diana chumbikino
JF-Expert Member
- May 29, 2018
- 428
- 368
WAKATI Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa leo akitarajiwa kuzindua Maonesho ya Pili ya Teknolojia na Uwekezaji kwenye Sekta ya Madini mjini hapa, Soko Kuu la Dhahabu Geita limeweka rekodi ya kwanza kwa mauzo ya jumla ya kilo 504.8 zenye thamani ya Sh bilioni 52.2 Mafanikio hayo yametajwa kuchangiwa kwa kiasi kikubwa na uamuzi wa serikali wa kuanzisha Soko Kuu la Dhahabu mkoani Geita, huku mkoa ukisambaza masoko mengine katika kila halmashauri.
Awali, upatikanaji wa dhahabu kutoka kwa wachimbaji wadogo haukuwahi kuvuka kilo 200 kwa mwezi. Lakini, sasa ni takribani kilo 500 kwa mwezi. Mkuu wa Mkoa wa Geita, Robert Gabriel alibainisha hayo jana mjini hapa ikiwa ni siku moja imepita tangu kuanza kwa Maonesho ya Teknolojia na Uwekezaji katika Sekta ya Madini awamu ya pili, yanazozinduliwa leo la Majaliwa ambaye ameshawasili mkoani hapa.
Gabriel alisema mauzo hayo, yatachangia kukua kwa uchumi na hivyo kuongeza pato la taifa kupitia mrahaba na ada ya ukaguzi. Alisema mkoa mkoa huo umefanya mapinduzi makubwa katika udhibiti, ukusanyaji na mauzo ya dhahabu. Katika maonesho hayo zaidi ya washiriki 260 wanahudhuria na Mkuu wa Mkoa alisisitiza kuwa kiwango cha uuzaji dhahabu, kimeongezeka mara dufu kutokana udhibiti na ufuatiliaji wa karibu.
Akifafanua, Gabriel alisema awali kwa mwezi kilo takribani 80 ndizo zilikuwa zinapatikana. Hiyo ilikuwa kabla ya utaratibu wa kuzuia makinikia ya dhahabu kutolewa nje ya mkoa. Kwamba baada ya kuanzishwa kwa masoko, likiwemo Soko Kuu la Dhahabu mjini Geita pamoja na masoko mengine madogo, ukusanyaji umeongezeka hadi kufikia kilo 500 kwa mwezi.
Kwamba kutokana na mauzo ya dhahabu kilo hizo 504.8, serikali imeweza kuingiza Sh bilioni tatu kutokana na mrahaba unaotokana na madini hayo. Mbali na kuiingzia serikali zaidi ya Sh bilioni tatu kama mrahaba, pia serkali imeweza kuingiza Sh milioni 522 zilizotokana na ada ya ukaguzi wakati wa mchakato wa uandaaji hadi kuuzwa kwa madini haya aina ya dhahabu.
Kwa twakimu hizo kiwango cha mrahaba ulioingia serkalini kutokana na uzalishaji huo, kilipanda kutoka Sh milioni 282 mwaka 2012/2013 hadi kufikia Sh bilioni 1.8. Zaidi ya Sh milioni 178 zililipwa kwa ajili ya ada ya ukaguzi kwa mwaka 2017/2018 “Kabla ya kuanzishwa kwa soko tulikuwa hatuna uwezo wa kukusanya kilo 200, lakini sasa mambo ni mazuri sana.
Katika hii miezi minane ya mwaka huu, tumeweka rekodi ya kukusanya kilo 1,900. Kufikia mwishoni mwa mwaka huu tunaweza kufika zaidi ya kilo 3,000. Tani tatu si mchezo, hii ina maana kubwa sana kiuchumi. “Mwaka 2017 kwa mwaka mzima dhahabu uliyopatikana kutoka kwa wachimbaji wadogo ilikuwa kilo 1,000, mwaka 2018 ikapanda hadi kilo 1,400 lakini sasa, ndani ya miezi minane tayari kilo 1,900 zimepatikana,” alisema Mkuu huyo wa mkoa.
Alisisitiza kuwa, dhahabu inakuja kuikomboa Geita na nchi kiuchumi, kutokana na ukweli kwamba asilimia 70 ya dhahabu yote nchini inapatikana Geita. Kwa mujibu wa Gabriel, kilo moja ya dhahabu katika soko la dunia kwa sasa ni wastani wa Sh milioni 100.
Alisisitiza kuwa, maonesho hayo yamelenga kuwa sehemu ya utatuzi wa changamoto zinazowakabili wachimbaji wadogo na wa kati, hivyo kutoa chachu ya ukuaji wa Sekta ya Madini na uchumi wa nchi kwa ujumla. “Tunafahamu kuwa, wachimbaji hususani wa kati na wadogo wamekuwa wakikabiliwa na changamoto mbalimbali kama vile ukosefu wa teknolojia bora za uchimbaji, vitendea kazi, mitaji, masoko ya uhakika pamoja na wabia katika hatua mbalimbali za uzalishaji. Sasa majibu haya yote yatapa tikana wakati wa maonesho. Wadau wote muhimu wapo,” alisema.
Maonesho hayo ni ya pili kufanyika toka mkoa wa Geita uanzishwe rasmi mwaka 2012. Maonesho hayo ya kihistoria katika ukanda wa Afrika Mashariki yenye Kaulimbiu; “Madini ni Chachu ya Ukuaji wa Uchumi wa ViwandaTuwekeze Kwenye Teknolojia Bora ya Uzalishaji na Tuyatumie Masoko ya Madini”, yataonesha teknolojia ya uchimbaji, uchenjuaji, uongezaji thamani na kutangaza fursa za uwekezaji na biashara katika Sekta ya Madini ya Dhahabu nchini.
Soko la Geita ni la kwanza katika ukanda huo, ukiondoa la Afrika Kusini, hivyo kulifanya kuwa la aina yake. Aidha, katika kuhakikisha uhakika wa soko unakuwepo, Serikali imefungua masoko mengine sita katika halmashauri mbalimbali za mkoa huku la saba likitarajiwa kufunguliwa hivi karibuni.