Wananchi wa Mbeya wamuomba JK amuondoe Mkuu wa Mkoa

BAK

JF-Expert Member
Feb 11, 2007
124,792
287,994
Wamchongea RC kwa JK

na Edward Ibabila, Mwanza
Tanzania Daima~Sauti ya Watu

WAKAZI kadhaa wa mkoani hapa, wamemchongea Mkuu wa Mkoa (RC) wao , Dk. James Msekela, kwa Rais Jakaya Kikwete, wakimtaka amwondoe mkoani humu kutokana na kutowatumikia vema.

Wakazi hao wamemwomba Rais Kikwete kumwondoa Dk. Msekela, kwa sababu hawaridhishwi na utumishi wake, kutokana na kile walichodai kuwa kushindwa kwake kusikiliza na kuzipatia ufumbuzi mahususi kero zinazowakabili.

Wakizungumza na Tanzania Daima mwishoni mwa wiki iliyopita nje ya ofisi ya mkuu huyo wa mkoa, baadhi ya wakazi hao walisema tangu Dk. Msekela alipoteuliwa katika wadhifa huo takriban miaka miwili iliyopita, kero nyingi za wananchi hazisikilizwi na kupatiwa ufumbuzi ipasavyo.

Walisema hilo linatokana na Dk. Msekela kutumia muda mwingi akiwa jimboni kwake, hasa mwishoni mwa vikao vya Bunge. Pamoja na cheo cha Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Dk. Msekela pia ni Mbunge wa Tabora Kaskazini (CCM).

Walisema muda mfupi anaokuwa ofisini huutumia kuzungumza na watu anaowataka yeye, hususan wafanyabiashara na watumishi wa serikali, huku wananchi wenye kero wakipewa majibu ya njoo kesho na katibu wa mkuu huyo wa mkoa.

Walidai kuwa wengi wao walikuwa wameandika barua nyingi za malalamiko mbalimbali yanayotakiwa kushughulikiwa na mkuu huyo wa mkoa, lakini wanapofuatilia huambiwa na karani wake kuwa barua walizoandika hazionekani, na kutakiwa kuandika barua nyingine, jambo ambalo walisema ni usumbufu mkubwa.

“Unavyoniona na hali yangu hii, leo ni mwezi wa tatu nafuatilia majibu ya barua yangu niliyomwandikia mkuu wa mkoa kumuomba anisaidie kupata kiwanja changu ambacho nilidhulumiwa. Lakini sijapata majibu hadi leo. Kila unapokuja unaambiwa rudi kesho, mwisho nimechoka kabisa,” alisema mwanamke mmoja mlemavu ambaye hakutaka jina lake litajwe gazetini.

Naye katibu tawala mstaafu ambaye kabla ya kustaafu alifanya kazi katika moja ya mikoa ya Kanda ya Ziwa, ambaye alikuwa miongoni mwa wananchi hao, akizungumza kwa sharti la kutotajwa jina lake gazetini, alieleza kusikitishwa kwa vitendo vinavyofanywa na mkuu huyo wa mkoa na kuongeza kuwa iwapo Rais Kikwete hatamuondoa mapema, wananchi mkoani hapa watazidi kuichukia serikali yake.

“Kwa kweli mambo anayofanya RC wetu yanakatisha tamaa. Mtu unaweza kufika ofisini kwake saa 2 asubuhi, ukatoka saa 8 mchana, bila kumuona au kutatuliwa kero yako. Utaona wanaosikilizwa ni wafanyabiashara na watumishi wa serikali. Hizi ni kasoro kubwa kwa kiongozi wa serikali. Iwapo rais hatachukua hatua ya kumuondoa haraka, serikali yake itaendelea kubebeshwa lawama,” alisema.

Aidha, wakazi hao walilalamika waziwazi juu ya hatua ya Rais Kikwete kuteua wakuu wa mikoa na wilaya ambao pia ni wabunge, na kuongeza kuwa ni vigumu kwao kutekeleza majukumu ya kazi hizo mbili kwa wakati mmoja, hali inayosababisha kuwapo kwa udhaifu wa kiutendaji, hususan katika nafasi za uongozi wa kuteuliwa.

Baadhi ya wakazi hao, walidai kuwa walifikisha kero zao kwa mkuu huyo wa mkoa zaidi ya miezi tisa iliyopita, lakini hawajasikilizwa hadi sasa.

Alipoulizwa juu ya malalamiko dhidi yake na ofisi yake kwa ujumla, Dk. Msekela alikiri kutumia sehemu ya ratiba yake kutembelea wananchi wa jimbo lake.

Hata hivyo, alisema hiyo haiwezi kuwa sababu ya kushindwa kutekelezwa kwa majukumu yaliyo chini ya ofisi yake, kwa sababu kila anapoondoka hukabidhi ofisi kwa mtu anayekaimu.

Kuhusu kupotea kwa barua za malalamiko ya wananchi, mkuu huyo wa mkoa alisema binafsi hajawahi kupokea malalamiko ya aina hiyo.

“Sijawahi kupokea malalamiko ya aina hiyo. Hata hivyo, kama yapo, wananchi watumie namba yangu ya simu ya mkononi kunijulisha, nami nitachukua hatua,” alisema.
 
Mkuu,

Badilisha kichwa cha habari maana hii haina uhusiano na mkoa wa Mbeya.

Huyu msomi mwenzetu Dr. Msekela naona anachemsha huko Mwanza.

Binafsi ningetegemea Msekela awe katika watu ambao wangeweza ku deliver lakini kama na yeye anashindwa, hapo kuna kazi kweli kweli.
 
pamoja na kwmaba wanayemzungumzia ni mkuu wa mkoa wa mwanza , lakini nako mbeya si haba, mkuu wao wa mkoa kazi yake ni kupambana na Dr Mwakyembe yule jemedari wa richmond aliyemtoa lowasa jasho

tunaambiwa kuwa mpaka leo ana ndoto ya kuwa tena mbunge wa kyela kiti anacbhokalia mwakyembe, kazi yake ni kupangua gia za maendeleo za mwakyembe, haishi kuwa kyela kila siku, majuzi alipata ajali ya gari ndogo akitokea huko usiku

atulie ofisini afanya kazi au kikwete ampeleke mtwara
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom