Wanafunzi wa zaidi 1000 vyuo vikuu wajiunga na CCM

M

MegaPyne

Guest
NI KUTOKA DODOMA NA MORO
JK AWAKABIDHI KADI AWAAHIDI AJIRA


Wanafunzi wa vyuo vikuu vilivyoko katika mikoa ya Morogoro na Dodoma wameipongeza Serikali ya Chama Cha Mapinduzi kwa uamuzi wake wa kuwapatia mikopo wanafunzi wa vyuo va elimu juu .

Wameeleza kuwa utaratibu huo wa Serikali ya CCM chini ya uongozi wa Rais Jakaya Kkikwete umewawezesha hata watoto wanaotoka katika familia za daraja la ‘tatu' nao kupata elimu ya juu.

Pongezi hizo zimetolewa na wanafunzi hao, muda mfupi kabla ya Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi, Rais Jakaya Kikwete kuwakabidhi kadi za uanachama wa CCM, baada ya wanafunzi hao zaidi ya 1000 kuamua kujiunga na chama hicho. Hafla hiyo ilifanyika jana jioni Jumatatu katika Makao Makuu ya CCM, Dodoma .


Wanafunzi hao ambao kwa kila chuo waliwakilishwa na wenzao wapatao 20 ni kutoka vyo vikuu vya Dodoma, Mtakatifu John, vyuo vya Mipango na Madini,(544), na SUA, Mzumbe na chuo kikuu cha Kiislamu vyote vya Morogoro (566))


"Mhe Rais na Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi, kwanza tunapenda tukupongeze kwa ushindi mnono ulioupata katika uchaguzi uliomalizika leo (Jumatatu), ushindi huu unaonyesha ni kwa namna gani wajumbe wa mkutano mkuu walivyo na imani nawe" akasema mwakilishi wa wanafunzi kutoka vyuo vya mkoa wa Dodoma.

Akaongeza " lakini pia tunapenda kutoa shukrani zetu kwa Serikali ya Chama Cha Mapinduzi kwa kuwa na mipango mizuri ya kuwapatia wanafunzi wa vyuo vikuu mikopo, asante kwa mikopo hii ambayo imewawezesha watoto kutoka familia za daraja la tatu kupata elimu"

Hata hivyo wamesema wanafunzi hao kuwa pamoja na utaratibu huo mzuri, wanamwomba Rais kuangalia uwezekano wa kuongeza kiwango cha mikopo, kuharakisha upatikanaji wake na pia kuwasaidia wale ambao hawajapata hadi sasa.

"Mhe. Rais kuchelewa kwa mikopo hii kunatufanya wengine tuuze vocha za simu ili tujikimu, lakini pia kuna wenzetu ambao hadi sasa hawajafanikiwa kupata mikopo tunaomba hili uliangalie" akasema mwakilishi wa wanafunzi kutoka Dodoma, kauli iliyoshangiliwa na wanafunzi hao

Wanafunzi hao walimweleza Rais kwamba wamehamasika na kuamua kujiunga na CCM, na kuahidi kuwa watakilinda na wanamuunga mkono Rais katika juhudi zake za kuwatumikia Watanzania ili waweze kuwa na maisha bora.

Aidha wanafunzi hao kwa ujumla wao wamempongeza Rais Jakaya Kikwete kwa ushindi mnono alioupata katika Uchaguzi Mkuu wa CCM, na kwamba ushindi wake huo ni kielelezo cha namna gani anavyokubalika mbele ya wajumbe wa Mkutano Mkuu na kubwa zaidi ni kwamba wana imani naye.

Wamemwomba Rais apange ratiba ya kuvitembelea vyuo vikuu na kuzungumza na wanafunzi ili nao wapate wasaa mzuri wa kumpongeza. Wamemhakikishia kwamba wataendelea kuwahimiza wanafunzi wa elimu ya juu kujiunga na CCM, na kwamba zile fikra kwamba kuna upinzani dhidi ya CCM katika vyuo vikuu si sahihi.

Akizungumza na wanafunzi hao baada ya kuwakabidhi kadi zao, Rais alisema amefurahishwa sana na idadi kubwa ya wanafunzi wa vyuo vikuu kutoka Dodoma na Morogoro ambao wameamua kwa hiari yao kujiunga na Chama Cha Mapinduzi.

Akawaeleza kuwa Chama kina mkakati maalum kwa kuwavutia wasomi wengi kujiunga na CCM na kwamba hiyo ni njia bora na sahihi ya kuwaandaa viongozi katika ngazi mbalimbali za serikalini na katika Chama.

"Nimefurahi sana kwa kweli, kwa sababu chama lazima kipate wasomi, na nchi haiwezi kuendelea bila ya wasomi, na duniani hakuna nchi ambayo imeendelea kwa kuwa na watu mbumbumbu. Na ndio maana tulipoingia serikalini tulitoa umuhimu wa pekee katika elimu" akasema Kikwete.

Amewahakikishia wanafunzi hao kwamba, Serikali ya Chama Cha Mapinduzi imejiwekea mkakati maalum wa kuwaajiri wanafunzi waliohitimu chuo kikuu kuanzia ngazi ya tarafa.

Akawaeleza kuwa wasisite kwenda kufanya kazi katika tarafa kwani huko ndio kunakowafungulia uzoefu na fursa ya kupanda katika safu za uongozi ziwe za ukatibu tawala, ukuu wa wilaya, ukuu wa mikoa na nafasi nyingine nyingi.

"Tunamkakati maalum wa kuwaajiri wanafunzi, na mwaka huu tunaanza na wanafunzi wapatao 500 kutoka SUA, na ninapenda niwahakikishie kwamba vijana wasomo ambao tumewaajiri katika nafasi ya ukuu wa wilaya 12 kati yao wanafanya vizuri sana, hii inaonyesha umuhimu wa kuwaajiri wasomi" akasisitiza Rais.

Akizungumzia kuhusu suala la mikopo ya wanafunzi, Rais amewaahidi wanafunzi hao, kwamba kabla ya kuondoka mkoani Dodoma atahakikisha anakutana na Waziri wa Sayansi, Teknolojia na Elimu ya Juu na Mwenyekiti wa Bodi ya Mikopo na kuangalia matatizo yaliyojitokeza ili kuyapatia ufumbuzi.

"Nataka niwahakikishie kwamba kabla sijaondoka hapa Dodoma nitakutana na Waziri na Mwenyekiti wa Bodi na kuangalia wapi pana tatizo na kulitafutia ufumbuzi, maana suala hili la mikopo limeingiliwa na watu wengi wakiwamo wanasiasa, lakini hatima yake anayeathirika ni mwanafunzi" akasema Rais na kushangiliwa na wanfunzi hao.

Amewaeleza kuwa Serikali inaandaa utaratibu wa kuboresha njia za mawasiliano kati ya Bodi ya Mikopo na wanafunzi wa vyuo vikuu.

Rais Kikwete pia alitumia fursa hiyo kuwaeleza wanafunzi hao juhudi na mikakati mbalimbali inayofanywa na Serikali katika uboreshaji na upanuzi wa elimu nchini kuanzia elimu ya awali hadi chuo kikuu na kwamba imejipanga vema kukabiliana na changamoto mbalimbali.

Kuhusu ombi la kutembelea vyuo vikuu, Rais ameahidi kupanga utaratibu na kwa kuanzia atakitembelea chuo kikuu cha Dodoma kabla hajaondoka.

Awali Katibu Mkuu wa CCM Yusufu Makamba aliwataka wanachama hao wapya kila mmoja wao kushawishi wanachama wapya watano kujiunga na Chama Cha Mapinduzi.

Source: Subirini Magazeti ya Kesho.
 
Mkuu,

Hawa vijana inaweza kuwa njaa zaidi ya mapenzi yao.

Inatakiwa vyama vya siasa visiwatumie wanafunzi kwenye mapambano yao. Wanafunzi wanajua CCM wameshika mpini na wao makali, kweli hapo kuna cha mapenzi tena?

Nafikiri ni makosa kwa JK na yeye kuingia kwenye politics za namna hiyo.
 
je wanawakilisha mawazo ya wanafunzi au wamechukuliwa kama propaganda?
hawa ni makada wa chama tu,nijuavyo mie..Mzumbe na sua ni tawi kubwa la watu wa sisiemu..
 
Hao nao njaa.Ila CCM wanafanya uharamia kuwawekea wanafunzi maisha magumu kwanza halafu baadae waone njia pekee ya kujiokoa ni kujiunga na CCM kupata mlo.Damn and shame! Hao wasomi nao uchwara yaani hawajaona nchi inavyooza kwa uongozi huu mbovu wa Vasco Da'Gama na hicho chama kokoro?

Ndio maana hata huyo mwakilishi wa wananchi amesisitiza kuhusu maswala yaq mkopo.CCM haina nchi inatakiwa iongoze kwa kufuata kanuni na sheria.Sasa Kuikwete asije akatumia suala Mikopo kwa ajili ya Maslahi ya CCm na kuwahujumu wanafunzi.Hata bila kujiunga na CCM ni wajibu wao kutoa mikopo kwa wanafunzi wote aidha wako upinzani ama laa.

Hii inatia kinyaa,Hao wanafunzi nao wanashindwa kufikiria yaani wasomi ambao tulitegemea wataichallenge govt kuhusu Ufisadi,utawala usio na madili ya kazi,rushwa nk ndio wamekua vinara wa kujikomba.

Najua ni haki ya kila mtu kuingia katika chama chochote cha siasa but sio kama hawa walivyofanya.WAMELISALITI TAIFA LETU.Damn!
 
Wasomi kwa sasa hawana msaada wowote katika kudai haki za wanyonge msiwategemee!!
Angalieni mitaala yao huko vyuoni ni siasa ya kulinda mafisadi nina uhakika wanayoyasema si kweli bali ni kujikomba tu

ndoto zao ni siku moja wawe nao mafisadi kama hao wanowapomgeza

nchi hii iko mbioni kukombolewa na wanyonge wenyewe wala si hao wanaojiita wasomi


Mungu akise ndiyo hakuna kiumbe chini ya mbingu kitasema hapana

Mungu ibariki Tanzania.
 
Kama ni kweli alishindwaje kuwasaidia wanafunzi waliokuwa Ukraine tayari na walianza kusoma baada ya mwaka moja akawatelekeza. AIBU HIYO JK, WEWE ULISOMESHWA KWA PESA YA WALIPA KODI.
 
yale yale maigizo wanafunzi 20 kuwakilisha wenzao 1000!!!

-kwani pesa za mikopo ni za CCM ama ni kodi zetu? ama ndo yale yale ya Amani na utulivu kuwa ni sera ya CCM

Tumechoka mbadala lazima miaka zaidi ya 40 umasikini tuuuu kisa UFISADI unao endekezwa na CCM, hata muigize kwamba wamejiunga wasomi laki saba na nusu .. kita eleweka tu!
 
Thats too cheap!!! Yale yale alofanya Mathayo kwa wanafunzi wa SUA 1998..Wanafunzi hao wanatumika bila wao kujua. Tatizo ninaloliona hapo ni mtu kushindwa kujua haki zake za msingi..hata kama huna chama ni wajibu wa serikali kusomesha na kutoa mikopo kwa wanafunzi wanafikia viwango. Sasa jamani JK ameamua kujizolea sifa za ubwete kwa hao wanafunzi 20 wakiwakilisha wenzao 1000 !!! Kali kweli kweli...

Jamani mwenye CV ya Makamba naomba anirushie huyo mzee sijui anaujuzi gani zaidi ya kuwa mfundisha siasa jeshini na kubebwa bebwa mpaka sasa... mzee anaweka usanii hata kwenye mambo ya msingi...I love you Makamba teh teh teh
 
Wangekuwa wamehamia upinzani hapo ingekuwa news au?

Anyway, wanafunzi wa vyuo vikuu huwa sielewi kabisa mambo yao.
Walivaa kijani na njano Diamond baada ya kufatwa na magari kutoka vyuoni, wakachukua kadi za ccm kibao, wiki iliyofuata walewale wakaandamana kwenda jangwani na kashfa kibao dhidi ya serikali kwa kushindwa kutekeleza habari yao ya mikopo.

Leo tena wanasifia na hapohapo anapouliza mtu asiyeridhishwa na mwenendo wa mikopo anashangiliwa, hiyo inatoa picha gani?

Na wao wameamua kuleta ushkaji na serikali ya kishkaji?
 
Njaa Mbaya sana.Jk anatumia silaha hiyo kuwakamata wasomi wetu,sidhani kama na wao wamejiunga kwa mapenzi yao
 
....njaa na nidhamu ya kujipendekeza ni vitu hatari sana katika demokrasi ya nchi yeyote duniani!
 
Jamani tulieni kidogo, hivi mtu akiamua kujiunga na chama anachokipenda ni kwa sababu ya njaa?!!! mbona huko CCM wapo maprofessa wengi wamepelekwa na njaa? Je Professa Wangwe ana njaa yoyote?...

Wametimiza haki zao jamani, tuwaache hao!!! naona FD amefurahi... sibiri sunami 2010,,, Mnyika atakuwa Prof. Tayari

si 1000 tu,,, wengine sijui 50,000 si wako upinzani? sasa tatizo nini?
 
Kilitime: Kwa hoja zako nyingi humu ndani, inaniwia vigumu sana kuamini kwamba wewe upo neutral kwa maana ya kuwa huna chama! Kwa nini usi-declare kama sisi (yaani: mimi, kada, FD, FMES, etc). Siku hizi mambo hadharani mkuu, hakuna shida, au siyo!
 
Jamani tulieni kidogo, hivi mtu akiamua kujiunga na chama anachokipenda ni kwa sababu ya njaa?!!! mbona huko CCM wapo maprofessa wengi wamepelekwa na njaa? Je Professa Wangwe ana njaa yoyote?...

Wametimiza haki zao jamani, tuwaache hao!!! naona FD amefurahi... sibiri sunami 2010,,, Mnyika atakuwa Prof. Tayari

si 1000 tu,,, wengine sijui 50,000 si wako upinzani? sasa tatizo nini?

Unajua mkuu, kinachobishaniwa hapa ni kwamba, ni hivi majuzi tu hapa wanafunzi hawa hawa walikuwa wanaandamana kupinga serikali ya kishikaji na chama chake, ambavyo vimewasahau kwa kutowapa mikopo ambayo raisi aliahidi,leo ndio hao hao tena wanapokea kadi za chama ambacho walikiponda pamoja na serikali yake.
Mgongano wa hoja na mawazo ndio unakuja hapa haswa. Kwamba, iweje hawahawa ndio waliponda chama majuzi na leo wanapokea kadi kwa chama hicho hicho? Nini kimewabadilisha mawazo ghafla?
Ugumu wa kufikiri unakuja hapa haswa mkuu.
Tuendelee kulumbana.
 
....njaa na nidhamu ya kujipendekeza ni vitu hatari sana katika demokrasi ya nchi yeyote duniani!

Hapa JF kuna unafiki wa hali ya juu kabisa. Kila leo watu mnasisitiza uhuru wa kujieleza / kutoa maoni nakadhalika. Leo vijana wameamua kujiunga na CCM, mnawasema vibaya kana kwamba nyie ndiyo mlioshika funguo za uhuru wao. Kwenda CCM siyo njaa ni matumizi ya uhuru wao kama vile nyie mnavyotumia uhuru wenu wa kujieleza.
 
Hapa JF kuna unafiki wa hali ya juu kabisa. Kila leo watu mnasisitiza uhuru wa kujieleza / kutoa maoni nakadhalika. Leo vijana wameamua kujiunga na CCM, mnawasema vibaya kana kwamba nyie ndiyo mlioshika funguo za uhuru wao. Kwenda CCM siyo njaa ni matumizi ya uhuru wao kama vile nyie mnavyotumia uhuru wenu wa kujieleza.

....njaa nyingine hii!
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom