Wasomi: CCM kimepoteza mvuto; lazima mabadiliko NEC uchaguzi kuwa huru...

nngu007

JF-Expert Member
Aug 2, 2010
15,862
5,797

Tuesday, 04 October 2011 20:13
mukama wilson.jpg


Katibu Mkuu wa CCM,Ndugu Wilson Mkama

Waandishi wetu

MATOKEO ya uchaguzi mdogo wa Jimbo la Igunga yamepokewa kwa mitazamo tofauti, huku baadhi ya wasomi wakikosoa nguvu nyingi za rasilimali zilizotumiwa na CCM kwamba hiyo ni ishara ya chama hicho kikongwe kupoteza nguvu na ushawishi wa kisiasa nchini.

Wakati wasomi wakikosoa pia mfumo wa utendaji wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP), Said Mwema amesema pamoja na changamoto mbalimbali zilizojitokeza katika uchaguzi huo, vyama vilivyoshiriki uchaguzi huo vimeonyesha ukomavu na uvumilivu wa kisiasa.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti, Dar es Salaam jana, baadhi ya wasomi waliohojiwa kuhusu uchaguzi huo walisema mfumo wa NEC utakaotoa matokeo yenye uwiano ndiyo unaokubalika kwa watu, kwani kutafanya wananchi kuchagua viongozi wanaowataka.

Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Dk Benson Bana alisema matokeo hayo yanaonyesha jinsi CCM kinavyozidi kupotea machoni mwa Watanzania. Alisema CCM hakiwezi kutembea kifua mbele wakati wananchi waliomchagua mbunge wa chama hicho wapo chini ya asilimia 50 ya idadi ya watu waliojiandikisha kupiga kura.


Alisema umefika wakatik wa CCM kujitizama upya kwa kuwa Chadema kinakuja kwa kasi na kimedhihirisha katika uchaguzi huo kwa kupata kura nyingi, licha ya kuwa hakikuwa na mtandao mkubwa katika jimbo hilo."Chadema wameibuka vizuri na wanaendelea kukubalika ila CCM kinazidi kupoteza ushawishi na mvuto wao kwa wananchi," alisema Dk Bana.

Alisema idadi ya watu waliojitokeza kupiga kura inatia shaka na kwamba ni jambo linaloacha maswali mengi... "Hii inaonyesha kuwa watu wamechoka, sasa wanaona hata wakichagua mbunge hakuna lolote wanalonufaika nalo, hivyo kuna kazi kubwa ya kuwashawishi wananchi waone umuhimu wa kupiga kura."

Mhadhiri Mwandamizi wa Siasa UDSM, mwingine, Cosmas Mogella alisema: "Serikali inapaswa kuangalia mfumo mzima wa uwiano wa kura ili kuondoa malalamiko ya baadhi ya vyama kuonekana vimeibiwa, inapaswa kuangalia matakwa ya wananchi."

Mogella alisema kutokana na hali hiyo, mfumo uliopo sasa unashindwa kubaini kiongozi sahihi aliyechaguliwa na wananchi kutokana na tofauti ndogo ya kura, jambo ambalo linasababisha kuwapo kwa malalamiko.

Alisema, kitendo cha wananchi kujiandikisha wengi na kushindwa kujitokeza kupigakura ni ishara ya kuwapo kwa tatizo. Alisema kutokana na hali hiyo, NEC inapaswa kuliangalia na kulifanyia kazi.

Alisema kitendo cha CCM kutumia nguvu kubwa wakati wa kuomba kura ni ishara ya kutumia rasilimali za wananchi vibaya kwa kuwa ndicho kilichopo madarakani hivyo fedha kinazotumia ni mali ya umma.

"CCM imetumia nguvu kubwa kwenye kampeni zake, hili ni tatizo kwa sababu wanatumia fedha za wananchi kuomba kura wakati wenyewe ndiyo wapo madarakani, bora fedha hizo zingetumika kwenye miradi ya maendeleo," alisema.

Mwanasheria maarufu nchini, Profesa Abdallah Safari alisema hakuna uchaguzi huru na haki bila ya kuwapo kwa mabadiliko NEC.Profesa Safari ambaye pia ni Mjumbe wa Baraza Kuu la Chadema, alisema kutokana na hali hiyo, Serikali inapaswa kufanya mabadiliko katika uundaji wa tume hiyo ikiwa ni pamoja na kuiwezesha ifanye kazi zake bila ya kuiingilia na isifungamane na upande wowote.

"Tume ya Uchaguzi inapaswa kuwa huru ili iweze kutoa matokeo ya haki kwa wananchi bila ya kufungamana na upande wowote. Kutokana na hali hiyo, Serikali inapaswa kuipa nguvu mamlaka hiyo ili ifanye kazi kivyake," alisema Profesa Safari.


Alisema, kutokana na hali hiyo matokeo yatakayotangazwa na tume hiyo yatakuwa sahihi na hakutakuwa na malalamiko kutoka kwenye vyama vitakavyoshindwa kwenye uchaguzi. Alisema wananchi wanapaswa kushirikiana kudai mabadiliko kwenye tume hiyo.

Mwanasheria kutoka Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHCR), Harold Sungusia alisema Serikali inapaswa kufanya maboresho ya daftari la wapigakura ili waweze kujitokeza kwa wingi wakati wa uchaguzi.


Alisema kitendo cha wananchi wa Igunga kujitokeza kidogo ni ishara ya kutokuwapo kwa maandalizi ya kutosha... "Wananchi wengi wameshindwa kujitokeza kwenye uchaguzi wa Igunga, hii inatokana na Tume ya Uchaguzi kushindwa kufanya maandalizi ya kutosha. Serikali inapaswa kujifunza ili kuondoa matatizo kama hayo."

Alisema Serikali inapaswa kufanya maandalizi ndani ya miezi sita au mitatu kabla ya uchaguzi mwingine ili kupunguza malalamiko kutoka kwenye vyama.

Mhadhiri mwingine wa UDSM, Dk Ambrose Kessy alisema, uchaguzi huo mdogo umeonyesha kuwa Watanzania wamekomaa kidemokrasia.Alisema ukomavu huo unatokana na kuwapo kwa ushindani mkubwa wakati wa kampeni, jambo ambalo limewafanya wananchi kushindwa kutabiri matokeo ya mshindi.Alisema kitendo cha wananchi kushiriki kwenye kampeni pamoja na wanasiasa wao ni suala la kujivunia kwa sababu wamebadilika na wanatambua umuhimu wa siasa na kushiriki kumtafuta kiongozi.

IGP asifu
Kwa upande wake, Mwema alisema uchaguzi mdogo wa Igunga uliomalizika juzi, umeonyesha ukomavu kwa vyama vya siasa na kuvitaka vizingatie sheria, haki na wajibu.Akizungumza Dar es Salaam jana, Mwema alisema: "Pamoja na changamoto zilizotokana na uchaguzi huo, subira na uvumilivu vilivyoonyeshwa na vyama vya siasa ni dalili njema ya siasa za ushindani. Natoa pongezi kwa wananchi wote na askari waliofanikisha uchaguzi huo."

"Hakuna haki bila wajibu wala hakuna uhuru bila mipaka, vyote hivyo viko chini ya sheria. Shughuli za uchaguzi wa Igunga zimekwisha, wananchi waendelee kufuata sheria, kanuni na taratibu zilizopo."

NCCR ‘kimeshinda' Igunga
Chama cha NCCR-Mageuzi ambacho kilijitoa kushiriki uchaguzi huo kimesema ndicho kilichoshinda uchaguzi huo kwa madai kuwa kilivitaka vyama vya upinzani kuungana na kusimamisha mgombea mmoja, lakini kikaonekana kama kinaipigia debe CCM.Katibu Mkuu wa chama hicho, Samwel Ruhuza alisema kushindwa kwa wapinzani katika uchaguzi huo ni matokeo ya ubishi na kutopenda kushirikiana."Sisi tulifanya tathimini kubwa Igunga na kugundua kuwa kuna ulazima wa vyama vya upinzani kukubaliana kusimamisha mgombea mmoja, tulipingwa na matokeo yake yameonekana," alisema Ruhuza.

Ruhuza alisema kama wapinzani wangesimamisha mgombea mmoja CCM kisingeweza kuibuka na ushindi na kwamba kitendo cha chama hicho tawala kushinda kwa asilimia chache kimedhihirisha ukweli wa kauli ya NCCR.Alisema wapinzani wana nafasi kubwa ya kushinda kama watakuwa na utaratibu wa kuachiana majimbo ambayo chama kimoja kitaonekana kuwa na nguvu kuliko kingine.

Sau chalia ukata
Chama cha Sauti ya Umma (Sau), ambacho mgombea wake aliambulia kura 63 tu katika uchaguzi huo, kimesema kimeshindwa kutokana na ukata.Mwenyekiti wa chama hicho, Paul Kyara alisema katika uchaguzi huo CCM, Chadema na CUF alivyodai kuwa ndivyo vyenye uwezo kifedha, vilikiuka Sheria ya Gharama za Uchaguzi.

"Vyama vilielezwa kutotumia zaidi ya Sh80milioni lakini kwa mtindo ule wa kutumia hadi helikopta, ni wazi kuwa sheria hii ilikiukwa, sisi hatukuwa na fedha hata za kuwalipa mawakala," alisema Kyara.

Imeandikwa na Fidelis Butahe, Elius Msuya, Patricia Kimelemeta na Ellen Manyangu.


 
“Hii inaonyesha kuwa watu wamechoka, sasa wanaona hata wakichagua mbunge hakuna lolote wanalonufaika nalo, hivyo kuna kazi kubwa ya kuwashawishi wananchi waone umuhimu wa kupiga kura.”



".....kitendo cha wananchi kujiandikisha wengi na kushindwa kujitokeza kupigakura ni ishara ya kuwapo kwa tatizo. NEC inapaswa kuliangalia na kulifanyia kazi..."



"Wananchi walijitokeza wachache kwa sababu waliogopa kumwagiwa tindikali"



Bwana Nape anaweza kupima weledi wake katika masuala ya siasa kwa kutizama kauli hizo tatu hapo juu.




 
Back
Top Bottom