Wabunge CCM warushiana vijembe waziwazi Bungeni

BAK

JF-Expert Member
Feb 11, 2007
124,789
288,011
Date::6/20/2008
Wabunge CCM warushiana vijembe waziwazi Bungeni
*Anna Abdallah ashambulia magazeti
*Spika asema kutofautiana ndiyo demokrasia

Na Midraji Ibrahim, Dodoma
Mwananchi

KATIKA hali inayoonyesha wabunge kugawanyika kuhusu suala la mafisadi waliochukua fedha kwenye Akaunti ya Malipo ya Nje (EPA), Mbunge wa Viti Maalum (CCM), Anna Abdallah amewashambulia wenzake waliochangia juzi.

Akichangia bajeti hiyo jana, Abdallah alisema baadhi ya wabunge walikuwa wakiwashangaa wenzao wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), ambao walikuwa wakisimama wanakosoa na baadaye wanaunga mkono.

''Nataka kusema tu kwamba suala hili la EPA lisije kutugawa. Tangu nimekaa humu ndani ya bunge sijasikia hata mbunge mmoja anayekataa zisirejeshwe, yupo? Sijamsikia, wote wanataka zirejeshwe,'' alisema na kuongeza:

''Tunatofautiana namna ya kusema tu humu ndani. Sasa kuna wengine wanasema sana, wanaweka na madoido, wengine wanasema kwa upole lakini lengo ni moja tu fedha zirejeshwe. Kwa hiyo, hatuogopi, hakuna anayetishwa, lengo letu ni moja tu.''

Mbunge huyo alishambulia magazeti kwa kuyaita kuwa ni chama ambacho hakijasajiliwa ndicho kinachosaidia kuonyesha mtafaruku ndani ya Bunge.

''Chama kingine cha siasa ambacho hakijaandikishwa kinachoitwa magazeti ndio wanaosaidia kufikiria humu ndani ya Bunge kuna mtafaruku, sijui kwa nini, kwa masuala haya ya msingi wote letu moja, hakuna anayeshabikia ufisadi wala hayo ya EPA, wote tunataka yachukuliwe hatua na ndio lengo letu, kwa hiyo nalo nataka nilitolee maelezo,'' alisema.

Katika hali ya kawaida mbunge hutakiwa kujibiwa na Waziri husika anayesimamia serikali, lakini inapotokea mbunge kumjibu mwenzake kama kujikweza.

Wakichangia bajeti hiyo juzi, Mbunge wa Same Mashariki, Anne Kilango Malecela, Mbunge wa Kishapu, Fred Mpendazoe na Mbunge wa Viti Maalum, Stella Manyanya wote wa CCM walitaka fedha hizo kurejeshwa na wahusika kutangazwa hadharani.

Kilango alisema, iwapo fedha hizo hazitarejeshwa na kuhakikishwa, bungeni patakuwa padogo na kuonya kuwa hawataki kuambiwa kwenye makaratasi bali wazihakikishe na kuongeza kuwa, ulinzi wa fedha za umma umeachwa wazi kwa muda mrefu.

Mpendazoe alisema, ubadhirifu uliotokea ni aibu kwa taifa na wananchi wanasubiri hatua za utekelezaji, huku Manyanya akisema, maswali yaliyoko nje ni mengi na yanahitaji majibu.

Akizungumza nje ya Bunge jana, Spika wa Bunge, Samuel Sitta alisema, kutofautiana kwa wabunge ndio uhai wa bunge na kwamba, haiwezekani zaidi ya wabunge 300 wakawa na mawazo sawa.

Sitta alisema, Bunge linajumuisha wabunge wenye uzoefu tofauti, wakiwemo waliokuwa mawaziri na wengi ni wapya, hivyo wanatofautiana kwa fikira na uzoefu na kwamba, ndio maana ya Bunge.

Alisema lengo la wabunge ni moja, hakuna tofauti baina yao bali inategemeana na uwasilishaji wa hoja.
 
Back
Top Bottom