Wadogo zangu, kabla TV hazijaja enzi hizo mgeni alikuwa anapewa album atazame picha za zamani. Yaani umpe Mtanzania album asichomoe picha hata moja?

Infantry Soldier

JF-Expert Member
Feb 18, 2012
15,893
16,317
Mambo vp JamiiForums.

Nyie watoto mliozaliwa mwaka 2003 mnajua nini maana ya album? Achana na hizo album ambazo baba/mama yako anakuonesha katika smartphones na tablets. Mimi siongelei albums za google photos, sujui google drive mara facebook mara sijui nini wenyewe mnaita Instagram.

Hivi mnajua hapo zamani mpiga picha alikuwa ni mmoja au wawili tu mtaa mzima na walikuwa wanaringa sana kwa maana wakati huo hakuna smartphones.

Ukitaka kupiga picha baada ya kushiba pilau la sikukuu ni lazima uende ukamuite baba Amina yule wa jirani au mama awachukue mpaka studio ya mzee Khamis kwa maana ndio studio pekee unayoweza kupiga picha mtaa mzima. Alafu kumbuka siku hiyo ni sikukuu hivyo ni lazima ukutane na foleni ya kufa mtu. Unafanya masihara nini na kupiga picha.

Anyway ngoja nisiende mbali sana wadogo zangu mliozaliwa mwaka 2003 kuja juu. Album ni likitabu limoja likuuuubwa hivi ambalo ndani yake zinahifadhiwa picha za kumbukumbu ambazo baba na mama walipiga wakiwa na rafiki zao pamoja na ndugu enzi za ujana wao. Kama baba yako alikuwaga Polisi zamani, tegemea kukuta amepiga picha akiwa amevaa bukta ya kazi na sio suruali kama sasa hivi.

Hizi albums ndizo ambazo zilikuwa ni burudani ya mwenyeji kumpa mgeni kabla ya TV kuingia hapa Tanzania miaka hiyooo ya zamani. Hahahahaaaaa, ona sasa unavyoshangaa mgeni kupewa album aangalie badala ya kumuwashia TV aangalie movies za DSTV au thamthilia ya sultani.

Enzi hizo kulikuwa hakuna TV kabisa mdogo wangu na kama zilikuwepo basi ni moja au mbili tu mtaa mzima, tena ni katika zile nyumba ambazo unakuta baba au mama alienda kusoma Ulaya kisha akarudi nayo. TV na deki na mikanda kibao ya Rambo, Anodi, Cheki Noris na wengineo kibao.

Familia nyingi hazikuwa na TV wala deki kwa ajili ya kumpa burudani mgeni baada ya kuwa amekwishakunywa soda. Wao walikuwa na album. Upo zako nje unatengeneza magari ya udongo unasikia "Edoooo, nenda chumbani juu ya kabati kuna album mbili mletee shangazi aone", walikuwa wanatoa album mbili au tatu kwa ajili ya mgeni kutazama picha zao za zamani enzi hizo za ujana wakiwa wanaruka majoka na muziki wa bendi kama Morogoro Jazz, Tabora Jazz, Tancut Almus, Sikinde, Msondo. Wakati huo viwanja vya kijanja ndio kama vile DDC keko, DDC Kariakoo, Billcanas.

Picha unakuta picha kweli hata kama ilikuwa ni black & white lakini ni HD ya maana. Unakuta mama anawaambia "unaona picha hii niliyopiga chini ya maua, ndio kipindi hiki ninakaa kwa shangazi Morogoro na baba yenu alikuwa anakaribia kuja kutoa posa" hahahahaaaaa basi watoto mnacheeeeeeeka hamna mbavu, lakini siku hizi jaribu kukaa sebule moja mama, watoto pamoja na mgeni kisha mtazame maigizo yale wanayoyaita bongo movie au kipindi kile cha channel ile ya vijana mara paaaaap tangazo la pedi au condom limepita na mama anauliza jamani remote ipo wapi.

Kuna wakati huwa ninajiuliza sijui wazee wa zamani walikuwa wanajua sana kutunza picha au cameras na printing materials zilikuwa imara zaidi ya sasa. Unakutana na picha mama anakwambia "Unamuona huyu? Huyu anaitwa ******** ndio waziri sasa hivi na hapa ni mwaka 1979 tunasubiri treni kurudi shule Tabora Girls" mpaka unabaki mdomo wazi hee kumbe flani alisoma na mama yangu shule moja, sasa muulize kijana wa mwaka 2003 picha yake ipo wapi kama hajakwambia ipo GOOGLE DRIVE.

Tatizo moja kuu ambalo TV limekuja kuokoa hizi album ni kasumbua hii ya uchomoaji wa picha. Yaaani mtanzania akute picha yake ya zamani enzi hizo ndio ametoka vita ya Kagera asiichukue?

Eti shangazi Sikujua akutane na picha yake aliyopiga mwaka 1971 alipokuwa anafanya kazi East African railways asiifiche ndani ya kitenge? Thubutu! Ilikuwa ni ngumu sana kumpa mtu album atazame kisha irudi kama ilivyo. Ngumu sana. Ni lazima tu siku moja utagundua kuna picha kadhaa huzioni. Hakika ya kale ni dhahabu.

USISAHAU: ENDELEA KUWA MZALENDO IPENDE TANZANIA. USICHAFUE TASWIRA NJEMA YA TAIFA LAKO. USTAWI WA NCHI YETU UNAANZA NA WEWE. TIMIZA WAJIBU WAKO IPASAVYO.
 
Nakumbuka mzee alikua na video tapes za Enrique Iglesias kulikua na videos kama bilamooooooos, sad eyes, maria maria za kina santana, kina Britney Spears, mzee alikua anamkubali sana Enrique mpaka akaniambukiza na mimi! Kipindi hicho Pierce Bosnan ndo alikua James Bond mpaka leo hii hizo ngona naskiliza! I realy miss me.
 
Ajabu akija kwenu kachomoa anaenda kwake anaiweka kwenye album yake.

Siku ukienda kwake anakupa album yake uangalie ghafla unakuta ile picha ambayo huionagi nyumbani

Kimoyomoyo unasema kumbe bibi / babu na wewe ni mwizi ee?

Mwisho wa siku album yenu inabaki tupu

Sijui kwanini
 
Dah, miaka ya 99 kipindi hcho nimeenda chuo mkoani yaani kila mgeni atayekuja anatolewa album yangu na nyingine za nyumbani, utasikia hyu ni mwanangu wa pili anasoma chuo huko mkoani, jamani karibia kila mgeni anaondoka na picha yangu mpaka nkawa najiuliza hivi mama yangu ananitakia nini.
 
Kumbukumbu nzuri enzi hizo mpira wa makaratasi sodo anayo mtu mmoja, huyo uwanjani hamtakiwi kumkanyaga na yeye ndio anapanga nani acheze au asicheze na mkimkanyaga mpira anaweka kwapani na mchezo unaishia hapo, au ilikua lazima mkamsaidie kazi kama kuteka maji au kuosha vyombo ili muwahi kwenda kucheza.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom