Utafiti: Unywaji soda husababisha kansa ya tezi kongosho?

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,316
33,125
Utafiti wasema unywaji wa angalau soda mbili kwa wiki huongeza hatari ya kupata kansa ya tezi kongosho; viwanda vyadai utafiti una walakini.

Pepsi.jpg
Mapema mwaka huu iliripotiwa na majarida kadhaa sehemu mbalimbali duniani kuwa, kwa mujibu wa utafiti mpya, unywaji wa angalau chupa mbili za vinywaji baridi (soda) kila wiki huongeza uwezekano wa kupata kansa ya tezi kongosho.

Tezi kongosho lipo nyuma ya tumbo likiwa na kazi ya kuzalisha homoni ya insulin ambayo hufanya kazi ya kuchochea seli zinyonye sukari kutoka katika damu mara baada ya mtu kula au kunywa kitu chenye sukari. Pia hutoa vimeng’enyo ambavyo husaidia katika usagaji wa vyakula vyenye mafuta na protini.

Walio fanya utafiti huo wanasema kuwa watu wanywao chupa mbili au zaidi za vinywaji baridi kama soda kwa wiki wana uwezekano wa karibu alimia 87 wa kupata kansa ya tezi kongosho ikilinganishwa na wale wasiotumia vinywaji vya aina hiyo. Matokeo ya utafiti huo yamechapishwa katika jarida la Cancer Epidemiology, Biomarkers & Preventionlinalomilikiwa na chama cha tafiti za saratani cha Marekani.

Hata hivyo makampuni yanayohusika na utengezaji wa vinywaji baridi wameupinga utafiti huo wakidai kuwa ulikuwa na walakini na makosa mengi, huku wakiegemea katika matokeo ya tafiti zilizowahi hapo kabla ambazo zilionesha kutokuwepo kwa uhusiano wowote kati ya unywaji soda na kansa ya kongosho.

Katika utafiti wa sasa uliojumuisha watu 60,524 wenye asili ya Singapore na China na ambao ulitumia karibu miaka 14 kukamilika (kuanzia mwaka 1993), watafiti walichunguza vyakula na vinywaji wanavyokula waliohojiwa na kama walipata kansa katika kipindi chote cha ufuatiliaji.

Watafiti waliuliza washiriki kuhusu vitu wanavyokula ikiwemo soda (ingawa hawakugusia kuhusu diet soda kwa vile kwa wakati huo matumizi ya diet soda nchini Singapore yalikuwa chini sana) na juisi na iwapo vinywaji hivyo vilikuwa vya kawaida au vilikuwa na vitu vya kuongeza ladha (utamu).

Washiriki waliwekwa katika makundi matatu, wale wasiokunywa kabisa vinywaji baridi (soda au juisi), wanaokunywa chini ya chupa mbili kwa wiki, na wale wanaokunywa chupa mbili au zaidi kwa wiki. Katika kipindi cha miaka 14 ya ufuatiliaji, watafiti wanadai walikuta washiriki 140 wakiwa na kansa ya tezi kongosho. Aidha watafiti wanadai kuwa, wale waliokuwa wanakunywa chupa mbili au zaidi kwa wiki walikuwa na hatari ya kupata kansa kwa karibu asilimia 87. Hata hivyo, hakukuwa na uhusiano wowote kati ya unywaji juisi na hatari ya kupata kansa ya kongosho.

Watafiti hao wanaamini kuwa sukari iliyomo katika soda husababisha ongezeko la homoni ya insulin kutoka katika tezi kongosho, hali ambayo hufanya tezi hilo kufanya kazi kupita kiasi na hatimaye kupata kansa.

Hata hivyo wanasayansi kutoka baadhi ya viwanda vya soda wamekosoa matokeo ya utafiti huo wakisema kuwa utafiti huo ulikuwa na mapungufu na udhaifu mwingi sana. Mojawapo ya mapungufu hayo, wanadai wanasayansi ni kuwa idadi ya watu waliogundulika kuwa na kansa ya kongosho ilikuwa ndogo mno na hata miongoni mwa hao 140 waliogundulika, bado washiriki 110 waliripotiwa kuwa katika kundi la wale wasiokunywa kabisa soda, 12 walikunywa soda chini ya mbili kwa wiki wakati ni watu 18 tu waliokuwa katika kundi la wanywaji soda mbili au zaidi kwa wiki. Hii inaonesha kuwa kulikuwa na idadi ndogo mno ya watu waliokutwa na kansa ikilinganishwa na umati ulioshiriki katika utafiti huo.
Pancrease.jpg

Utafiti mwingine uliofanyika mwaka 2008 ulishindwa kuonesha uhusiano wowote kati ya matumizi ya soda na kutokea kwa kansa ya kongosho; wakati mtafiti mmoja kutoka kituo cha saratani cha Yale nchini Marekani alisema kuwa matokeo haya hayana budi kuchukuliwa kwa tahadhari kubwa kwa kuzingatia idadi ndogo ya watu waliogundulika kuwa na kansa na kushindwa kwa utafiti huo kuonesha jinsi unywaji soda unavyoweza kusababisha saratani.

Hata hivyo pamoja na tafiti nyingi kutofautiana na matokeo ya utafiti huu, zipo baadhi ya tafiti ambazo zilitoa matokeo yenye kuonesha kufanana kiasi fulani. Kwa mfano mtafiti Laurence N. Kolonel kutoka Kituo cha Utafiti wa Saratani katika chuo kikuu cha Hawaii, Honolulu huko Marekani alisema kuwa matokeo ya utafiti huu kwa kiasi fulani yanafanana na ya utafiti wao wa mwaka 2007 ambapo waligundua kuwepo kwa uhusiano kati ya utumiaji wa vinywaji vyenye kiwango kikubwa cha sukari aina ya fructose na saratani ya kongosho. Anasema kuwa kwa vile vinywaji baridi vingi vinatumiafructose kwa ajili ya kuongeza ladha, matokeo ya utafiti wao yanafanana sana na matokeo ya utafiti huu.

Tatizo jingine linaloonekana katika matokeo ya utafiti huu ni kushindwa kwa watafiti wake kuonesha ni kwa vipi walifikia hitimisho la kuwepo kwa uwezekano wa 87% wa mtu kupata saratani kutokana na unywaji wa soda, tukitilia maanani ukweli kuwa saratani ya kongosho ni ugonjwa unaotokea kwa nadra sana duniani kote (huwapata wastani wa watu 12 kwa kila watu 100,000).

Kwa maneno mengine ni kuwa matokeo ya utafiti huu hayawezi kutumika kutoa hitimisho kuwa unywaji wa soda unasababisha saratani ya tezi kongosho isipokuwa yanaonesha wanywaji wa soda huelekea kupata saratani ya kongosho zaidi ya wale wasio wanywaji.
Tafiti za afya
 
[h=2]Pombe ina magonjwa 60 kwa binadamu[/h]
MOJA ya vyanzo vinavyolipatia taifa mapato kupitia makusanyo ya kodi ni pombe.
Lakini pamoja na faida zote tunazozipata, ukweli unabaki palepale kwamba pombe ina athari katika maisha ya binadamu.

Mwanzoni mwa mwaka huu wataalamu wa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii na madaktari wastaafu walikutana na wanahabari jijini Dar es Salaam na kuzungumzia juu ya mkutano utakaozungumzia athari za pombe katika jamii.

Mkutano huo unaotarajia kufanyika Jan 13 hadi 14 mwaka huu mkoani Arusha, utashirikisha nchi za Afrika Mashariki.
Watunga sheria na wataalamu wengine kutoka serikalini watahudhuria huku ujumbe wa mkutano huo ni: ‘Kilevi si bidhaa ya kawaida na ni kikwazo katika maendeleo.'

Mkurugenzi Msaidizi na Katibu wa Magonjwa yasiyoambukiza, Dk. Joseph Mbatia, kutoka Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii anasema serikali ipo mbioni kutengeneza sera itakayohusu utumiaji wa pombe ili kupunguza athari zake katika jamii.

Dk. Mbatia anasema wamelazimika kutunga sera hizo baada ya kuona matatizo yanayotokana na pombe yanaongezeka kila kukicha.
Anasema kabla ya sera hizo kupitishwa watafanya utafiti katika maeneo mbalimbali ili

kujua ni jinsi gani jamii inavyolichukulia suala la pombe na madhara yake.
"Mfano, katika vijiji vichache tulivyofanya utafiti, wananchi walikuwa wakijitetea kwamba pombe imewasaidia kuendesha maisha yao…lakini ukweli ni kwamba pamoja na faida ambazo zimekuwa zikiorodheshwa, hasara ni nyingi kuliko faida.

"Kwa mfano, bima zimekuwa zikilipwa kutokana na ajali zinazosababishwa na kulewa kupita kiasi," anasema Dk. Mbatia.
Anabainisha kwamba sera zitakazowekwa si katika kupiga vita biashara ya pombe na badala yake zitakuwa zikiangalia njia bora za matumizi yake na kwa wale wataoonekana

wameshaathirika watawekewa utaratibu wa kupatiwa tiba.
Kwa upande wake Mwakilishi wa Kanda ya Afrika Mashariki ya ‘IOGT-NTO Movement', ambao ni waandaaji wa mkutano huo, Gunnar Lundstrom, anasema bado kuna

changamoto zinazolikabili taifa katika kupunguza athari za pombe.
Anasema changamoto hizo ni pamoja na pombe kupatikana kwa gharama nafuu na hivyo kusababisha watu kunywa kupindukia.

Tatizo lingine anasema ni pombe kuwa moja ya chanzo cha mapato nchini, jambo linalofanya serikali kushindwa kupiga marufuku.
Naye Daktari mstaafu, Maletnlema Tumsifu, anasema kuna jumla ya magonjwa 60

yanayosababishwa na unywaji wa pombe.
Anataja baadhi ya magonjwa hayo kuwa ni mfarakano katika familia, maambukizi ya ugonjwa wa ukimwi, unene kupita kiasi, utapiamlo hasi, mimba kuharibika na kisukari.

Dk. Maletnlema anasema kuna madhara ya pombe ya aina mbili. Kwanza ni kuathirika kwaa mishipa ya fahamu mwilini kote kwa kupunguzwa uwezo na pili ni kuungua baadhi ya ogani za mwili hasa tumbo pindi mtu anapokunywa.

Anaeleza kwamba katika kuathirika mishipa ya fahamu kumetizamwa kwa hatua nne za wanywaji, hatua ya kwanza ni ile ya kuchangamka.
Hapa mtu hujisikia mzima zaidi ya kawaida, moyo unapiga haraka, tumbo linameng'enya chakula haraka na hamu ya chakula kuongezeka.

Hatua ya pili, mtu akiendelea kunywa anachanganyikiwa na kuzungumza sana, kukosa aibu, utu kubadilika, kutawala tabia za kimwili, hamu ya chakula kuongezeka na hapa ndipo watu wanaagiza nyama choma kwa wingi.

Mnywaji akiendelea kunywa pombe hucharuka kutokana na neva zake za ubongo kushindwa kumiliki mwili.
Mambo yote anayoyafanya hayana utaratibu kwani mnywaji huwa mkorofi.
Dk. huyo anasema mnywaji huwa mkorofi na anaongea maneno yasiyo na maana, baadhi

ya wanywaji huchukulia hatua hii kama raha yao. Hapa kitu kinachojitokeza ni kupoteza hamu ya kula.
Hatua ya nne mtu akilewa kupita kiasi huwa hajijui na analala fofofo kutokana na

kupoteza fahamu. Huenda akajikojolea au kutapika, inategemea na kiasi cha pombe alichokunywa.
Wakati kwa upande wa ogani, pombe huathiri zaidi viungo vinavyopata pombe nyingi kila wakati mtu akiwa anakunywa.

Mfano wa viungo hivyo ni mdomo, koo na tumbo, ambavyo vyenyewe hufikiwa na pombe nyingi mara mtu anapomeza.
Tumbo likiumia inaonekana kama maumivu ya tumbo, pengine kutapika na kuharisha.

kutokana na utaratibu wa tumboni, lazima chakula chote pamoja na sumu au madawa vinavyonyonywa tumboni vipitie katika ini kuondoa sumu na vyakula visivyohitajika.
Na kwa sababu hii, pombe yote mtu anayokunywa hupita katika seli za ini na zinajaribu kuiondoa lakini nazo zinalewa chakari na baadhi zina kufa.


  1. Ieleweke kwamba tukinywa kidogo seli chache zinakufa na tukinywa sana zinakufa seli nyingi na nafasi yake inajazwa nyuzi nyuzi za kovu. Ini huwa na mabilioni ya seli ambazo ni imara, hata mtu akinywa pombe nusu, seli zake bado zitaendelea na maisha kama inafikia kikomo ini linashindwa kufanya kazi na kujikuta njia za nyongo na mishipa ya damu inaziba. Kila ogani ya mwili inaumia kivyake, lakini tumbo na ini ni mifano wazi.
 
Madhara ya kuvuta sigara


Mwili wa mvutaji sigara


Kila sekunde nane, mtu mmoja hufariki kutokana na utumizi wa tumbako. Imebainika kuwa saba kati ya wavutaji sigara kumi, huanza uraibu huu wakiwa wangali watoto. Wanaoendelea kuvuta sigara kwa muda mrefu hufupisha maisha yao kwa miaka 20 hadi 25. Sababu ni kuwa sigara ina kemikali zaidi ya 4,000 ambazo zina uwezo wa kudhhuru afya ya binadamu. Madhara yanayosababishwa na uvutaji sigara ni mengi na yamesambaa mwilini kote. Yafuatayo ni baadhi tu ya maradhi yatokanayo na utumiaji wa tumbako.

Yaliyomo





1.Kung'oka kwa nywele

Uvutaji sigara hudhoofisha kinga ya mwili na kisha kudhuru mizizi ya nywele . hii husababisha kung'oka kwa nywele mapema.

2.Magonjwa ya macho

Wavutaji sigara hupata magonjwa ya macho mara nyingi kuliko wasiovuta. Sehemu ya macho inayopitisha mwangaza inaweza kufichwa kama vile wingu linavyoficha jua(yaani kwa ikimombo) na kusababisha upofu. Ugonjwa huu husababishwa kwa njia mbili. Kwanza moshi wa sigara huwasha macho na pili kemikali zilizo ndani ya sigara hupita kwenye mishipa , damu na hatimaye kudhuru macho. Sigara pia husababisha kudhoofika kwa sehemu ya kati ya macho(retina) na hivyo kupunguza uwezo wa macho kuona vizuri na hata kutofautisha rangi(macular degeneration).

3.Kukunjana kwa ngozi

Kemikali zinazopatikana ndani ya sigara hupunguza uwezo wa ngozi kujirekebisha hivi basi ngozi huzeeka haraka na kupoteza uwezo wa kulainika. Mvutaji wa sigara huonekana mzeee zaidi kuliko umri wake haswa.

4.Magonjwa ya masikio

Uvutaji sigara huleta magonjwa mengi ya masikio . Sababu ni kwamba uvutaji wa sigara husababisha uchafu kuganda kwenye mishipa ya damu na hivyo kupunguza mwendo wa damu hadi kwenye sehemu za ndani za masikio. Moshi na kemikali za tumbako pia hujeruhi sehemu za ndani za masikio na majeraha hayo yanaweza kuambukiza hata ubongo(menengitis). Yote haya yanaweza kusababisha uziwi.

5.Saratani ya ngozi

Uvutaji sigara unasababisha saratani ya ngozi. Kemikali za sigara husababisha vidonda kwenye ngozi na ambavyo haviponi kwa urahisi. Baada ya muda hugeuka kuwa saratani.

6.Magonjwa ya meno

Sigara hutatiza mdomo na kuongeza uchafu unaoganda kwenye meno hivi kusababisha kuoza kwa meno, harufu mbaya mdomoni na uchafu wa meno. Sigara pia hutatiza kupona kwa vidonda hasa baada ya kung'olewa kwa jino. Saratani ya mdomo na ulimi inapatikana zaidi kwa wavutaji sigara na watumiaji wa tumbako za aina nyingine.

7.Magonjwa ya mapafu

Uvutaji wa siagara ndio sababu kubwa zaidi ya saratani ya mapafu. Pia husababisha kupasuka kwa vibofu vya hewa safi na kutoa harufu mbaya mwilini. Wavutaji pia hupata saratani ya koromeo na kuziba njia ya hewa na hivo basi inabidi kutobolewa kwa kishimo kwenye shingo hili kuwezesha mwadhiriwa kupumua.

8.Mifupa

Sigara inasababisha mifupa kuwa myepesi na kupunguza nguvu. Sababu ni kuwa kemikali zilizoko ndani ya sigara hupunguza uwezo wa mwili kujenga mifupa iliyo na nguvu. Mifupa kama hii huvunjika kwa urahisi na kuchukua muda mrefu sana(asilimia 80 zaidi ya mifupa ya kawaida)kupona.

9.Ugonjwa wa moyo

Sigara ndio sababu kubwa zaidi ya magonjwa ya moyo. Inasababisha moyo kupiga kwa kasi zaidi na hivyo kuongeza msukumo wa damu mwililni(high blood pressure). Mwishowe husababisha mshtuko wa moyo na hata kifo.Moja kati ya kila vifo tatu ulimwenguni hutokana na magonjwa ya moyo na huua zaidi ya watu milioni moja kwenye nchi za Afrika.

10.Vidonda vya tumboni

Sigara hupunguza uwezo wa mwili kujikinga dhidi ya viini vinavvyosababisha vidonda tumboni. Pia hupunguza uwezo wa tumbo kustahimili nguvu ya asidi baada ya kula. Vidonda vya mvutaji basi huwa ni vigumu kutibu, na mara nyingi hutokea tena baada ya kupona.

11.Vidole

Kutu ya sigara hukusanyika na kuganda kwenye kucha na vidole vya mvutaji. Kisha hubadilisha rangi ya vidole na kucha kuwa za manjano au maji ya kunde. Ngozi ya vidole pia hukauka na kuwa ngumu sababu ya joto na kemikali za sigara.

12.Wanawake

Sigara huongeza hatari ya kupata saratani ya fuko la uzazi(cancer of theuterus ). NI vigumu zaidi kwa mwanamke mvutaji sigara kutungwa mimba na ni rahisi sana kwake kumpoteza mtoto katika mimba.(miscarrige). Uvutaji wa sigara pia humfanya mwanamke kumzaa mtoto aliyekufa(stillbirth) au aliye na uzito usiotimia wa kawaida. Watoto hawa huwa na afya duni baadaye. Sababu ni kuwa kemikali za sigara hupunguza mwendo wa mtoto kukua akiwa angali mimbani. Sigara pia husababisha ugumba(menopause) kabla ya wakati wake. Sigara pia inaweza kumfanya mwanamke kuwa tasa.

13.Wanaume

Sigara inapunguza mpigo wa damu kwenye sehemu za uume. Sigara pia huharibu mbegu za wanaume na kwa hiyo watoto wanaowazalisha huwa na uwezekano mkubwa zaidi wa kupata magonjwa ya saratani. Sigara pia huwafanya wanaume kuwa tasa.

14.Magonjwa ya ngozi

Sigara huleta magonjwa mengi ya ngozi kama vile uvimbe, kuwashwawashwa na hudhoofisha hali ya ngozi.

15.Ugonjwa wa ‘Buerger'

Huu ni ugonjwa wa uvimbe kwenye mishipa ya damu ya miguuni na mikononi. Mishipa hii huzibika na kuzuia mwendo wa damu kwenye sehemu zilizoathirika. Isipotibiwa kwa haraka,mvutaji anaweza kukatwa miguu au mikono.

16.Saratani

Zaidi ya kemikali 40 zinazopatikana kwenye tumbako zimethibitishwa kusababisha saratani. Ukilinganisha na asiyevuta sigara :

16(a).Mapafu

Mvutaji ana uwezekano wa mara 22 zaidi wa kupata saratani ya mapafu

16(b).Pua

Mvutaji ana uwezekano wa mara 2 zaidi kupata saratani ya pua.

16(c).Ulimi

Mvutaji ana uwezekano wa mara 2 zaidi kupata saratani ya ulimi.

16(d).Tumbo

Mvutaji ana uwezekano wa kupata saratani ya tumbo mara 3 zaidi.

16(e).Figo

Mvutaji ana uwezekano wa kupata saratani ya figo mara 5 zaidi.

Saratani Zinginezo

Uchunguzi unaonyesha kuwa saratani ya mdomo ni hadi mara 27, koo(mara 12), koromeo(mara10).Uchunguzi pia umebaini kuwa kuna uhusiano fulani kati ya uvutaji sigara na saratani ya matiti.

Chanzo: Madhara ya kuvuta sigara - Wikipedia, kamusi elezo huru.Mkuu.@mathematics

https://www.jamiiforums.com/jf-doctor/79870-madhara-ya-kuvuta-sigara.html
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom