sajo
JF-Expert Member
- Nov 8, 2010
- 3,021
- 5,253
NDOA NA MATOKEO YA NDOA (TALAKA, UGONI)
Mambo ya ndoa sio mageni sana masikioni mwetu kwani wengine tupo ndoani na wengine marafiki zetu wapo ndoani na hata wazazi wetu wamekuwa ndoani. Kwa hiyo baadhi yetu ni matokeo ya ndoa za wazazi wetu na wengine tumepata matokeo ya ndoa zetu wenyewe (watoto, mali nk). Hivyo nitafundisha juu ya ndoa na matokeo yake kwa urahisi ili tuweze kuelewa na kujua hatua za kuchukua pindi tutapotaka kufanya jambo fulani lihusianalo na mambo ya ndoa. Tanzania, masuala ya Ndoa yanatawaliwa au yanaongozwa na Sheria ya Ndoa Sura ya 29 Rejeo la 2019 (The Law of Marriage Act Cap 29 R.E 2019).
Naitwa Lusajo W. Mwakasege, ni Mwanasheria, namba yangu ya simu ni 0713-368153 (inapatikana whatsapp In WhatsApp teilen na telegram) na barua pepe yangu ni mwakasege@gmail.com. Tuanze somo letu:
A: Nini Maana ya Ndoa?
Ndoa ni muungano wa hiyari kati ya mwanamke na mwanaume kwa nia au dhumuni la kuishi pamoja mpaka mwisho wa maisha yao au ya mmoja wao. Yaani wanakubaliana kuishi pamoja mpaka kifo kitapowatenganisha.
Kuna aina (kinds) mbili (2) za ndoa ambazo ni;
Ndoa ya mke mmoja (monogamous marriage) – ambapo mwanaume mmoja anamuoa mke mmoja tu
Ndoa ya wake wengi (polygamous) au huenda ikawa ya wake wengi (potential polygamous marriage) – ambapo mwanaume mmoja wakati wa kipindi cha ndoa yake ya awali anaweza kuoa mwanamke mmoja na kumwambia kuwa ataoa tena au kama alishaoa ni ile ambayo mwanaume anaoa wanawake wengine
Je, ndoa ni kweli kuwa ndoa ya kiislamu ni ya wake wengi?
Sio lazima iwe ya wake wengi - Ndoa iliyofungwa katika imani ya uislamu au kimila – hudhaniwa kisheria (presumption) kuwa ni ndoa ya wake wengi isipokuwa kama kutakuwa na uthibitisho kuwa sio ya wake wengi.
Hapa ni kuwa kama wanandoa wakati wa kusajili ndoa yao (katika cheti chao cha ndoa) walikubaliana na kusaini kuwa ndoa yao itakuwa ya mke mmoja, basi ndoa hii haitakuwa ya wake wengi hata kama ilifungwa kwa imani ya uislamu;
Je, ndoa ya kikristo ni ndoa ya mke mmoja tu? Mwanaume mkristo anaweza kufunga ndoa ya wake wengi?
Ndoa iliyofungwa kwa imani nyingine yoyote (ikiwa ni pamoja na ukristo) – itadhaniwa kisheria kuwa ni ndoa ya mke mmoja tu – isipokuwa kama kutakuwa na uthibitisho kuwa ni ya wake wengi;
Kama wanandoa wakati wa kusajili ndoa yao walikubaliana na kusaini kuwa itakuwa ya wake wengi kwenye cheti cha ndoa, basi ndoa ya kikristo inaweza kuwa ya wake wengi, ingawa ni amri ya dhehebu kuamua kuibali ndoa hiyo au la.
Je, Ndoa inatakiwa kudumu kwa muda gani? Umri wa Ndoa kudumu
Ndoa inapofungwa inatakiwa kudumu kwa maisha yote ya wanandoa mpaka kifo cha mwanandoa, au
Umri unaoruhusiwa wa mtu kuingia kwenye ndoa
Ili mtu aruhusiwe kufunga ndoa na iwe halali,
- Mwanaume anatakiwa kuwa na miaka 18 na kuendelea; NA
- Mwanamke anatakiwa kuwa na miaka 15 na kuendelea
B: MAHUSIANO YASIYORUHUSIWA
Je, mtu anaruhusiwa kuoa au kuolewa na mtu yeyote yule ili mradi wameridhiana?
HAPANA, Kisheria, sio kila mahusiano yanakubalika kwani kuna baadhi ya mahusiano hayaruhusiwi kisheria. Mahusiano yasiyoruhusiwa ni kama;
- Mtu kuoana na babu au bibi yake, mzazi wake, mtoto wake, mjukuu wake, kaka au dada yake, shangazi au mjomba, mtoto wa kaka au dada yake - yaani mpwa (niece or nephew),
- vivyo hivyo mtu kuoa ndugu wa aina hiyo wa upande wa mwenza wake
- Mtu kuoana na mwenza wa zamani wa babu au bibi, mzazi wake au mjukuu.
- Mtu kuoana na ndugu wa kuzaliwa na mzazi mmoja (kuchangia baba au mama)
Haya yote ni mahusiano haramu na mtu anayekuwa na mahusiano ya namna hii anafanya kosa kisheria, na ikiwa itathibitishwa mahakamani anaweza kuhukumiwa kifungo cha miaka 2 jela. Ila mahusiano mengine kwa baadhi ya mila yanatambulika kama halali na hivyo yanaweza yasiwe haramu - japo hayaandikwa kisheria, mfano mtu mume kuoa mtu na dada yake nk
Je, mtu aliye na ndoa anaweza kuoa tena na ndoa ikawa halali? (Ndoa ndani ya ndoa)
HAPANA, Mwanaume aliye na ndoa ya mke mmoja, hataruhusiwa kuoa mwanamke mwingine wakati wa uhai wa ndoa yake hiyo, na akifanya hivyo ndoa hiyo itakuwa ni batili
Vilevile, Mwanaume mwenye ndoa ya wake wengi, hataruhusiwa kufunga ndoa ya mke mmoja na mwanamke mwingine,
Upande wa Mwanamke Je?
Mwanamke aliyeolewa iwe kwa ndoa ya mke mmoja au ya wake wengi, hataruhusiwa kuolewa na mwanaume mwingine kwa ndoa ya aina yoyote ile wakati ndoa yake ikiwa hai.
C: UTARATIBU WA KUFUNGA NDOA;
Taarifa ya Ndoa (notice)
Ni lazima watu wanaotaka kuoana kutoa taarifa ya ndoa (notice) kwa msajili wa ndoa ya angalau siku 21 kabla ya tarehe ya kufunga ndoa, ingawa kukiwa na haraka sana kuna taarifa (notisi) ya siku 7 ambayo pia ni halali kisheria.
Taarifa hiyo,
- Itaonesha umri wao, anuani zao za makazi, hali zao za kindoa (single nk), aina ya ndoa wanayotaka kufunga, kama ndoa ni ya wake wengi – majina ya wake waliotangulia, tarehe ya ndoa na mahali ndoa itakapofungwa
- itasainiwa na wahusika wote (wanandoa watarajiwa)
Ukitoa taarifa za uongo wakati wa kuandika tangazo la ndoa, unakuwa umefanya kosa la jinai na likithibitishwa mahakamani, utapata adhabu ya kifungo cha miaka 3 jela.
Mapingamizi ya ndoa
Baada ya tangazo la ndoa kuwekwa hadharani, mtu yeyote anaweza kuwasilisha pingamizi la ndoa kwa msajili wa ndoa akiwa na sababu za msingi kuzuia ndoa hiyo isifungwe;
Kama muoaji ni mume wa ndoa ya wake wengi, mkewe wa kwanza au mke yoyote kati ya wakeze anaweza kuwasilisha pingamizi kwa msajili kuzuia ndoa hiyo kwa sababu kama vile,
- uwezo wa kifedha wa mumewe upo chini kiasi kwamba kuleta mke wa pili kutafanya maisha yawe magumu sana kwa mke mwenyewe na watoto,
- Mwanamke anayetarajiwa kuolewa ni mkorofi (kipele),au mwenye ugonjwa wa kuambukiza ambao unaweza kuleta majanga kwenye familia
Watu wengine wanaweza kuja na sababu nyingine zozote wanazoona zinafaa kuzuia ndoa inayotarajiwa lakini muamuzi wa mwisho juu ya mapingamizi ya ndoa atakuwa ni msajili wa ndoa.
Mapingamizi yatayowasilishwa atayachambua na ikiwa anaona yana uzito atawaita wapingaji pamoja na wanadoa watarajiwa na kuyasikiliza na kuyatolea uamuzi.
Mapingamizi yanawasilishwa kwa njia ya barua (maandishi).
Aina au Namna (Manner) za ufungaji Ndoa
Ndoa inaweza kufungwa
Ndoa iliyofungwa kimila ni lazima isajiliwe na msajili wa ndoa ili iweze kurasimishwa na kuingia kwenye daftari la ndoa.
Hata watu wa imani moja ya dini bado wanaruhusiwa kufunga ndoa ya kiserikali ikiwa wataona wanapendezwa kufanya hivyo.
Shuhuda wa Ndoa
Ndoa lazima iwe na mashahidi angalau wawili (2)
Ni lazima mashahidi wawe na umri ambao unaruhusiwa kwa mtu kufunga ndoa.