Vurugu vyuoni zinachangiwa na viongozi wa vyuo

Lunyungu

JF-Expert Member
Aug 7, 2006
8,873
1,894
John Nditi
Daily News;
Tuesday,June 10, 2008


MAFANIKIO ya maendeleo yawe ya kijamii ama kiuchumi kwa taifa lolote lile duniani, hayawezi kupatikana pasipo watu wake kuwa na elimu ya kutosha na utaalamu wa fani mbalimbali.

Hivyo kwa kutambua hivyo, Nchi changa za dunia ya tatu, ikiwamo Tanzania, mara baada ya kupata uhuru mwaka 1961, iliamua kuanzisha Chuo Kikuu chake badala ya kutegemea kupeleka wanafunzi wake nje, kama Chuo Kikuu cha Makerere na Cambrige nchini Uingereza.

Uamuzi huo wa kuwa na vyuo vikuu nchini, unatokana na juhudi za serikali za awamu zote nne. Kuanzia Awamu ya kwanza ya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, awamu ya pili ya Rais Ali Hassan Mwinyi, ya tatu ya Rais Benjamin Mkapa na awamu ya nne ya Rais Jakaya Kikwete. Serikali inaendelea kuhakikisha kuwa misingi ya elimu kuanzia shule za msingi hadi vyuo vikuu, inakuwa endelevu.

Inaboreshwa na kuendeleza uanzishwaji wa vyuo vikuu vingine katika kuhakikisha kuwa watoto wanaomaliza elimu ya sekondari, wanaipata elimu ya juu bila vikwazo.

Katika kutambua umuhimu huo, taasisi za dini na watu binafsi nchini, wamejitokeza kuanzisha vyuo vikuu kwa nia ya kuongeza idadi ya wahitimu. Lengo lake ni kuliwezesha taifa kupata wataalamu wengi zaidi katika fani mbalimbali ili watumike kuleta maendeleo nchini.

Hivyo, kwa kutambua umuhimu wa taasisi za dini na watu binafsi katika utoaji elimu ya juu kupitia vyuo vikuu, Waziri Mkuu , Mizengo Pinda , hivi karibuni alifanya ziara fupi mkoani Morogoro ambapo alitembelea Chuo Kikuu cha Waislamu cha Morogoro. Lengo la ziara hiyo, ilikuwa ni kufahamiana na viongozi wa chuo hicho.

Pia ilikuwa fursa ya kuelimishana hasa kutokana na kutambua kuwa chuo kikuu hicho ni kichanga, tofauti na vyuo vingine nchini. Pinda anaeleza kuwa viongozi wa vyuo vikuu, wanatakiwa kuwajibika kikamilifu katika kuboresha huduma, miundombinu ya mazingira na kutoa elimu bora ya mazingira ya kusomea wanafunzi.

Vyuo vikuu vya taasisi za dini, kikiwamo chuo kikuu hicho, vinakabiliwa na uhaba wa walimu, Waziri Mkuu Pinda, ameonyesha nia ya kutatua tatizo hilo. Waziri Mkuu ameonyesha nia ya kweli katika kuhakikisha chuo kikuu hicho, kinapata msaada endelevu.

Akiwa katika ziara yake ya hivi karibuni nchini Misri, alifanya mazungumzo na Waziri Mkuu mwenzake wa nchi hiyo na moja ya maombi yake, yalikuwa ni nchi hiyo isaidie wataalamu wa kufundisha Chuo Kikuu cha Waislamu cha Morogoro.

"Nilipokuwa Misri hivi karibuni nilipata nafasi ya kukutana na Waziri Mkuu wa nchi hiyo. Ni mtu mzuri wa kiroho na nilizungumza naye ili kuona uwezekano wa Serikali yake kusaidia Chuo Kikuu cha Waislam cha Morogoro" anasema Pinda.

Anaongeza kuwa "Nilimwambia wazi kuwa chuo kikuu chetu ni kichanga na yeye amekubali kutusaidia na kwamba atamwagiza Balozi wake hapa nchini, kusimamia mazungumzo kati ya Misri na uongozi wa chuo hiki, juu ya uwezekano wa kutoa wataalamu." Kwa mujibu wa Waziri Mkuu, nchi ya Misri ina walimu wengi na vyuo vikuu.

Ikiwa mazungumzo hayo yatafikiwa na kufikia makubaliano, nchi hiyo itatoa wataalamu na kuwalipia mishahara na posho. Jambo kubwa kwa upande Serikali ya Tanzania na uongozi wa chuo ni kuangalia namna gani kugharamia huduma zao, kwa mfano kuwapatia nyumba za kuishi. Hilo linawezekana. "Wao wapo tayari kutoa mishahara na posho na tutagharimia nyumba tu…hili linawezekana…matatizo ya kushughulikia ni maktaba.

Anasema "Mambo muhimu ya kuangalia ni kuweka mipango endelevu ya muda mrefu katika nyanja za uwekaji na kuweka miundombinu mizuri itakayokidhi ongezeko la wanafunzi siku za usoni." Kwa mujibu wa Waziri Mkuu, mipango hiyo endelevu, inatokana na msukumo wa kufaulu kwa idadi kubwa ya wanafunzi wa kidato cha sita na ongezeko la wanaohitaji kujiunga na vyuo vikuu.

"Nawashauri mkianza mazungumzo yenu na Ubalozi wa Misri, mtakapo kamilisha ripoti yenu, mniletee na mimi nitampatia Balozi wao kwa ajili ya kuwasilisha kwa Waziri Mkuu wake. Jambo muhimu tengenezeni mpango unaozingatia kukua kwa chuo chenu," anasema Pinda.

Kuwapo kwa chuo kikuu hicho mkoani Morogoro, kumeongeza idadi ya vyuo vikuu nchini na kufikia 30, ambapo 21 ni vya umma na tisa ni vya taasisi dini na watu binafsi. Baadhi ya matatizo yanayovikumba vyuo vikuu nchini ni vurugu zinazotokea mara kwa mara kutokana na kero nyingi zilizopo ndani ya uwezo wa vyuo husika.

Vyuo hivyo vinashindwa kuyapatia ufumbuzi matatizo ya muda mrefu, hivyo kuchochea wanafunzi kuleta vurugu. Vurugu zinachangiwa na utawala wa vyuo, kushindwa kuwajibika katika kuondoa kero za muda mrefu za wanafunzi.

"Viongozi wanapofumbia macho kero, baadaye wanafunzi wa vyuo vikuu wanaiona serikali yao ni mbaya, kumbe sivyo," anasema Pinda. Kwa mujibu wa Waziri Mkuu, taarifa iliyowasilishwa mezani kwake na Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Profesa Jumanne Maghembe, baada ya kuvitembelea vyuo vikuu vya serikali, imeweka bayana matatizo ya vyuoni.

Imeonyesha kuwa matatizo mengi yanayochangia kutokea vurugu yanachangiwa na utawala wa vyuo kushindwa kuwajibika katika kuondoa kero za muda mrefu za wanafunzi.

"Nilimwagiza Waziri anayehusika na Elimu Profesa Maghembe avitembee vyuo hivyo kujua vina matatizo gani. Amegundua kuna matatizo ya uhaba wa mabweni pale Chuo Kikuu Dar es Salaam (UDSM), chumba kimoja wanalala wanafunzi wanane hadi 10," anasema Waziri Mkuu. Anasema "Tatizo la maji nalo ni kubwa.

Baadhi ya wanafunzi wanabeba maji kwa ndoo na kupandisha ghorofani, hii si kwa mara moja. Pale chuoni kuna wanafunzi zaidi ya 16,000. Haya ni matatizo ya kuzembea kwa viongozi. Wakati umefika wa kuyarekebisha ili kupunguza ama kukomesha migomo vyuoni."

Vyuo vikuu vya taasisi za dini, zisijitumbukize katika vurugu zinazotokea katika vyuo vya umma. Ni bora viongozi wao wasikilize matatizo ya wanafunzi na kuboresha miundombinu yao. "Juhudi za pamoja zinahitajika katika kukisaidia chuo hiki ili kiweze kufikia malengo yake yaliyowekwa wakati wa kuanzishwa kwake na kuendeleza nia njema iliyoonyeshwa na serikali ya Awamu ya Tatu ya kutoa majengo na kuanzisha chuo hiki," anasema Waziri Mkuu.

Anasema "Sisi kwa upande wetu, tunataka kuendeleza mazuri ya Rais mstaafu wa Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa aliyoyafanya ya kuidhinisha majengo haya yaliyokuwa mali ya Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) kuwa Chuo na kuyatoa kwa Waislamu ili yatumike kama Chuo Kikuu chao."

Hata hivyo, Waziri Mkuu anasema pamoja na uchanga huo, ni jambo la muhimu uongozi wa chuo hicho ukaandaa mipango endelevu itakayoweza kukabiliana na changamoto zinazojitokeza wakati huu za ushindani katika utoaji elimu za juu nchini.

Mipango endelevu ni ile itakayokiwezesha chuo hicho kuongeza idadi ya wanafunzi wanaomaliza kidato cha sita kujiunga na chuo hicho na kuboresha miundombinu, itakayo zuia migogoro ya wanafunzi wakati huo. Makamu wa Mkuu wa Chuo hicho, Profesa Hamza Njozi, katika taarifa yake kwa Waziri Mkuu, anasema tatizo kubwa linalokabili chuo hicho ni uhaba wa wataalamu na walimu.

Anasema uongozi wa chuo hicho,umefurahishwa na kitendo chake cha kukisemea chuo hicho kwa Waziri Mkuu mwenzake wa Misri. Makamu huyo wa Mkuu wa Chuo anasema chuo hicho kina walimu 35, ambao ni wachache. Anasema hawatoshelezi mahitaji ya wanafunzi waliopo chuoni.

"Tatizo la walimu ni kubwa kwetu, hapa chuoni hivi sasa tuna walimu 35 na chuo kina jumla ya wanafunzi 650 wa masomo ya shahada ya kwanza ya sanaa ya ualimu na mawasiliano ya umma na uandishi wa habari," anasema.

Anasema uhaba huo wa walimu, umetokana na kushindwa kupatikana kwa wataalamu wengi na wale wachache waliopo wamekuwa na ushindani mkubwa kuweza kuwapata kutokana na mahitaji ya vyuo mbalimbali vya ndani na nje.

"Chuo chetu kina wanafunzi 650, kati yao 555 wanachukua shahada ya kwanza ya sanaa ya ualimu na waliobaki ni masomo ya mawasiliano na umma. Wanawake katika chuo ni 243, hii ni theluthi moja ya wanafunzi wote, wanafunzi 650 wanaishi hosteli," anasema Profesa Njozi.

Anasema uongozi wa chuo ulikusudia kutafuta walimu kutoka Nigeria na Misri, kwa makubaliano maalumu, ili kuweza kupunguza pengo hilo. Kutokana na uhaba mkubwa wa kuwapata wataalamu wa kufundisha katika vyuo vikuu, Chuo hicho kimeamua kuanzisha kozi ya shahada ya uzamili ya elimu.

Kozi hiyo itaanzishwa mwaka ujao wa masomo, lengo ni kuwapata walimu wao wenyewe. "Tumekuwa katika mchakato wa kuhangaika kuwapata walimu. Nchi ya Nigeria na Misri wapo tayari kutupatia wataalamu wao, lakini masharti yao ni kuhakikisha tunakuwa na nyumba za wao kuishi," anasema Profesa Njozi.

"Tuliposikia Waziri Mkuu anakwenda Misri, sio siri mioyo yetu ilijawa na furaha kuwa utatusemea juu ya tatizo letu hili," anasema. Profesa Njozi, anasema chuo kinatambua mchango wa Waziri Mkuu, kuwa mtetezi wa elimu.

Serikali ya awamu ya tatu ya Rais Benjamin Mkapa, Oktoba 23, 2004 iliyakabidhi majengo yaliyokuwa yakitumika kama Chuo cha Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), kwa Taasisi ya Mfuko wa Maendeleo ya Waislamu (MDF), chini ya Mwenyekiti wake Kitwana Kondo. Taasisi hiyo ya MDF iliamua kuanzisha Chuo Kikuu cha Waislamu cha Morogoro. Kilianza rasmi katikati ya mwaka 2005.
 
MZIMU WA VURUGU VYUONI NA SHULENI
UKEMEWE HARAKA.
Siku baada ya siku, visa vya vurugu mashuleni vimekuwa vikiripotiwa toka sehemu mbalimbali za Taifa letu.
Sababu za vurugu hizo zimekuwa zikitolewa kwa sura mbalimbali.
Lengo langu katika barua hii siyo kuainisha sababu za vurugu hizo kwani mimi naona kama kitendawili. Mimi nataka kutia changamoto kwa wanafunzi , Uongozi wa shule/vyuo, serikali na wanajamii wote kwa ujumla.

• KWA UPANDE WA WANAFUNZI
Wanafunzi wamehusika katika vurugu hizi wakiharibu mali, kuwavunjia walimu wao heshima, kugoma kuingia madarasani,n.k
Maswali ya kujiuliza ni kwamba,
- je vurugu na migomo ni njia sahihi ya kutatua matatizo ya wanafunzi?
- Je, hakuna njia nyingine salama ambazo wanafunzi wanaweza kuzitumia kuelezea au kuyaweka wazi matatizo yao?
- Je, kuharibu mali za shule na kuwapiga au kuwatukana waalimu kunatatua matatizo ya wanafunzi?

• KWA UPANDE WA WAALIMU na Viongozi.
Nimekuwa nawaza kuhusu wanafunzi kuleta vurugu mashuleni na kujiuliza maswali haya:
- Je walimu/viongozi wanatabia ya kukaa na wanafunzi wao kujadili kuhusu matatizo yao au wanawatawala kidikteta?

• KWA UPANDE WA JAMII na SERIKALI:
- Vurugu hizo zinapotokea sisikii jamii na serikali wakionyesha nia ya dhati ya kupima hoja za wanafunzi.Ninachokiona ni vitisho na lawama tu.Je kulikoni?
- Ama hakuna uhusiano mzuri kati ya wanafunzi, waalimu, jamii na serikali?
- Au je, vurugu hizi na migomo ni maamuzi ya wanafunzi wenyewe au kuna ushawishi toka nje ya shule na vyuo?
Kwa ujumla wake, visa vya vurugu mashuleni na vyuoni vimejaa maswali kuliko majibu.
DAWA YA HALI HII TETE NI NINI?

EXAUD J. MAKYAO
0784347001
 
me naona vyuo vimefululiza migomo ya mara kwa mara, mara udom , st. john , ud ,duce, na ss nackia mkwawa , ila mbona me tangu nimefika saut cjawahi ckia historia ya mgomo hapa? inamaana kila kitu kiko sawa hapa? kama loan board beneficiaries na hapa tupo, mbona hatulalamiki? tunaogopa nn?
 
me naona vyuo vimefululiza migomo ya mara kwa mara, mara udom , st. John , ud ,duce, na ss nackia mkwawa , ila mbona me tangu nimefika saut cjawahi ckia historia ya mgomo hapa? Inamaana kila kitu kiko sawa hapa? Kama loan board beneficiaries na hapa tupo, mbona hatulalamiki? Tunaogopa nn?
mlalamikie nini wakati hamna matatizo subirini yatokee mtaandamana tu
 
kila kukicha ni migomo kila mahali. UDSM, TUMAINI, ARDHI, ....

Chanzo kikuu cha migomo hii yote ni madai kuhusu fedha za mikopo.
Pamoja na mambo yote yaliyotokea inaonesha polisi nao hawajifunzi kuacha kutumia mabavu! wiki iliyopita polisi walipiga risasi juu kuwatawanya wanafunzi wa MUHAS, Jana ilikuwa zamu ya Mlimani na hakuna dalili mambo haya kuisha leo wala kesho.
Sasa wanaCCM na serikali yenu hamuoni kuwa yote haya ni matokeo ya sera zenu mbovu? Hamuoni haja kurekebisha hali hii? AU NDIO LILE SIKIO LA KUFA..........?!
 
Kuna tatizo mahali...!

Aidha uongozi wa vyuo, urasimu uliokidhiri, mifumo mibovu ya utawala lakini kikubwa zaidi ni usiri mkubwa wa kufanya mambo...! Vijana hawapewi taarifa ya hatma ya mambo yanayowahusu...!

Bado hatuna na hatujajijengea utaratibu wa kutoa taarifa na kuwa wawazi inapohiajika, vitu vingi vinafanywa kichini chini sana...! Ndio maana vijana wanapata hasira na kuamua kuingia barabarani...!
 
Back
Top Bottom