Wabunge wenzangu waniunge mkono, Mimi niko tayari Bunge hili livunjwe

Kibo10

JF-Expert Member
Aug 20, 2013
11,277
8,840
"Wabunge tunataka tupate fursa ya kufuta misamaha ya Kodi Inayoifilisi Nchi hii kwa sababu mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) amesema misamaha ya Kodi kwa mwaka jana 2013/2014 Ilikuwa 1.5Tillions. Mhe.Naibu Spika, naomba muongozo wako, ni lini Serikali italeta Bungeni muswada wa kufutwa kwa misamaha ya Kodi na kusomwa kwa mara ya kwanza na nitakuwa Mbunge wa kwanza kuja na hoja ya kumfukuza na kumwondoa Spika Bungeni. Haya mambo ya Wabunge kutishwatishwa kwa Sababu ya kukwamisha bajeti ya Serikali, nawaomba Wabunge wenzangu waniunge mkono, Mimi niko tayari Bunge hili livunjwe nirudi Mwibara huko Bunda nikalime pamoja na kuvua dagaa". Alisema Mheshimiwa Kangi Lugola ambaye ni Mbunge wa (CCM) Jimbo la Mwibara lililopo Bunda, Mara.
======================================


Dodoma. Mbunge wa Mwibara (CCM), Kangi Lugola amesema iwapo Muswada wa Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT), hautapelekwa bungeni, atakusanya saini za wabunge ili kumwondoa madarakani Spika wa Bunge, Anne Makinda.

Lugola aliyasema hayo jana alipokuwa akiomba mwongozo wa Spika ni lini muswada huo unaolenga kufuta misamaha ya kodi utaletwa bungeni.

Alisema amepata taarifa kutoka kwa Mwenyekiti wake wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali ya Mitaa (Laac), Rajab Mborouk Mohamed ambaye ni mjumbe wa Kamati ya Uongozi kuwa kamati hiyo iliiagiza Serikali kuwasilisha haraka Muswada wa VAT.

Alisema lengo la kutaka muswada huo uletwe bungeni ni kupitia na kufuta misamaha yote ya kodi isiyo na tija.

Alisema ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa mwaka 2012/2013 inaonyesha kuwa kuna misamaha ya kodi ya Sh1.5 trilioni nchini.

"Bajeti yetu ya mwaka jana inaonekana ina upungufu wa Sh1.5 trilioni na kusingekuwa na misamaha ya kodi mwaka jana tusingekuwa na upungufu huo," alisema.

"Wabunge tumekuwa tukiilazimisha Serikali iongeze fedha. Wabunge ndiyo waliomchagua Spika na Spika ameonyesha kuipendelea Serikali ilhali wananchi wanashindwa kupata maendeleo," alisema.

Alihoji ni lini muswada huo utaletwa bungeni kwa sababu karibu Bunge la Bajeti linaelekea ukingoni.

"Haya mambo ya wabunge kutishwatishwa kwamba tukikataa Bajeti ya Serikali Bunge litavunjwa. Mimi niko tayari Bunge livunjwe nirudi Mwibara nikalime na kuvua dagaa," alisema.

Alisema kama muswada huo hautaletwa katika Bunge la Bajeti atakuwa mbunge wa kwanza kuleta hoja ya kumtaka spika afukuzwe kwenye kiti hicho kwa sababu anaibeba Serikali.

Alipoulizwa baadaye jana jioni sababu ya kumng'ang'ania Spika, Lugola alisema: "Ndiye Mwenyekiti wa Kamati ya Uongozi ambayo hupanga ratiba. Ukitazama ratiba ya mkutano huu, hakuna mahali panapoonyesha Serikali italeta muswada huo wa VAT badala yake, Serikali inasema tu kwa mdomo na yeye ndiye Mwenyekiti wa Kamati ya Uongozi," alisema Lugola.

Akijibu, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi alisema Serikali ndiyo iliyoomba kuleta Muswada wa VAT katika Bunge hili bajeti... "Hana sababu ya kumsingizia Spika kuibeba Serikali.

Tunakusudia kuuleta katika Bunge hili ili usomwe mara ya kwanza na tungependa upite katika hatua zote."

Siku chache kabla ya kuanza kikao hicho cha Bunge, Lukuvi alisema Serikali itawasilisha bungeni rasimu ya maboresho ya VAT ambayo itafuta misamaha ya kodi hiyo na kwamba mpango huo unafanyiwa uchambuzi na Serikali na kwamba utawasilishwa katika wiki ya pili ya Bunge la Bajeti.

Kwa nyakati tofauti, mwenyekiti wa CUF ambaye pia ni mtaalamu wa uchumi, Profesa Ibrahim Lipumba na wadau mbalimbali wa uchumi walikuwa wakipigia kelele wingi wa misamaha ya kodi wakisema imekuwa ikipoteza kiasi kikubwa cha mapato ya Serikali.

Profesa Lipumba alisema hivi karibuni kuwa ili kuondoa kasi ya ukuaji wa nakisi, Serikali inatakiwa kufuta kabisa misamaha holela ya kodi inayofikia Sh1.8 trilioni ambayo ni sawa na asilimia tano ya pato la taifa.

Waziri wa Fedha, Saada Mkuya wakati akiwasilisha mpango wa Bajeti ya mwaka 2014/15 kwa wabunge, alisema Serikali imepanga kukamilisha utungwaji mpya wa Sheria ya VAT.

Alisema hatua hiyo itakwenda sambamba na kuongeza wigo wa kodi kwa kuimarisha vyanzo vilivyopo na kuanzisha vyanzo vipya pamoja na kurasimisha sekta isiyo rasmi ili iingie kwenye mfumo rasmi wa kodi.

Chanzo:Mwananchi
 
hiyo Ndio serekali ya ccm.
ningemuona wa maana kama angejitenga nayo ili asiwe sehemu ya mfumo unao ifilisi nchi hii.
 
Back
Top Bottom