Cannabis
JF-Expert Member
- Jan 20, 2014
- 8,933
- 25,268
Dar es Salaam. Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Abdallah Ulega amesema watawapa wasanii misamiati mipya kwa ajili ya kuitumia kwenye nyimbo zao ili kukuza lugha ya Kiswahili.
Miongoni mwa wasanii hao ni Daimond, Ali Kiba, Harmonize, Zuchu, Nandy, Maromboso, Rayvan na wengine akisema watakuwa mabalozi wa kukitangaza
Kiswahili kupitia nyimbo zao.
Ulega ameeleza hayo leo Jumanne Machi 2, 2021 alipotembelea makao makuu ya Uhamiaji pamoja na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM). Ziara hiyo ililenga kuhamasisha na kukuza lugha ya Kiswahili kwa taasisi hizo katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.
Amesema Kiswahili ni lugha adhimu inayopaswa kukuzwa na kusambaa katika nchi mbalimbali, akibainisha kuwa kuwapa wasanii misamiati mipya itakayotolewa na Baraza la Kiswahili Tanzania (Bakita) itasaidia kukuza lugha hiyo.
"Kwa mujibu wa kanuni za Bakita za mwaka 2019 zinaelekeza kazi za wasanii kupelekwa kwenye baraza hilo kusanifiwa kabla ya kuingizwa sokoni. Bakita wana misamiati mingi mipya ambayo tunaweza kuwapa wasanii kuitumia ili kukuza lugha hii.”
"Sasa hivi watoto wadogo hasa wa shule za awali wanaimba kwa ufasaha nyimbo za wasanii wetu maarufu akiwemo Daimond, Alikiba, Zuchu na Harmonize. Hawa wana fuasi na mashabiki wengi kupitia kwenye akaunti zao na wanasikilizwa nje na ndani ya nchi kwa hiyo wakiweka misamiati mipya itasaidia sana," amesema Ulega.
Ulega amewataka BAKITA kutojifungia ndani badala yake watoke nje na kuwafuata wasanii kwa ajili kuwapa misamiati wakati ukifika.
Ulega amesema hatua hiyo itasaidia pia kupanua wigo wa misamiati ya Kiswahili na kurasimisha maneno na istilahi zilizoeleka kwenye jamii.