (udeleva, ufundi na ujasiliamali kwa ujumlawake). Umefika wakati sasa wa kutumia shule zetu kufundisha hata alama za barabarani na alama (indicators) zioneshwazo na vyombo vya usafiri angalau kupunguza ajali.

Kama Ninyi wasomi wetu mkikaa kimya kuhusu uboreshaji wa elemu, nitaendelea kuamini kuwa Nchi hii ina wasomi wa madesa yasiyo msaada kwa jamii inayowazunguka ambayo ni kubwa kwa idadi mara dufu yenu.
 
...Kama Ninyi wasomi wetu mkikaa kimya kuhusu uboreshaji wa elemu, nitaendelea kuamini kuwa Nchi hii ina wasomi wa madesa yasiyo msaada kwa jamii inayowazunguka ambayo ni kubwa kwa idadi mara dufu yenu.
Naona wasomi wanakacha kujibu!
 
prophet una maana gani unaposema nyinyi wasomi? Define education from greece word educo means get from within' then define education from their get the meaning of educated hapo utapata majibu yako, ustoe mada kimajungu kama umebanwa na haja kubwa. Think before you write.
 
Wimbi la wasomi waliobobea katika fani mbalimbali Tanzania kukimbilia siasa limenifanya nijiulize maswali yasiyokuwa na majibu.

Katika nchi zilizoendelea mtu akihitimu katika ngazi ya Phd na hata Professor mchango wa wa fani au taaluma yake katika jamii anamoishi siyo wa kutafuta kwani uko dhahiri.

Kama ni engineer, daktari, astronomers,botanists,psychologist, meteorologist n.k basi lazima atafanya kitu kipya tangible kitakacho acha legacy na atakita ktk fani yake hadi mwisho wa maisha yake. Wenzetu wana tabia ya kudhamini taaluma zao na sio rahisi wazitupe kando na kukimbilia cheap politics.

Tofauti hii ya attitude kati ya wasomi wa TZ na wale wa nchi za ughaibuni inachangia kwa kiasi kikubwa katika maendeleo ya nchi hizo.

Kama ni entomologist au botanist atafanya tafiti zake kuhakikisha anachangia kuleta mapinduzi ktlk kilimo na kama ni engineer atahakikisha kabla hajafa anabuni na kutengeneza kitu kitakachochangia katika maendeleo ya nchi yake na ulimwengu kwa ujumla. Hii ndiyo sababu wenzetu wanatupita kwa maendeleo na kutuacha pale pale miaka nenda rudi.

Ukija hapa TZ wasomi kktk ngazi ya Dokta na maprofesa wengi wanaishia kuwa Lecturers ktk vyuo vyetu vikuu na umri ukisongo au akikaribia kustaafu anaanza kujiingiza katika masuala ya siasa.

wengi wakishajiingiza katika siasa katika ngazi ya udiwani au ubunge huwa wanahisi wametimiza malengo yao bila kuionea huruma elimu yao pamoja na muda waliotumia shule. Fikiria profesa anaona ni sawa tu kufa bila hata kuacha mchango wowote katika nchi yake tofauti na wenzetu.

Inapofikia mahali profesa anagombea nafasi y a udiwani ili awe meya ni jambo linalotia doa na aibu kwa wasomi wa WaTZ.

Professor au Phd holder anapotafuta favour ya kuchaguliwa katika political post yoyote, iwe mkuu wa wilaya, mbunge, mkuu wa mkoa n.k ni ishara kwamba hawa wataalam wameshatupa kando fani zao na wanawaza tu kupata fedha kirahisi kupitia cheap politics.

Hii ni aibu na hasara ambayo Tanzania imekuwa ikipata kwa wasomi wake kujiingiza ktk siasa ambazo mchango wake kwa maendeleo ya taifa ni mdogo kuliko angejikita katika kufanya utafiti unaohusiana na fani yake. Siasa tuwaachie wanasiasa na sisi tumepewa kipawa cha kutumia akili za kiutafiti ktk kutatua matatizo na kuleta maendeleo ya WaTZ.

Ukweli ni kwamba kama wameshindwa kuonyesha mchango wao kwa maendeleo ya TZ kupitia fani zao ni vigumu sana kuleta maendeleo kupitia politics .Badala ya kujipendekeza kupata favour za kupewa nafasi za bure au kuomba kupigiwa kura kwa nini usitumie skill hiyo ya lobbying kuomba fund ya kufanya utafiti utakaowanufaisha watanzania.

Tumekuwa tuki-import teknolojia nyingi kutoka nje wakati tunawasomi wetu walioamua kuwa vilaza na kutafuta kazi rahisi za kisiasa.

Huwa mara nyingi nina question kama hawa jamaa walikariri au walielewa walichokisoma au ni ile tabia ya kusomea mitihani badala ya kuelewa ndo inatuponza.

Imefika mahali ambapo wasomi wa TZ inabidi tujitahmini kuangalia kama kweli kiwango cha elimu tulichopata kinalingana na mchango wetu katika maendeleo ya Taifa letu.

Ninapata uchungu wakati bado tunaendelea ku-import wataalamu wengi kutoka nje ili hali tunao watu wenye fani hizo hapa hapa TZ ila tu wameamua kuzitundika juu ya miti au kwa makusudi au kutojua na kujiingiza kwenye siasa ambazo hauhitaji kutumia akili sana lakini bado siku yako inaingia.
 
Watanzania mnathamini mchango wa wanasiasa na sio wasomi.

Mfano:dawa ya babu loliondo haijatafitiwa lakini kwa shinikizo la wanasiasa hamsikii la kuambiwa ni kugida kikombe kama togwa,shame on you acha wote tuwe politicians!
 
Kama ndivyo hali ilivyo always tutakuwa wasindikizaji lakini wanyarwanda wanakuja kwa spidi nyuma yetu na tusipo change mindset watatupita tukiwa hatujasogea hata hatua moja.
 
Wanyarwanda walishapita siku nyingi mkuu. Sasa hivi tunakula tu waliyotuachai wakoloni. Hakuna tunalofanya zaidi ya kupiga tu madomo. "NADHANI HATA MUNGU HATUELEWI WATZ"
 
Back
Top Bottom