Miss Zomboko
JF-Expert Member
- May 18, 2014
- 4,495
- 9,275
IGP Simon Sirro
MKUU wa Jeshi la Polisi Tanzania, IGP Simon Sirro amesema, watu watano wanaoshukiwa kuhusika katika tukio la mauaji ya Watanzania tisa nchini Msumbiji, wanashikiliwa na vyombo vya dola nchini. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
IGP Sirro amesema hayo katika hafla ya uzinduzi wa nyumba 20 za polisi mkoani Geita leo tarehe 15 Julai 2019.
Aidha, IGP Sirro amesema mtuhumiwa mmoja kati ya watano waliokamatwa, amefariki dunia.
“Hata tukio la Msumbiji, niliahidi kwa Watanzania kwamba waliofanya hilo tukio, damu ya Watanzania haipotei bure. Mpaka sasa watu watano wamekamatwa na mmoja wao ametangulia mbele ya haki na wanatajana,” amesema IGP Sirro.
Wakati huo huo, IGP Sirro amesema mpango wa utekelezaji wa tukio hilo ulifanyika nchini Tanzania, huku utekelezaji wake ukifanyika nchini Msumbiji.
IGP Sirro amesema, Jeshi la Polisi nchini linashirikiana na Jeshi la Polisi la Msumbiji kuwachukulia hatua waliohusika na mauaji hayo.
“Inaonekana kwa kweli plan ‘mpango’ yote ilifanyika nchini kwetu, tukio lilifanyika Msumbiji. Kimsingi wote wamepatikana wanaendelea kutajana, operesheni inafanyika kwa kushirikiana na wenzetu wa Msumbiji,” amesema IGP Sirro.