Unaweza kudhibiti u.t.i mwenyewe..!

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,268
33,040
UNAWEZA KUDHIBITI U.T.I MWENYEWE..!

U.T.I ni ugonjwa sugu unaosumbua sana watu wengi hivi sasa, wakubwa kwa wadogo. U.T.I (Urinary tract Infection) ni ugonjwa unaoathiri njia ya mkojo na huweza kusababisha maumivu makali na unapojiimarisha mwilini kwa muda mrefu huathiri figo pia.

Dalili za ugonjwa huu ni pamoja na mtu kusikia haja ya kukojoa kila wakati na kusisimka wakati wa kujisaidia, kusikia maumivu, kutoa mkojo mchafu na hata kutoa haja ndogo iliyochanganyika na damu.

Wataalamu wetu wa masuala ya tiba wanatueleza kuwa tatizo hili hujitokeza pale mlango wa njia ya haja ndogo inaposhambuliwa na bakteria ambao husambaa na wasipotibiwa mapema huenea hadi kwenye figo na athari zake ni mbaya.

UNAWEZA KUDHIBITI U.T.I KWA TIBA MBADALA

Kwa kawaida kila ungonjwa una tiba mbadala, siyo lazima kwenda hospitali. Unaweza kuudhibiti au kuponya ugonjwa huu kwa kunywa maji mengi pamoja na juisi itokanayo na matunda halisi, iwapo utawahi kabla tatizo halijawa sugu.

Kwa maana nyingine, unaweza kujikinga na ugonjwa huu kwa kuwa na mazoea ya kunywa maji ya kutosha kila siku.

Ukinywa maji ya kutosha yatakufanya uende haja ndogo kila mara na kwa njia hiyo wale bakteria watakuwa wakitoka na hatimaye kuisha kabisa. Aidha, njia nyingine ya kuudhibitibi ugonjwa huu ni kunywa maji mengi au kwenda haja ndogo mara baada ya kufanya tendo la ndoa, kitendo hiki husaidia kuwaondoa mapema bakteria wote ulioambukizwa wakati wa kujamiiana na mwenzio.

Katika hali ya kawaida, ugonjwa wa UTI hutoweka ndani ya siku tatu mara baada ya kuanza kutumia tiba asili ya kunywa maji mengi na juisi ya matunda halisi, iwapo ugonjwa utaendelea kuwepo baada ya siku hizo, hiyo itakuwa na maana ugonjwa wako umeshakomaa na hivyo hauwezi kutibika kwa tiba hii ya nyumbani.

Katika hali kama hii, utakuwa huna njia nyingine isipokuwa kwenda hospitalini na kuonana na daktari ambaye atakufanyia uchunguzi na kukupatia dozi sahihi ambayo utatakiwa kuizingatia bila kukosa.

Uamuzi huu ni muhimu hasa kama unasikia maumivu makali ambayo yanaweza kuwa yanasababishwa na kuathirika kwa figo. Kwa kawaida tiba ya kidaktari kwa ugonjwa huu huhusisha matumizi ya dawa kali za antibiotics, ambazo watu wengi wanazikimbia kutokana na athari zake za baadae (side effects).

Lakini ni muhimu kufuata ushauri wa dokta na kumaliza dozi ili kuepuka uwezekano wa kurejea kwa ugonjwa, tena kwa kasi kubwa.

KUZUIA

Ili kujiepusha na ugonjwa huu, suala la usafi na kuwa na tabia ya kunywa maji ya kutosha ni jambo muhimu sana. Hakikisha unajisafisha vizuri mara baada ya kwenda haja na kubadilisha mara kwa mara nguo yako ya ndani, hasa kwa akina mama.

Vile vile usikae na haja ndogo kwa muda mrefu, nenda kajisaidie mara nyingi kadri unavyosikia kufanya hivyo. Kitu cha mwisho cha kuzingatia kwa mgonjwa wa UTI ni kupunguza unywaji wa pombe na vinywaji vingine vyenye sukari, kwa sababu sukari ni chakula cha bakteria hivyo kwa kuendelea kunywa kinywaji chenye sukari kutaifanya hali kuendelea kuwa mbaya.

Ugonjwa huu ni rahisi kuepuka kwa mtu anayependa kunywa maji ya kutosha na kunywa juisi halisi kila siku.

DAYATI MUHIMU KUDHIBITI UTI

Katika kuudhibiti ugonjwa huu, pendelea kula vyakula ama vinywaji vyenye kiwango kikubwa cha vitamini C ambayo utakipata kwenye matunda ya aina mbalimbali yakiwemo machungwa, mboga za majani n.k.

Jiepushe na ulaji wa vyakula vya kupaki kama vile chizi, chokoleti na bidhaa nyingine zilizotengenezwa kutokana na maziwa.

Pia jiepushe na ulaji wa vyakula vyenye viungo vingi kama pilau, epuka vyinywaji vyenye caffeine, kilevi na sigara na mwisho achana na vinywaji kama soda na vinavyofanana na soda.
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom