BAK
JF-Expert Member
- Feb 11, 2007
- 124,790
- 288,007
- Amshangaa Kikwete kusema ni mpasuko kidogo
- Yeye asisitiza uliopo ni mkubwa unaoligawa taifa
- Asema tatizo ni tofauti ya kipato cha tajiri, maskini
Majira
29 September 2009
WAZIRI Mkuu Mstaafu, Jaji Joseph Warioba amevunja ukimya na kusema kuwa upo mpasuko mkubwa ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambao unaweza kuwagawa Watanzania katika matabaka ya udini na ukabila.
Jaji Warioba alitoa kauli hiyo jana alipozungumza na baadhi ya vyombo vya habari ofisini kwake Dar es Salaam ili kutoa ujumbe wa miaka 10 ya Tanzania bila Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere.
Alisema Watanzania wanafahamu kuwa upo mpasuko ndani ya chama, ambao pia ulithibitishwa na Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete alipozungumza na wananchi kupitia Televisheni ya Taifa (TBC) kuwa upo mpasuko kidogo.
Hata hivyo, Jaji Warioba aliyeshika maraka ya Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais kati ya mwaka 1985-90, alisema kauli hiyo ya Rais Kikwete ilimshangaza kwa mwenyekiti wa chama kusema kuwa upo mpasuko mdogo, wakati uliopo ni mkubwa.
Alisisitiza kuwa ndani ya CCM kuna mpasuko mkubwa, akitolea mfano kauli ya Rais Kikwete kuwa wabunge wa CCM sasa hawaaminiani hata kuachiana glasi zao za maji kwa kuhofia kuwekeana sumu, jambo ambalo Jaji Wariona alisema linathibitisha kuwa kuna mpasuko mkubwa ndania ya chama.
Kiongozi huyo alisema wakati taifa linaelekea kwenye Uchaguzi Mkuu mwaka 2010, yameibuka makundi na matabaka kiasi kwamba mtu akitangaza adhima ya kugombea uongozi ndani ya vyama vya siasa anaonekana kuwa adui kiasi cha kutafutiwa sababu, tofauti na zamani ambapo wagombea uongozi walitaniana kabla ya kushindana.
Kwa mujibu wa Jaji Warioba, msingi umeanza kusambaratika tofauti na enzi za Mwalimu Nyerere, ambapo wananchi walikuwa na mshikamano bila ubaguzi, wakiitana ndugu, tofauti na sasa ambapo wamegawanyika katika makundi na matabaka.
Akizungumzia sababu ya mgawanyiko huo, Jaji Warioba alisema unatokana na tofauti kubwa kati ya matajiri na masikini, jambo ambalo halikuwapo wakati wa utawala wa Mwalimu Nyerere ambaye alijitahidi kuleta usawa kwa wananchi.
"Wananchi walikuwa na sauti katika kuongoza nchi, leo matajiri ndio wenye sauti. Viongozi wako karibu na matajiri, zamani ukiwa serikalini lazima utunze siri za serikali, leo siri zinavuja sana, watu wanaona yanayotendeka, wengine wanalipwa milioni tano na marupurupu, wengine wanaambulia laki moja, ndio maana sasa kuna migomo ya walimu, wanafunzi na wananchi," alisema.
Jaji Warioba alisema imani yawananchi kwa serikali imepungua, matokeo yake yameibuka matabaka, huku wengine wakiwaunga mkono wabunge wanaohubiri mapambano dhidi ya ufisadi na wengine wakiwakatisha tamaa kwa kuwaona wasaliti ndani ya chama.
Jamii itaamini nini kuhusu mgawanyiko ulioibuka ndani ya CCM na kusababisha Spika Bw. Samuel Sitta kukumbwa na wakati mgumu na baadaye tuhuma zake kumalizwa kimya kimya. NEC ilitoa msimamo kuwa Spika anafanya mambo peke yake, baadaye wakakanusha, mgogoro huu ukiisha kimya kimya utazua maswali mengi kwa wananchi," alisema Jaji Warioba na kufafanua kuwa CCM ina ushawishi mkubwa, mgawanyiko unapotokea ndani yake unaweza kuigawa Tanzania nzima.
Alizungumzia pia Tanzania kujiunga OIC na Waraka wa Maaskofu, Jaji Warioba: "Niliangalia majadiliano ndani ya bunge, akisimama mbunge mkiristo anapinga hoja, akisimama mwislamu anaunga mkono, baada ya hapo umekuja waraka na mwongozo, sijui msingi wake, kila tunapoelekea Uchaguzi Mkuu mambo haya hujitokeza, ilianza 1994, ikaibuka tena 1999 na 2004," alisema.
Jaji Warioba amesema Watanzania wameanza kuchanganya dini na siasa, wakati wa Pasaka mtu anakaribisha watu sikukuu kwa msingi wa siasa, hivyo hivyo wakati wa Mwezi wa Ramadhani kiongozi wa siasa anaandaa futari wakati hakufunga, jambo ambalo amesema lisipewe nafasi na Watanzania
Jaji Warioba amesema Hayati Mwalimu Nyerere alifanya kazi kwa uadilifu, hakuchanganya dini na siasa kama ilivyo kwa baadhi ya wanasiasa sasa, alikuwa msikivu sana pamoja na wananchi kusema kuwa Mwalimu alikuwa mtu mbishi asiyeambilika, jambo ambalo si kweli.
Kuhusu vita dhidi ya Ufisadi, Jaji Warioba amesema inatia matumaini baada ya watu wazito kufikishwa kwenye vyombo vya sheria, huku akitoa tahadhali kuwa kesi za aina hii zinatokana na msukumo wa kisiasa, na kwamba kuna hatari zake, akitoa mfano kesi za uhujumu uchumi mwaka 1983, ambapo serikali ililipa fidia.