Ikulu, huu ni udhalilishaji
Na Salehe Mohamed
UKWELI daima humuweka huru mtu, na husaidia kurekebisha mambo pale yanapokwenda tofauti ama kwa makusudi au kwa bahati mbaya, nami nimeamua kuwa mkweli.
Kwanza napenda kuishukuru Ikulu, kwa kulialika gazeti la Tanzania Daima kuwamo kwenye ziara ya siku nne ya Rais Jakaya Kikwete, katika mikoa mitatu ya Lindi, Mtwara na Pwani, lengo kuu likiwa ni kuweka mawe ya msingi ya ujenzi wa baadhi ya barabara na nyingine kuzifungua.
Nimeamua kuipongeza Ikulu, kwa hatua yao hiyo, kwa kuwa kwa muda mrefu gazeti hili halikupata fursa hiyo, kwa kile kinachodaiwa kuandika vibaya habari za serikali na wakati mwingine kumgusa rais kwa mambo yanayodaiwa kuwa na lengo la ama kumchafua au kumdhalilisha.
Pongezi hizi nazitoa si kwa kujipendekeza kwa kuwa nilikuwamo katika safari hiyo, bali ni kwa ajili ya mwamko na kufumbuka macho kwa watendaji wa Ikulu na kujua nini maana ya uhuru wa vyombo vya habari pamoja na kuheshimu demokrasia ya kutoa na kupokea habari.
Pamoja na pongezi hizo, lakini si vibaya nikaweka bayana yale yaliyonikera, ambayo mimi pamoja na wenzangu tuliona ni ya kutudhalilisha na yasiyopaswa kufanywa na watendaji makini wenye kufanya kazi katika taasisi nyeti kama Ikulu.
Kwanza, ni pale maofisa waliposhindwa kutuweka katika orodha ya watu waliomo kwenye msafara wa rais, jambo ambalo lilitufanya tupate shida ya kupata malazi tulipofika Ikwiriri, mkoani Pwani, ambapo ilitulazimu kuhangaika sana mpaka ilipotimu majira ya saa tano usiku.
Katika kuhangaika huko, Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu, Salvatory Rweyemamu, alilazimika kutoa fedha kutoka mfukoni mwake ili tutafute malazi, huku akituhakikishia kuwa siku ya pili tusingepata tabu kama hiyo na kumpa majina yetu ofisa usalama tuliyemjua kwa jina moja la Bomba, ambaye hakuweza kutimiza ahadi yake kama alivyotuahidi.
Cha kusikitisha zaidi, siku ya pili tulilala mkoani Lindi, ambako hali ilikuwa mbaya zaidi, kwani wageni walikuwa wengi na nyumba nyingi za kulala wageni zilikuwa zimejaa, hali iliyotulazimu kuzunguka mji mzima kutafuta sehemu ya kulala, ambapo tuliipata saa sita, lakini mazingira yake hayafai kuzungumzia mbele ya jamii ya kistaarabu na hasa kwa ujumbe ambao unaongozana na rais.
Siku ya tatu tulilala wilayani Masasi, huko hali ilikuwa ni ile ile, tuliendelea kuwa mashuhuda wa majina ya wenzetu kama ilivyokuwa siku zilizotangulia, lakini safari hii tulikuwa werevu na tulianza kutafuta sehemu ya kulala mapema na kwa bahati nzuri tuliipata kwenye majira ya saa mbili usiku, huku mazingira yake nayo yakiwa hayaridhishi.
Siwezi kusahau siku ya mwisho ya ziara hiyo ambapo tulidhalilika kiasi cha kutosha kwa kushushwa kwenye ndege huku tukiwa tayari tumekaa kwenye viti na kufunga mikanda tayari kwa safari.
Siku hiyo rais alikuwa na shughuli ya kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa barabara ya Masasi kwenda Mangaka, ambapo katika sherehe hizo tulitangaziwa kuwa watu waliopo kwenye msafara wa rais watapaswa kwenda Katika Uwanja wa Ndege wa Mtwara ili warejee Dar es Salaam kwa kuwa rais ana shughuli nyingine.
Kibaya zaidi, baada ya kushushwa kwenye ndege tuliulizwa maswali yasiyo ya kiiungwana na wanausalama, ambao waliongozwa na mtu mmoja aliyejitambulisha kwa jina moja la Joachim, ambaye alionyesha kushangazwa na kukasirishwa na uzamiaji tulioufanya.
Joachim, na timu yake baada ya kutuuliza maswali ya hapa na pale yasiyo na mantiki kwetu, alituahidi kuyafanyia kazi zaidi majina yetu ili kujiridhisha kama si watu wabaya magaidi na kuturuhusu kuendelea na utaratibu wetu wa safari kwa njia ya barabara.
Hivi kweli katika mazingira ya kawaida ni mtu gani ambaye anaweza kujichomeka katika msafara wa rais, tena kupanda ndege moja na rais na watu wa usalama wakamuangalia tu? Hilo haliwezekani hata kidogo, watu wa usalama walituacha tuingie kwenye ndege kwa kuwa walijua sisi tupo pamoja nao, kwa sababu safari yetu ilianza pamoja, tena mwanzo mwa makazi ya rais (Ikulu) na hata katika ziara nzima tulijumuika nao kuhakikisha kile kinachosemwa au kufanywa na rais, jamii inakijua.
Kama Ikulu inaweza kuwasahau kwenye orodha yao waandishi waliowapigia simu na kuwagharimia, je, umakini wa watendaji waliokuwa wakishughulikia suala hilo upo wapi?
Nilidhani taasisi hiyo ndiyo inapaswa kuwa kinara wa kufanya mambo yake kwa usahihi, kwa kuwa ina watendaji ambao naamini hawakupewa nafasi walizonazo kwa upendeleo.
Ikulu ina waandishi na wapiga picha wake ambao kwa kipindi chote hicho walipata malazi bora na hata wakati wa kurejea Dar es Salaam walikuwamo kwenye ndege, kwa nini haikuwafanyia vitendo hivyo wao?
Kama iliona haina shida na waandishi wengine, basi isingewaalika ili kukwepa kuwadhalilisha kuliko vitendo ilivyowafanyia. Watendaji wake wangeweza kutuambia waandishi mapema kuwa tusiende Mtwara.
Tungeambiwa mapema tusingepata aibu hiyo, kwa kuwa tulikuwa na gari ambalo tulipewa kabla ya kuondoka Dar es Salaam na tulikuwa na maamuzi nalo, hivyo tungeweza kumwambia dereva turejee makwetu, naye akatutii bila matatizo.
Kama watendaji wangetaka kutuambia hatumo kwenye orodha ya msafara wa rais wa kurejea, walikuwa na nafasi nzuri ya kufanya hivyo, kwa kuwa Mkurugenzi wa Mawasiliano niliongea naye wakati tunaondoka Masasi, akiwa analalamikia kichwa cha habari kilichoandikwa na gazeti langu.
Nimeamua kuandika mambo haya, si kwa nia mbaya, bali kuwarekebisha watendaji waliozoea kufanya mambo kwa mazoea na kuwapuuza wajumbe wengine wanaoambatana na msafara wa rais kwa kudhani kuwa si wa muhimu kama walivyo wao.
Binafsi nilitarajia baada ya kadhia ile Mkurugenzi wa Mawasiliano baada ya kufika Dar es Salaam angetupigia simu kujua mambo yalivyokwenda, baada ya kutuacha pale Mtwara, lakini hakufanya hivyo hadi jana asubuhi alipofanya hivyo, tena baada ya kusikia kutoka kwa baadhi ya watu jinsi tulivyotendewa na hatua tulizopanga kuchukua kuhusu udhalilishwaji ule.
Lakini ningependa kumshukuru Katibu wa rais niliyemfahamu kwa jina la Jairo, ambaye alilazimika kushuka kwenye ndege na kutukimbilia tulipokuwa tunatoka kwa aibu kiwanjani na kutukabidhi kwa dereva wake kuwa ahakikishe anatufikisha Dar es Salaam.
Binafsi naona katibu huyo alijisikia vibaya kuhusu kushushwa kwetu, tena rais akiwa amekwisha kuingia ndani ya ndege, jambo ambalo ni kinyume cha itifaki.
Kwa kutumia kalamu yangu, nimeamua kutolinyamazia jambo hili hata kama watendaji wa Ikulu watachukia na kuamua kutolialika gazeti hili katika ziara za rais, naamini hatukualikwa kwa kuogopwa, bali ni kwa kuthamini mchango wetu ndani ya jamii.
Nasi tuliona fahari kuwamo katika msafara, lakini hatutafumbia macho tabia ya kushusha hadhi na utu wa mtu, hata kama wanaofanya vitendo hivyo wana uwezo wa kifedha au kidola.
Source: Tanzania Daimahttp://www.freemedia.co.tz/daima/habari.php?id=8006
Na Salehe Mohamed
UKWELI daima humuweka huru mtu, na husaidia kurekebisha mambo pale yanapokwenda tofauti ama kwa makusudi au kwa bahati mbaya, nami nimeamua kuwa mkweli.
Kwanza napenda kuishukuru Ikulu, kwa kulialika gazeti la Tanzania Daima kuwamo kwenye ziara ya siku nne ya Rais Jakaya Kikwete, katika mikoa mitatu ya Lindi, Mtwara na Pwani, lengo kuu likiwa ni kuweka mawe ya msingi ya ujenzi wa baadhi ya barabara na nyingine kuzifungua.
Nimeamua kuipongeza Ikulu, kwa hatua yao hiyo, kwa kuwa kwa muda mrefu gazeti hili halikupata fursa hiyo, kwa kile kinachodaiwa kuandika vibaya habari za serikali na wakati mwingine kumgusa rais kwa mambo yanayodaiwa kuwa na lengo la ama kumchafua au kumdhalilisha.
Pongezi hizi nazitoa si kwa kujipendekeza kwa kuwa nilikuwamo katika safari hiyo, bali ni kwa ajili ya mwamko na kufumbuka macho kwa watendaji wa Ikulu na kujua nini maana ya uhuru wa vyombo vya habari pamoja na kuheshimu demokrasia ya kutoa na kupokea habari.
Pamoja na pongezi hizo, lakini si vibaya nikaweka bayana yale yaliyonikera, ambayo mimi pamoja na wenzangu tuliona ni ya kutudhalilisha na yasiyopaswa kufanywa na watendaji makini wenye kufanya kazi katika taasisi nyeti kama Ikulu.
Kwanza, ni pale maofisa waliposhindwa kutuweka katika orodha ya watu waliomo kwenye msafara wa rais, jambo ambalo lilitufanya tupate shida ya kupata malazi tulipofika Ikwiriri, mkoani Pwani, ambapo ilitulazimu kuhangaika sana mpaka ilipotimu majira ya saa tano usiku.
Katika kuhangaika huko, Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu, Salvatory Rweyemamu, alilazimika kutoa fedha kutoka mfukoni mwake ili tutafute malazi, huku akituhakikishia kuwa siku ya pili tusingepata tabu kama hiyo na kumpa majina yetu ofisa usalama tuliyemjua kwa jina moja la Bomba, ambaye hakuweza kutimiza ahadi yake kama alivyotuahidi.
Cha kusikitisha zaidi, siku ya pili tulilala mkoani Lindi, ambako hali ilikuwa mbaya zaidi, kwani wageni walikuwa wengi na nyumba nyingi za kulala wageni zilikuwa zimejaa, hali iliyotulazimu kuzunguka mji mzima kutafuta sehemu ya kulala, ambapo tuliipata saa sita, lakini mazingira yake hayafai kuzungumzia mbele ya jamii ya kistaarabu na hasa kwa ujumbe ambao unaongozana na rais.
Siku ya tatu tulilala wilayani Masasi, huko hali ilikuwa ni ile ile, tuliendelea kuwa mashuhuda wa majina ya wenzetu kama ilivyokuwa siku zilizotangulia, lakini safari hii tulikuwa werevu na tulianza kutafuta sehemu ya kulala mapema na kwa bahati nzuri tuliipata kwenye majira ya saa mbili usiku, huku mazingira yake nayo yakiwa hayaridhishi.
Siwezi kusahau siku ya mwisho ya ziara hiyo ambapo tulidhalilika kiasi cha kutosha kwa kushushwa kwenye ndege huku tukiwa tayari tumekaa kwenye viti na kufunga mikanda tayari kwa safari.
Siku hiyo rais alikuwa na shughuli ya kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa barabara ya Masasi kwenda Mangaka, ambapo katika sherehe hizo tulitangaziwa kuwa watu waliopo kwenye msafara wa rais watapaswa kwenda Katika Uwanja wa Ndege wa Mtwara ili warejee Dar es Salaam kwa kuwa rais ana shughuli nyingine.
Kibaya zaidi, baada ya kushushwa kwenye ndege tuliulizwa maswali yasiyo ya kiiungwana na wanausalama, ambao waliongozwa na mtu mmoja aliyejitambulisha kwa jina moja la Joachim, ambaye alionyesha kushangazwa na kukasirishwa na uzamiaji tulioufanya.
Joachim, na timu yake baada ya kutuuliza maswali ya hapa na pale yasiyo na mantiki kwetu, alituahidi kuyafanyia kazi zaidi majina yetu ili kujiridhisha kama si watu wabaya magaidi na kuturuhusu kuendelea na utaratibu wetu wa safari kwa njia ya barabara.
Hivi kweli katika mazingira ya kawaida ni mtu gani ambaye anaweza kujichomeka katika msafara wa rais, tena kupanda ndege moja na rais na watu wa usalama wakamuangalia tu? Hilo haliwezekani hata kidogo, watu wa usalama walituacha tuingie kwenye ndege kwa kuwa walijua sisi tupo pamoja nao, kwa sababu safari yetu ilianza pamoja, tena mwanzo mwa makazi ya rais (Ikulu) na hata katika ziara nzima tulijumuika nao kuhakikisha kile kinachosemwa au kufanywa na rais, jamii inakijua.
Kama Ikulu inaweza kuwasahau kwenye orodha yao waandishi waliowapigia simu na kuwagharimia, je, umakini wa watendaji waliokuwa wakishughulikia suala hilo upo wapi?
Nilidhani taasisi hiyo ndiyo inapaswa kuwa kinara wa kufanya mambo yake kwa usahihi, kwa kuwa ina watendaji ambao naamini hawakupewa nafasi walizonazo kwa upendeleo.
Ikulu ina waandishi na wapiga picha wake ambao kwa kipindi chote hicho walipata malazi bora na hata wakati wa kurejea Dar es Salaam walikuwamo kwenye ndege, kwa nini haikuwafanyia vitendo hivyo wao?
Kama iliona haina shida na waandishi wengine, basi isingewaalika ili kukwepa kuwadhalilisha kuliko vitendo ilivyowafanyia. Watendaji wake wangeweza kutuambia waandishi mapema kuwa tusiende Mtwara.
Tungeambiwa mapema tusingepata aibu hiyo, kwa kuwa tulikuwa na gari ambalo tulipewa kabla ya kuondoka Dar es Salaam na tulikuwa na maamuzi nalo, hivyo tungeweza kumwambia dereva turejee makwetu, naye akatutii bila matatizo.
Kama watendaji wangetaka kutuambia hatumo kwenye orodha ya msafara wa rais wa kurejea, walikuwa na nafasi nzuri ya kufanya hivyo, kwa kuwa Mkurugenzi wa Mawasiliano niliongea naye wakati tunaondoka Masasi, akiwa analalamikia kichwa cha habari kilichoandikwa na gazeti langu.
Nimeamua kuandika mambo haya, si kwa nia mbaya, bali kuwarekebisha watendaji waliozoea kufanya mambo kwa mazoea na kuwapuuza wajumbe wengine wanaoambatana na msafara wa rais kwa kudhani kuwa si wa muhimu kama walivyo wao.
Binafsi nilitarajia baada ya kadhia ile Mkurugenzi wa Mawasiliano baada ya kufika Dar es Salaam angetupigia simu kujua mambo yalivyokwenda, baada ya kutuacha pale Mtwara, lakini hakufanya hivyo hadi jana asubuhi alipofanya hivyo, tena baada ya kusikia kutoka kwa baadhi ya watu jinsi tulivyotendewa na hatua tulizopanga kuchukua kuhusu udhalilishwaji ule.
Lakini ningependa kumshukuru Katibu wa rais niliyemfahamu kwa jina la Jairo, ambaye alilazimika kushuka kwenye ndege na kutukimbilia tulipokuwa tunatoka kwa aibu kiwanjani na kutukabidhi kwa dereva wake kuwa ahakikishe anatufikisha Dar es Salaam.
Binafsi naona katibu huyo alijisikia vibaya kuhusu kushushwa kwetu, tena rais akiwa amekwisha kuingia ndani ya ndege, jambo ambalo ni kinyume cha itifaki.
Kwa kutumia kalamu yangu, nimeamua kutolinyamazia jambo hili hata kama watendaji wa Ikulu watachukia na kuamua kutolialika gazeti hili katika ziara za rais, naamini hatukualikwa kwa kuogopwa, bali ni kwa kuthamini mchango wetu ndani ya jamii.
Nasi tuliona fahari kuwamo katika msafara, lakini hatutafumbia macho tabia ya kushusha hadhi na utu wa mtu, hata kama wanaofanya vitendo hivyo wana uwezo wa kifedha au kidola.
Source: Tanzania Daimahttp://www.freemedia.co.tz/daima/habari.php?id=8006