EINSTEIN112
JF-Expert Member
- Oct 26, 2018
- 21,713
- 35,524
Na: Emmaus Bandekile Mwamakula
Hawa wako wengi sana! Wengine niliwahudumia wakiwa mashuleni kwa zaidi ya miaka 18 nilipokuwa nahudumia wanafunzi nchini; wengine niliwafundisha Chuo Kikuu, St. John's University of Tanzania kwa zaidi ya miaka 9; wengine tulisoma nao Itunge, Kipawa, Azania na IFM; wengine tulifundisha nao Chuo, wengine ni ndugu, jamaa na marafiki; wengine ni majirani katika maeneo yote niliyowahi kuishi katika Wilaya za Kyela, Ubungo, Temeke, Ilala na Kinondoni! Wengine ni Wachungaji na Maaskofu, na wengine ni ma-ulamaa, mashehe na hata maimamu! Wapo watumishi wa Serikali na wamo wafanyabiashara na wajasiliamali! Nasikia kuwa waalimu ndio wengi zaidi! Wengine wengi ni Watanzania wasionijua ila wamesikia mapambano na harakati zangu za kupigania Haki!
Wengine ni Usalama wa Taifa na wengine ni wafuasi wa CCM wakiwemo wastaafu waliotumikia CCM na serikali zake zote! Wengine ni ndugu wa waathirika wa vyeti feki na wengine ni wahanga wa Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2020. Nimeambiwa pia wengine ni Mabalozi wanaoziwakilisha nchi zao katika Tanzania. Nimeambiwa pia kuwa Wanajeshi ndio wengi zaidi kuliko hata Polisi.
Wote hao wanaunga mkono jitihada zinazofanywa na Askofu Mwamakula na watu wengine katika kutetea Haki, Tume Huru, na Katiba Mpya. Ila hawawezi kusema hadharani kwa kuhofia nafasi zao, mahusiano na hata maisha yao. Wanabaki kunong'ona katika familia zao au katika makundi ya watu wawili wawili. Wapo wanaoogopa hata kumtembelea Askofu ila hutuma ujumbe kupitia watu wanaowaamini wakisema Askofu asirudi nyuma na kwamba 'akamatie hapohapo'!
Siku moja nilikutana na Mwandamizi mmoja wa TISS alipokuwa akitokea Dodoma! Alishuka kutoka katika "chuma" lake jeusi, akanisalimia na kusema ananisoma kila siku na kwamba nisikate tamaa! Alisema kuwa wapo wengi wa aina yake hata ndani ya TISS.
Makundi yote haya wanajiandaa kusherekea ushindi kuliko hata walio mstari wa mbele katika mapambano.
Wapo ambao baada ya ushindi watajitokeza kuonyesha kuwa wanatujua zaidi na kutusifia hadharani. Watafufua hata picha tukizowahi kupiga nao au matukio ya nyuma ya kuonyesha jinsi wanavyotufahamu! Lakini kwa sasa hawawezi! Wamejawa na hofu ya kuogopa kupoteza hayo wanayoyadhani kuwa ni ya muhimu kwao kwa sasa! Kuongozana na kujitambulisha na sisi ni hatari kubwa! Majina yetu yanawakilisha hatari kwa watawala! Majina yetu yamepakwa kinyeshi na wapambe wa watawala! Lakini siku moja majina yetu yatakuja kuwa manukato nzuri na ghali kuliko vito vya thamani!
Jeuri yetu haipo katika makundi yanayotuunga mkono! Jeuri yetu ipo katika YEYE aliye HAKI (Zaburi 121). Huyo ndiye msaada, ulinzi na kimbilio. YEYE ni zaidi ya TISS, KGB, Scotland Yard, CIA, Mossad, nk.
Ninaendelelea kukualika katika Matembezi ya Hiyari na ya Amani nitakayoyaongoza nchi nzima kuanzia Januari 2021 kwa lengo la kuhamasisha Kuundwa kwa Tume Huru na Kuandikwa kwa Katiba Mpya!
Mwana Kondoo Ameshinda! Tumfuate!
Askofu Mkuu Emmaus Bandekile Mwamakula - Kanisa la Moravian la Uamsho Tanzania & Afrika Mashariki.