Wabunge Fungeni Virago mwende kwenu - Fr. Karugendo

Sumaku

Member
Feb 17, 2009
53
1
Wabunge Fungeni Virago Mwende Kwenu!

Na Padri Privatus Karugendo

KATIKA hali ya kawaida hakuna Mtanzania aliyekuwa na imani kwamba Wabunge wetu wangeweza kukwamisha Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka 2009/2010; wengi tuliamini ingepitishwa kama zinavyopitishwa zote kila mwaka. Kuna sababu nyingi za kuamini hivyo: Idadi kubwa ya Wabunge ni ya chama tawala, Bajeti inaandaliwa na serikali, na !serikali inaongozwa na chama tawala: Haiwezekani chama kikajikwamisha hata kama bajeti ingekuwa mbaya namna gani. Rais wa nchi anatoka chama tawala yeye ndiye mwenyekiti wa chama hicho tawala; hotuba yake kabla ya bajeti ilikuwa inatengeneza njia; uchaguzi mkuu ni mwaka kesho, wabunge wote wa chama wanapita katika mchakato wa chama, hivyo ni lazima kuwa “watoto” wazuri ili wateuliwe kugombea tena katika uchaguzi mkuu ujao; hata hivyo hakuna historia ya Bunge la Tanzaniaa kukwamisha bajeti.

Tunajua sote na wala hili halihitaji majadiliano; wananchi hawashirikishwi katika kuandaa bajeti; mashirika yasiyokuwa ya serikali (NGO na CBO) hayashirikishwi katika kuandaa bajeti; mashirika ya kidini hayashirikishwi katika kuandaa bajeti. Mfumo wa kuandaa bajeti ni mbovu! Tunautumia, na tunaendelea kuutumia – lakini ukweli unabaki palepale kwamba huu ni mfumo gandamizi. Ni wazi historia itakuja kutoa hukumu; kwa vile tutakuwa tumeondoka ni bora wale watakaokuwepo kubaini kwamba si lazima akioza samaki mmoja wote wanaoza; uwepo ushahidi kwamba kuna walioona mambo tofauti. Hivyo siandiki makala hii kubadilisha mfumo wa bajeti uliopo – CHAMA kina nguvu na kinatawala; wengine wanaamini kitatawala milele! Naandika kujitofautisha na mfumo huu wakati wa kuhukumiwa. Naandika ili vizazi vijavyo visituweke sote kapu mmoja.

Wakati wa biashara ya utumwa, mfumo wa utawala uliokuwepo wakati ule uliuunga mkono; watu waliuzwa kama samaki; watawala wa wakati ule walitanguliza utajiri na nguvu za kiuchumi ili kuwa na uwezo wa kununua silaha za kulinda na kupanua falme zao. Uhai na heshima ya binadamu halikuwa swala la msingi; haki za binadamu zilikuwa mikononi mwa watawala (Walikuwa na uhuru wa kulinda au kutelekeza haki, walikuwa na uhuru wa kutoa haki au kuifungia haki – walijipatia madaraka ya Mwenyezi Mungu).

Kuna baadhi ya watu waliopinga ukatili huu katika jamii hizo za zamani, watu hao walifungwa, walipigwa na wakati mwingine nao waliuzwa kama watumwa. Leo hii wale waliopinga utumwa ndo washindi; leo hii kila mtu mwenye kuheshimu haki za binadamu analaani vikali watawala wa enzi zile walioendesha biashara haramu ya utumwa. Historia inatoa hukumu, ingawa wakati unakuwa umepita; wa kujifunza wanajifunza na wakujirekebisha wanajirekebisha kutokana na historia. Anayekataa
kujifunza kutokana na historia ni mjinga anayejichimba shimo lake mwenyewe.

Tunajua kabisa kwamba kuna mtikisiko wa uchumi duniani. Mtikisiko huu uliyaanza mataifa makubwa; mataifa yanayotupatia misaada; mataifa yanayosaidia kuendesha bajeti yetu ya kila mwaka, mataifa yanayonunua mazao yetu: Pamba, Kahawa nk, mataifa yanayonunua madini yetu na kuja kuwinda wanyama wetu. Kule nyuma tulipoambiwa kwamba mtikisiko huu hauwezi kutugusa; tulijua wazi kabisa kwamba hayo yalikuwa majibu ya kisiasa. Haiwezekani mtu anayekupatia misaada na kununua mazao yako atikisike kiuchumi wewe ubaki umesimama imara. Hiyo ni miujiza ya divai kugeuka damu na mkate kuwa mwili; ni miujiza ya msafiri kutaka kwenda nchi za mbali bila viza, paspoti na tiketi.

Sasa tumetangaziwa kwamba mtikisiko unakuja; na kusema kweli ni mtikisiko wa kutuangusha kabisa. Hata kama siasa zitaendelea kutupumbaza kwamba tutatikisika kidogo – Mwenye macho haambiwi tazama; na atakayekuwepo atashuhudia!

Kama kuna mtikisiko wa uchumi, si ni lazima watu wafunge mkanda? Si ni lazima watu waache utamaduni wa kunywa chai maofisini. Kama tunaamini nchi yetu inaelekea kwenye mtikisiko wa kiuchumi, kwanini viongozi wetu wasiachane na safari za nje ya nchi, wakaendeleza miradi tuliyonayo hapa nchini? Kiongozi wa Mapinduzi kule China, Mao, alifanya safari mmoja katika uongozi wake. Safari hiyo ilikuwa ya kutoka China kwenda Urusi kuweka sahihii mkataba wa silaha. Alisafiri kwa Train kwenda na kurudi. Miaka mingine yote ya uongozi weake, alikaa China akifanya kazi ya kuhimiza maendeleo ya watu wake. China haikurudi nyuma kwa vile kiongozi wake alikaa ndani ya Nchi.

Kama ni kweli kuna mtikisiko si ni lazima kufunga mkanda? Si ni lazima kuhakikisha tunazalisha ya kutosha? Si lazima kuhakikisha nguvu zetu zinaelekezwa kwenye kilimo? Kwanini fedha hizi zinazotengwa kwa chai ya viongozi wetu zisielekezwe kwenye kilimo, na viongozi wetu wakanywa chai kutoka mifumoni mwao? Kwanini fedha zinazotengwa kwa safari zisielekezwe kwenye kilimo na viongozi wetu wakaacha kabisa kusafiri? Hata hivyo tunafaidi nini na safari hizo zaidi ya wao kufanya manunuzi ya familia zao?

Je ni kweli tuko makini na mtikisiko huu ambao tunauandalia bajeti yenye lengo la kupambana na kuzuia mtikisiko usiwe na nguvu zaidi? Swali la kuujiuliza ni kama kweli tuko makini, tunaweza vipi kupanga matumizi ya bilioni 19 kwa chai na bilioni 35 kwa safari za nje na ndani kwa viongozi wetu? Ikiwa takwimu hizi ni za kweli, basi kuna matatizo makubwa katika mfumo wetu wa utawala; wale wanaochangia bajeti yetu, wakikubali kuleta fedha zao ili viogozi wanywe chai na kusafiri kutakuwa na tatizo sehemu fulani au watakuwa na agenda ya siri. Walipa kodi wa nchi za wenzetu wakijua wanachangia chai na safari za viongozi wa Tanzania, hawawezi kukubali fedha hizo ziletwe na zikiletwa ni lazima viongozi wao wawekwe kitimoto.

Je wabunge wetu waliochaguliwa na watu maskini wa Tanzania, wanatumia vigezo gani kukubali kupitisha bajeti yenye kutenga bilioni 19 kwa chai na bilioni 35 kwa safari za viongozi?

Je, ni kweli fedha zote hizo zitatumika kwa chai na safari au ni namna ya kuwekeza fedha sehemu ili zichotwe bila swali wakati wa uchaguzi mkuu? Kwa vile zimepitishwa, ujanja utatumika kuonyesha zimetumika ili zitumike kununulia shahada na kufanya kampeni za vishindo kwenye uchaguzi mkuu wa 2010. Bado kuna utata kwamba KAGODA, ilichota fedha za EPA na kuzipeleka kwenye uchaguzi mkuu wa 2005. Ugonjwa wa CCM kutumia fedha nyingi wakati wa uchaguzi umekuwa mkubwa. Kwa mtizamo huu mtu anaweza kuelewa sababu ya Wabunge wetu (CCM) kukubali kuipitisha bajeti: Ubunge ni muhimu sana kuliko maisha ya watanzania, CCM ni muhimu sana kushika dola kuliko maisha ya watanzania – ni lazima kutumia kila mbinu ili kuhakikisha CCM inabaki madarakani!

Kuna haja gani wabunge kuendelea kubaki Dodoma, wakijadili matumizi ya kila wizara kama inafahamika lengo ni kupitisha kila kitu kwa kusema “Ndiyo”? kwanini waendelee kupata posho? Kwanini waendelee kutumia fedha za walipa kodi maskini wa Tanzania kupitisha kila kitu kwa ushabiki wa kisiasa? Siku walizotumia kujadili bajeti zinatosha! Wabariki bajeti nzima, wafunge virago na kurudi nyumbani kwao; wasubiri hukumu yao uchaguzi mkuu wa 2010 au hukumu ya historia!

CHANZO: kwanzajamii.com
 
Kwa bunge hili lililojaa matapeli wa sisi Maf...... nakwambia hakuna hata siku moja watakwamisha bajeti. Wacha tu hizi bla bla unazisikia nje ya bunge.
Wanapoitwa kwenye hiyo wanaita kamati ya wabunge wa chama majambazi wanatishwa na au kuahidiwa hewa na wanarudi na kauli mpya. "NAUNGA MKONO HOJA ASILIMIA MIA MOJA"
 
Nothing is more right than what was said in the opening thread above.

Wabunge wanatakiwa kulinda heshima yao na ya jamii wanazoziwakilisha kwa kufanya maamuzi sahihi, bila uoga, wala hamasa za kisiasa.

Mwalimu Nyerere aliwahi kusema "Endapo mjinga akikuambia kitu cha kijinga, nawe ukakikubali hasa akijua kuwa unajua ni cha kijinga, atakudharau".

Inatakiwa kuwa na uzalendo kwa Taifa kabla ya kuangalia maslahi ya wachache ndani ya chama tawala. Wananchi masikini wanateseka kila sehemu ya jamii yetu. Wanateseka vijijini kwa kukosa huduma mbalimbali. Wanateseka mahospitalini kwa kukosa dawa, huduma mbovu, kulala sakafuni na kukosa vipimo sahihi kwa magonjwa yao. Wanateseka barabarani kwa kupoteza maisha/viungo vya miili ya kwenye ajali zisizo na msingi, barabara mbovu na nyembamba n.k. Mateso ya wananchi hawa ambao serikali yao haionyeshi nia thabiti ya kuyatazama na kuyapatia ufumbuzi, ni laana kwa Taifa na serikali inayotawala. Tuwaache wanywe chai, labda wakishiba wataona mateso ya wananchi wao.

Wabunge kama wanaona hawana lolote linaloweza kuleta tija, kama wanashindwa kuisimamia serikali kwa mujibu wa sheria zilizopo, kwanini wasiamue kurudi majumbani kwao wakakaa na watoto na wajukuu zao? Warudi majumbani wakabaki wakiangalia serikali yao ikiharibu nchi makusudi. Hii itawatoa kwenye lawama ya kuhusika moja kwa moja kwenye uharibifu huo.

Nchi hii si yetu tena. Ni nchi ya wachache hadi hapo tutakapopata uhuru mpya kwa wananchi wote. Mungu ibariki Tanzania na watu wake.
 
Back
Top Bottom