Wajumbe wamfungia ofisi Katibu wa CCM (w)

Candid Scope

JF-Expert Member
Nov 8, 2010
11,883
6,884
Wajumbe wa kamati ya siasa ya Chama cha Mapinduzi (CCM) wilayani Namtumbo mkoa wa Ruvuma wamemkataa Katibu wa CCM wa wilaya hiyo, Getruda Lupola na kufunga ofisi yake kwa makufuri zaidi ya mawili kwa madai kuwa hajawahi kuitisha vikao vya kamati hiyo kwa kipindi cha miezi nane. Akiongea na waandishi wa habari Katibu Mwenezi wa chama wa wilaya hiyo, Reagan Luambano, alisema licha ya kutoitisha kamati ya siasa kwa kipindi hicho pia kwa kipindi cha miaka mitano ameshindwa kuitisha vikao vya Halmashauri Kuu ya CCM ya wilaya. Alisema kila mara kamati ya siasa ilikuwa ikimtaka aitishe vikao lakini katibu huyo alikuwa akikataa jambo ambalo limekuwa kikwazo kikubwa kwa maendeleo ya chama hicho.

Luambano alidai kuwa Januari 29, mwaka huu kamati hiyo ilikutana na katibu huyo wa chama wa wilaya ambapo walimwuliza kwa nini haitishi vikao vya chama lakini aliwajibu kuwa angeitisha Februari 20, mwaka huu jambo ambalo halikufanyika. "Ilipofikia tarehe hiyo alifunga simu zote za mikononi na tulipomfuata alitueleza kuwa hawezi kuitisha vikao hivyo kwani aliagizwa na CCM makao makuu kupitia kwa katibu wake wa chama wa mkoa asiitishe vikao hadi kipindi cha uchaguzi mwaka 2015," alisema Luambano.


Alisema baada ya wajumbe wa kamati ya siasa kuona mwenendo wa chama sio mzuri Machi 16, mwaka huu walikutana chini ya mwenyekiti wao wa CCM wa wilaya, Edmund Ngonyani, kujadili kwa kina mstakabali mzima wa suala hilo na baadaye walifikia uamuzi wa kumkataa katibu huyo kutofanya shughuli zote za CCM katika wilaya. Alifafanua kuwa kamati ya siasa inapaswa kukutana kila mwezi mara moja lakini imekuwa tofauti jambo ambalo ni hatari kwa uhai wa chama.


Alibainisha zaidi kuwa mapato na matumizi ya chama hicho yamekuwa hayasomwi na kwamba katibu huyo amekuwa akikusanya fedha toka kwa wafadhili mbalimbali kwa ajili ya ujenzi wa ofisi ya CCM wilaya bila kamati ya siasa kujua. Hata hivyo katibu wa CCM wa wilaya ya Namtumbo alipoulizwa na NIPASHE kuhusiana na tuhuma zinazomkabili alisema yeye hafahamu lolote na kwamba hana tatizo lolote na baadaye alikataa kuongea zaidi.
 
Back
Top Bottom