Utafiti: Wasaidizi wa mama lishe chanzo kipya cha ukahaba Dar

Ambakucha

JF-Expert Member
Aug 16, 2019
277
445
*Wengi wabeba mimba na kutelekezwa

*Baadhi ya Bodaboda, Bajaj, mafundi gereji, madereva wa daladala watajwa kuwarubuni

* Tamaa yadaiwa kuwaponza, wenyewe wadai ujira mdogo.

Biashara ya wanawake kuuza miili (ukahaba) imekuwa ikitoa ajira haramu katika baadhi ya nchi duniani, Tanzania ikiwemo. Lakini baadhi ya nchi, biashara hiyo imehalalishwa na kulipiwa mapato serikalini.

Nchini Tanzania, biashara hiyo haramu imekuwa ikifanywa katika miji mikubwa, lakini Jiji la Dar es Salaam linatajwa zaidi kuwepo kwa kufanywa na wanawake, hasa wasichana wa makabila mbalimbali kwa makundi makubwa matano.

Makundi hayo ni kama yafuatavyo; wasiyokuwa na ajira kabisa. Wenye ajira isiyokuwa na uhakika. Wenye ajira yenye vipato vidogo. Wenye tamaa ya maisha ya ufahari na wasiyokuwa na sababu yoyote zaidi ya hulka.

Maeneo ya Sinza ya Afrika Sana, Buguruni ya Chama, Stendi. Chang'ombe Kwa Sokota, Manzese ya Tip Top, Kinondoni ya Makaburini na baadhi ya baa kubwa ndiyo yanatajwa kuwepo kwa makahaba kwa kiwango cha juu.

MAENEO YANAYOTAJWA
Hata hivyo, utafiti wa kina uliyofanywa na mwandishi wetu umebaini kuwa, biashara ya ukahaba kwa sasa imezoa kundi lingine na kujikita huko kwa lengo la kujiingizia kipato zaidi. Kundi hilo ni wasichana wanaofanya kazi kwenye mabanda ya kuuzia chakula maarufu kama Mama Lishe.

Utafiti wa mwandishi umegundua kuwa, kutanuka kwa biashara ya kuuza chakula katika jiji la Dar ambalo kwa sasa linajulikana kuwa ni jiji la kibiashara, kumewapa ajira wasichana wengi ambao malipo yao hutegemea makubaliano na wamiliki wa biashara hiyo.

Aidha, utafiti huo uliyofanywa kwa wiki mbili, unaonesha kuwa, kutokana na ujira mdogo wanaolipwa wasaidizi hao, wengi wao wamejikuta wakiingia kwenye ukahaba kwa kuuza miili yao kwa wateja ambao kwa upande wa pili ndiyo wanaowahudumia chakula.

Maeneo ambayo baadhi ya wasaidizi hao wa Mama Lishe hujikwaa katika mitego ya ukahaba ni kwenye vituo vikubwa vya daladala, kama; Mbezi Mwisho, Mawasiliano Simu 2000, Tandika, Makumbusho, Mbagala Mwisho, Tegeta Nyuki, Kigamboni, Buguruni Sokoni, Machinga Complex n.k.

Maeneo mengine ambayo yametajwa kuwepo kwa wateja wa chakula wa Mama Lishe ambao pia ndiyo wanaowanunua wasichana hao ni; kwa madereva wa Bajaj, Bodaboda, mafundi wa magari kwenye magereji, wauzaji wa bidhaa masokoni na baadhi ya ofisi ambazo zipo mijini hususan katikati.

WANAVYOSEMA WASICHANA WENYEWE
(Majina yatakayotumika siyo halisi). Aisha Ally, yeye ni msaidizi wa Mama Lishe kwenye banda moja lililopo Kituo cha Daladala cha Mbezi Mwisho kwenda Kinyerezi, Tabata Segerea, Gongo la Mboto na kwenda Tandika. Yeye anasema:

"Ni kweli, ingawa siyo wote, lakini wasichana wengi tunaofanya kazi kwenye mabanda ya mama lishe tumetumbukia kwenye biashara ya kuuza miili pia mbali ya kuuza chakula. Tatizo ni malipo wanayotulipa mabosi wetu ambao wengi ni wanawake.

"Mfano mzuri; mimi, bosi wangu ananilipa shilingi elfu nne kwa siku. Ndivyo alivyoniambia. Mimi naishi Banana. Nauli ya kutoka kule mpaka hapa Mbezi ni shilingi elfu mbili kwa siku kuja na kurudi jioni. Kwa hiyo kwenye malipo yangu ya siku nabakiza shilingi elfu mbili ambayo haitoshi kwa mahitaji yangu. Maana nahitaji kununua vocha, nahitaji kula usiku, mchana tunakula bure. Pia nahitaji kuvaa na kulipa kodi ya chumba.

"Kutokana na hali hiyo nimejikuta nikimkubalia kila mteja anayenitongoza ilimradi tu kinywa chake kinitamkie habari ya pesa. Nimekuwa nikimwomba bosi wangu aniongeze malipo kwa siku lakini majibu yake ni kwmaba, biashara kwa sasa ni ngumu, nivumilie."

Salama Jumanne, yeye ni msaidizi wa Mama Lishe kwenye Kituo cha Daladala cha Mbagala Mwisho wilayani Temeke, Mkoa wa Dar es Salaam. Kwa upande wake anasema kuwa, ukiachia mbali uhitaji wa maisha yake kuwa mkubwa huku kipato kidogo, lakini wasichana wengi ambao wanahudumu kwenye mabanda ya Mama Lishe wanaelemewa na vishawishi kutokana na mazingira ya kazi zao.

Huyu hapa Salama: "Kwa kawaida kila Mama Lishe anakuwa na wasaidizi zaidi ya mmoja. Katika wasaidizi hao, wapo wanaotoa huduma palepale kwenye banda, halafu wapo wanaokwenda kwa wateja kuchukua oda ya siku hiyo Hawa ndiyo wapo hatarini zaidi.

"Mfano; bosi akishaivisha chakula mchana, mhudumu wa kutoka anawafuata wateja wake wa kila siku kuwauliza kama watakula. Wateja hao ni; madereva wa bodaboda, mafundi wa gereji, madereva wa daladala na wauza sokoni na kwingine. Wale wateja wana tabia ya kutushikashika makalio au kutukumbatia. Mwingine anakulazimisha denda. Lakini sasa na sisi ni binadamu, tunajikuta tunashawishika kwa sababu unakuta mtu anakwambia mkienda, mkimaliza atakupa elfu tano wakati wewe kwa siku unalipwa elfu nne au tano hiyohiyo.

"Lakini ukweli ni kwamba, mazingira ndiyo adui yetu mkubwa. Hivi, binti ana miaka ishirini, mwili bado ni damu changa, mtu anakulazimisha denda huku anakutajia elfu tano, nani atachomoka hapo?"

Mwandishi: "Wewe umewahi kufanya hivyo?"

Salama: "Mh! Kwa kweli sijui niseme ni ujana au vipi. Ila niliwahi kufanya nikaacha. Nilifanya kwa wateja ambao ni mafundi wa gereji. Tatizo wakawa wanaambiana.Yaani leo ukitembea na huyu, kesho anamwambia mwenzake, naye anakutaka. Mwisho wa siku nikajikuta nimetembea na watatu bila kutegemea. Ikabidi niache kazi maana watu walikuwa wakinitania."

Mwingine aliyezungumza na Mwandishi ni Anjela Simon. Yeye yupo Kituo cha Daladala cha Tandika. Anjela anasema kuwa, Novemba mwaka jana alijikuta akiangukia kwenye uhusiano wa kimapenzi kwa konda na dereva wake kwenye daladala linalofanya safari zake kati ya Tandika na Kariakoo jijini Dar es Salaam.

Anjela anasema kuwa, uhuni huo aliufanya kwa kishawishi kikubwa cha kutolipa nauli kwenye daladala hilo.

"Bosi wangu ana fremu ya chakula Tandika. Sasa alikuwa akinituma mimi kupeleka chakula kwa wateja Kariakoo kila siku. Hata Jumapili. Alikuwa akinipa nauli shilingi elfu moja kwenda na kurudi. Ndipo konda na dereva wake wakanizoea na kunitongoza.

"Ikawa nakwenda Kariakoo bure na kurudi bure ili tu kubana elfu moja ya nauli. Dereva ndiye aliyeanza kunitumia. Aliponichoka konda wake akanichukua. Nilikwenda naye mpaka alipooa, akaniacha," anasema Anjela.

Mwandishi: "Wakati unatembea na hao ulikuwa na uhusiano na mwanaume mwingine?"

Anjela: "Msema kweli ni mpenzi wa Mungu. Nilikuwa naye, ila hawa wa kwenye daladala nilivutiwa na vya bure tu."

Mwandishi: "Unajutia lolote?"

Anjela:"Najuta sana. Kwanza baadhi ya watu pale stendi walijua. Nikawa nachukuliwa mimi ni changudoa."

MANENO YA WANAONYOOSHEWA VIDOLE
Mwandishi aliweza kuzungumza na watu kutoka kwenye makundi yaliyotuhumiwa kuwa wateja wakuu wa wahudumu hao.

Bodaboda

"Kusema ule ukweli, hapa 'kijiweni' kwetu asilimia kubwa ya madereva tunaponea kwa hawa wasichana wanaofanya kazi kwenye mabanda ya chakula. Kwanza ni bei rahisi, pili huumizi kichwa kwa hela ya gesti. Asikudanganye mtu. Hawa mademu wengine mtaani ni pasua kichwa sana," anasema Hamees Ibra wa kituo cha Magomeni.

Daladala

"Mimi nawaona tu na vijana. Lakini sina munkali nao. Ila kwa kweli, kama kweli Ukimwi upo, hili kundi litamalizika sana kwa sababu wanafanya ngono bila kinga na ni kila siku. Inabidi serikali iwaangalie sana na kuwapa elimu," Dulla, dereva wa daladala la Mbagala- Simu 2000.

Mafundi gereji

"(kicheko kwanza) wale baadhi yao wanajiuza kwa makusudi tu ili wapate vitu vizuri kama simu janja. Viwalo vya kisasa. Wengine wanataka kuishi maisha ya kukopi mahali kwingine. Hata hapa gereji nawaona wakileta chakula lakini hawaondoki haraka, wanashikwashikwa ndani ya magari wee, wakitoka tayari macho mekundu. Wengine hata sahani walizobebea chakula wanasahau.

"Unajua nini! Gereji nyingi wanaofanya kazi ni vijana. Wanaojifunza ufundi pia ni vijana, tena vijana wadogo. Na wahudumu wanaotoa huduma ya chakula, nao wengi ni vijana. Kwa hiyo wote bado damu zinachemka," anasema Ramadhani, fundi gereji, Ilala jijini Dar es Salaam.

Jimmy, yeye ni mfanyakazi kwenye ofisi moja ya serikali iliyopo katikati ya Jiji la Dar es Salaam. Kwa upande wake, alisema:

"Tatizo la hawa wasichana ni dogo tu. Wajitambue. Watambue na kuiheshimu biashara wanayoifanya. Kuna wengine wanakuja wamevaa kikahaba kabisa. Hapo tofautisha na kuvaa vizuri. Sasa mwanaume wa leo, umvalie kikahaba, mchoro wote wa ndani unaonekana, atakuacha?

"Halafu kuna wengine mbali na kuvaa kikahaba, wameumbwa vizuri, sura nzuri na wanaume siku zote wanatamani vizuri."

NGONO HUFANYWA MAZINGIRA HATARISHI
Kwa kuongea na wasichana hao, wamekiri kuwa ngono na wateja wao huifanya katika mazingira yasiyo na ustaarabu kama vile kwenye vyoo vya mitaani (HAPA TUNATOA HUDUMA YA CHOO NA KUOGA), kwenye nyumba zinazojengwa, kwenye vichochoro vyenye kiza kinene, kwenye mabanda ya biashara (baada ya kufungwa usiku), ndani ya daladala na ndani ya magari mabovu yaliyoegeshwa gereji.

Uchunguzi unaonesha kuwa, wasichana hao wanaojishughulisha pia na kuuza miili, baadhi yao wamekuwa wakichelewa kurudi kwenye makazi yao kwa sababu ya kutenga muda wa kukutana na wateja wao kwa vile muda mzuri kwao ni baada ya giza kutamalaki katika uso wa dunia.

MALIPO YAO KWA SIKU
Kwa mujibu wa wasichana waliyokiri kujiuza, wateja wao ni kama wanaambiana, kwani baada ya kufanya ngono 'hulipwa' shilingi elfu tano mpaka elfu nane.

Ni habari njema kwao akimpata mteja ambaye atalipa shilingi elfu kumi kwa siku. Madereva wa daladala ndiyo wanatajwa kuwa watoaji wa kiasi kikubwa cha pesa huku wauzaji wa sokoni wakilalamikiwa kwa ubahiri.

Hata hivyo, wanakiri kwamba, wateja 'wanaotoka' nao hujitutumia kwa kuwanunulia chai asubuhi au chakula kingi mchana wakati mabosi wao huwapa chakula kichache kisicho na vikorombwezo vyovyote.

MAMA LISHE NAO WANENA
Baadhi ya Mama Lishe waliyozungumza na Mwandishi wamekiri kuwepo kwa matendo ya kuuza miili kwa baadhi ya wasichana wao wa kazi huku wakiwatupia lawama kwamba, wengi wanaofanya hivyo wana tamaa ya maisha na siyo vinginevyo.

"Mimi nilimpata msichana toka Mahenge, Morogoro. Alikuwa na miaka ishirini na moja tu. Alikuwa anaishi kwangu, anakula kwangu, anaoga kwangu, chooni anakwenda kwangu na kila siku nilikuwa namlipa shilingi elfu tano kila siku. Lakini kaondoka na mimba kurudi kwao na aliyempa hiyo mimba hamjui. Je, kama siyo tamaa ni nini?" anasema Mama Lishe aitwaye Maria Charles, mkazi wa Mbezi Kibanda cha Mkaa lakini biashara yake ipo Mbezi Stendi ya Kinyerezi, Dar es Salaam.

Mama huyo alikuwa akipingana na madai kwamba, wanawalipa ujira mdogo wasaidizi wao wa kazi kwenye biashara.

Mwingine aliyezungumza na Mwandishi ni Mama Kilangila, mkazi wa Ubungo Msewe akifanya biashara ya kuuza chakula, Mawasiliano, anasema kuwa, biashara ni ngumu kwa sasa, hailipi, hivyo ujira anaoulipa ni jukumu la mlipwaji autumieje.

"Msichana wangu namlipa shilingi elfu tano kila siku, na wala nauli siichanganyi. Lakini nimeshamshuhudia mara kadhaa akikumbatiwa na madereva wa daladala hapa stendi. Nimemuonya lakini wapi. Unaweza kumtuma apeleke chakula mahali akarudi baada ya masaa. Wengine ni hulka zao tu. Mbona hata baadhi ya Mama Lishe wenyewe pia wapo wanaojiuza ili kuongezea mitaji, " alisema Mama Lishe huyo.

Mama Lishe wengi waliyozungumza na Mwandishi walionekana kuwaponda wasichana wao wakidai kuwa, wana tabia ya uhuni tu na si vinginevyo. Wakawataka wanaume, hasa wenye familia kuheshimu ndoa zao na wale wasiyokuwa kwenye ndoa, hasa vijana kujichunga kwani dunia imebadilika, magonjwa ni mengi.
 
Waache wauze papuchi.
Ubakaji umepungua kwa kiasi kikubwa.
Watu wanamaliza genye zao kwao dada poa.
 
Maeneo ya Sinza ya Afrika Sana, Buguruni ya Chama, Stendi. Chang'ombe Kwasokota, Manzese ya Tip Top, Kinondoni ya Makaburini na baadhi ya baa kubwa ndiyo yanatajwa kuwepo kwa makahaba kwa kiwango cha juu.
... ijue jiografia ya nchi yako; maeneo uliyotaja hayapo katika jiji la dar es salaam! Ila jamaa alituweza kweli kweli!
 
Mjini hatuna mashamba Wala kulima ila tunakula......

Maeneo ya Dar hususani uswahilini yanaongoza kuwa na IDADI kubwa ya vijana watafutaji....vijana wasio na wake wala familia....wengine hulala NJE baada ya shughuli zao za Kutwa nzima....hawa huhusisha wale walalao ndani ya madaladala(makonda).....

Vijana wote hao hutaka "kupona"...."waponyeshaji" wenyewe ni mabinti wanaofanana nao kiuchumi........

Maisha ya huku uswahilini ni dunia nyingine kabisa japokuwa sisi sote mkuu wetu wa mkoa ni mh.AMOS MAKALLA....🤣
 
  1. Kama jukwaa tunawashauri nini serikali
  2. Tunawashauri nini wazazi
  3. Tunawashauri nini waajiri
  4. Tunawashauri nini wasichana
  5. Tunawashauri nini bodaboda ()
  6. Tunawashauri nini wazee wa mitaa na miji husika
 
Back
Top Bottom