Walimu 'cha pombe' watavumiliwa hadi lini?

Pdidy

JF-Expert Member
Nov 22, 2007
50,907
22,053
Walimu 'cha pombe' watavumiliwa hadi lini?

Kuruthum Ahmed

ALHAMISI iliyopita niliamka alfajiri kama ilivyo ada kwa ajili ya kujiandaa kuelekea kibaruani.Ilipofika saa 1:00 asubuhi nilianza safari ya kwenda kituoni Mwembeni kwa ajili ya kupanda gari.

Nilipokuwa kwenye gari linalofanya kazi kati ya Ubungo na Tabata kijana mmoja wa makamu aliingia akaja kuketi karibu yangu.

"Dada za saa hizi?", alinisabahi, nami nikamjibu, "Nzuri tu". Ukweli ni kwamba alipofunua kinywa chake kusalimia, sote tuliokuwa karibu tuligeukiana maana ni kama pombe iliyochalala imemwagika kutokana na harufu iliyotoka ndani ya mdomo wake.

"Kaka unaelekea wapi?" nilimuuliza haraka ili nijue kama alikuwa anakaribia kushuka ili niondokane na kadhia hiyo.

"Naenda kazini", alinijibu. Sikuridhika na jibu hilo nikabandika jingine; "Kazi gani?"

Naye akidhani kwamba huenda nilikuwa 'nimemzimia' akanijibu haraka; "Mimi ni mwalimu.Vipi dada yangu una wasiwasi nami?" alinihoji nami nikamwambia ni vizuri binadamu kufahamiana.

Ndiyo hakufika mbali akashuka na kuacha abiria waliokuwa karibu yetu wakiuliza maswali bila kujibiwa. "Hivi huyo ni mwalimu kweli? Anakwenda kufundisha nini? Hawa si ndio wanatuharibia watoto wetu," aliuliza mama mmoja.

"Iwapo harufu kali kama hiyo iliyotoka mdomoni kwake imekuwa kero kwetu kwa muda mfupi tu, je, wale anaoshinda nao, walimu na wanafunzi anaowafundisha?" nilihoji.

"Kwa nini serikali haiwadhibiti wafanyakazi kama hao au imewashindwa?"nilijisemea kimoyomoyo.

Nilisema hivyo kutokana na ukweli kwamba viongozi kadhaa wamekuwa wakitoa kauli na matamko ya kupiga marufuku ulevi kazini, kunywa wakati wa kazi na hata siku za kazi yaani Jumatatu hadi Ijumaa isipokuwa Jumamosi na Jumapili.

Huyo si mwalimu pekee 'cha pombe' kwani uchunguzi uliofanywa na Mwananchi nchi nzima unaonyesha kwamba hili ni tatizo sugu. Wengi wao ni wale wanaokatishwa tamaa na mazingira ya kazi.

Mathalani katika wilaya ya Newala mkoa wa Mtwara walimu 117 wa shule mbalimbali za msingi inadaiwa wamekithiri katika unywaji wa pombe, hali inayowafanya washindwe kutekeleza vyema majukumu yao ya kazi kama inavyotakiwa.

Afisa elimu wa wilaya hiyo, Uzia Ibrahimu analijua tatizo hilo. Wananchi wa vijiji vya Tawala na Chihangu walimbwagia tatizo hilo walipokuwa wakichangia mjadala kuhusu maendeleo ya elimu wakati wa maadhimisho ya wiki ya elimu duniani hivi karibuni.

Afisaelimu huyo mwenye dhamana ya kusimamia elimu wilayani humo, alijibu hoja nyingi lakini hiyo ilikuwa chungu aliishia kusema idara yake iliwaagiza walimu wakuu na maafisa elimu kata, kuorodhesha walimu wanaojihusisha na vitendo vya ulevi, utoro na uzembe kazini na kupatikana kwa idadi hiyo.

"Nataka niwaeleze ndugu zangu wazazi, kuwa tatizo hili tayari tumeliona na tumeanza kulifanyia kazi na kwa kuanzia walimu hawa tumewakabidhi kwa Idara ya Huduma za Walimu (TSD) wilayani kwa hatua za awali, kabla ya kuendelea na utaratibu mwingine wa kinidhamu.

Lakini katika hili ninyi pia mnachangia, kwani ndio mnaowapa pombe walimu tena hata muda wa madarasani mnakunywa nao, tubadilike," alisema Uzia.

Tofauti na miaka iliyopita wakazi wa vijijini sasa wanajua umuhimu wa elimu kwa watoto wao ndiyo maana wakazi wa Chihangu kata ya Mkunya walikuwa wa kwanza kulalamika juu ya tabia ya baadhi ya walimu wa shule zao za msingi kujihusisha zaidi na masuala ya ulevi na kusahau majukumu ya kazi zao.

Walidai hali inawafanya watoto wao kukosa masomo na hivyo kupoteza ari ya kwenda shule na matokeo yake ni kukithiri kwa utoro shuleni.

"Sisi kila siku, tunawaona walimu wakiwa katika vibanda vya pombe wakati watoto wanacheza nje katika muda ambao walitakiwa kuwepo darasani. Hii ni hujuma ya wazi kwani wanalipwa mishahara inayotokana na kodi zetu bila ya kuzifanya kazi, tunaomba hali hii irekebishwe,"alisema Zainabu Bakari mkazi wa kijiji cha Chihanga.

Tatizo la ulevi kama anavyokiri mratibu wa elimu kata ya Mchuli II, Frederick Mmole, linajulikana. Jamii inawajua walimu walevi, lakini inawachukulia hatua gani kudhibiti maana kujua tatizo ni sehemu ya ufumbuzi. Kwa mtazamo wangu, pamoja na madai ya hali ngumu ya maisha, udogo wa mishahara nk, kulewa kupita kiasi au kwenda shuleni mwalimu (mfanyakazi) akiwa amelewa (eti wanaahirisha matatizo) haikubaliki. Watu hao waadhbiwe kwa mujibu wa sheria.
 
Hii hebu iwekeni kule kwenye jukwaa la elimu, itasaidia kujua moja ya sababu ya kushuka kwa kiwango cha elimu nchini.
 
Back
Top Bottom