Unapenda movies? Tazama hizi weekend hii!

SteveMollel

JF-Expert Member
Jul 12, 2015
8,411
23,698
Habari wapenda filamu wenzangu. Ni siku nyingine tena tumepewa nafasi ya kukutana hapa na kujadiliana mambo kadhaa kadhaa kuhusu utazamaji wa filamu, starehe ambayo kwa sasa ukizingatia na hali ya mlipuko wa Corona inatufaa zaidi kwa kutuhamasisha tukae ndani kujiepusha na michangamano isiyo ya ulazima.

Kwa wale waliobahatika kupitia 'session' ya kwanza, nadhani wanajua ni nini kinafanyika, kama lah! basi waweza kupitia sehemu hiyo hapa...

Unapenda movies? Pitia hapa kidogo - JamiiForums

Na kuhusu kupata filamu hizo ambazo zimeanishwa katika huo uzi ama ambazo zitaainishwa katika uzi huu wa sasa, kwa urahisi kama ambavyo tulichangiwa na mwenzetu, waweza tumia 'application' ya POPCORN TIME, ambayo inapatikana google. Huko utadownload filamu zote kwa urahisi na ubora unaopendeza. Uzuri wake ni app ambayo haitakutaka uwe na kingine cha ziada, yenyewe inajitosheleza.

Basi pasipo na kupoteza muda, leo tutazamie filamu hizi mpya, hazina hata mwaka, ambazo kwa namna moja ama nyingine, binafsi, nimeona zinafaa kuzipatia muda wako. Hivyo basi kama utaona zitakupendeza, kutokana na mchanganuo wake, waweza kuzipakua uakafurahia muda wako.



VIVARIUM ya 2020.
vivarium.jpg

Filamu hii ni picha halisi ya 'modern horror'. Kwa wale ambao pengine huwa hatufuatilii haya ni hivi, kuna 'classic horror' na 'modern horror', zote ni filamu za kutisha lakini zikitengwa na muda na mtindo wa maudhui.

Classic horror ni zile filamu za kuogofya za zamani ingali modern horror ni hizi za sasa. Kwenye upande wa maudhui, Classic Horrror hujikita zaidi kwenye kugawa pande mbili (mema dhidi ya mabaya) na visa vyake huwa 'straight' huku vikihusisha mambo ya majumba yanayochungwa na roho za ajabu ama majini-majini na mashetani (rejelea filamu za kibongo kama Nsyuka), ingali modern Horror ikiwa imejikita kwenye kukanganya zaidi (confusing and ambiguous), haiko wazi, na pia ikiwa na uhalisia zaidi na huku mwisho wake ukiwa si wa kufurahisha (unhappy endings).

Jambo hili, la mwisho wa filamu usio wa kufurahisha, huwa linawaudhi sana watazamaji kwa kuona kiu chao hakijakatwa ama wameachwa hewani, lakini inabidi tujue kwamba huo ndo' uhalisia wenyewe wa maisha. SI KILA JAMBO HUISHIA VILE WEWE UNAVYOTAKA.

Filamu hii, Vivarium, kama nilivyonasibu hapo mwanzoni, ni modern horror hivyo kwa namna moja ama nyingine yakanganya kimawazo kiasi kwamba kuielewa na kuifurahia yahitaji uweke 'attention' kwenye kila jambo kwani kwenye filamu 'nothing comes by a chance' - hakuna ambacho kinawekwa ili tu kijaze nafasi.

IPO HIVI: Wapenzi wawili ambao wapo kwenye mahusiano motomoto na machanga wanavutiwa na kutafuta makazi mapya kwa ajili ya kujenga maisha yao. Kutokana na hilo, wanatafuta 'agency' inayohusika na mambo ya makazi (kwa jina: Prospect Properties) , ambapo wanakutana na bwana aitwaye Martin akiwaeleza kuhusu mradi wa makazi mapya waliopa jina la 'Yonder - the forever home'.

Lakini bwana huyu, Martin, kwa macho tu ya binadamu anaonekana si mtu wa kawaida. Tabasamu lake ni la picha. Macho yake hayaendani na uso. Na hata 'body movements' zake ni robotic. Kwa namna moja, wageni wake wanashangazwa na hili lakini hitaji lao la makazi linawapumbaza, haswa mwanamke ambaye anatoa usafiri wake kwenda kuona makazi hayo.

Wanapofika huko, wanaonyeshwa nyumba namba 9, na bwana Martin anawaonyesha ndani, eneo kwa eneo. Wanafika kwenye chumba fulani ambacho kimetengwa mahususi kwa ajili ya mtoto, kimepakwa rangi ya bluu - hivyo kumaanishwa kimetengwa kwa ajili ya mtoto wa kiume. Mwanamke anashangazwa kwa kuuliza swali lakini hapewi jibu.

Kidogo bwana Martin anapotea na kuwaacha wageni kwenye makazi haya mapya. Wapenzi hao wanajaribu kuondoka hapo lakini hawafanikiwi abadani. Kila njia wanayoitumia inawarudisha palepale kwenye nyumba namba 9! Mpaka giza linaingia na kulazimika kulala humo ndani.

Kesho yake wanajitahidi kufanya kila namna lakini hamna wanachofanikiwa. Mwanaume anapanda juu ya paa kutazama njia kwa juu lakini hakuna anachoambulia. Nyumba zote zinafanana na hakuna mtu mwingine yeyote aliyekuwepo hapo. Wapo peke yao!

Ajabu katika makazi hayo, tofauti na makazi ya binadamu wa kawaida, kuna ukimya mno. Miti midogo iliyokuwepo 'around' haitikisiki. Na zaidi, anga ni la ajabu kwa mawingu yake yenye maumbo yanayofanana! Mawingu ambayo si ya kawaida ukiyatazama kwa mpangilio wake.

Kama hayo hayatoshi, wapenzi hawa wanapewa mtoto wa kiume ndani ya boksi (ndo' maana kile chumba kilikuwa na rangi ya bluu, yalikuwa ni maandalizi ya mtoto wa kiume ajaye), pamoja naye akiambatana na ujumbe uloandikwa "mlee mtoto huyu na mtaachiwa huru".

Hivyo sasa wapenzi hawa wanakabiliwa na mtihani mpya, si wa kutafuta kujiokoa tena, bali kumlelea mtoto ambaye si wa kwao. Mtoto ambaye anakua kupita kiasi ... mtoto ambaye huiga matendo ya walezi wake .... mtoto ambaye si binadamu wa kawaida kwa matendo yake!

Basi kutokana na maajabu hayo, huku akiwa haridhishwi kabisa na yanayoendelea, mwanaume anachimba shimo kwenye bustani ya mbele ya nyumba akitafuta namna ya kujikomboa. Kadiri bwana huyo anavyofukua anasikia sauti huko chini. Japo anachoka lakini anapambana kila siku kutimiza adhma yake kiasi kwamba afya yake inaanza kudhoofu.

Naye mwanamke sababu ya kukosa muda zaidi na mpenzi wake anayehangaika na kuchimba shimo, anapata wasaa wa kuwa karibu na mtoto huyo wa ajabu, ukaribu ambao unapelekea mwanamke huyo kupata picha ya mtu ambaye huwa anamtuma na kumwendesha mtoto huyo baada ya kumuiga umbo lake (huwa anatabia ya kuiga).

Basi, kwa kasi kubwa, mtoto anakuwa kijana mkubwa na yule mwanaume kutokana na afya kudhoofu zaidi, anakufa. Kitendo ambacho kinamkasirisha mwanamke baada ya kuona mtoto aliyemlelea , yani yule wa ajabu, hakuwa na msaada wowote ule zaidi ya kuleta mfuko wa kuhifadhi maiti.

Kwa hasira hizi anaamua kumjeruhi mtoto huyu kwa kutumia sururu, NA HAPA NDO INAKUWA TURNING POINT YA FILAMU. Anapata kugundua sauti halisi ya mtoto aliyemlelea (kwani ile aliyokuwa anaitumia tangu mwanzo ilikuwa ya kuiga), anapata kugundua pia mwendo halisi mtoto huyo, na pia anagundua uwepo wa makazi mengine chini ya yale ya kwao baada ya mtoto kukimbilia chini ambako hakuwahi kupadhania.

Uwepo wa makazi hayo chini ndo inatupa sasa picha kuwa hata lile anga la mawingu ya mafungu tuliloona hapo awali lilikuwa ni kiini macho tu. Si anga. Ile miti, si miti. Lille Jua, si Jua la kawaida. Hata zile nyumba zote zilizopo hapo walipokuwapo, zote ni replica moja tu ya nyumba namba 9. Nyumba ni moja tu! ...wamo kifungoni ndani ya boksi kama neno VIVARIUM linavyomaanisha (kontena inayotunzia wanyama kwa ajili ya kuwasoma ama kuwafuga tu) ... pia kama cover ya filamu inavyoonyesha, nyumba hii moja ikiwa na milango yenye watu pande zote kumaanisha kuna nyumba zingine juu ya hii kama ilivyokuwa kwa chini ya hii.

Na kifo cha mwanamke huyo ndo kinafungua fumbo la ndege anbao tunawaona mwanzoni kabisa mwa filamu. Namna ambavyo ndege aliyepandikizwa kwenye kiota (kitaalamu huwa inaitwa brood parasitism) alipowatoa wazawa na kisha akakua kupita kiasi katika hali ambayo anataka kumla mama yake mlezi kabisa!

Hivyo ndege huyo ndo' yule mtoto ambaye anapandikizwa kwa binadamu apate kulelewa. Na kiota kile ndo dunia. Na kinachoendelea, ni hawa watu wa ajabu waki-take over ulimwengu wetu kwa kuwageuza binadamu kuwa mateka katika ulimwengu wao wa kipekee.

Japo wapo miongoni mwetu, wanajitahidi kutuiga wafanane na sisi kwa kila kitu (kama sauti, matendo na mwendo) ili kutupambaza, lakini bado hawajafanikiwa kuwa binadamu kamili ...

Katafute utazame....



SWEETHEART ya 2020.

sweetheart.jpg


Hii ni filamu ambayo hutuonyesha ni kwa namna gani binadamu anaweza kumbana na changamoto mbalimbali za maisha, kuanzia kiakili mpaka kiuhalisia, lakini bado akashinda.

Ukitazama vema ndani ya filamu hii utaona namna ambavyo mhusika mkuu anavyopigana vita mbili kwa wakati mmoja, vita ya kwanza ni ile ambayo ipo mbele yake (hii iko wazi, kila mtu anaiona) na vita ya pili ni ile ambayo inakuja kuonekana baadae (hii yataka mazingatio kuibaini) vita ya mapenzi yasofaa (toxic relationship).

IPO HIVI: Binti aitwaye Jennifer anajibaini amesukumiwa fukweni baada ya kupata ajali mbaya ya boti iliyokumbwa na kimbunga kikali baharini wakiwa kwenye tafrija.

Kidogo binti huyo anabaini kuna mwenzake pia amesukumiwa ufukweni, aitwa Brad, lakini alikuwa amejeruhiwa vibaya na jiwe la bahari. Mwenzake huyo hadumu muda mrefu, anamuuliza Jennifer kama amekiona kiumbe fulani, na kabla hajajieleza vema, kidogo baada ya Jennifer kumtafutia maji, anakufa.

Hivyo basi Jennifer anakuwa peke yake rasmi ndani ya kisiwa, hivyo inamlazimu ajifunze upesi kujenga makazi, kuvua samaki na kuishi dhidi ya chochote atakachokikuta humo kisiwani.

Kwa sababu za kibadamu, Jennifer anamzika Brad lakini kesho yake anabaini mwili wa Brad umefukuliwa! Anafanya namna kujiokoa kwa kurusha fataki juu kuwahabarisha watu wapitao na ndege lakini matokeo yake fataki hilo linamjuza kiumbe kilichopo kwenye maji juu ya makazi ya Jennifer.

Sasa basi Jennifer anakuwa na kazi ya kupambana haswa, akitumia akili na mwili, dhidi ya kiumbe cha ajabu ambacho kinakuja kila usiku kutafuta chakula. Kiumbe hicho kinaishi baharini ndani ya shimo lakini usiku hutoka.

Baada ya siku kadhaa, Jennifer anapata kuwaona watu wemgine wakiwa baharini ndani ya boti ndogo ya hewa. Watu hao mmoja ni mpenziwe, aitwa Lucas, na mwingine ni mwanamke kwa jina, Mia.

Baada ya watu hao kupumzika, Jennifer anawasihi kwamba hapo kisiwani si salama kabisa. Hivyo wafanye namna waondoke kabla usiku haujaingia. Ubaya haaminiki. Anajaribu sana kuwashawishi wenzake pasipo mafanikio, mwishowe anajaribu kutoroka kwa kutumia boti walokuja nayo wenzao lakini anadhibitiwa na kufungwa kwenye mti mpaka usiku.

Anapokuja kuamka, mpenzi wake Lucas anamshambulia kwa lawama kumhusu huku akijigamba kumgharamia mwanamke huyo kwa kila kitu lakini bado amekuwa kama wingu jeusi juu yake! ... hivyo hapa tunaoata kuona mahusiano baina ya watu hawa si mazuri. Mwanamke huyu ni mtu wa chini, anayenyanyaswa kwa uhitaji wake (hii ndo vita ya pili mbali na ya yule kiumbe).

Wakiwa hapo bado wanazozana, yule mwanamke aitwaye Mia anadakwa na kiumbe kile cha ajabu na kuvutiwa baharini! Hapo sasa Lucas anaamini yale alokuwa anayasema Jennifer.

Kunapokucha, wanaamua kujitafutia chakula na kisha kujipaki waondoke zao lakini ajabu kiumbe kinawashambulia nyakati za mchana, kinaharibu boti na kufanikiwa kumbeba Lucas!

Hivyo basi Jennifer anarudi tena kisiwani, na sasa anaamua kutomkimbia tena kile kiumbe bali asimame kupambana nacho ... ni aidha afe yeye ama adui!

Anajipanga vilivyo na kisha anamkaribisha mgeni wake katika pambano la kukata na shoka.

Atatoboa? Na je atafanikiwa kuondoka kisiwani? Pakua filamu ufurahie!



THE INVISIBLE MAN ya 2020.
the invisible man.jpg


Kwa waliotazama filamu hii watakubaliana na mimi kwamba tumelaghaiwa. Haikua vile tulivyokuwa tumetaraji tokea mwanzoni kuwa ni zile aina za filamu ambazo huogofya (Horror) bali ni tungo tu ya kisayansi (Sci-fi). Kwa hili, nawapa kongole. Mfumo huu umefanikiwa kutengeneza kimuhemuhe na kihoro, lakini baadae humfanya mtu ajione hakuipa filamu mazingatio ya kutosha kuelewa ujanja wa watengenezaji (producers).

Zaidi ya hapo, filamu hii hutuonyesha kitu cha thamani kubwa kwa binadamu – UHURU. Binadamu unaweza ukampa vyote, ukamtimizia kila hitaji lakini bado kama atakosa uhuru, maisha yake yatakosa maana. Bila shaka ndo’ maana hata adhabu kwa binadamu huwa ni kifungo, ushawahi kujiuliza? Kwanini mtu aliyekosa asinyimwe mavazi? Asinyimwe makazi ama chakula? Badala yake anapewa vyote hivyo lakini ananyimwa uhuru. Anatiwa ndani!

Haijalishi utaishije humo ndani, utatembelewa na ndugu, utakula na kunywa, lakini hutapata amani. Kwanini? Sababu unakosa kitu kikubwa na cha thamani. Unakosa uhuru.

IPO HIVI: Mwanamke aitwaye Cecillia yupo kwenye mahusiano na mwanaume tajiri mkubwa mwenye kampuni ya kisasa kabisa inayohusika na bidhaa za macho. Mwanaume huyo ni mtu mwenye uwezo mkubwa kifedha na kiuchumi lakini shida yake ni moja – mtawala kupita kiasi. Anasimamia kuanzia kile anachosema mwanamke wake, anachokula, anapokwenda, anachovaa na hata anachokifikiri pia! Kiasi kwamba Cecillia anajiona yupo kifungoni. Hafurahii kabisa mahusiano haya. Kama ukimuuliza kati ya fedha na kuwa huru toka kwa mwanaume huyu utachagua nini, bila shaka atachagua uhuru wake.

Cecilia anajaribu kujiokoa lakini anashindwa. Kuna muda anasema aliwahi kufikiria kutoroka lakini mwanaume wake akasoma mawazo yake na kumwambia kamwe asije akawaza hilo jambo kwani haijalishi atakimbilia wapi, atampata tu. Tena atamjia akiwa haonekani!

Vitisho hivyo havikumzuia Cecillia, siku moja katikati ya usiku, ambapo ndo’ tunaona mwanzoni kabisa mwa filamu, anatoroka nyumbani mwa tajiri huyo baada ya kumtilia madawa. Kwasababu anafahamu vema makazi haya, anafanikiwa kuzima ‘alarm’ zote ndani ya nyumba, anafuta rekodi za picha zake na kubadilisha mielekeo ya kamera.

Anatoka nje ya nyumba lakini si bahati anasababisha ‘alarm’ ya gari kuanza kulia. Anakimbilia nje na kukutana na dada yake ambaye tayari alishampanga kuhusu tukio lake, dada yake huyo amekuja na gari. Anapanda gari na kabla ya mwanaume wake kumkamata, wanafanikiwa kutoroka!

Anaenda kuishi kwa bwana mmoja ambaye ni askari kwa usalama wake zaidi, lakini maisha yake yanakuwa ya tabu sana sababu za kutojiamini. Kila saa anahisi bwana wake anaweza kujiri na kumdhuru wakati wowote ule hali inayompelekea asifurahie maisha yake kabisa.

Baada ya siku kadhaa, anapata habari kuwa bwana wake amefariki. Habari hizo analetewa na dada yake na kumtaka Cecy awe huru sasa kwani mtu aliyekuwa anamhofia hayupo tena duniani. Lakini kwa namna moja ama nyingine, Cecy haonyeshwi kubebwa na habari hiyo. Ni kama vile ana mashaka.

Na kweli, baada ya siku chache, anaanza kuhisi kuna mtu yu karibu naye akimfuatilia. Anaanza kujihisi hayupo peke yake. Ajabu zaidi, anakuja kuona chupa ya dawa aliyoitumia kumu – overdose mwanaume wake ikiwa ndani ya chumba alichopo!

Anahaha na kujaribu kuwaambia watu kuhusu kile anachokiamini ya kwamba mwanaume wake amerudi na ndiye anamtesa lakini hamna anayemwamini. Wanahisi ana matatizo ya akili kwa kumdhania mfu kutenda mambo hayo. Hapa ndo Cecy anakumbuka ahadi ambayo mwanaume wake, Adrian, alimpatia ya kuwa hawezi kumkimbia. Atamrudia hata katika njia ambayo haonekani!

Kama haitoshi, Adrian akiwa katika hali yake ya kutoonekana, anamfitinisha Cecilia na watu wake wa karibu kabisa hivyo kumfanya Cecy kuwa mpweke. Katika namna hiyo, kwa kuona vielelezo vya hapa na pale, Cecy anajiaminisha kuwa Adrian hakufa, hivyo sasa anatakiwa kupambana na adui yake uso kwa uso!

Adui ambaye haonekani.

Cecy anafanikiwa kurudi nyumbani kwa Adrian na kubaini siri kubwa ya kwamba Adrian akufa bali ametumia ujuzi wake wa sayansi kutengeneza suti ambayo inamfanya asiweze kuonekana kwa macho ya kawaida. Baada ya kugundua hilo, anamjuza dada yake wakiwa wameketi mgahawani, lakini katika kuhakikisha siri haivuji, mtu yule asioyeonekana anamkata shingo dada mtu na kisha kisu anakitia mkononi mwa Cecy!

Cecy anaoekana muuaji. Anakamatwa na kutiwa kifungoni wakiendelea kumpima kama ni mzima ama amerukwa na akili, lakini napo huko bado bwana Adrian anaendelea kumfuata na kusababisha mauaji.

Ni nini haswa bwana huyu anachokitaka? Kwanini amuui Cecilia?

Ni hivi, ingali Cecy akiwa anaishi na bwana huyo na huku akiwa amedhamiria siku moja kuja kumtoroka, katika kuhakikisha haji kuwa na mahusiano yoyote yale na Adrian, aliamua kutumia dawa za uzazi wa mpango ili asije kushika mimba. Lakini pasipo kujua, in fact anakuja kujuzwa na ndugu yake Adrian, kuwa muda wote huo alikuwa anajiongopea kwani Adrian alibadili madawa hayo na kuweka mengine yasokuwa na madhara.

Sasa Cecy ana mimba ya Adrian. Na hili yote yaishe inabidi akubali kurudi nyumbani apate kuishi naye na walelee mtoto kwa pamoja. La sivyo, hatomuua, ila atahakikisha wale wote awapendao wanateseka na kufa!

Je yupo tayari kwa kipi? Ni umbali gani anaweza kwenda kuhakikisha anapata UHURU wake wa thamani? Na ni wazi uhuru wake hauwezi kuja ingali Adrian akiwa hai, je atamkabili vipi mtu huyo asiyeonekana? Mtu ambaye jamii inaamini amekwisha kufa?

Katafute ufurahie…

innocent dependent kajojo elly obedy rejea ekomu1 Vladimir Lenin Ignas lyamuya Yna aika Penison Neylu ndukulusudicho IMERN Amorbwoy fofre kemisho chaliifrancisco jooohs Manlax Braibrizy Zoë kathago Tit 4 Tat Leonard Robert free lander TELLO kiwaki kizaizai Otorong'ong'o Marvelous King The Gunners Mshuza2 troublemaker miminimkulimaakachekasana vesta zipompa mpinyo mkorea Sweta LA Tanzania Rubawa safuher Prodigy Oligarchy nguvu gabby jacoby THEBADDEST dubwang AMMARITO Carleen del moe Lili masta Zuriel_cfc super black Washawasha travellwr
 
Asante mkuu kwa kutujuza na kutupa story za hizo movie binafsi nimevutiwa na story zake na nitazipakua ila naomba msaada kidogo je nitapataje English subtitle kwenye movie kupitia popcorn time?
Mkuu ukidownload kupitia popcorn time, substitle unazipatia hukohuko automatically!
 
. Shukran sana mkubwa, unazidi kufanya nizidi kuenjoy movies, barikiwa sana mzee ikiwezekana tutajiorganise wapenda movies wa jf tukutafutie japo shekeli ya soda 😁
Hahaha usijali mkuu, huwezi amini nimejifunza mengi sana kupitia post ya kwanza. Nimebaini kwamba kila mtu ana kitu ndani yake ambacho chaweza kuwa na manufaa kwetu wote. Ni muhimu kuchangamana.
 
Ukitaka usipate shida, download, usi-stream. Wewe nenda moja kwa moja kwenye kile kitufe cha download badala ya cha play. Ikija lile tangazo la VPN, bonyeza continue, select torrent, mambo mswano!

Sent using Jamii Forums mobile app
Asante mkuu kwa maelezo yako mazuri ulionipa vipi je inakula mb nyingi? Ninaweza kupata movie kuanzia mb 450 kushuka chini kupitia hiyo app?
 
Ni Horror na Thriller pia. Si ya kutisha kama hizo zingine udhaniazo. Hata pia The Invisible Man. Tunaweza ziita soft Horror
Hiyo sweetheart hata sikuimaliza ikanibore nikaifutilia mbali. Sio mpenzi wa horror movies kabisaaaa.
 
Je? Ukiingia play store kuitafuta popcorn time! Maana unaweza kuandika zikaja nyingi tu! Je yenyewe ina muonekano gani? Kwa mfano
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom