Wanafunzi Vyuo Vikuu waibana CCM viongozi kujilimbizia madaraka

Status
Not open for further replies.

BAK

JF-Expert Member
Feb 11, 2007
124,792
287,994
Posted Date::11/17/2007
Wanafunzi waibana CCM viongozi kujilimbikizia madaraka
*Wahoji iweje mtu awe na vyeo vitano
*Walalamikia rushwa, matajiri kukiteka chama

*Msekwa akiri chama kimeingiliwa na rushwa

Na Joyce Mmasi
Mwananchi

WANAFUNZI wa vyuo vikuu nchini wamekibana Chama Cha Mapinduzi (CCM) na kuhoji sababu ya vingozi wake kujilimbikizia madaraka huku wakiendelea kukumbatia rushwa katika kupata uongozi.

Wanafunzi hao walioa kauli hizo jana walipokuwa wakizungumza katika Kongamano la Wanafunzi wa Vyuo vya Elimu ya Juu nchini lililoandaliwa na CCM na kufunguliwa na Makamu Mwenyekiti wa Chama hicho, Pius Msekwa.

Walisema ni jambo linalowakatisha tamaa wasomi na vijana kuona kiongozi mmoja wa CCM anashikilia nafasi ya ubunge, uwaziri, ujumbe wa NEC, ujumbe wa Kamati Kuu na bado anateuliwa kuwa mwenyekiti wa bodi fulani.

"Kwa nini mawaziri wanakimbilia kwenye NEC, inavyoonekana wanakwenda kule ili kulinda maslahi yao na si ya chama. Inakuaje mtu mmoja huyo huyo awe NEC, CC, mbunge, waziri na bado eti ni mjumbe wa bodi fulani, hivi kweli ina maana hakuna wana CCM wengine wenye uwezo," alihoji Martin Genos wa Chuo cha Mwalimu Nyerere jijini Dar es Salaam.

Genos ambaye alijitambulisha kama mwanafunzi kutoka chuo Kikuu cha Mwalimu Nyerere alisema pamoja wakati umefika wa viongozi wa juu wa CCM kukubali ukweli na kutoa nafasi kwa vijana na wasomi kuweza kupata nafasi za uongozi ndani ya Chama hicho.

Mwanafunzi mwingine, Chaguna Richard kutoka Chuo Kikuu cha Kairuki Memorial alisema CCM inaonekana kupoteza dira yake ya kuwa Chama cha wananchi wa nchini na sasa kinakuwa chama cha matajiri.

Chaguna alisema CCM ambacho awali kilikuwa chama cha wakulima na wafanyakazi kimegeuka kuwa chama cha wafanyabiashara wenye pesa na kwamba umefika wakati wa viongozi wake kuchunguzana wenyewe kwa wenyewe.

"CCM inapoteza mwelekeo wake, haijulikani ni chama cha kijamaa au kibepari, huwezi kuondoa rushwa kwenye chama kama unawaingiza wafanyabiashara kwenye chama, wafanyabiashara waachwe wafanye biashara zao na si kujipenyeza ndani ya chama," alisema.

Naye Polycarp Benedict wa Chuo cha Ustawi wa Jamii aliuomba uongozi wa juu wa CCM utafute kitabu kinachoitwa �Tujisahihishe� na kukipitia upya kwa maelezo kuwa kinaweza kuwasaidia.

Alisema yapo mambo mengi yanayofumbiwa macho na uongozi wa juu wa CCM na serikali kutokana na viongozi wengi kuoneana aibu hali aliyosema inatokana na viongozi hao kujisahau na kutojua wajibu wao kama viongozi.

Chacha Mwita wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam alisema, baadhi ya viongozi wa CCM na serikali yake walijinufaisha na janga la ukame lililoikumba nchi hii na matunda yake ndio matokeo ya makampuni kama Richmond.

Alisema serikali imeonyesha mafanikio makubwa ikiwemo kuondoa ujambazi licha ya kuwa wapo viongozi wachache wanaofanya kazi ya kujinufaisha na kusahau wajibu wao kama viongozi wa watu.

Akihitimisha mjadala huo, Dk Harrison Mwakyembe alisema, tatizo kubwa linaloonekana ni kuwa hakuna mawasiliano kati ya wanafunzi wa vyuo vikuu na serikali au na CCM.

DK Mwakyembe alisema pamoja na kuwa yeye ni mbunge wa kuchaguliwa lakini si mwanasiasa, hivyo anapenda kusema ukweli wakati wote na akasema CCM inapaswa kujipanga upya na kuwashirikiasha wasomi ndani ya chama hicho.

Alisema Makamu Mwenyekiti mpya wa Chama hicho anaelewa maana ya damu mpya ndani ya chama na umuhimu wa kuwashirikisha wasomi ndani ya chama na alitoa mfano akiwa katibu wa CCM miaka ya sabini alipowachukua wasomi wengi na kuwapeleka kwenye chama.

Awali, Msekwa akifungua kongamano hilo alikiri chama hicho kuingiliwa vibaya na rushwa, lakini akabainisha kuwa sera ya chama ni kupambana na rushwa na si kuikumbatia.

"Kuhusu suala la uongozi wa chama chetu kupatikana bila hila, rushwa au ujanja wa aina yoyote, wote tunajua wazi kwamba chama chetu kimeingiliwa vibaya sana na tatizo kubwa la rushwa katika chaguzi zake, hilo halo halifichiki hata kidogo," alisema.

Alisema katiba ya CCM inasema kuwa Rushwa ni adui wa haki, na inawahimiza wanachama wake wote wasitoe wala kupokea rushwa, na akasisitiza sera iko wazi isipokuwa imekwamishwa na utekelezaji wa sera hiyo.

Wakati huo huo, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, John Chiligati amesema kuwa wanafunzi wa vyuo vikuu wasitarajie kuwa baada ya kumaliza masomo wote wataajiriwa na serikali na badala yake wajiandae kujiajiri wenyewe, anaripoti Habel Chidawali kutoka Dodoma.

Chiligati ambaye pia ni Waziri wa Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana alisema kuwa ikiwa wanafunzi hao watakuwa na ndoto ya kuwa zipo ajira serikalini huenda mawazo hayo yakawa ni ndoto.

Haiwezekani serikali kuajiri vijana wote badaaa yake tumeamua kuboresha vyuo vikuu vya ufundi Ifunda na Moshi ili pindi mtakapomaliza muweze kujiunga na vyuo hivyo na baada ya hapo muweze kujiajiri Chiligati aliwaeleza wanafunzi waliokusanyika katika Chuo cha St John, mjini Dodoma.

Kutoka Mwanza, Frederick Katulanda anaripoti kuwa Mkuu wa Mkoa huo, Dk Alex Msekela alibanwa na wanafunzi waliokusanyika katika Chuo Kikuu cha Mtatifu Augustino aili aeleze kwa nini yeye ni Mbunge na pia ni Mkuu wa Mkoa, swali ambalo hivi karibuni aliulizwa na Waziri Mkuu, Edward Lowassa alipotembelea wilaya ya Ukerewe.

Akijibu swali hilo, Dk Msekela alisema nafasi anazoshikilia yeye ni za uteuzi si ajira, hivyo hakuwa naziba soko la ajira ya watu wengine. Alimtetea pia Lowassa kuwa hakujibu swali hilo Ukerewe kwa kuwa alighafilika tu.

 
swafii sanaaa yani kilichobaki ni kubana hata penalty...hadi waone aibuuuu mijitu mizima ovyooooooo milafiiiii!!
 
Looh! hata wanafunzi sasa wameshutuka? Mwaka huu kuna kazi kweli kweli.

Inaelekea CCM sasa wameamua kumtumia Mwakyembe kuzima moto unaowaka. Suala ni je kweli wanataka damu mpya? Au ni geresha tu ili kupita hiki kipindi kigumu kwao.
 
swafii sanaaa yani kilichobaki ni kubana hata penalty...hadi waone aibuuuu mijitu mizima ovyooooooo milafiiiii!!
Neno AIBU ni msamiati ambao CCM haiufahamu kabisa na kama ni kwa hiari itawachukua karne kulielewa neno hilo.
 
Status
Not open for further replies.
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom