Nazungumza hapa nikiwa ni mmoja wa wanaofuatilia suala hili na ninaomba mamlaka husika zilichunguze kwa kina, baadhi ya wanafunzi wa University of Dar es Salaam (UDSM) tuliingiziwa fedha za mkopo (boom) mara mbili kimakosa kutoka Bodi ya Mikopo (Higher Education Students' Loans Board - HESLB).
Kwa maelezo yanayotolewa, baadhi ya wanafunzi walitoa na kutumia fedha hizo kabla ya kubaini kuwa ziliingizwa kimakosa. Baada ya kosa hilo kugundulika, wahusika walifuatiliwa na kubainishwa.
Hata hivyo, malalamiko makubwa si kuhusu kurejesha fedha, bali ni namna ambayo baadhi ya wanafunzi wanadai wamekuwa wakifuatiliwa. Inadaiwa kuwa mchakato huo, unaohusisha TAKUKURU, umekuwa ukiambatana na vitendo vinavyodaiwa kuwa vya manyanyaso, ikiwemo kuwashikilia baadhi yao mahabusu (lockup) bila kufuata taratibu zinazostahili au kuwapa taarifa za kutosha kuhusu kituo wanachopelekwa.
Tunaomba mamlaka husika kuchunguza kwa kina namna zoezi hilo linavyotekelezwa ili kuhakikisha haki zETU wanafunzi zinalindwa huku serikali ikiendelea kurejeshewa fedha zilizolipwa kimakosa kupitia taratibu za kisheria na zinazozingatia utu wa kila mwananchi.
Pia tunaomba taasisi zinazohusika zitoe ufafanuzi kuhusu suala hili ili kuondoa sintofahamu na kuhakikisha hatua zinazochukuliwa zinazingatia sheria, haki na misingi ya utawala bora.