Viongozi CHADEMA wasimulia walivyokamatwa na Polisi

comte

JF-Expert Member
Dec 11, 2011
8,171
5,905
Mwanza. Baadhi ya viongozi wa Chadema waliokamatwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa Mwanza kuhusiana na kongamano la Katiba Mpya lililozuiwa, wamesimulia jinsi walivyokamatwa usiku wa kuamkia Julai 21.

Pamoja na simulizi hizo, viongozi hao wakiongozwa na mjumbe wa Kamati Kuu, John Heche walisisitiza msimamo wa kuandaa upya kongamano hilo mkoani Mwanza wakidai kufanya hivyo hawavunji sheria yoyote ya nchi.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti wakati wa mkutano na waandishi wa habari jijini Mwanza jana, Heche na katibu wa Chadema Kanda ya Victoria, Zakaria Obadi waliahidi kutangaza tarehe mpya na eneo kutakapofanyika kongamano hilo litakalokuwa la tatu kuandaliwa na chama hicho.

“Polisi walizuia kongamano letu la Katiba Mpya la Julai 16 na Julai 21 kwa sababu ambazo ni kinyume cha sheria. Tutaandaa kongamano lingine siku na eneo tutakalotangaza baadaye,” alisema Heche, kauli iliyoungwa mkono na Obadi.

Huku akionyesha msisitizo kuhusu kuandaa kongamano lingine, Heche alisema; “Kama polisi wanadhani kutukamata kutatuogopesha tuache msimamo wetu wa kudai Katiba Mpya, basi wamejidanganya kwa sababu wataendelea hadi Taifa litakapopata katiba inayosimamia misingi ya haki na kuwawajibisha viongozi wanaokiuka sheria na viapo vyao.

Simulizi ya kukamatwa

Akisimulia jinsi alivyokamatwa na polisi usiku wa kuamkia Julai 21, Heche alisema tukio hilo lilitokea saa 8:00 usiku wakati yeye na viongozi wengine walipomsindikiza Mwenyekiti wa Chadema Taifa, Freeman Mbowe katika hoteli Kingdom, iliyopo Mtaa wa Ghana jijini Mwanza.

Alisema baada ya kufika hotelini, baadhi ya viongozi walimsindikiza Mbowe chumbani kwake huku yeye aliyekuwa akiendesha gari alilopanda mwenyekiti huyo alibaki kwenye gari kuwasubiri wenzake ndipo ghafla watu wenye bunduki walifika wakiwa kwenye magari zaidi ya matatu kuziba njia huku wakiruka kwa haraka kulifuata gari lake.

“Nilijua tumevamiwa na majambazi kutokana na jinsi watu wale walivyovaa ikiwamo baadhi kuziba nyuso kwa kuvaa kofia maarufu kama boshori. Wawili kati ya wale watu walinifuata na kuniamuru kutoka nje ya gari na niliposhuka walinishika na kuniongoza kwenye gari lao,” alisema Heche.

Alisema ndani ya gari hilo aliwakuta watu wawili wenye bunduki waliovaa sare za polisi ndipo alipobaini waliowavamia walikuwa askari polisi.

“Baadaye wenzangu waliobaki kwenye magari nao waliletwa na wote tukapelekwa kituo kikuu cha polisi na kuingizwa mahabusu bila waliotukamata kujitambulisha wala kutueleza tuhuma zetu kama sheria inavyoelekeza,” alisema Heche.

Alisema mchana wa siku iliyofuata walitolewa mahabusu na kutakiwa kuandikisha maelezo, jambo alilosema aliligomea akishinikiza kuelezwa tuhuma zao; ndipo walipoambiwa wanatuhumiwa kujiandaa kushiriki kongamano la Katiba Mpya kinyume cha amri ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Robert Gabriel la kupiga marufuku mikusanyiko isiyo ya lazima.

Kwa upande wake, Obadi aliyedai kushuhudia tukio zima la wenzake kukamatwa baada ya kupishana na askari waliodhani alikuwa mteja hotelini hapo alisema kilichomponza hadi kutiwa mbaroni siku iliyofuata ni kitendo chake cha kufuatilia suala la huduma ya chai na chakula kwa waliokuwa mahabusu.

Akizungumza na Mwananchi kwa simu kuhusu dhamana za viongozi hao, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Ramadhani Ng’anzi alisema polisi iliwaachia baada ya kutimiza masharti.

Mwananchi
 
Poleni Wana CHADEMA,hata sisi Wana CCM tunaojitambua tunataka katiba mpya,msiogooe kupambana kwani tupo nyuma yenu.
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom