Wachagossia waanza kuona mwanga baada ya Uingereza kukubali kufanya mazungumzo juu ya hatma ya visiwa vyao

ldleo

JF-Expert Member
Jan 9, 2010
1,010
1,034
VCG31N1145557226.jpg

PILI MWINYI

Uingereza hivi karibuni ilitangaza kukubali kufanya mazungumzo na Mauritius juu ya hatma ya visiwa vya Chagossia, ikionekana kurudi nyuma kidogo baada ya kugoma kwa siku nyingi kufanya mazungumzo hayo licha ya shinikizo kubwa iliyokuwa ikipata kutoka nchi mbalimbali duniani. Kwa juu juu tunaweza kusema hii ni hatua ambayo inajaza matumaini hasa kwa wazawa wa kisiwa hicho ambao kwa miaka mingi wamenyimwa haki na uhuru wao wa kuishi kwenye nchi yao.

Wachagossia kwa miongo kadhaa wamekuwa wakitaka kurejea nyumbani kwao baada ya Serikali za Marekani na Uingereza kuwafukuza zaidi ya watu 1,000 katika miaka ya 1960 na 1970 ili kutoa nafasi ya kujenga kambi ya kijeshi ya Marekani kwenye kisiwa cha Chagossia “Diego Garcia” huku ikiwaacha wenyeji wa visiwa hivyo bila chochote. Tangu kufukuzwa kwao, Wachagossia wamekuwa wakiishi katika umaskini na kuhangaika kurejea katika nchi yao na kudai kupewa fidia ipasavyo kwa yote waliyoteseka.

Mauritius, ambayo ilijipatia uhuru wake kutoka kwa Waingereza mwaka 1968, inashikilia kuwa visiwa hivyo ni vyake na Wachagossia wamepigania kurudi kwao katika mahakama za Uingereza. Sasa mahakama ya juu zaidi ya Umoja wa Mataifa, Mahakama ya Kimataifa ya Haki mjini The Hague, imeamua kwamba utawala wa Uingereza kwenye eneo hilo ni "kinyume cha sheria" na ni lazima ukomeshwe.

Awali mwaka 2019 mahakama hiyo ilitoa uamuzi kama huo, lakini Uingereza iliupuuzilia mbali uamuzi huo eti ikidai kuwa ulitolewa kwenye misingi ya ushauri tu, lakini msimamo huu wa Uingereza ukawa hauwezi kuvumiliwa tena kwani bila shaka unaonekana kukiuka sheria za kimataifa.

Ingawa Uingereza sasa imekubali kukaa chini na wahanga hao lakini bado hatujajua maamuzi halisi yatakayotolewa na upande huo unaoonekana kutumia nguvu na ubabe kupata kile inachotaka, na kama kweli itaikabidhi Mauritius visiwa vyake vya Chagossia. Ikumbukwe kuwa tangu mwanzoni kumekuwa na kauli tata kidogo zinatolewa na Uingereza na Mauritius. Mara nyingi zimekuwa zikisisitiza kuwa makubaliano yoyote kati ya nchi hizo mbili yatahakikisha kuwa operesheni ya kambi ya pamoja ya kijeshi ya Uingereza na Marekani, ambayo ina jukumu muhimu katika usalama wa kikanda na kimataifa huko Diego Garcia inaendelea kwa ufanisi.

Hivyo kuelekea mazungumzo hayo kuhusu mustakabali wa Visiwa vya Chagossia, Uingereza inapaswa kuzingatia haki za watu wote wa Chagossia, kwasababu ushauri na ushiriki wa wahanga walioumizwa vibaya kwa kufukuzwa kwa nguvu ni muhimu kwenye mazungumzo haya, ambayo pia yanapaswa kuhakikisha malipo kamili ikiwa ni pamoja na haki ya kurudi kwa Wachagossia wote kisiwani kwao.

Kufunguliwa kwa mazungumzo hayo pia kunaipatia Uingereza, Marekani, na mamlaka ya Mauritius fursa ya kipekee ya kusahihisha makosa waliyotendewa watu wa Chagossia kwa nusu karne sasa. Pia inamaanisha kuwa Uingereza ni lazima iwapatie malipo kamili, haki yao ya kurejea kwa heshima na ustawi wao, pia kuwapa fidia kamili kwa madhara waliyoyapata na kuhakikisha kwamba dhuluma kama hizo hazitatokea tena.

Tukio hilo ambalo ni la aibu zaidi kufanywa na ukoloni wa Uingereza baada ya vita, lilivigeuza tena visiwa hivyo na kuwa kama chombo cha kikoloni na pia Eneo la Bahari ya Hindi kuwa la Uingereza, huku kisiwa chake kimoja cha Diego Garcia kuwa kambi ya Marekani. Hivi sasa kwenye kambi hiyo kuna wafanyakazi zaidi ya 2,000 wanaohudumu wa Marekani, pamoja na wafanyakazi wa muda, hasa Wafilipino.

Juu ya yote hayo, bado tunaweza kusema kuwa kwa hatua hii ya Uingereza kukubali kukaa chini kuzungumza, mwanga unaanza kuonekana kwa mbali baada ya giza nene kutawala katika kipindi chote hicho. Na pia Wachagossia pamoja na Afrika kwa ujumla wana kila haki ya kukunjua mioyo yao kwani ushindi unaelekea kupatikana. Kwa sababu ni Dhahiri kuwa dunia imetambua nchi kubwa kama Uingereza au Marekani kufanya ukoloni mambo leo kwa nchi ndogo kama hiyo ya kisiwa cha Chagossia, ni kitendo kisichovumiliwa na jamii ya kimataifa na kinapingwa vikali.
 
Back
Top Bottom