Utajiri wa dhahabu wageuka laana Geita - Wakazi Waishi kwenye Mahema kama Wakimbizi

nngu007

JF-Expert Member
Aug 2, 2010
15,862
5,797
Deus Bugaywa

Toleo la 237
2 May 2012

237_geita.jpg



  • Wakazi waishi kama wakimbizi
  • Kambi yao ya mahema yaitwa Darfur

UKISOMA taarifa ya mwaka 2011 ya Wakala wa Ukaguzi wa Madini Tanzania (TMAA) kuhusu kuogezeka kwa uzalishaji wa dhahabu na mapato yatokanayo na madini hayo, unaweza kufikiri kuwa hii ni miongoni mwa nchi chache katika Afrika zenye neema ya maziwa na asali.


Kwa mujibu wa ripoti ya mwaka 2011 ya uzalishaji wa madini ya TMAA, mapato yaliyotokana na dhahabu kutoka kwa migodi sita mikubwa nchini yaliongezeka kwa asilimia 38.1 kutoka dola za Kimarekani bilioni 1.58 mwaka 2010 hadi dola bilioni 2.11 mwaka 2011, ongezeko hilo likichangiwa na kuongezeka kwa bei ya dhahabu katika soka la dunia.

Wastani wa bei ya dhahabu iliongezeka kwa asilimia 28.4 kutoka dola za Kimarekani 1,223.98 kwa wakia mwaka 2010 mpaka dola za Kimarekani 1,571.28 kwa wakia mwaka 2011 kutokana na kuwa na mahitaji makubwa ya dhahabu yaliyosababishwa na kuyumba kwa thamani ya pesa na mtikisiko wa uchumi duniani.


Katika kipindi hicho pia uzalishaji wa dhahabu kutoka katika migodi hiyo uliongezeka kwa asilimia 4.9 kutoka wakia milioni 1.22 mwaka 2010 mpaka kufikia wakia milioni 1.28 mwaka 2011, ongezeko hili lilitokana na kuongezeka kwa uzalishaji katika mgodi wa Geita (GGM).


Mgawanyo wa usafirishaji dhahabu kwa migodi hiyo kwa asilimia ni Geita Gold Mine (GGM) asilimia 37.4, Bulyanhulu 18.9%, Buzwagi 14.4%, North Mara 13.4%, Golden Pride 9.5% na Tulawaka 6.5%.


Kiwango cha dhahabu kilichozalishwa mwaka 2011 kinaifanya Tanzania kuwa nchi ya nne kwa uzalishaji wa dhahabu barani Afrika ikizifuatia Afrika Kusini iliyozalisha wakia milioni sita, Ghana wakia milioni tatu na Mali wakia milioni 1.4.


Katika kipindi hicho, mrahaba uliolipwa kwa Serikali ulitakiwa kuongezeka kwa asilimia 42.4 kutoka dola za Kimarekani milioni 41.29 mwaka 2010 mpaka kufikia dola za Kimarekani milioni 58.80 mwaka 2011. Hata hivyo, kiasi halisi cha marahaba kilicholipwa mwaka 2011 ni dola milioni 57.61 kwa wastani wa dola milioni 4.8 kwa mwezi. Mrahaba uliolipwa ni asilimia 3 ya asilimia 90 ya mapato ghafi ya dhahabu.


Ukaguzi wa TMAA uliifanya migodi mine inayomilikiwa na African Barrick Gold (ABG) kulipa dola milioni mbili kama kodi ya mafuta (fuel levy) ambazo kampuni hizo hazikuwa zimelipa mpaka kufikia mwaka 2010, ukaguzi huo ulibaini kuwa North Mara Gold Mine ilikuwa inadaiwa dola milioni moja, Buzwagi Gold Mine dola 600,000, Bulyahulu Gold Mine dola 200,000 na Tulawaka Gold Mine Dola 200,000.


Katika hali ya kawaida, taarifa hizi za TMAA ni habari njema kwa nchi inayotaka kukuza uchumi ili kuuhudumia vyema umma wake.


Muulize Bi. Mwajuma Hussein (74) na wenzake, kama habari hii ni njema kwao, na watakuambia bora madini hayo yangebaki ndani ya ardhi kama alivyopata kusema Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere.


Yeye na wenzake hao wanasema wamekutana na sura mbaya na halisi ya uwekezaji usiojali umma katika migodi mikubwa nchini.


Nilikutana naye saa 12 jioni wakati nilipofika yalipo ‘makazi' yake na wenzake yanayojulikana kama ‘Darfur' kwa wakazi wengi wa mji wa Geita, kutokana na kufananishwa na kambi za wakimbizi wa Darfur huko Sudan. Kambi hii iko katikati ya mji wa Geita.


Kama nisingekuwa nimeelekezwa vizuri, isingekwa rahisi kutambua kwamba haya ni mahema wanayoishi binadamu, kwa sababu ukiyaona kwa mara ya kwanza, ni rahisi sana kuyafananisha na lundo la taka zilizotelekezwa. Huwezi kufikiri kama yanaweza kuwa makazi ya binadamu.


Wakati nakaribia ‘hema' lake, anaacha kazi ya kulikarabati hema hilo ambalo limechakaa sana, ananishangaa kuona ninakatisha njia kuelekea kwake. Uso wake unaonyesha dalili za kukata tamaa na kutokuwa na matumaini, ninamfikia namsalimia na kujitambulisha.


Ananikaribisha hemani kwake, tunaanza mazungumzo, sauti yake, hata hivyo, ni ya kukwaruza na inasikika kwa tabu kwa sababu anasumbuliwa na kikohozi kwa muda sasa. Namuuliza kama atamudu kuendelea kuzungumza, anasema kwa shida alizopata mpaka sasa, haoni kama hilo ni tatizo.


Anakumbuka mgogoro kati yao na mwekezaji, Geita Gold Mine (GGM), ulianza mwaka 2003 kati yao na mwekezaji huyo.


Wakalazimika kwenda kwa Mkuu wa Wilaya wa wakati huo, wakashindwa kuelewana, na hivyo Mkuu huyo wa Wilaya akawaambia anayedhani ana haki akafungue kesi mahakamani.


Wakashitaki katika Mahakama ya Wilaya, wakashinda, lakini mwekezaji akakata rufaa akashinda. Na wao wakakata rufaa, lakini sasa kwa kuchanganyikiwa na maisha hata hawajui ni nini kinaendelea juu ya hatma yao.


Lakini anakumbuka vizuri jinsi safari yao kuelekea kambi hiyo anayoiita ya mateso ilivyoanza.


Anasema Julai 31, 2007, saa 10 alfajiri, walikuja watu wa Serikali na kumuamsha balozi wao wa wakati huo na kumweleza kuwa wanatakiwa watoke hapo kwa sababu wamevamia eneo la Mzungu mwekezaji.


Anasema siku hiyo yeye na familia za wenzake zipatazo 86 walitolewa kwa nguvu katika eneo linaloitwa Mine mpya, na kupelekwa katika jumba la Mahakama wilayani hapo na kutupwa humo, ambako walikuwa wakilala hapo familia zote hizo kwenye eneo moja katika mchanganyiko wa wakwe, wakamwana, watoto na wazazi, hali ambayo anasema iliwafadhaisha sana na kuwavua utu wao kama binadamu.


Hata hivyo baada ya kutelekezwa hapo anasema serikali ya wilaya haikufanya chochote kuwasaidia. Hata hayo mahema wanayotumia sasa walipewa msaada na Kanisa la AIC, wilayani hapo, lililowachimbia pia vyoo.


Anasema Serikali imewapiga marufuku watu kuwasaidia kwa kuwa watakuwa wanawapa kiburi cha kuendelea kukaa hapo.


Anakumbuka maisha yake katika eneo walilohamishwa kuwa alikuwa anamiliki nyumba na shamba la eka tatu ambazo alikuwa analima mihogo, mahindi viazi na migomba vikimwezesha kuendesha maisha yake na mwanae bila shida.


Vyote hivyo sasa hana na analazimika kuwa omba omba na kufanya vibarua katika umri huo mpevu.


"Mwanangu kama haya ndiyo maisha yenu mnavyotaka kutufanyia sisi wazazi wenu haya. Nimeteseka mateso yote ambayo umewahi kuyasikia. Wakati wa uhuru Nyerere alituambia tunapigania uhuru ili nchi yetu iwe huru, tusinyanyaswe na wakoloni.


" Lakini kumbe uhuru ule ulikuwa kazi bure, leo tunakuwa wakimbizi kwenye nchi yetu wenyewe na viongozi wetu ndiyo wanakubali tuteseke hivi kweli?!" analalamika Bi. Mwajuma.


Bibi Mwajuma hayuko peke yake katika kuwanyooshea kidole viongozi. Yupo pia Bi. Veneranda Thomas, mjane mweye watoto wawii ambaye alifiwa na mumewe, Balatazar Emmanuel, katika kambi hiyo hiyo Juni, 2010. Yeye anasema sasa hivi wanaishi maisha kama ya chura katika hayo mabanda.


"Kaka yangu we si umeingia ndani ya hayo mahema umeona? Humo anaweza kweli kuishi binadamu, au sisi Serikali inatuonaje? Sasa hivi baada ya mvua ya mchana humo pamejaa maji, tunalala kama vyura na watoto wadogo. Hivi kweli jamani sisi ni Watanzania?


" Mbona tunanyanyasika hivi kwenye nchi yetu? Hivi huu utajiri wa dhahabu ndio unaotutesa hivi?" anahoji Veneranda mama mwenye watoto wawili wenye umri wa miaka 10 na 7 huku machozi yakimtoka.


Anasema tokea watupwe hapo miaka mitano sasa hakuna kiongozi yeyote aliyehangaika kwenda kuwaona isipokuwa aliyekuwa mbunge wa Geita Ernest Mabina, wakati akiwa mbunge alipita kuwasalimia na kuwaachia shilingi 20,000 na akaahidi kwenda kuwaona na kuwasikiliza lakini hakutokea mpaka alipopoteza ubunge.


Wengine ni viongozi wa CCM Wilaya waliowahi kwenda kuwaona na kuahidi kushughulikia tatizo lao lakini mpaka sasa hawajawaona tena.


Bakari Juma, mmoja wa wakazi wa eneo hilo, anasema wakati wanahamia hapo walikuwa familia 86 lakini sasa zimebaki familia 20 tu, wengine wakikata tamaa na kuondoka au kusadiwa na ndugu zao lakini wengine wamefia hapo hapo katika kambi hiyo. Anasema tangu wapelekwe hapo wakuu wa familia tisa wamefariki dunia kambini.


Yeye pia, kama wenzake, anasema hana kazi za kufanya baada ya kunyang`anywa ardhi aliyokuwa akiitumia kwa kilimo kukimu familia yake. Sasa analazimika kufanya vibarua ambavyo navyo havimhakikishii kipato cha kutosha kumudu gharama za juu za maisha.


Hata hivyo anasema wamepimiwa viwanja katika eneo la Samina ambavyo anasema eneo hilo ni lukili (ardhi yenye mavumbi laini, hailimiki) lakini pia hajui watavifanyia nini viwanja hivyo kwa sababu hawana uwezo wa kujenga na hawawezi kulima eneo hilo.


Wakati wananchi hao wakipata mateso hayo ambayo chanzo chake ni utajiri wa rasilimali katika nchi yao, Tanzania ni kati ya nchi nyingi za Afrika zenye utajiri mkubwa wa risilimali inayoelekea kukumbwa na laana ya rasilimali.


Laana ya rasilimali ni msamiati unaotumika kuelezea nchi zenye rasilimali nyingi zinazoshindwa kuzitumia rasilimali hizo kwa manufaa ya wananchi wake. Nchi inakuwa tajiri wa rasilimali lakini watu wake wanakuwa masikini kupindukia huku rasilimali hizo zikinufaisha wawekezaji wa kigeni.


Wakati wananchi waliokuwa wakiishi katika maeneo yenye utajiri wa dhahabu wakiwa katika mateso yanayotokana na kutimuliwa katika maeneo yao ya asili, wawekezaji wanaendelea kunufaika na rasilimali hizo.


Nyakabale Matandani na liwalo na liwe

Katikati ya mapato makubwa haya ya makampuni ya madini wananchi wa kijiji cha Nyakabale wako katika mgogoro mkubwa na mgodi wa Dhahabu wa Geita kutokana na kuamua kuweka kambi mahususi ya kusaga magwangala (mawe yaliyotumika mgodini na kutupwa) ili kujipatia mabaki ya dhahabu waweze kumudu kuendesha maisha yao.

Kambi hiyo inayojulikana kwa jina la Nyakabale Matandani katika muda wa mwaka mmoja ilioanzishwa tena baada ya kuwa imesambaratishwa na Serikali sasa ina zaidi ya wachimbaji wadogo elfu moja ambao wanazidi kuongezeka kila uchao.


Kambi hiyo iko chini ya kilomita tano kutoka vilipo vifusi vya mawe hayo vinavyomwagwa kutoka mgodini Geita na kwa mujibu wa sheria kuchukua magwangala hayo ni wizi na hivyo hawaruhusiwi. Lakini wao wameamua makusudi kupambana na Serikali inayowadhibiti wasichukue mawe hayo ambayo ni mali ya mgodi wa GGM.


Kwa mujibu wa kamanda wa Sungusungu wa kijiji cha Nyakabale, Yusuf Bangili, mtazamo wa wananchi wa kambi hiyo na kijiji hicho ni kuwa wanachofanya si wizi isipokuwa ni kuchukua mabaki ya mali yao ili waweze kujikumu kimaisha kwa kuwa kabla ya migodi kuja uchimbaji mdogo ndiyo ilikuwa shughuli yao.


" Sababu kubwa ni kwamba kabla hata Wazungu hawa hawajaja, haya yalikuwa maeneo ya wachimbaji wadogo wadogo, sasa hivi tumefukuzwa na ardhi yetu unaiona hauwezi kulima, hata ardhi ya kulima haipo, kila ukigusa mahali unaambiwa kuna leseni ya Mzungu. Sasa inabidi tu wakachukue hayo magwangala ili wasage wapate chochote kile kuendesha maisha," alisema kamanda huyo.


Anasema Serikali isiendelee kuwapuuza na kutuma askari kuwapiga risasi, gololi na mabomu kwa kuwa hizo ni dalili za kilio cha wananchi wake. Inatakiwa iwasikilize, badala kuwa wanakimbizana nao kama kama paka na panya.


"Mahusiano ya wananchi wa hapa na mgodi ni mabaya sana. Watu wanachukua mabaki wanaambulia mabomu na risasi. Tunapata tabu, Serikali isipokuwa makini, huu unaweza kuwa mwanzo wa machafuko na yenyewe itakuwa ndiyo chanzo. Hawa wengi walikuwa kwenye machimbo ya Nyamatagata huko nako pamechukuliwa na kumewekwa ulinzi, sasa watu waende wapi,'' anahoji.


Pendo Edward ni miongoni mwa wanawake wengi walioko katika kambi hii ambaye anasema ameamua kufanya kazi hiyo kwa kuwa ndiyo njia pekee inayoweza kumpatia kipato kwa sababu hana ardhi ya kulima hata kama akiamua kulima.


"Maisha yetu ni kukimbizana na polisi, kila siku wanaletwa kulinda mali za hao Wazungu. Lakini sisi hatuna pa kwenda, tunakimbizana hivyo hivyo.


Majeraha haya mkononi niliyapata wiki iliyoisha nilipokuwa ninawakimbia polisi waliokuwa wanapiga risasi kutufukuza", anasema kuonyesha vidonda kwenye mikono yake vinavyoanza kupona.


Mbali na hilo ana kilio kingine cha maji katika kijiji hicho, anasema kijijini hapo maji ni ya shida sana na wanakunywa maji machafu sana, lakini hawana namna. Wakati analalamikia maji kuwa ya tabu kijijini hapo, bomba la maji linalotoa maji Ziwa Victoria kupeleka kwenye mgodi wa GGM linapita chini ya kilomita mbili kutoka kijijini hapo.


Mkuu wa Mkoa mpya wa Geita, Said Magalula, akizungumzia hali hiyo katika kijiji hicho cha Nyamalembo alisema kuwa kwanza hana taarifa kuwa kuna kambi hiyo ya Nyakabale Matandani lakini anakiri kuwapo wananachi wanaovamia eneo la mgodi na kuiba mawe katika eneo hilo na hatua za mwanzo tayari zinachukuliwa kuwadhibiti kwa kufanya doria ya askari katika maeneo hayo wakati wakitafuta suluhu ya kudumu.


Alipoulizwa kuwa haoni kuwaweka wananchi hao katika kundi la wezi si sawa kwa kuwa wanafanya hivyo si kwa dhamira mbaya isipokuwa ni matokeo ya sera mbaya alisema mwizi ni mwizi na wizi haukubaliki.


"Bwana mwizi ni mwizi tu, mtu akiwa na njaa si sababu ya kuhalalisha wizi, wizi ni kitu kisichokubalika, kama wanataka tuwasikilize waache kwanza kuiba ndipo waje tuzungumze" alisema Mkuu wa Mkoa.


Hata hivyo mbunge wa Geita, Donald Max, anakiri kuwa uwekezaji huo umeleta matatizo makubwa kwa watu wake na yeye kama mwakilishi wa wananchi hao anajitahidi kufikisha kilio cha wananchi mahali kinapotakiwa kupata suluhu.


"Mambo ya machimbo ni magumu sana, suala la kambi hiyo ya wananchi waliotolewa Mine mpya, nimelifikisha kwa Mkuu mpya wa Mkoa ili pamoja tuone tunalitafutia ufumbuzi vipi, niko ziarani vijijini, nikimaliza ziara nitalifuatilia kwa Mkuu wa Mkoa," anasema.


Hata hivyo, mbunge huyo anasema kuwa matatizo katika jimbo lake yanayohusiana na uwekezaji wa madini ni mengi na yako kila mahali, hivyo anapanga kukutana na wachimbaji wadogo wadogo wote kwa pamoja ili kujadiliana nao namna gani nzuri wanaweza kutatuliwa matatizo yao.


Tangu kuingia kwa uwekezaji wa madini katika migodi mikubwa kumekuwa na kilio toka kwa wananchi wanaoishi kuzunguka migodi hiyo wakilalamika kunyanyaswa kwa gharama ya wawekezaji na wao kutofaidika na rasilimali hizo ipasavyo na badala yake wageni wamekuwa wakihamisha utajiri huo na kuwaacha wananchi katika lindi la umasikini mkubwa.











 
Ulafi wa Viongozi wetu; Wametuletea laana ya Madini ya Dhahabu serikali haipati chochote yaani asilimia 3 ni nini?
 
Laana ya milele iwe juu ya viongozi wa ccm na serikali yake, wanaowasababishia tabu na mateso wananchi wa Geita.
 
Ona sasa, mali zetu katika nchi yetu, lakini damu yetu inatumika kutolewa sadaka ili wezi wafanikishe kuiba, tena na watanzania wenzetu.
Siku ipo, tutanza vituo vya polisi hadi shimoni. Ipo siku tutaamka na kuitafuta damu ya wawekezaji weupe migodini, iwe kafara...nitaifurahia siku hiyo!
Jamani yote haya hatuoni bado, hadi tunaendelea kukumbatia sera zao? Mbona tunafundishana ukoloni mamboleo under UN ugents WB, IMF, UNESCO, nazo ICC, SAP,je? Ukifikiria sana haya, unalia kuanzia asubuhi hadi jioni, hayaingii akilini hata kidogo. INAUMAAAAA!
Mungu wetu anaita!
 
Wananchi tunalalamika wabunge wanalalamika rais analalamika wezi wanaendelea kuiba nani achukue hatua??au tunasubiri hadi tuanze kufungwa minyororo kama wakati wa utumwa!!acha tu tuteseke hadi akili irudi vichwani mwetu!!
 
Ndo maana tunataka states gvt. Haiwezekani madini yapo Geita, afu wanafaidi mawaziri, na raisi ambaye yuko Dar es Salaam.

Ndugu zangu tupiganie states gvt kwenye katiba mpya. Itaziba hii mianya yote ya rushwa na uonevu wa rasilimali zetu.

Ukienda marekani, California ni state tajiri kutoka na resources zake. California ni tajiri kuliko Washngton anapokaa raisi wa nchi.
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom