BAK
JF-Expert Member
- Feb 11, 2007
- 124,790
- 288,009
Na Saed Kubenea
Mwanahalisi~Maslahi ya Taifa Mbele
Mwanahalisi~Maslahi ya Taifa Mbele
UTEUZI wa wakuu wapya wa wilaya, uhamisho wa baadhi na kustaafishwa kwa wengine, vinadaiwa kuingiliwa na mtandao wa aliyekuwa waziri mkuu, Edward Lowassa, MwanaHALISI limeelezwa.
Taarifa zinasema kati ya wakuu wa wilaya 15 walioteuliwa wengi wao ni wale wanaodaiwa kuwa ni wafuasi wa karibu wa kundi la Lowassa, huku wakuu wa wilaya watano walioachwa wakiwa miongoni mwa wale waliowahi kugombana naye.
Aidha, taarifa ambazo hazikuthibitishwa zinadai kuwa inawezekana orodha ya wakuu wa wilaya iliyotangazwa ni tofauti na ile ya awali.
Kwa mujibu wa taarifa hizo, baadhi ya wakuu wa wilaya waliotangazwa hawakuwamo katika orodha hiyo,huku wengine wakipelekwa wilaya tofauti na zile walizoarifiwa mapema kuwa watahamishiwa.
Angalau mmoja ambaye ametajwa kupelekwa ambako alikuwa hakuandaliwa awali, ni mkuu mpya wa wilaya ya Bahi, Dodoma, Betty Mkwassa. Awali alipangwa Makete, Iringa.
Gazeti lilipowasiliana na Betty kujua kilichotokea hadi akakwepa kwenda Makete alisema, "Kwanza, sijui kama nilikuwa nimepangiwa kwenda Maketa. Pili, sijui kilichotokea. Waulizeni wanaopanga."
MwanaHALISI limethibitishiwa kwamba Betty alijulishwa kuwa anahamishiwa Makete, na kwamba hata Betty mwenyewe aliwahi kulalamika kwa watu kadhaa juu ya hatua hiyo.
Walioteuliwa ambao wanatajwa kuwa wafuasi wakubwa wa Lowassa, ni pamoja na Norman Sigalla (Hai) Francis Isaac (Mbulu), Erasto Sima (Korogwe) na Christopher Ryoba Kangoye (Kwimba).
Isaac anatajwa kuwa ni mfuasi wa karibu wa kundi la mtandao maslahi, akihusishwa zaidi na mwenyekiti wa zamani wa UV-CCM Emmanuel Nchimbi.
Isaac akiwa Katibu Mkuu wa UV-CCM, Nchimbi alikuwa mwenyekiti wa umoja huo, huku Lowassa akiwa mwenyekiti wa Baraza la Wadhamini.
Wakati mkataba wa UV-CCM na mbia wake kampuni ya M.M. Integrated Steel Mills Limited., unasainiwa, "Isaac alikuwa mtu muhimu akishika nafasi ya Mkuu wa Idara ya Fedha na Uchumi ya UV-CCM.
Ilikuwa ni vigumu kwa kambi ya Lowassa kumuacha nje Isaac, hasa baaada ya kupoteza ukatibu mkuu," taarifa zinasema.
Kabla ya kutangazwa kuwa mkuu wa wilaya, Isaac tayari alikuwa anachunguzwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana Rushwa (TAKUKURU) kwa tuhuma za kumiliki mali nyingi kinyume na kipato chake.
Kangoye alikuwa mgombea ubunge katika jimbo la Tarime mkoani Mara. Anatajwa kuwa ni mfuasi wa karibu wa Lowassa ingawa hakuna maelezo zaidi juu ya mahusiano yao.
Mjumbe mmoja wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM (NEC) aliyezungumza kwa sharti la kutotajwa jina, alisema uteuzi huu umeaibisha serikali.
Alisema, "Huwezi kuteua mtu ambaye anakabiliwa na tuhuma lukuki kama hizi za matumizi mabaya ya madaraka. Basi hakukuwa hata na sababu ya kumuondoa Mnali."
Albert Mnali alikuwa mkuu wa wilaya ya Misenyi. Aliondolewa baada ya kumuamuru askari kupiga walimu viboko.
Kwa upande wa waliostaafishwa, wanaotajwa kuwa walikwaruzana na Lowassa, iwe hadharani au kwa siri, ni pamoja na aliyekuwa mkuu wa wilaya ya Nyamagana, Kanali mstaafu, Peter Madaha, mkuu wa wilaya ya Muleba, Deusdedit Mtambalike na aliyekuwa mkuu wa wilaya ya Kyera, Mashimba Mashimba.
Kanali Madaha alikuwa mtendaji wa kwanza kumkosoa Lowassa hadharani. Akiwa katika ziara ya kikazi wilayani Nyamagana mapema mwaka 2007, Kanali Madaha alimrushia kumbora Lowassa, "Usinifundishe kazi. Nimefanya kazi hii kwa zaidi ya miaka 15."
Kuna taarifa kwamba Lowassa alizozana na Mtambalike kiasi cha kumsainisha "hati ya kumfukuza kazi." Kwa mujibu wa taarifa, Mtambalike alilazimishwa na Lowassa kusaini hati isemayo, "Kama itatokea ukafanya kosa la pili utakuwa umefutwa kazi."
Haijafahamika Mtambalike amefanya kosa gani la pili hadi kuondolewa ukuu wa wilaya.
Kwa upande wake, Mashimba alikosana na kundi la Lowassa baada ya kumtetea Nape Nnauye aliyepinga mkataba wa UV-CCM wa kupangisha jengo na ujenzi wa mradi katika Kiwanja Na. 108/2 barabara ya Morogoro jijini Dar es Salaam, kati ya UV-CCM na mbia wake unaomhusisha moja kwa moja Lowassa.
Miongoni mwa waliobakishwa na ambao haikutegemewa wabakizwe ni Kanali Edmund Mjengwa ambaye wakati huo aliteuliwa kuwa mkuu wa wilaya ya Shinyanga.
Kanali Mjengwa anatuhumiwa kuiba fedha za Mfuko wa Maendeleo ya Elimu Mbarali. Wananchi wa Mbarali walifungua kesi Mahakama Kuu baada ya serikali kukataa kufanya hivyo.
Hata hivyo, kesi hiyo ilichukuliwa na Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) lakini baadaye akaifuta.
Mwingine ni Thomas ole Sabaya. Huyu ana tuhuma za kuandaa na kushiriki katika ukandamizaji wa haki za wananchi wa Serengeti.
Miongoni mwa tuhuma zinazomkabili ni kuamrisha kuchoma moto nyumba za wananchi na kuhamisha zaidi ya familia 135 katika kijiji cha Nyamuma Iliyobaki, wilayani Serengeti.
Katika uchunguzi wake, Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, ilibaini kuwa aliongoza kunyang'anya wananchi ardhi yao. Tume iliagiza serikali kumchukulia hatua za kisheria.
Kutokana na hali hiyo, haikutarajiwa kuwa Rais Kikwete angembakiza katika utumishi wa umma.
Mwingine ni Pascal Mabiti, aliyehamisha kutoka Manyoni kwenda Singida Vijijini. Mabiti akiwa mkuu wa wilaya ya Tarime, mkoani Mara, anatuhumiwa kuvunja haki za binadamu katika mahusiano yake na wananchi, hasa kuhusiana na wamiliki wa migodi ya Nyamongo wilayani Tarime.
Ni Mabiti aliyekamata na kuweka chini ya ulinzi waandishi wa habari waliokwenda kuchimbua taarifa kuhusu unyanyasaji katika migodi hiyo.
Tundu Lissu, wakili mahiri aliyefuatilia kwa karibu matatizo ya Migodi ya Nyamongo alipata kusema, "Tokea mwaka 2003 tuhuma za Mabiti ziko wazi. Rais alipaswa kumwambia, ‘Una tuhuma. Pengine si za kweli, lakini pengine ni za kweli. Sikutaki, utaniharibia katika serikali yangu mpya.' "
Katika orodha hiyo, wamo Hawa Mchopa, James Yamungu na Philemon Shelutete. Wote hawa wanadaiwa kuwa wamebaki kutoka na kile kinachoitwa, "wanamtandao kuingilia kati."
Kuna madai kwamba kati ya wakuu wa wilaya wapya 17 walioteuliwa na Kikwete mwaka 2006, saba (7) walitoka mkoa wa Arusha.
Lakini wapo wanaodai kwamba wakuu wengi wa wilaya wakati ule, waliteuliwa au kubakishwa katika nafasi zao kutokana na shinikizo la aliyekuwa waziri mkuu, Edward Lowassa.