Vigogo CCM hali tete!

Ex Spy

JF-Expert Member
Jan 15, 2007
213
1,726
  • Kikwete aongoza kikao cha maadili kwa usiri
Imeandikwa na Habel Chidawali, Dodoma
Gazeti la Mwananchi

KAMATI ya Maadili ya CCM jana ilifanya kikao chake mjini hapa na kujadili mambo mbalimbali, ikiwa ni pamoja na kitendo cha baadhi ya vigogo wa chama hicho kuonekana kuwa mwiba mkali kwa serikali.

Kikao hicho kilifanyika mjini hapa jana chini ya mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete huku kukiwa na usiri mkubwa wa mambo ambayo yanajadiliwa.

Kikao hicho kimefanyika siku moja kabla ya vikao viwili vikubwa kichama, yaani Kamati Kuu ambayo kikao chake kitafanyika leo na Halmashauri Kuu ya Taifa (Nec) kesho.

Habari ambazo zililifikia gazeti hili juu ya kile kilichojadiliwa na kamati ya maadili, zilisema kwamba, walijadili kwa undani hali ya mvutano na upinzani ambayo inaonekana kushika kasi ndani ya CCM katika siku za karibuni na hata kuiweka serikali katika wakati mgumu.

Kikao hicho cha maadili kwa kawaida kinakuwa na wajumbe wachache ambao idadi yao ni kati ya 12 na 13 na ndicho kikao pekee kinachotunza siri za chama ndani na nje na maamuzi yake huwa hayawezi kupingwa.

Wajumbe wanaounda kamati hiyo ni pamoja na mwenyekiti wa CCM, katibu mkuu, manaibu katibu wa Bara na Zanzibar, makamu wenyeviti pande zote pamoja na marais wastaafu.

Wengine ni pamoja na wajumbe wa kuteuliwa ambao kwa upande wa Bara ni Andrew Chenge na Pindi Chana, ambao waliwasili jana katika ukumbi huo majira ya mchana.

Chanzo chetu ndani ya CCM kilieleza kwamba, moja ya mambo makubwa yaliyojadiliwa ni wabunge wa CCM kuishika pabaya serikali kuhusiana na utekelezaji wa maazimio ya Bunge juu ya kashfa ya utoaji wa zabuni ya kuzalisha umeme wa dharura kwa kampuni tata ya Richmond Development LLC.

Mkutano wa Bunge uliomalizika hivi karibuni uliikataa ripoti ya serikali ambayo ilionekana wazi kumsafisha mkurugenzi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Dk Edward Hosea pamoja na Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Johnson Mwanyika.

Wabunge wengi wa CCM, wakishirikiana na wale wa upinzani waliweka wazi misimamo yao kwamba, serikali itoe upya ripoti ya utekelezaji wa maazimio hayo katika kikao kijacho cha bunge kitakachokuwa Novemba mwaka huu na iwapo hawataridhika nayo watatoa msimamo wao.

Wabunge kadhaa walionyesha msimamo wa kutokuwa na imani na serikali kwa namna ilivyoshughulikia suala hilo, jambo ambalo linaweza kusababisha kuilazimisha serikali kujiuzulu na kuitishwa uchaguzi mwingine.

Jambo jingine ambalo chanzo chetu kimetutaarifu kuwa lilijadiliwa kwenye kamati hiyo ya maadili ni mzozo ulioshika kasi hivi karibuni kuhusu vita ya ufisadi ambayo imewaparaganyisha viongozi wengi wa chama kimsimamo, wakiwemo makada wanaoheshimika.

Suala hilo la ufisadi limeigawa CCM katika makundi mawili yanayohasimiana, moja likiwa ni la wale ambao wanapambana na ufisadi na ambao wamekuwa wakijionyesha hadharani na pili ni lile linalotuhumiwa kwa ufisadi, ambalo vita yake imekuwa ni ya chini kwa chini.

Tayari baadhi ya wabunge walio mstari wa mbele kupambana na ufisadi wamelalamika kuwa, wanafanyiwa visa na kundi hilo la mafisadi, vikiwepo vitisho pamoja na mikakati ya kuhakikisha hawapitishwi au kushinda katika Uchaguzi Mkuu ujao.

Hatua ya mwanasiasa mkongwe wa CCM, Kingunge Ngombale-Mwiru kufanya kikao na waandishi wa habari nyumbani kwake na kukemea viongozi wanaokikosoa chama hadharani, ni dalili mojawapo ya kwamba kikao hicho kingejadili ajenda hiyo.

Ingawa Kingunge alifanya mkutano wake nyumbani kwake, lakini maandalizi yote yalifanywa na ofisi ndogo ya CCM na hata viongozi wa Umoja wa Vijana wa chama hicho waliohudhuria.

Pia katibu mkuu wa CCM, Yusuf Makamba alinukuliwa juzi akidai kwamba, wale wote ambao wamekuwa wakikituhumu chama hicho kwa ufisadi lazima waondoke.

Tofauti na siku nyingine, kwenye kikao cha jana kulikuwa na ulinzi mkali wa chama na waandishi walizuiwa hata kulikaribia jengo.

Akizungumza na Mwananchi juzi, Makamba alisema kuwa, hawezi kuzungumza kitu chochote nje ya kikao, hivyo akasema hawezi kuanika hadharani agenda za kikao hicho.

Kauli ya Makamba iliungwa mkono na ofisa habari wa CCM, Gabriel Athuman ambaye jana alizungumza na mwandishi wa gazeti dada la Citizen akisema kikao cha jana kingekuwa cha siri kubwa na akawatahadharisha waandishi kutofika wala kupiga picha.

Majina ambayo yalitajwa kuwa yangeweza kujadiliwa ni pamoja na mbunge wa Nzega Lukas Selelii, Spika wa Bunge Samuel Sitta na Mbunge wa Ilemela; Anthony Diallo. Hata hivyo, Mwananchi haikuweza kuthibitisha habari hiyo.

Kikao hicho kilipangwa kuanza asubuhi, lakini kikachelewa hadi saa 9:40 baada ya Rais Kikwete kuwasili.
 
Wacha tusubiri maamuzi ya Halmashauri Kuu kesho.

Kama na Andrew Chenge ni mjumbe pamoja na marais wastaafu (yaani BWM, Mzee Mwinyi na Komandoo) pamoja na Makamba basi matokeo ya kikao hicho ni rahisi kuyatabiri!
 
Hata wakae kama kamati bado mambo yamewashinda, mawazo na fikra zao ni ya zamani wanataka kushindana na mawazo ya kizazi cha sasa, watatumia ubabe tu hakuna mpya hapo hata iwe siri vp.
 
Mbona kamati nzima haina moral support? Ila wakilikoroga tu, wamekisha.
 
Zaidi ya nusu ya CC wana tuhuma nzito za ufisadi, hapa tutegemee kauli za kujaribu kuwasafisha watu fulani au labda kujaribu kuahirisha mjadala ili wananchi wasahau.
 
Hawana jipya hawa jamani walikaa vikao Butiama na kila wakati hakuna kitu kipya zaidi ya majungu
 
Hata wakiwanyamazisha wana sisiemu wenzako, wananchi wengine hatunyamazi, tumeshawajua.....2010 Mpaka kieleweke
 
Sidhani kama sisiemu itameguka mwakani kwani ni kikundi ambacho kipo kwa ajili ya mshiko. Hivyo kama mgawanyo wa keki ya Taifa utaweza kuwanufaisha wote, basi tutarajie mshikamano zaidi utakaokuwa umejengwa juu ya fedha. Vilevile tutarajie ufisadi zaidi na zaidi.

Pamoja na hayo yote, Taifa lipo kwenye njia muafaka katika mapambano dhidi ya Ufisadi.
 
Mugo"The Great";554075 said:
Sidhani kama sisiemu itameguka mwakani kwani ni kikundi ambacho kipo kwa ajili ya mshiko. Hivyo kama mgawanyo wa keki ya Taifa utaweza kuwanufaisha wote, basi tutarajie mshikamano zaidi utakaokuwa umejengwa juu ya fedha. Vilevile tutarajie ufisadi zaidi na zaidi.

Pamoja na hayo yote, Taifa lipo kwenye njia muafaka katika mapambano dhidi ya Ufisadi.

Lazima watameguka tu, kwani kasungura kao ni kadogo na kanaelekea kuisha bila wengine kuambulia chochote wakati ugali ndio kwanza umekaribia kutengwa 2010, unasema tutarajie mshikamano hapo? mshikamano gani kijikundi kidogo kipate sana na wengine (wengi) wakose halafu utegemee kundi kubwa kuunga mkono usiokuwa na chochote? uzuri wa jambo hili ni kwamba CCM wanamalizana wenyewe kwa kutumia remote waliyoshika wenyewe eg marupurupu ya Bungeni, mafisadi kutenga fedha za kuwalipua vidomodomo mwakani etc,
 
Back
Top Bottom