Miss Zomboko
JF-Expert Member
- May 18, 2014
- 4,500
- 9,279
Dar es Salaam. Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imewataka wakuu wa kituo cha polisi Kijitonyama na Oysterbay kufika mahakamani hapo leo Ijumaa Oktoba 25, 2019 kueleza sababu za kukaa na mtuhumiwa kwa siku 14 badala ya kumpeleka gereza la Segerea.
Mtuhumiwa huyo, Elizabeth Balali alifikishwa mahakamani hapo Oktoba 10, 2019 akikabiliwa na mashtaka ya kujipatia Sh25 milioni kwa njia ya udanganyifu na utakatishaji fedha.
Elizabeth anayedaiwa kuwa msimamizi wa mali za mke wa gavana wa zamani wa Benki Kuu Tanzania (BoT), marehemu Daudi Balali, siku hiyo alisomewa mashtaka na wakili Wankyo Simon mbele ya hakimu mfawidhi, Kelvin Mhina.
Jana Alhamisi Oktoba 24, 2019 mshtakiwa huyo alifikishwa katika mahakama hiyo akitokea kituo cha polisi Kijitonyama, na Mhina ambaye alisikiliza kesi hiyo mara ya kwanza kuagiza arejeshwe kituoni na kutaka wakuu wa vituo hivyo kufika mahakamani kesho kujieleza.
“Nataka kesho waje wajieleza kwa nini wamekaa na mshtakiwa kwa siku 14 katika vituo vya polisi badala ya kumpeleka Segerea kama mahakama ilivyoagiza,” amesema Mhina.
Akimsomea mashtaka Oktoba 20, 2019 wakili wa Serikali Wankyo Simon alidai kati ya Oktoba 19 na Desemba 21, 2017 jijini Dar es Salaam, mshtakiwa alijipatia Sh25 milioni kwa ulaghai kutoka kwa Dk Roderick Kisenge kwa kumuuzia eneo la mita 900 ambalo halijapimwa lililopo Boko Dovya wilayani Kinondoni wakati akijua si lake.
Katika shtaka la utakatishaji fedha, Wankyo alidai katika kipindi hicho mshtakiwa alipokea Sh25 milioni kutoka kwa Dk Kisenge kupitia akaunti yake iliyopo Benki ya CRDB wakati akijua fedha hizo ni zao la kosa la kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu.
Baada ya kusomewa mashtaka hayo, Elizabeth hakuruhusiwa kuongea chochote kwa sababu mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza makosa ya uhujumu uchumi.
Hakimu Mhina katika kesi hiyo ya uhujumu uchumi namba 109/2019 alimueleza mshtakiwa huyo kuwa licha ya mahakama kutokuwa na uwezo wa kuisikiliza, pia shtaka la utakatishaji wa fedha halina dhamana.
Siku hiyo ilielezwa mahakamani hapo kuwa upelelezi wa kesi hiyo haujakamilika na kuahirishwa hadi leo ambapo imebainika kuwa alikuwa katika vituo hivyo badala ya Segerea.
======
CHANZO: Mwananchi