Wakati tunamzika simba wa vita mzee rashid kawawa leo yawapasa viongozi wetu kujiuliz

Mtambuzi

Platinum Member
Oct 29, 2008
8,810
15,395
Katika familia zote duniani baba mwenye busara na mama mwenye upendo wanapofariki, vilio huwa vingi na mashaka huzikumba familia. Baba ambaye ni baba tu kwa sababu alioa na kuzaa watoto na mama ambaye ni mama tu kwa sababu aliwaweka watoto tumboni kwa miezi tisa na kuwanyonyesha lakini wote wakiwa hawajui majukumu yao na hawakufanya lolote kubadili na kujenga maisha ya familia, hao wanapoliliwa ni kwa sababu ya mazoea tu.

Hali hii pia ipo kwa viongozi katika jamii zote duniani. Kiongozi ambaye mchango wake wa mawazo uligeuzwa kuwa vitendo na umeusaidia jamii, ni kiongozi ambaye hawezi kufa. Kiongozi wa namna hii huendelea kudumu kwa kadri dunia inavyoendelea kuwepo. Kiongozi ambaye ni kiongozi kwa sababu amekalia kiti cha enzi na anayo nafasi ya kutoa amri na hana mchango wowote katika jamii huyo hata akifa jamii haiwezi kujali, huyo akifa ni kwamba kafa, yaani amekufa kabisa hana tofauti na mzururaji asiyejua anakoelekea.

Leo hii Edward Moringe Sokoine, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, na hivi Juzi Rashid Mfaume Kawawa, wamekufa, lakini bado wanaishi na jamii ya Watanzania. Kwa watu wenye Utambuzi wanawakumbuka na watawakumbuka kwa muda mrefu. Pamoja na baadhi ya watu kuwadharau viongozi hawa ukweli utaendelea kusimama kwamba walikuwa wabunifu.

Hebu tuanze kujiuliza kama viongozi wetu kwenye nafasi zao wakiwa ni makatibu kata, wakuu wa wilaya, wakuu wa mikoa, makatibu wakuu, mawaziri na wengine, uongozi wao una maana gani, je wanajua dhamana ambayo wameibeba kwa wananchi ambao wanawaongoza au wanadhani kukalia viti ndio uongozi wenyewe?

Kila mmoja mwenye nafasi yake ajiulize, kama akifa kesho jina lake litabaki hapa duniani kwa kile au vile alivyofanya au litabaki kinafiki tu kwa mtaa au barabara fulani kupewa jina lake? Kama wewe ni kiongozi kwa wiki nzima huwa unajitathimini na kuona umewatendea nini wananchi? Kama hufanyi hivyo ni upi basi uongozi wako? Au ni kusimama jukwaani na kupayuka tu na baadaye kwenda kula kunywa na kulala?

Wakati Viongozi wetu leo hii wanalia kwa kuondokewa na shujaa huyu Simba wa Vita Mzee Rashid Kawawa, nadhani huu ni wakati muafaka kwao kujifanyia tathmini ili kujua kama na wao watakumbukwa kwa lipi umauti ukiwafika?

Bila shaka Mungu alituumba kama binadamu kwa malengo, kwani ungekua ni ujinga mkubwa kwake kutuumba tu akiwa hana malengo kwa kuwa ingekuwa na maana kwamba naye hana malengo pia. Malengo yetu kama binadamu hapa duniani ni nini hasa? Bila shaka hilo ni swali gumu sana kwa wengi wetu kwa sababu huenda haijatupitia hata mara moja kujiuliza swali hilo. Tunachojua ni kwamba tunatafuta fedha, kula, kulala na starehe na huenda tunaamini hayo ndiyo malengo yetu.

Ndiyo maana wengi wetu huwa tunathubutu kusema “fulani ana fedha siku hizi, maisha yameshamnyookea” kwa sababu kwetu kuwa na fedha na kustarehe hata katikati ya fukuto la umasikini wa wengine ndiyo lengo letu maishani. Hata viongozi wengi wanaonekana kuamini kwamba lengo la maisha kwao na hata sababu za uongozi wao ni kutafuta starehe.

Kiongozi anayekaa madarakani bila kubuni chochote na badala yake kuwa kusuku wa mambo anapaswa kuona aibu sana, kwani kama wengi wetu hata yeye hajui njia anayoifuata ni wazi tutapotea zaidi. Kiongozi ambaye hawezi kulala na kuamka asubuhi akiwa na mawazo mapya ambayo yanapoingizwa kwenye utekelezaji yatabadili hali ya maisha ya wananchi hapaswi kujiita kiongozi, kwa sababu huyo siyo kiongozi.

Hebu viongozi walio madarakani sasa wajiulize, katika kipindi ambacho wamekaa katika uongozi watakumbukwa na nani, kwa yale waliyoyabuni ambayo yamepelekea watu au eneo fulani la nchi kubadilika angalau kwa kiwango kidogo sana. Kama kiongozi hawezi kujiuliza mchango wake kama yeye kwa jamii, hapaswi kuitwa kiongozi, kwani ni sawa na kujidhihaki mwenyewe na pia kudhihakiwa na jamii.

Kwa nini mkuu wa mkoa au waziri akae kwenye kiti hicho kwa miaka mitano au kumi ikwa na maana yasiku 1,825 au siku 3,650 na bado hata baada ya mda huo akashindwa kubuni lolote la maendeleo ambalo litamfanya aendelee kudumu vichwani mwa wananchi? Uongozi maana yake ni kulala na kufikiria lengo la kuipeleka jamii mbele. Sasa iweje mtu ashindwe katika zaidi ya siku elfu moja kubuni angalau jambo moja la maana kwa jamii, kwa nini kushindwa huko isiwe ni aibu kubwa kwake?

Umefika muda bila shaka kwa jamii kuwajali tu wale viongozi ambao wanaweza katika muda wao wa uongozi kubuni angalau jambo moja lenye kulenga kubadili hali ya wanajamii.
 
Back
Top Bottom