barafu
JF-Expert Member
- Apr 28, 2013
- 6,726
- 32,818
Imekuwa ni kawaida kuwepo kwa malalamiko mengi sana katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere(JNIA).Malalamiko haya ni ya wadau wa usafiri wa anga wa ndani na nje ya nchi.
Imekuwa ni kama tatizo sugu,kila mara na kila wakati watu wanaotumia uwanja wa JNIA wamekuwa wakilalamika sana juu ya hali,uduni wa huduma,uchafu,kadhia ya joto na mambo mengi yenye kukera na kupoteza taswira nzuri ya uwanja wetu.Hiki ni kioo na sura ya Taifa,lakini uwanja huu unatia aibu.
Rais amefanya ziara za kushitukiza kama mara mbili,lakini holaa watu hawana cha kubadilika,Mh.Waziri Mbarawa kazungukia pale zaidi ya mara tatu,naambiwa wakati mwingine akienda rasmi,na wakati mwingine kimyakimya bila vyombo vya habari,lakini bado watu hawabadiliki.Mambo ni yaleyale ya "bussiness as usual".Hapa kuna tatizo sio bure.
Kumekuwa na tatizo "sugu" linalotokana na "usugu" wa viongozi waliokabidhiwa mamlaka ya kuongoza kiwanja/viwanja vya ndege Tanzania.Haiwezekani kwa malalamiko yale yote na tuhuma za abiria wa ndani na nje ya nchi,lakini kila kiongozi akifika hapo anakuta mambo ya hovyo ni yaleyale au zaidi ya yale aliyoyakuta mwanzoni.Hapa pana tatizo kubwa
Kwa taarifa rasmi kutoka watu wa ndani ya mamlaka hiyo,ni kuwa toka mwaka 2015 mpaka sasa 2017,kuna Wakurugenzi wanne (04) waliopewa nafasi ya kuongoza uwanja wa JNIA na wote kwa sababu moja au nyingine wameshindwa na kuondolewa kwenye kiti hicho.Yaani ndani ya kipindi cha miaka miwili,wakurugenzi wanne wamekalia kiti na kuondoka.Hii ni uthibitisho kuwa suala la "Management" limewashinda.
Hii ni kusema ndani ya taasisi hiyo,uweledi na umakini katika suala la "Management" ni butu.Wanajaribiana uongozi kama kiatu cha mtumba,anajaribu huyu na huyu bila mafanikio.Sasa huwezi kufanya majaribio yasiyo na kikomo,matokeo yake inakosekana "Sustainability" katika kufikia kile ambacho nchi washindani katika masuala ya "aviation" wanakifikia.
Kwa taswira hii,bila shaka ni ni moja kati ya mamlaka ambayo walio na dhamana,hawana utaratibu wa kuandaa viongozi wa baadae kwa kufuata uweledi na si kujuana na kupendeleana.Waziri Prof.Mbarawa usipofanya uamuzi mgumu,kila siku utakuwa unakutana na madudu na kuondoa uongozi,mwisho wa siku kunakuwa hakuna maendeleo endelevu.
Haiwezekani,mtu anaharibu kitengo hiki,halafu anapelekwa kitengo kingine,ukifumba na kufumbua anaibukia kwenye ukurugenzi wakati huku nyuma rekodi yake ni chafu na ya hovyo,ila sababu ana ndugu au rafiki,basi anapanda kwa kasi kuelekea katika vyeo.Aviation haiitaji "vilaza" na "wanaogushi" uweledi,mwisho wa siku tunaabika kama Taifa na si mtu mmoja.
Kwa msongamano wa abiria wa kuja na kuondoka katika uwanja wa JNIA,uchafu,uzembe,uweledi mdogo wa viwango vya kimataifa kwa wafanyakazi wa uwanja,mikataba inayotia shaka pamoja na uzembe kwa level ya Management ya TAA kama Operator wa kiwanja,mambo haya yanaweza kuwa kama hatua kuelekea kupunguza changamoto hizi.
(1)Mh.Waziri Prof Mbarawa unaweza kufanya "Secondment".Kuchukua watu wenye uweledi wa masuala ya "management",waliobobea ili waje kusaidiana na watu wenye uwelewa wa mambo ya aviation na kuiondoa mamlaka hii,kutoka hapo ilipokwama kwenda hatua nyingine.Jambo hili liliwezekana kwa Mchechu,kutoka katika sekta ya fedha mpaka kwenye mambo ya nyumba NHC,na kwa kiasi fulani ikaonekana kuna mabadiliko.Achana na hizo degree za kuchukua asubuhi pale GongolaMboto Kampala na kuzikabishi kiwanja kikubwa kama hicho.
(2)Kwa kupunguza suala la msongamano wa abiria nyakati za "Peak hours",ambapo kwa JNIA naambiwa inaanza saa 1500hrs-1730hrs.Kupunguza msongamano huu,TCAA kama regulator wa usafiri wa anga na TAA kama Operator wa viwanja vya ndege,wawashauri "Airlines" wanaokuja Tz,kubadili kidogo "slots" zao ili kupunguza uwezekano wa ndege zote kubwa kuingia kwa wakati unaokaribiana.
Haiwezekani jengo kama lile,lipokee abiria zaidi ya 2000 kwa wakati mmoja.Muda huohuo Emirates analeta Boeing 7777-300ER inashusha abiria 410,Ethiopia analeta B777-300 abiria 400,Qatar na Dreamliner abiria 350,S.Africa abiria 180,Oman Air 150,Mozambique,Air Zimbabwe,Etihad,Kenya Airways na RwandAir.Hawa wote wakishuka ndani ya muda huo...Lazima uwanja uzidiwe.Hivi ndivyo imefanyika katika viwanja vingine duniani,kueleza hali ya uwanja na kuomba mabadiliko kidogo ya ratiba.
(3)Ukarabati wa mara kwa mara wa miundombinu chakavu.Hakuna ubishi kuwa kwa sasa uwanja wetu umezidiwa na uchakavu,na hii ni kutokana na uzembe wa muda mrefu,ama wa serikali yenyewe au management ya kiwanja.Kuandikia dokezo la ununuzi wa AC lakini mtu anatia ndani hela yote.AC nzuri zinanunuliwa zile za VIP LOUNGE wanakopita wakubwa,huku kwa kina mie,inapotezewa.Jengo la TBII tumelitumia toka 1980's.Nakumbuka lile la TBI tulizindua na Mzee Songambele wakati huo mkuu wa mkoa wa Dsm.Ukarabati/Matengenezo ya hapa na pale,yafanyike kwa umakini na si kwa zima moto.Zabuni za wanaopewa kukarabati zifuate taratibu na si kupeana kama sasa.
(4)Kuboresha uweledi wa Wafanyakazi wa Kiwanja.Huwezi kuwa mfanyakazi wa kiwanja cha kimataifa halafu unakuwa "locoloco" tu.Unakutana na mtu wa security anafungua begi huku anakutupia lugha chafu,wanafikiri kuwa mlinzi basi ni kutoa lugha za vitisho na kukaripia.Hii ni kwa sababu hawa wanakuwa hata nchi nyingine hawajfika kujua wenzao wanafanyaje kazi.
Msiwe wabahiri,pelekeni training hawa watu hata wajue huko duniani watu wanahudumiaje mteja.Wazungu wanesama "Travelling is like reading a book,those who do not travell,read only one page".Watumishi wengi wa JNIA wanaonekana wamesoma "page" moja tu.
(5)Ajiri watu wenye uweledi na mishahara yenye unafuu.Kuna skendo hapo kuwa wengi wa security officers na "wacheza mpira".Yaani mkubwa mmoja hapo ni kiongozi wa team ya mpira ya wizara ya uchukuzi,ili apate team ya kwenda SHIMIWI kwa urahisi na apige panga posho za SHIMIW,anapachika wacheza mpira kitengo cha security,ambao atawatumia wakati wa michezo.Hii inasababisha kuwepo na watu wasio serious sana na kazi sbb wanajua wao wapo pale kwa mkono wa mkubwa na wanajishikiza tu ili wakati wa mshindano wawe na sifa za kuunda team ya uchukuzi.Si ajabu ukakutana na security anakutolea lugha chafu kama mgambo wa jiji
(6)Ipeni TAA mamlaka kamili kama mlivyofanya kwa idara nyingine za Uchukuzi kama TCAA.Mamlaka hii kuwa "Semi-Autonomous" inapunguza uwezo wake wa kufanya mambo kwa haraka.Hivyo kuzorotesha utendaji wa kazi na utatuzi wa changamoto za hapa na pale.Serikali kuchukua kila kitu katika mapato ya mamlaka hizi,na kuondoa uwezo wa zenyewe kujipangia bajeti za matumizi ya ndani ni makosa.Huwezi kuwa na uwanja mkubwa kama huo,halafu pesa ya kununua "Conveyer Belt" inasubiliwa kuombwa hazina.Sasa nini umuhimu wa Gvt Agency Acts iliyoanzisha haya mashirika ya umma?
Ni kweli watu walikuwa wapigaji,watu wamejipa safari za nje,watu wamejipa training kiundugu,lakini hizi kwa sasa zinawez kutafutiwa dawa na kuthibitiwa.Ipeni mamlaka hii uwezo wa kujiendesha.
(7)Pitia mikataba yenye utata.Hii ni pamoja na hicho kimgahawa cha ajabujabu hapo nje,mara ya mwisho juzi nimeshuka hapo bado kipo.Unajenga kibanda juu ya maandishi ya "NO PARKING",tena kwenye eneo la kiwanja?Ni aibu sana.Migahawa na maduka kule juu departure Lounges...Fuatilia wale watu wanalipa kweli kodi?Hebu fuatilia hiyo kampuni ya Porters,ina uhalali kweli au ni biashara za watu?
(8)Serikali iharakishe ufunguzi wa Uwanja wa Terminal Three.
Hii inaweza kuwa suluhisho,itapunguza msongamano na aibu zinazopatikana Terminal Two.Wizara na serikali kwa ujumla,itilie mkazo uwanja huu uishe kwa wakati ili kukabiliana na changanoto za TBII.
Mwisho,ninakutakia yote mema Ami Prof Mbarawa.Katika watu ambao wanajitahidi katika kuongoza bila mihemko ya hapa na pale,wewe ni mmoja wao.Ninakutakia kila la heri.Huu ni mtazamo wangu,sina chuki na mtu.Yaliyo na umuhimu yabebe,ushauri unaweza kupokelewa au kukataliwa.
barafu wa JF,mapumzikoni Arusha Tz